Kusaidia Wengine Waabudu Mungu
“Ikiwa . . . asiyeitikadi yeyote au mtu wa kikawaida anakuja ndani,... siri za moyo wake zinakuwa dhahiri, hivi kwamba yeye ataanguka juu ya uso wake na kuabudu Mungu.”—1 WAKORINTHO 14:24, 25, NW.
1-3. Ni jinsi gani wengi katika Korintho walivyosaidiwa kupata kibali cha Mungu?
KATIKA safari yake ya pili ya umisionari, mtume Paulo alikaa katika jiji la Korintho kwa mwaka mmoja na nusu. Humo yeye ‘alisongwa sana [alishughulika mno, NW] na lile neno, akishuhudia.’ Tokeo likawa nini? “Wakorintho wengi waliposikia, waliamini, wakabatizwa.” (Matendo 18:5-11) Wao wakawa “waliotakaswa . . . , walioitwa wawe watakatifu.”—1 Wakorintho 1:2.
2 Baadaye Apolo alizuru Korintho. Mapema kidogo, Prisila na Akila walikuwa wamemsaidia aelewe “njia ya Bwana kwa usahihi zaidi,” kutia na ubatizo. Hivyo yeye akawa Mkristo mwenye nia njema au kibali cha Mungu. (Matendo 18:24–19:7) Apolo naye, kwa zamu yake, alisaidia Wakorintho ambao hapo kwanza ‘walikuwa wamechukuliwa kufuata sanamu zisizonena.’ (1 Wakorintho 12:2) Inaelekea kuwa watu hao walipewa maagizo ya Biblia katika maskani zao; wangeweza pia kujifunza kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo.—Matendo 20:20; 1 Wakorintho 14:22-24.
3 Tokeo la fundisho hilo lilikuwa kwamba wengi ambao hapo kwanza walikuwa ‘wasioitikadi na watu wa kikawaida’ walivutwa kwenye ibada ya kweli. Lazima iwe iliridhisha sana kuona wanaume na wanawake wakifanya maendeleo kuelekea ubatizo na kibali cha Mungu! Jambo hilo lingali linaridhisha.
Kusaidia ‘Wasioitikadi na Watu wa Kikawaida’
4. Ni katika njia gani wengi leo wanasaidiwa kama wale waliokuwa katika Korintho?
4 Mashahidi wa Yehova leo pia wanatii amri ya Yesu “kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza.” (Mathayo 28:19, 20, NW) Baada ya kupanda mbegu za ukweli katika mioyo yenye upokezi, wao wanarudi na kuzitia maji. (1 Wakorintho 3:5-9; Mathayo 13:19, 23) Mashahidi wanatolea watu mafunzo ya Biblia ya kimaskani kila juma bila malipo ili watu hao waweze kujibiwa maswali yao na waweze kujifunza kweli za Biblia. Watu hao wanaalikwa pia kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova mitaani mwao, hata kama vile “wasioitikadi” wa karne ya kwanza walivyohudhuria katika Korintho. Lakini inawapasa Mashahidi wa Yehova wawe na rai gani juu ya watu ambao wanajifunza Biblia na kuja mikutanoni?
5. Kuna msingi gani wa Kimaandiko wa kuwa na tahadhari katika kushughulika pamoja na watu fulani?
5 Sisi tunafurahi sana kuwaona wakimkaribia Mungu. Na bado, sisi tunazingatia akilini kwamba wao si waitikadi waliobatizwa. Kumbuka pia masomo mawili ambayo msingi wayo ni makala iliyotangulia. (1) Waisraeli walionyesha hadhari kuelekea walowezi wa kigeni ambao, ingawa walikuwa karibu-karibu na watu wa Mungu na walitii sheria fulani-fulani, hawakuwa waongofu waliotahiriwa, akina ndugu katika ibada. (2) Wakristo Wakorintho wenye kushughulika pamoja na ‘wasioitikadi na watu wa kikawaida’ walikuwa chonjo kwa sababu ya maneno ya Paulo: “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, kwa jinsi isivyo sawasawa; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi?”—2 Wakorintho 6:14.
