Sura ya 19
Baada ya Har-Magedoni, Dunia-Paradiso
1. (a) Watu wengi wana maoni gani juu ya Har-Magedoni? (b) Biblia inasema nini juu yake?
“HAR-MAGEDONI” ni neno lenye kuogopesha watu wengi. Mara nyingi viongozi wa ulimwengu wanalitumia kutaja Vita ya Ulimwengu ya Tatu inayoweza kutokea. Walakini, Biblia inaisema Har-Magedoni kuwa ndipo mahali pa vita ya uadilifu itakayopiganwa na Mungu. (Ufunuo 16:14, 16) Vita hiyo ya Mungu itatayarisha njia ya kuwapo taratibu mpya yenye uadilifu.
2. (a) Nani watakaoharibiwa penye Har-Magedoni? (b) Basi ni mazoea gani ambayo imetupasa kwa hekima tuyaepuke?
2 Tofauti na vita vya wanadamu, vinavyoua wote wazuri na wabaya, Har-Magedoni itaangamiza wabaya peke yao. (Zaburi 92:7) Yehova Mungu atakuwa ndiye Hakimu, naye ataondoa watu wo wote ambao kwa kukusudia wanakataa kutii sheria zake za uadilifu. Leo watu wengi hawaoni ubaya wa uasherati, kulewa, kusema uongo au kudanganya. Lakini, kulingana na Mungu, mambo hayo ni mabaya. Hivyo penye Har-Magedoni hataokoa wale wanaoendelea kuyatenda. (1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8) Kwa kujua sheria za Mungu zinazokataza mambo hayo, ni jambo la maana watu ambao huenda wakawa wanazoea mabaya hayo wageuze njia zao.
3. (a) Yesu aliulinganisha mwisho wa ulimwengu wa sasa na nini? (b) Ni nini kitakachompata Shetani na mashetani wake? (c) Kulingana na Maandiko yaliyo katika kurasa zifuatazo, ni hali za aina gani zitakazofurahiwa katika dunia-paradiso?
3 Baada ya Har-Magedoni hakuna sehemu ya ulimwengu huu mbovu itakayobaki. Watu wanaomtumikia Mungu peke yao ndio watakaoendelea kuishi. (1 Yohana 2:17) Yesu Kristo alilinganisha hali iliyopo na ile ya siku za Noa. (Mathayo 24:37-39; 2 Petro 3:5-7, 13; 2:5) Baada ya Har-Magedoni, ufalme wa Mungu utakuwa ndiyo serikali pekee itakayotawala dunia. Shetani na mashetani wake watakuwa wametoweka. (Ufunuo 20:1-3) Angalia, katika kurasa zinazofuata, baadhi ya baraka ambazo Biblia inaonyesha watu watiifu watafurahia.
WANADAMU WOTE WANAKAA KWA AMANI
“Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake . . . Mfalme wa amani. Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.”—Isaya 9:6, 7.
“Katika siku zake mwadilifu atachipuka, na wingi wa amani mpaka mwezi utakapokuwa haupo. Naye atakuwa na raia kutoka bahari mpaka bahari na kutoka ule Mto mpaka miisho ya dunia.”—Zaburi 72:7, 8, NW.
HAKUNA VITA TENA
“Njoni myatazame matendo ya [Yehova], jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:8, 9.
NYUMBA NZURI NA KAZI YENYE KUPENDEZA KWA KILA MTU
“Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine . . . wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu; kwa sababu wao ni wazao wa hao waliobarikiwa na [Yehova], na watoto wao pamoja nao.”—Isaya 65:21-23.
UHALIFU, JEURI NA UOVU VIMETOWEKA
“Maana watenda mabaya wataharibiwa Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, utapaangalia mahali pake wala hatakuwapo.”—Zaburi 37:9, 10.
“Waovu watatengwa na nchi, nao wafanyao hila watang’olewa.”—Mithali 2:22.
DUNIA YOTE INAKUWA PARADISO
Yesu alisema: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:43, NW.
“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29, NW.
CHAKULA TELE KWA WATU WOTE
“[Yehova] wa majeshi atawafanyia mataifa yote karamu ya vinono vilivyojaa mafuta, karamu ya divai iliyokaa juu ya urojorojo wake, iliyochujwa sana.”—Isaya 25:6.
