Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w94 8/1 kur. 27-30
  • Kuonyesha Upendo wa Kikristo kwa Wazee-Wazee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuonyesha Upendo wa Kikristo kwa Wazee-Wazee
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • “Ghala za Ujuzi”
  • ‘Kujizoeza Ujitoaji Kimungu’
  • Uangalifu wa Kawaida kwa Mahitaji ya Kiroho
  • Jambo Ambalo Kutaniko Laweza Kufanya
  • ‘Wazee, Wakashiba Siku’
  • Familia ya Kikristo Huwasaidia Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • ‘Kuendelea Kuangalia’ Masilahi za Watu Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Ni Daraka la Kikristo Kuwatunza Walio Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Jinsi Wakristo Wanavyoweza Kuwasaidia Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
w94 8/1 kur. 27-30

Kuonyesha Upendo wa Kikristo kwa Wazee-Wazee

SAMUEL JOHNSON, mtunga-vitabu wa karne ya 18, alisimulia hadithi ya kijana mmoja aliyesahau alikoweka kofia yake alipotembelea marafiki wake. Tukio hilo halikutokeza jambo lolote. “Lakini ukosefu wa uangalifu kama huo ukionekana kwa mtu mzee-mzee,” Johnson aliendelea kusema, “watu watainua mabega na kusema, ‘Anapoteza kumbukumbu lake.’”

Hadithi ya Johnson yaonyesha kwamba wazee-wazee, labda kama vikundi vingine vinavyodharauliwa, huonwa kwa njia isiyo ya haki. Ingawa kutunza mahitaji ya walio wazee-wazee ni jambo gumu, wote wanaohusika hupata manufaa. Ni yapi baadhi ya magumu na thawabu, na kwa nini habari hii inaathiri watu wengi zaidi na zaidi?

Kulingana na tarakimu, asilimia 6 ya idadi ya watu ulimwenguni wana umri wa miaka 65 au zaidi, na katika nchi zilizoendelea asilimia hiyo ni kubwa mara mbili. Katika nchi za Jumuiya ya Ulaya, iliyotangaza 1993 kuwa “Mwaka wa Ulaya wa Wazee-Wazee na Umoja Kati ya Vizazi,” mtu 1 kwa 3 ana umri unaozidi miaka 50. Huko, kama ilivyo na nchi nyingine zilizoendelea kibiashara, kiwango kinachoshuka cha wanaozaliwa na kuongezeka kwa tarajio la maisha kwafanya idadi kubwa zaidi ya watu wawe wenye umri wa kupita makamo. Kwa wazi ni jambo gumu sana kuwatunza wale ambao wana umri mkubwa kwa hali kama hizo. Mambo yalikuwa tofauti kama nini wakati wa zamani katika sehemu ya Mashariki!

“Ghala za Ujuzi”

Kitabu Handwörterbuch des Biblischen Altertums für gebildete Bibelleser (Kitabu cha Mambo ya Kale ya Biblia Kwa Ajili ya Wasomaji Wenye Elimu ya Biblia) chasema kwamba katika mambo ya kale ya sehemu ya Mashariki “wazee-wazee walionwa kuwa wahifadhi wa adili za kitamaduni za hekima na ujuzi wa juu zaidi, jambo lililofanya vijana wahimizwe kutafuta kukaa nao na kujifunza kutoka kwao.” Kamusi Smith’s Bible Dictionary yaeleza: “Katika maisha ya faragha [walio wazee-wazee] walionwa kuwa ghala za ujuzi . . . [Vijana] waliwaruhusu watoe maoni yao kwanza.”

Staha kwa wazee-wazee ilionyeshwa kwa Sheria ya Musa kwenye Mambo ya Walawi 19:32: “Mwondokeeni mtu mwenye mvi; heshimuni uso wa mtu mzee.” Kwa hiyo wazee-wazee walikuwa na cheo cha pendeleo katika jumuiya nao walionwa kuwa watu wenye thamani kubwa. Bila shaka hivyo ndivyo Ruthu Mmoabu alivyomwona mama-mkwe wake Mwisraeli, Naomi.

Ruthu aliamua kwa uthabiti kuandamana na Naomi kutoka Moabu kwenda Israeli, na baadaye akasikiliza shauri la Naomi kwa uangalifu. Walipofika Bethlehemu, ni Naomi aliyeona kwamba mkono wa Yehova ulikuwa ukiongoza mambo naye akamfundisha Ruthu namna ya kujiendesha kitabia. (Ruthu 2:20; 3:3, 4, 18) Maisha ya Ruthu yalifanyizwa kwa njia ya kitheokrasi alipokuwa akijifunza kwa Naomi mwenye ujuzi wa siku nyingi. Mama-mkwe wake alithibitika kuwa ghala ya ujuzi.