6. Ni jinsi gani ‘wasioitikadi’ wanavyoweza ‘kukaripiwa’ na mikutano, na karipio hilo linakuwa la hali gani?
6 Kwa hiyo ingawa sisi hukaribisha ‘wasioitikadi na watu wa kikawaida,’ tuna habari kwamba wao hawajatimiza bado viwango vya Mungu. Kama vile Biblia inavyoonyesha kwenye 1 Wakorintho 14:24, 25, NW, huenda watu hao wakahitaji ‘kuchunguzwa kwa ukaribu,’ hata ‘kukaripiwa’ (kubainishwa, UV), na mambo ambayo wanajifunza. Karipio hilo si la namna ya kihukumu; hawaitwi mbele ya halmashauri ya hukumu ya kundi kwa kuwa bado wao si washiriki walo waliobatizwa. Badala ya hivyo, kutokana na wanayojifunza, wapya hao wanakuja kusadiki kwamba Mungu hushutumu njia zozote za ubinafsi na za kukosa adili.
7. Ni maendeleo gani zaidi ambayo wanafunzi wengi watataka kufanya na kwa nini?
7 Wengi wasiobatizwa huenda baadaye wakataka kuchukua hatua inayozidi kuhudhuria mikutano tu wakiwa wajifunzi wenye kupendezwa. Maneno haya ya Yesu yanaonyesha kwa nini: “Mwanafunzi hawi mkuu kuliko mwalimu wake, lakini kila mtu ambaye amehitimu hulingana na mwalimu wake.” (Luka 6:40) Mwanafunzi wa Biblia anaweza kuona kwamba mwalimu wake ana rai ya kwamba huduma ya shambani ni muhimu na anapata furaha kutokana nayo. (Mathayo 24:14) Kwa hiyo imani inapokua, yule ambaye amekuwa akijifunza kweli za Biblia na kuhudhuria mikutano huenda akathamini moyoni maneno haya: “Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima miguu yake aletaye habari njema, yeye aitangazaye amani, aletaye habari njema ya mambo mema, yeye autangazaye wokovu.” (Isaya 52:7; Warumi 10:13-15) Ingawa hajabatizwa, huenda yeye akataka kuwa mhubiri wa Ufalme mwenye kujifuatanisha na kundi la Mashahidi wa Yehova.
8, 9. (a) Ni jambo gani linalopasa kufanywa wakati mwanafunzi wa Biblia anapotaka kushiriki katika huduma ya peupe? (b) Wakati wazee wawili wanapokutana pamoja na anayetazamiwa kuwa mhubiri na mwalimu wake, wao watafanya nini? (c) Mhubiri mpya anakuwa akijitwalia daraka gani?
8 Wakati Shahidi anayeongoza funzo la Biblia anapopata kwamba mwanafunzi huyo anatamani kushiriki katika utumishi wa shambani, yeye anaweza kuzungumzia jambo hilo pamoja na mwangalizi-msimamizi, ambaye atapanga wazee wawili wakutane pamoja na yule mwanafunzi wa Biblia na mwalimu wake. Wazee wanafurahi wakati mpya anapotaka kutumikia Mungu. Wao hawatatarajia kwamba awe na kipimo cha maarifa kilicho na wale waliobatizwa wakasonga mbele zaidi katika ukweli, ambao mengi zaidi yanatakwa kwao. Na bado, wazee watataka kuona kwamba kabla mpya yule hajashiriki katika huduma ya shambani pamoja na kundi, yeye ana maarifa ya kadiri fulani juu ya mafundisho ya Biblia na amepatanisha maisha yake na kanuni za Mungu. Hivyo kuna sababu njema za wazee wawili kukutana na yule anayetazamiwa kuwa mhubiri pamoja na Shahidi anayeongoza funzo hilo.a
9 Wazee wawili hao watajulisha mwanafunzi yule kwamba wakati astahilipo kwa ajili ya utumishi wa shambani na kuushiriki, angeweza kutoa ripoti ya utumishi wa shambani na kadi ya Maandishi ya Mhubiri wa Kundi itatayarishwa ikiwa na jina lake. Hiyo itaonyesha ukamatano wake kwa tengenezo la kitheokrasi la Mashahidi wa Yehova na ujitiisho wake kwalo. (Ingekuwa hivyo pia kuhusu wengine wote wanaotoa ripoti za utumishi wa shambani.) Zungumzio hilo linapasa pia kuhusisha ndani mashauri ya Biblia, kama yale yaliyopangwa katika kurasa 98 na 99 za Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu.b Kwa sababu hiyo, huo ungekuwa wakati unaofaa mwanafunzi ajipatie nakala ya kibinafsi ya kitabu hicho.