“Kutakuwako na nafaka tele juu ya dunia; na juu ya milima kutakuwako mfuriko.” “Dunia yenyewe hakika itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.”—Zaburi 72:16; 67:6, NW.
4, 5. (a) Ni hali gani ambazo hazitakuwapo tena katika dunia-paradiso? (b) Ni mambo gani ambayo hayawezi kufanywa leo mahali pengi ambayo watu wataweza kufanya?
4 Bila shaka unataka uishi katika dunia-paradiso kama ile bustani ambamo mtu wa kwanza Adamu aliumbwa. (Mwanzo 2:8; Luka 23:43, NW; ZSB) Ebu fikiri—vita, uhalifu wala jeuri havipo tena. Utaweza kutembea po pote wakati wo wote wa mchana na usiku bila kuogopa kuumizwa. Waovu hawatakuwapo tena.—Zaburi 37:35-38.
5 Maana yake ni kwamba hawatakuwapo wanasiasa wadanganyifu na viongozi wa biashara wenye pupa ili wagandamize watu. Wala watu hawatalemezwa na gharama kubwa za kodi ili kulipia silaha za kijeshi. Hakuna mtu atakayekaa tena bila chakula kizuri na makao ya starehe kwa sababu ya kutokuwa na fedha za kuvilipia. Ukosefu wa kazi, infuleshoni na bei za juu sana hazitakuwapo tena. Taabu zinazoleta kuteseka kwa jamaa za leo hazitakuwapo tena. Wote watakuwa na kazi ya kupendeza, na wataweza kuona na kufurahia matokeo ya kazi ngumu.
6. (a) Ni kazi gani ambayo waokokaji wa Har-Magedoni watafanya? (b) Mungu atabarikije kazi itakayofanywa?
6 Kwanza, wale watakaookoka Har-Magedoni watakuwa na kazi ya kuisafisha dunia na kuondoa magofu yote ya taratibu (mfumo) hii ya kale. Kisha watakuwa na pendeleo, chini ya uongozi wa utawala wa Ufalme, la kuilima dunia na kuifanya iwe mahali pazuri pa kuishi. Itakuwa kazi yenye furaha kama nini! Mungu atabariki kila jambo litakalofanywa. Atafanyiza hali inayofaa ya hewa ya kukuza mazao na kufuga mifugo, na atahakikisha kwamba vitu hivyo vimelindwa visipatwe na magonjwa na madhara.
7. (a) Ni ahadi gani ya Mungu itakayotimizwa? (b) Wakristo wanangojea nini kulingana na ahadi ya Mungu?
7 Ahadi hii ya Muumba mwenye upendo, kama ilivyotolewa kupitia mtunga zaburi wa Biblia, itatimizwa: “Waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” (Zaburi 145:16) Ndiyo, matakwa yote yanayofaa ya watu wenye kumwogopa Mungu yatashibishwa kabisa. Hatuwezi hata kuwazia namna maisha yatakavyokuwa mazuri katika paradiso hapa duniani. Akieleza juu ya mpango wa Mungu wa kubariki watu wake, mtume Petro aliandika hivi: “Ziko mbingu mpya na dunia mpya ambazo sisi tunangojea kulingana na ahadi [ya Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13, NW; Isaya 65:17; 66:22.
8. (a) Sababu gani hatuna haja ya mbingu mpya halisi? (b) “Mbingu mpya” ni nini?
8 “Mbingu mpya” hizo ni nini? Si mbingu mpya halisi. Mungu alizifanya mbingu zetu halisi kwa ukamilifu, nazo zinamletea utukufu. (Zaburi 8:3; 19:1, 2) “Mbingu mpya” maana yake ni utawala mpya wa dunia. “Mbingu” za sasa ni serikali zilizoundwa na wanadamu. Penye Har-Magedoni hizo zitatoweka. (2 Petro 3:7) “Mbingu mpya” zitakazokaa mahali pa hizo ni serikali ya Mungu ya kimbingu. Mfalme atakuwa Yesu Kristo. Lakini watakaotawala pamoja naye wakiwa sehemu ya “mbingu mpya” ni wafuasi wake waaminifu 144,000.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3.