Kwa njia iyo hiyo, wanawake Wakristo walio wachanga leo waweza kunufaika kwa kushirikiana na wanawake wenye umri mkubwa katika kutaniko. Labda dada afikiria ndoa au anapambana na tatizo la binafsi linalomsumbua. Ni jambo la hekima kama nini kutafuta shauri na utegemezo wa dada mzee-mzee aliye na ujuzi wa siku nyingi kwa jambo hilo!

Na zaidi, baraza la wazee laweza kunufaika kwa kutwaa ujuzi wa wazee-wazee walio kati yao. Twaweza kujifunza na hali ya Loti ya kushindwa kufanya hivyo. Ugomvi uliohusisha wachungaji wa mifugo ya Abrahamu na Loti ulihitaji uamuzi ambao ungeathiri kila mmoja. Loti alifanya uchaguzi usio wa hekima. Ingalikuwa afadhali kama nini kama angaliuliza shauri la Abrahamu kwanza! Loti angepokea mwongozo mkomavu naye angaliepusha familia yake isipatwe na huzuni iliyotokea kwa sababu ya uchaguzi wake wa haraka-haraka. (Mwanzo 13:7-13; 14:12; 19:4, 5, 9, 26, 29) Je! wewe husikiliza kwa uangalifu wasemayo wazee wakomavu kabla ufikie uamuzi wako kwa suala fulani?

Wazee-wazee wengi sana wana bidii ya kudumu ya kazi ya Yehova, kama walivyokuwa Simeoni na Ana katika karne ya kwanza. (Luka 2:25, 36, 37) Kuhusisha wazee-wazee kama hao katika utendaji mbalimbali wa kutaniko kadiri nguvu zao ziruhusuvyo, hata wakiwa wazee zaidi kwa umri, ni ishara ya kuwastahi na ni wonyesho wa mtazamo wa kuwatunza. Labda kijana anahitaji msaada wa kutayarisha mgawo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mzee mwenye akili aweza kuamua kwamba mshauri afaaye ni mshiriki wa kutaniko aliye mzee-mzee, yule mwenye hekima nyingi, tabia ya upole, na aliye na wakati mwingi.

Hata hivyo, kutunza mahitaji ya pekee ya wazee-wazee yahusisha mengi zaidi. Wengi hufadhaishwa na upweke, hofu ya uhalifu, na magumu ya kifedha. Isitoshe, mara mtu mzee-mzee awapo mdhaifu kimwili, matatizo hayo huongezwa na afya mbaya na kutamauka kwa sababu ya nguvu zao zinazokwisha. Basi hapo wahitaji uangalifu wa karibu zaidi. Watu mmoja-mmoja na kutaniko zima lapaswa kuitikiaje?

‘Kujizoeza Ujitoaji Kimungu’

Katika karne ya kwanza, Paulo aliandika hivi akiwa chini ya pumzi ya Mungu kwenye 1 Timotheo 5:4, 16, NW: “Lakini ikiwa mjane yeyote ana watoto au wajukuu, acha hawa wajifunze kwanza kuzoea ujitoaji kimungu kwa watu wa nyumbani mwao wenyewe na kufuliza kulipa wazazi na mababu wao malipo yapasayo, kwa maana hili ni lenye kukubalika mbele ya macho ya Mungu. Ikiwa mwanamke yeyote mwenye kuamini ana wajane, acha yeye awasaidie wao, na acha kutaniko lisiwe chini ya mzigo wenye kulemea. Ndipo laweza kusaidia wale ambao ni wajane kwelikweli.” Kuwatunza wazee-wazee kulikuwa daraka la familia. Ikiwa mshiriki mzee-mzee wa kutaniko alihitaji msaada baada ya familia yake kumfanyia yote iliyoweza, daraka lilikuwa la kutaniko. Kanuni hizo hazijabadilika.

Ni nini kimesaidia Wakristo waonyeshe upendo wa Kikristo kuelekea wazee-wazee kwa kujizoeza ujitoaji kimungu katika nyumba zao wenyewe? Ebu ona maelezo yafuatayo ya Mashahidi kadhaa ambao wana ujuzi wa kiasi fulani wa kuwatunza wazee-wazee.