10. (a) Ni jinsi gani mhubiri asiyebatizwa anavyoweza kuzidi kufanya maendeleo, na akiwa na mradi gani? (b) Kwa nini rekebisho linafanywa sasa kuhusu ule mtajo wa “mshiriki anayekubaliwa”? (Ona elezo la chini.)
10 Mtu ambaye amestahili kuwa mhubiri asiyebatizwa wa habari njema amejongea kuelekea upande wa kuwa ‘mtu mwenye nia njema.’c (Luka 2:14, NW) Ingawa yeye si aliyejiweka wakfu na kubatizwa, sasa anaweza kuripoti utendaji wake pamoja na mamilioni ya watendaji wa duniani pote ambao ‘wanalihubiri neno la Mungu.’ (Matendo 13:5; 17:3; 26:22, 23) Kundi linaweza kufanyiwa tangazo la kwamba yeye ni mhubiri mpya asiyebatizwa. Inampasa yeye aendelee kujifunza Biblia, kushiriki katika mikutano, kutumia mambo anayojifunza, na kushiriki mambo hayo pamoja na wengine. Muda si muda, yeye atataka kuchukua hatua ya ubatizo wa Kikristo, hivyo akiwa mwenye kukubaliwa na Mungu na ‘kutiwa alama’ ya wokovu.—Ezekieli 9:4-6.
Msaada kwa Mmoja Anayefanya Kosa
11. Kundi linashughulika jinsi gani pamoja na wakosaji wasiobatizwa?
11 Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia maandalizi ya kundi ya kusaidia Mkristo yeyote aliyebatizwa ambaye anafanya dhambi nzito. (Waebrania 12:9-13) Na tuliona kutokana na Biblia kwamba ikiwa mtenda kosa aliyebatizwa haonyeshi toba, huenda kundi likahitaji kumwondosha nje na baada ya hapo liepuke ushirika wowote pamoja naye. (1 Wakorintho 5:11-13; 2 Yohana 9-11; 2 Wathesalonike 2:11, 12) Ingawa hivyo, ni hatua gani zinazoweza kuchukuliwa ikiwa mhubiri asiyebatizwa anafanya kosa au dhambi kwa uzito?
12. (a) Kwa nini msaada wenye rehema unapatikana pia kwa wahubiri wasiobatizwa ambao wanatenda dhambi? (b) Ni jinsi gani kanuni iliyo kwenye Luka 12:48 inavyohusiana na kupasishwa wajibu kwa kutenda kosa?
12 Yuda alihimiza kwamba rehema ionyeshwe kwa Wakristo wapakwa mafuta waliokuwa wamekuza mashaka, au wakawa wametumbukia ndani ya dhambi za mnofu, maadamu walikuwa wenye kutubu. (Yuda 22, 23; ona pia 2 Wakorintho 7:10.) Basi, je! haingefaa hata zaidi rehema ionyeshwe kwa mtu asiyebatizwa mwenye kukosa ambaye anaonyesha toba? (Matendo 3:19) Ndiyo, kwa maana msingi wake wa kiroho si imara kadiri hiyo, na ujuzi wake katika maisha ya Kikristo ni kidogo zaidi. Huenda ikawa yeye hakujifunza jinsi Mungu anavyofikiri juu ya mambo fulani. Yeye hajapitia ule mfululizo wa mazungumzio ya Biblia yanayofanywa pamoja na wazee kabla ya ubatizo, na hajajiweka chini ya ile hatua nzito ya uzamisho katika maji. Waaidha, Yesu alisema kwamba “kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi.” (Luka 12:48) Kwa hiyo, mengi yanatarajiwa kwa watu waliobatizwa ambao, pamoja na kuwa wenye maarifa na baraka zilizoongezeka, wanapasishwa wajibu wa pekee.—Yakobo 4:17; Luka 15:1-7; 1 Wakorintho 13:11.