9. (a) “Dunia mpya” ni nini? (b) Dunia itakayoharibiwa ni nini?
9 Basi, “dunia mpya” ni nini? Si sayari mpya. Mungu aliiumba sayari hii Dunia ikafaa wanadamu kuishi juu yake, na ni mapenzi yake idumu milele. (Zaburi 104:5) “Dunia mpya” maana yake ni kikundi kipya au jamii mpya ya watu. Mara nyi-ngi Biblia inatumia neno “dunia” kwa njia hiyo. Kwa mfano, inasema: “Dunia nzima [maana yake, watu] ilikuwa na lugha moja.” (Mwanzo 11:1, ZSB) “Dunia” itakayoharibiwa ni wale watu wanaojifanya kuwa sehemu ya mfumo (taratibu) huu mbovu wa mambo. (2 Petro 3:7) “Dunia mpya” itakayokaa mahali pa hiyo itakuwa ni watumishi wa kweli wa Mungu ambao wamejitenga na ulimwengu huu wa watu waovu.—Yohana 17:14; 1 Yohana 2:17.
10. (a) Ni nani sasa wanaokusanywa, na wanaingizwa ndani ya nini? (b) Kulingana na Maandiko yaliyo katika kurasa zinazofuata, ni mambo gani yatakayofanywa katika dunia-paradiso yasiyoweza kufanywa na serikali za wanadamu?
10 Sasa hivi watu wa jamii na mataifa yote watakaokuwa sehemu ya hiyo “dunia mpya” wanakusanywa kuletwa katika kundi la Kikristo. Ule umoja na amani vilivyo kati yao sasa ni mfano mdogo tu wa kuonyesha kitakachofanya maisha katika dunia-paradiso baada ya Har-Magedoni yawe yenye kufurahisha sana. Kweli kweli, ufalme wa Mungu utatimiza yale ambayo serikali ya kibinadamu haikuweza hata kutumaini kutimiza. Ebu ziangalie baraka chache kama hizo katika kurasa zinazofuata.
UDUGU WENYE UPENDO WA WANADAMU WOTE
“Mungu hana ubaguzi. Mtu wa taifa lo lote anayemcha Mungu na kutenda yaliyo haki anapokelewa naye.”—Matendo 10:34, 35, HNWW.
“Tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha . . . Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena.”—Ufunuo 7:9, 16.
“Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.”—Isaya 11:6; Isaya 65:25.
HAKUNA MAGONJWA TENA, HAKUNA UZEE WALA KIFO
“Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
“Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.
WAFU WANAFUFULIWA
“Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.
“Bahari ikatoa wafu waliokuwa ndani yake; Mauti na Hadeze zikatoa wafu waliokuwa ndani yao.”—Ufunuo 20:13, ZSB.
11. Mara nyingi ni mambo gani yanayoharibu aina ya paradiso inayotengenezwa na watu?
11 Lo! jinsi paradiso chini ya ufalme wa Mungu itakavyokuwa bora kuliko cho chote kinachoweza kuletwa na mfumo huu wa kale! Ni kweli kwamba watu fulani leo wamepafanya mahali wanapoishi paonekane kama paradiso. Lakini watu wanaoishi pamoja katika mahali hapo huenda wakawa ni wakorofi na wachoyo, na huenda hata wakachukiana. Na, muda si muda wanakuwa wagonjwa, wanazeeka na kufa. Walakini, baada ya Har-Magedoni paradiso hiyo ya duniani itakuwa na vitu vingi kuliko nyumba nzuri, bustani na mashamba ya starehe tu.
12, 13. (a) Ni hali gani za amani zitakazokuwapo baada ya Har-Magedoni? (b) Ni nini linalohitajiwa ili hali hizo zitokezwe?
12 Ebu fikiri. Watu wa jamii zote na mataifa yote watajifunza kuishi pamoja wakiwa jamaa moja ya ndugu na dada. Watapendana kweli kweli. Hakuna atakayekuwa mchoyo wala asiye na fadhili. Hakuna atakayemchukia mwenziye kwa sababu tu ni wa jamii nyingine, rangi nyingine, au ni wa kutoka mahali pengine. Ubaguzi utakoma. Watu wote duniani watakuwa marafiki na majirani wa kweli. Kweli kweli, itakuwa paradiso kwa jinsi ya kiroho. Wewe ungependa kuishi katika paradiso hiyo chini ya hizo “mbingu mpya”?
13 Leo watu wanazungumza sana juu ya kuishi pamoja kwa amani, na hata wameunda tengenezo la “Umoja wa Mataifa.” Hata hivyo sasa ndipo watu na mataifa wamegawanyika hata kuliko zamani. Ni nini linalohitajiwa? Mioyo ya watu inahitaji kubadilishwa. Lakini haiwezekani kabisa kwa serikali za ulimwengu huu kufanya mwujiza huo. Walakini, ule ujumbe wa Biblia juu ya upendo wa Mungu unaufanya mwujiza huo.
14. Ni mambo gani yanayotendeka sasa kuhakikisha kwamba hali hizo za paradiso zitatimizwa?
14 Wanapojifunza juu ya mfumo (taratibu) mpya wenye uadilifu, mioyo ya watu wengi inaongozwa impende Mungu. Hivyo wao vilevile wanaanza kutendea wengine kwa upendo, kama vile Mungu anavyotenda. (1 Yohana 4:9-11, 20) Hiyo inamaanisha badiliko kubwa katika maisha zao. Watu wengi waliokuwa wakorofi na wenye kujaa chuki, kama wanyama wakali sana, wamekuwa wapole na wenye kuamanika kwa njia hiyo. Kama kondoo wenye kutii, wao wamekusanywa ndani ya kundi la Kikristo.
15. (a) Kuna vikundi gani viwili vya Wakristo? (b) Ni nani watakaokuwa wa kwanza kuwa “dunia mpya”?
15 Kwa miaka zaidi ya 1,900 kumekuwako kazi ya kukusanya pamoja “kundi dogo” la Wakristo 144,000 watakaotawala pamoja na Kristo. Ni wachache tu wa hao waliobaki duniani; wengi wao tayari wanatawala pamoja na Kristo mbinguni. (Luka 12:32; Ufunuo 20:6) Lakini akinena habari ya Wakristo wengine, Yesu alisema: “Na kondoo wengine ninao, ambao si wa zizi hili [yaani, lile “kundi dogo”]; na hao nao imenipasa kuwaleta; na sauti yangu wataisikia; kisha kutakuwako kundi moja na mchungaji mmoja.” (Yohana 10:16) “Mkutano mkubwa” wa hao “kondoo wengine” sasa unakusanywa. Watakuwa ndio wa kwanza wa ile “dunia mpya.” Yehova atawalinda waipite “dhiki ile iliyo kuu” wakati wa mwisho wa huu mfumo (taratibu) mbovu waendelee kuishi katika paradiso ya kidunia.—Ufunuo 7:9, 10, 13-15.
16. Ni mwujiza gani utakaofanya kuishi pamoja na wanyama kuwe furaha?
16 Baada ya Har-Magedoni mwujiza mwingine utaongezwa kwenye hali za paradiso. Wanyama kama simba, simba-milia, chui na dubu, ambao sasa wanaweza kuwa hatari, watakaa kwa amani. Itakuwa vizuri kama nini wakati huo kutembea katika miitu kisha simba ajiunge kutembea nawe kwa muda, au labda baadaye dubu mkubwa ajiunge nawe! Hakuna mtu ye yote atakayehitaji tena kuogopa kitu kingine kilicho hai.
17, 18. (a) Ni mambo gani yanayoleta huzuni ambayo hayatakuwapo tena katika dunia-paradiso? (b) Sababu gani tunaweza kuwa na hakika kwamba afya bora itafurahiwa na watu wote?
17 Lakini hata nyumba ziwe nzuri namna gani, hata bustani ziwe nzuri namna gani, hata watu wawe wenye fadhili na upendo namna gani au wanyama wawe na urafiki namna gani, tukiwa wagonjwa, tukizeeka na kufa, bado kungekuwako huzuni. Lakini ni nani anayeweza kuletea watu wote afya bora? Serikali za wanadamu zimeshindwa kuondoa kansa, magonjwa ya moyo na magonjwa mengine. Lakini hata kama zingefanya hivyo, madaktari wanakubali kwamba hilo halingezuia watu wasizeeke. Bado tungekuwa tukizeeka. Mwishowe macho yetu yangekuwa na kiwi, minofu yetu ingelegea, ngozi yetu ingekuwa na makunyanzi, na viungo vilivyo ndani ya miili yetu vingeharibika. Kifo kingefuata. Huzuni kama nini!
18 Baada ya Har-Magedoni, katika dunia-paradiso, mwujiza mkubwa wa Mungu utabadili yote hayo, maana ahadi ya Biblia ni hii: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani alionyesha uwezo wake wa kuponya aina zote za magonjwa na maradhi yanayotokea kwa sababu ya dhambi tuliyorithi kwa Adamu. (Marko 2:1-12; Mathayo 15:30, 31) Vilevile kuzeeka kutazuiwa chini ya utawala wa Ufalme. Walio wazee watakuwa vijana tena. Ndiyo, ‘nyama ya mtu itakuwa nyororo zaidi kuliko ile ya ujana wake.’ (Ayubu 33:25, NW) Utakuwa msisimuko kama nini wakati huo kuamka kila asubuhi na kujua kwamba uko katika afya bora kuliko jana!
19. Ni adui gani wa mwisho atakayebatilishwa, na kwa jinsi gani?
19 Bila shaka hakuna mtu mwenye kuishi katika afya bora kabisa ya ujana katika hiyo dunia-paradiso atakayetaka kufa. Na hakuna mtu atakayehitaji kufa! Mwishowe kupokea kwao zile faida za dhabihu ya ukombozi kutakuwa na maana ya kufurahia zawadi bora kutoka kwa Mungu ya “uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Warumi 6:23) Kama Biblia isemavyo, “sharti [Kristo atawale akiwa mfalme], hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.”—1 Wakorintho 15:25, 26; Isaya 25:8.
20. Ni nani, zaidi ya watu wanaoishi sasa, watakaoifurahia dunia-paradiso, na hilo litawezekanaje?
20 Hata watu ambao sasa wamekufa watafurahia kuishi katika dunia-paradiso. Watarudi kwenye uzima! Basi, wakati huo, badala ya matangazo ya vifo, kutakuwako ripoti zenye furaha juu ya wale ambao wamefufuliwa. Weee! itakuwa vizuri kama nini kukaribisha akina baba, akina mama, watoto na wapendwa wengine waliokufa wanaporudi kutoka makaburini! Nyumba za kuwekea wafu, makaburi wala mawe ya kuonyesha wafu walipozikwa hayatabaki yaharibu uzuri wa dunia-paradiso.
21. (a) Ni nani watakaosaidia kuhakikisha kwamba sheria na maagizo ya hizo “mbingu mpya” yanafuatwa? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba kweli sisi tunazitaka hizo “mbingu mpya” na hiyo “dunia mpya”?
21 Ni nani watakaoongoza au kusimamia shughuli zitakazofanywa katika dunia-paradiso? Sheria zote na maagizo yote yatatokana na zile “mbingu mpya” zilizo juu. Lakini duniani hapa patakuwapo wanaume waaminifu watakaowekwa wahakikishe kwamba sheria na maagizo hayo yanafuatwa. Kwa sababu wanaume hao wanawakilisha serikali ya kimbingu kwa njia ya pekee, Biblia inawaita “wana-wafalme.” (Isaya 32:1, 2; Zaburi 45:16, NW) Hata katika kundi la Kikristo leo wanaume wanawekwa kwa njia ya roho takatifu ya Mungu waangalie na kusimamia shughuli zake. (Matendo 20:28) Baada ya Har-Magedoni tunaweza kuwa na hakika kwamba Kristo atahakikisha kwamba wanaume wanaofaa wamewekwa ili waiwakilishe serikali ya Ufalme, maana wakati huo atakuwa akiongoza moja kwa moja mambo ya kidunia. Unawezaje kuonyesha kwamba wewe unazitazamia kwa hamu zile “mbingu mpya” na “dunia mpya” za Mungu? Ni kwa kufanya kila jambo unaloweza utimize matakwa ya kuishi katika mfumo (taratibu) mpya huo wenye uadilifu.—2 Petro 3:14..