Uangalifu wa Kawaida kwa Mahitaji ya Kiroho

“Kusoma andiko la siku pamoja kulisaidia sana,” akumbuka Felix, aliyemsaidia mke wake atunze wazazi wake. “Maono ya binafsi ya maishani na tamaa ya kutimiza wajibu ilichanganywa na kanuni za Yehova.” Hakika, katika kukabili ugumu wa kutunza watu wa ukoo walio wazee-wazee, jambo kuu ni kuangalia kwa uangalifu hali yao ya kujifunza kiroho. Hilo lapatana na akili kwa kufikiria maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:3, NW: “Wenye furaha ni wale wenye kufahamu uhitaji wao wa kiroho.” Andiko la siku laweza kuongezewa programu ya usomaji wa Biblia, kwa mazungumzo ya vichapo vyenye msingi wa Biblia, na kwa sala. “Yaonekana wazee-wazee hupenda ukawaida fulani ufuatwe wakati wote,” asema Peter.

Ndiyo, ukawaida fulani ni muhimu sana katika mambo ya kiroho. Wazee-wazee hawathamini ukawaida kwa mambo ya kiroho tu bali pia katika maisha ya kila siku. Hata wale wenye udhaifu mdogo-mdogo waweza kutiwa moyo kwa uchangamfu “kuamka kitandani na kuvaa vizuri kila siku,” asema Ursula. Bila shaka, twataka kuepuka tusionekane kama tunawashurutisha wazee-wazee. Doris akiri kwamba jitihada zake zenye makusudi mazuri mara nyingi hazifaulu. “Nilifanya kila aina ya kosa. Siku moja nilimwuliza baba yangu abadili shati yake kila siku. Mama yangu akanikumbusha hivi: ‘Angali mume wangu!’”

Pindi moja wazee-wazee walikuwa vijana, lakini ni vigumu sana kwa vijana kujiweka katika hali za wazee. Lakini, huo ndio ufunguo wa kuelewa mahitaji yao ya pekee. Umri unaozidi kuongezeka hutokeza mfadhaiko. Gerhard aeleza: “Baba-mkwe wangu alikuwa akijikasirikia mwenyewe kwa sababu hangeweza kufanya kila kitu alichokuwa akifanya zamani. Kukubali hali hiyo kulimsononesha sana. Utu wake ukabadilika.”

Chini ya hali zinazobadilika, ni kawaida kuona wazee-wazee wakitokeza hasira za mfadhaiko kwa kuchambua wengine, hasa wale wanaowatunza. Ni rahisi kujua sababu. Upendo wao wenye uangalifu kwake wamkumbusha juu ya nguvu zake zinazokwisha. Unapaswa kuitikiaje kwa uchambuzi au lawama lisilofaa?

Kumbuka kwamba hisia hizo zisizofaa hazimaanishi kwamba Yehova aziona jitihada zako kwa njia iyo hiyo. Endelea kutenda mema, na udumishe dhamiri safi, hata ikiwa nyakati nyingine unaambiwa maneno yasiyofaa. (Linganisha 1 Petro 2:19.) Kutaniko la kwenu laweza kukutegemeza sana.

Jambo Ambalo Kutaniko Laweza Kufanya

Makutaniko mengi yana sababu nzuri ya kushukuru sana jitihada za wakati uliopita za ndugu na dada zetu walio wazee-wazee. Labda ni wao walioweka msingi wa kutaniko hilo, wakilijenga kutokea wahubiri wachache miongo ya miaka iliyopita. Kutaniko lingekuwa wapi bila utendaji wao wenye bidii wa wakati uliopita na, labda, utegemezo wa kifedha wa wakati huu?

Utunzaji zaidi unapohitajika kabisa kwa habari ya mhubiri mzee-mzee, si lazima watu wa ukoo wachukue daraka hilo peke yao. Wengine waweza kusaidia kwa kuwafanyia mambo fulani-fulani, kuwapikia, kuwafanyia usafi, kuwatembeza wazee-wazee, kuwapa usafiri wa kwenda kwa mikutano ya Kikristo, au kuzungumza naye tu katika Jumba la Ufalme. Wote waweza kujiunga pamoja, ingawa ubora wa kazi na ukawaida mzuri hupatikana zaidi jitihada ziuanganishwapo.

Wazee waweza kufikiria kufanya kazi kwa kupatana wanapopanga ziara za uchungaji. Baadhi ya makutaniko ni vielelezo vizuri kwa habari hiyo, wazee wakihakikisha kwamba ziara za kawaida za uchungaji zinafanywa kwa wazee-wazee na walio dhaifu kimwili, hata wale wanaotunzwa vizuri na familia zao. Lakini, yaonekana kwamba makutaniko mengine yapaswa kuwa macho zaidi kuona wajibu wao kuelekea wazee-wazee.