13. Mhubiri asiyebatizwa akifanya kosa, wazee watafanya nini ili kusaidia?
13 Kwa upatano na ushauri wa Paulo, ndugu wenye sifa za kuwastahilisha kiroho wanataka kusaidia mhubiri yeyote asiyebatizwa ambaye anachukua hatua bandia kabla ya kuwa na habari. (Linganisha Wagalatia 6:1.) Wazee wangeweza kuomba wawili kati yao (labda wale waliokutana naye mapema kidogo) wajaribu kumrekebisha upya ikiwa yeye anataka kusaidiwa. Wangefanya hivyo, si kwa tamaa ya kukaripia kwa ukali, bali kwa njia ya rehema na katika roho ya upole. (Zaburi 130:3) Katika visa vilivyo vingi, himizo la Kimaandiko na madokezo yenye mafaa yatatosha kutokeza toba na kumweka kwenye kijia kinachofaa.
14, 15. (a) Ni jambo gani lingeweza kufanywa ikiwa mtenda kosa ana toba halisi? (b) Ni elezo gani lisilo na maneno mengi la kuelewesha wazi ambalo lingeweza kufanywa katika visa fulani?
14 Wazee wawili hao wataandaa mielekezo inayofaa hali ya mtenda kosa huyo asiyebatizwa. Katika visa fulani, wangeweza kupanga kwamba kwa muda fulani mkosaji asiwe katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au asiruhusiwe kutoa maelezo mikutanoni. Au wangeweza kumwagiza asishiriki katika huduma ya peupe pamoja na kundi mpaka atakapokuwa amefanya maendeleo zaidi ya kiroho. Halafu wanaweza kumwambia kwamba angeweza kushiriki tena katika huduma ya shambani. Ikiwa kosa lenyewe halikuleta sifa mbaya yenye kujulikana sana na halikutokeza hatari kwa usafi wa kundi la kondoo, haihitajiwi kabisa kutia kundi chonjo kwa tangazo lolote.
15 Ingawa hivyo, namna gani ikiwa wazee wawili wale wanapata kwamba mtu huyo ana toba halisi, lakini kosa lile linajulikana kwa mapana? Au namna gani ikiwa kosa hilo linakuja baadaye kujulikana kwa mapana? Katika chochote cha visa hivyo, wao wanaweza kuarifu Halmashauri ya Utumishi ya Kundi, ambayo itapanga kuwe na tangazo jepesi, kama ifuatavyo: “Jambo linalohusu . . . limekwisha kushughulikiwa, na yeye anaendelea kutumikia akiwa mhubiri asiyebatizwa pamoja na kundi.” Kama ilivyo katika mambo yote ya jinsi hiyo, baraza la wazee linaweza kuamua kama ingeshaurika wakati fulani wa baadaye kutoa hotuba ya Kimaandiko pamoja na mashauri juu ya namna ya kosa lililohusika.
16, 17. (a) Ni hali gani mbili zingeweza kuwa msingi wa tangazo tofauti? (b) Tangazo hilo linakuwa la jinsi gani?
16 Pindi kwa pindi, mhubiri asiyebatizwa aliye mkosaji hataitikia usaidizi wenye upendo. Au mhubiri asiyebatizwa huenda akaamua kwamba hataki kuzidi kufanya maendeleo kuelekea ubatizo, na anaarifu wazee kwamba yeye hataki kutambuliwa kuwa mhubiri. Jambo gani lifanywe? Kitendo cha kutenga na ushirika hakichukuliwi kuhusu watu kama hao ambao kwa kweli hawajawa wenye kukubaliwa na Mungu. Mpango wa kutenga na ushirika wakosaji wasiotubu unatumika kwa wale ‘wanaoitwa ndugu,’ kwa waliobatizwa. (1 Wakorintho 5:11) Ingawa hivyo, je! hiyo inamaanisha kwamba kosa hilo linapuuzwa tu? Sivyo.
17 Wazee wana daraka la ‘kuchunga kundi la Mungu lililo katika uangalizi wao.’ (1 Petro 5:2, NW) Ikiwa wazee wawili wanaotoa msaada wanapata kwamba mkosaji asiyebatizwa hana toba na hastahili kuwa mhubiri, wao wataarifu mtu huyo.d Au ikiwa mtu fulani asiyebatizwa anaambia wazee kwamba hataki tena kutambuliwa kuwa mhubiri, wao watakubali uamuzi huo. Katika chochote cha visa hivyo, inafaa Halmashauri ya Utumishi ya Kundi kupanga tangazo jepesi lifanywe wakati unaofaa, likisema “. . . si mhubiri wa habari njema tena.”
18. (a) Baada ya tangazo hilo, Wakristo watazingatia nini akilini katika kujiamulia kibinafsi jinsi ya kutenda? (b) Je! inahitajiwa kabisa kuwaepuka kabisa watu wasiobatizwa waliokuwa na hatia ya kosa wakati uliopita?
18 Baada ya hapo Mashahidi watakuwa na rai gani juu ya mtu huyo? Basi, mapema kidogo yeye alikuwa mtu ‘asiyeitikadi’ mwenye kuhudhuria mikutano. Wakati huo yeye alitaka na pia alistahili kuwa mhubiri wa habari njema. Hivyo sivyo ilivyo tena, kwa hiyo kwa mara nyingine yeye ni mlimwengu. Biblia haitoi takwa la kwamba Mashahidi waepuke kunena pamoja naye, kwa maana yeye si aliyetengwa na ushirika.e Na bado, Wakristo watatumia hadhari kuhusu mlimwengu wa jinsi hiyo ambaye haabudu Yehova, hata kama vile Waisraeli walivyofanya kuhusu walowezi wa kigeni wasiotahiriwa. Hadhari hiyo inasaidia kuhami kundi lisipatwe na “chachu kidogo” yoyote, au kitia-ufisadi. (1 Wakorintho 5:6) Ikiwa wakati fulani wa baadaye yeye anaonyesha tamaa halisi kwamba funzo la Biblia lifanywe pamoja naye, na linaonekana kuwa jambo lenye kufaa kwa wazee, labda hilo litamsaidia aje kuthamini tena jinsi lilivyo pendeleo kuabudu Yehova pamoja na watu Wake.—Zaburi 100.
19. Ni jinsi gani wazee wanavyoweza kuandaa kwa faragha msaada zaidi katika visa fulani?
19 Ikiwa wazee wanaona kwamba mtu fulani wa namna hiyo ni tisho kubwa isivyo kawaida kwa kundi la kondoo, wanaweza kwa faragha kuonya wale wenye kuhatarishwa. Mathalani, huyo aliyekuwa mhubiri huenda akawa ni kijana ambaye amejiachilia katika ulevi au ukosefu wa adili. Kujapokuwa na tangazo la kwamba yeye si tena mhubiri asiyebatizwa, huenda akajaribu kufanya starehe za kirafiki pamoja na vijana katika kundi. Katika hali hiyo, wazee wangenena kwa faragha kwa wazazi wa wale wenye kuhatarishwa, na labda kwa vijana hao pia. (Waebrania 12:15, 16; Matendo 20:28-30) Katika kisa kisichotukia mara nyingi cha mtu mwenye kuvuruga-vuruga mipango au aliye na fujo hatari zenye jeuri, yeye anaweza kuambiwa kwamba hakaribishwi mikutanoni na kwamba jaribio lolote la kuingia humo litachukuliwa kuwa ni mkanyago wa mahali pasipompasa.
Kusaidia Watoto Waabudu Mungu
20. Wazazi Wakristo wanaandalia watoto wao msaada gani, na kwa tokeo gani?
20 Biblia inawapa wazazi daraka la kuagiza watoto wao katika njia ya ukweli wa kimungu. (Kumbukumbu 6:4-9; 31:12, 13) Hivyo, kwa muda mrefu Mashahidi wa Yehova wamezitia moyo jamaa za Kikristo ziwe na funzo la Biblia la kila juma. Wazazi Wakristo wanapaswa kuwatia moyo wadogo-wadogo wao kufanya maendeleo kuelekea wakfu na ubatizo na hivyo wapate kibali cha Mungu. (Mithali 4:1-7) Tunaona katika makundi tokeo la kufurahisha sana kutokana na jambo hilo—mamia ya maelfu ya vijana walio kielelezo ambao wanapenda Yehova na kutaka kumwabudu milele.
21-23. (a) Kwanza hasa, kosa la mtoto mdogo hushughulikiwa jinsi gani? (b) Ni fungu gani ambalo wazee wa kundi wanatimiza katika hali kama hizo?
21 Wazazi Wakristo ndio wenye daraka la kwanza kuwatia nidhamu na kuwakaripia watoto wao, kuweka vizuizi vyovyote au adhabu zenye upendo ambazo wanaona zinahitajiwa kabisa. (Waefeso 6:4; Waebrania 12:8, 9; Mithali 3:11, 12; 22:15) Ingawa hivyo, ikiwa mtoto mdogo ambaye amekuwa katika ushirika akiwa mhubiri asiyebatizwa anakuja kuhusika katika kosa zito, jambo hilo ni la kuhangaikiwa na wazee ‘wanaolinda nafsi’ za kundi la kondoo.—Waebrania 13:17, NW.
22 Kwa msingi, kosa hilo linapasa kushughulikiwa kama ilivyopangiliwa mapema kidogo katika makala hii. Wazee wawili wanaweza kugawiwa kuchunguza jambo hilo. Mathalani, wao wanaweza kwanza kuzungumza pamoja na wazazi (au mzazi) ni jambo gani lililotukia, mwelekeo wa mtoto ni nini, na ni hatua gani za usahihisho zimechukuliwa. (Linganisha Kumbukumbu 21:18-21.) Ikiwa wazazi Wakristo wameweza kuchunga vizuri hali ile, wazee wanaweza kuwa wakiwauliza-uliza mara kwa mara tu kama wanaweza kutoa mashauri yenye msaada, madokezo, na kitia-moyo chenye upendo.
23 Ingawa hivyo, nyakati fulani zungumzo pamoja na wazazi huonyesha kwamba ingekuwa vizuri zaidi wazee wakutane pamoja na mtoto mwenye kupotoka na wazazi wake. Kwa kuzingatia akilini mapungukiwa na mibetuko ya vijana, waangalizi watajitahidi kumwagiza kwa upole mhubiri mchanga asiyebatizwa. (2 Timotheo 2:22-26) Katika visa fulani, huenda ikawa wazi kwamba yeye hastahili tena kuwa mhubiri na kwamba tangazo linalofaa linapasa kufanywa.
24. (a) Hata ikiwa mtoto ameshiriki katika kosa zito, inafaa wazazi wafanye jambo gani, na wangeweza kufanya hivyo jinsi gani? (b) Hiyo ingetumika jinsi gani kwa mtoto ambaye ametengwa na ushirika?
24 Baada ya hapo, wazazi wangefanya nini kwa ajili ya mtoto wao mdogo mwenye kukosa? Bado wao ndio wenye daraka kwa mtoto wao, ingawa ameonwa kuwa asiyestahili kuwa mhubiri asiyebatizwa au hata ikiwa ametengwa na ushirika kwa sababu ya kufanya kosa baada ya ubatizo. Sawa na vile ambavyo wao wataendelea kumwandalia chakula, nguo, na makao, wao wanahitaji kumwagiza na kumtia nidhamu kupatana na Neno la Mungu. (Mithali 6:20-22; 29:17) Hivyo wazazi wenye upendo wangeweza kupanga kuwa na funzo la Biblia la kimaskani pamoja naye, hata ikiwa ametengwa na ushirika.f Labda atapata manufaa iliyo na usahihisho mkubwa zaidi kutokana na kujifunza kwao pamoja naye akiwa peke yake. Au wangeweza kuamua kwamba yeye anaweza kuendelea kushiriki katika mpango wa funzo la jamaa. Ingawa yeye ametoka kwenye njia inayofaa, wao wanataka kumwona akirudia Yehova, kama alivyofanya mwana mpotevu katika kielezi cha Yesu.—Luka 15:11-24.
25. Kwa nini upendezi na msaada wenye upendo unaelekezwa kwa ‘wasioitikadi’ leo?
25 Mradi wa kuhubiri na kufundisha kwetu ni kusaidia wengine wawe waabudu wenye furaha wa Mungu wa kweli. ‘Wasioitikadi na watu wa kikawaida’ katika Korintho walisukumwa na moyo ‘kuanguka juu ya uso wao na kuabudu Mungu, wakitangaza hivi: “Mungu yupo pamoja na nyinyi kweli kweli.”’ (1 Wakorintho 14:25, NW) Ni shangwe iliyoje leo kuona watu wengi zaidi na zaidi wakija kuabudu Mungu! Huo ni utimizo mtukufu wa lile tamko rasmi walilofanya malaika: “Atukuzwe Mungu juu mbinguni, na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia [au, watu wenye nia njema].”—Luka 2:14.
[Maelezo ya Chini]
a Mmoja wa wazee hao anapaswa kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Utumishi ya Kundi. Yule mwingine angeweza kuwa mzee anayefahamiana zaidi na mwanafunzi au mwalimu wake, kama vile Kiongozi wa Funzo la Kitabu.
b Kilichotangazwa na Sosaiti ya Mnara wa Mlinzi Biblia na Trakti ya New York, 1983.
c Wakati uliotangulia, mtu asiyebatizwa aliyestahili kushiriki katika huduma ya shambani alitajwa kuwa “mshiriki anayekubaliwa.” Hata hivyo, “mhubiri asiyebatizwa” ni mtajo sahihi zaidi, hasa kwa sababu ya wonyesho wa Biblia kwamba kibali cha Mungu hutokana na wakfu halali na ubatizo wa Kikristo.
d Ikiwa mtu yule hatosheki na neno hilo lililokatwa, angeweza kuomba (katika muda usiozidi siku saba) kwamba jambo hilo lipitiwe upya.
e Wakati uliotangulia, watu wasiobatizwa waliotenda dhambi bila kutubu waliepukwa kabisa. Ingawa, kama ilivyorekebishwa hapo juu, haitakiwi iwe hivyo, shauri lililo kwenye 1 Wakorintho 15:33 lingali linapasa kufuatwa.
f Watu wa ukoo waliotengwa na ushirika ambao wanaishi nje ya maskani ile wanapaswa kushughulikiwa kulingana na mashauri ya Kimaandiko yaliyo katika Mnara wa Mlinzi wa Aprili 15, 1988, kurasa 26-31; Januari 1, 1982, kurasa 18-24.
Wewe Unakumbuka?
◻ Ni nini rai ya Wakristo kuelekea ‘wasioitikadi’ wanaohudhuria mikutano?
◻ Wakati mwanafunzi wa Biblia anapotaka kushiriki katika utumishi wa shambani, ni hatua gani ambazo wazee wanafuata, na ni daraka gani ambalo mwanafunzi anakubali?
◻ Ni jambo gani linalofanywa ikiwa mhubiri asiyebatizwa anafanya dhambi nzito?
◻ Ni jinsi gani wazazi na wazee wanavyoweza kusaidia watoto wadogo wanaoishi kwenye maskani yao, hata ikiwa vijana hao wanakosa kwa uzito?
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kuwa mhubiri, ingawa asiyebatizwa bado, ni hatua ya maana na yenye daraka kuelekea kupata kibali cha Mungu