Ndugu mmoja mwaminifu, aliye katika miaka ya mwisho-mwisho ya 80, alikuwa akitunzwa na binti yake na mwana-mkwe wake, walioacha Betheli ili kumtunza. Lakini, ziara za washiriki wengine wa kutaniko bado zilikuwa za maana kwake. “Nilipokuwa nikizuru wagonjwa,” ndugu huyo akaomboleza, “nilikuwa nikisali pamoja nao. Lakini hakuna mtu aliyepata kusali pamoja nami.” Uangalifu wenye upendo wa watu wa ukoo hauondolei wazee wajibu wa ‘kulichunga kundi la Mungu lililo kwao.’ (1 Petro 5:2) Na tena, wale wanaotunza wazee-wazee huhitaji kujengwa na kutiwa moyo kuendelea na kazi yao nzuri.

‘Wazee, Wakashiba Siku’

Alexander von Humboldt, aliyekuwa mwanasayansi Mjerumani wa karne ya 19, alikuwa na umri mkubwa sana wakati mwanamke mmoja kijana alipomwuliza kama hakuona hali ya kuzeeka kuwa jambo la kuchosha. “Umesema kweli,” akajibu msomi huyo. “Lakini ndiyo njia ya pekee ya kuishi muda mrefu.” Ndugu na dada wengi vilevile leo huweka kielelezo kizuri cha kukubali magumu ya umri kwa ajili ya pendeleo la kuishi muda mrefu. Wao huonyesha mtazamo ulioonyeshwa na Abrahamu, Isaka, Daudi, na Ayubu, ambao walikuwa ‘wazee, wakashiba siku.’—Mwanzo 25:8; 35:29; 1 Mambo ya Nyakati 23:1; Ayubu 42:17.

Umri unaoendelea huleta magumu ya kukubali msaada kwa upole na ya kuonyesha shukrani kwa unyoofu. Hekima yaonyesha kwamba kila mmoja atambue mipaka ya nguvu zake. Lakini, hilo halimaanishi kwamba mtu anayezeeka hawezi kutenda. Maria amezidi sana umri wa miaka 90, lakini angali anahudhuria mikutano ya kutaniko na kutoa maelezo huko. Yeye anafanyaje? “Siwezi kusoma tena, lakini mimi husikiliza Mnara wa Mlinzi kwenye kaseti. Mimi husahau mambo mengi, lakini mara nyingi mimi huweza kutoa maelezo.” Kama Maria, kujishughulisha na mambo yenye kujenga husaidia mtu abaki akiwa mtendaji na adumishe utu wa Kikristo.

Chini ya Ufalme wa Mungu, hakutakuwa tena kuzeeka. Pindi hiyo wale waliokuwa wazee-wazee katika mfumo huu na labda hata walikufa watakuwa na kumbukumbu zuri ajabu la jinsi walivyotunzwa kwa uangalifu. Wazee-wazee kama hao wapatapo uhai na nguvu tena, kwa kweli watahisi upendo wenye kina sana kwa Yehova na shukrani za ndani kuelekea wale walioshikamana nao wakati wa majaribu yao katika mfumo huu wa kale.—Linganisha Luka 22:28.

Vipi juu ya wale wanaotunza wazee-wazee sasa? Upesi hivi karibuni, Ufalme uchukuapo mamlaka yote juu ya dunia, watatazama nyuma kwa shangwe na faraja kwamba hawakukiuka wajibu wao bali walijizoeza ujitoaji kimungu kwa kuonyesha upendo wa Kikristo kwa wazee-wazee.—1 Timotheo 5:4.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Wazee-Wazee Watathamini Ziara Zako

Waweza kutimiza mengi mazuri kwa kupanga ziara, labda kwa dakika 15, ya kumtembelea mzee-mzee mmoja baada ya utendaji wa kuhubiri. Lakini ni bora zisiwe ziara za kutukia tu, kama ono lifuatalo lionyeshavyo.

Brigitte na Hannelore walikuwa wakihubiri pamoja, wakizungumza na mtu fulani mzee-mzee mlangoni pake. Dada hao waliongea naye kwa dakika tano kabla ya kugundua kwamba yeye pia alikuwa Shahidi wa Yehova, mshiriki wa kutaniko lilelile. Ni aibu kama nini! Lakini ono hilo lilikwisha kwa hali nzuri. Hannelore alifanya mipango mara hiyo ya kumzuru ndugu huyo na kumsaidia ahudhurie mikutano ya kutaniko.

Je! wajua jina na mahali wanapoishi kila mhubiri aliye mzee-mzee katika eneo unalohubiri? Je! waweza kupanga kuzuru kifupi? Yelekea ziara hiyo itathaminiwa sana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki