Ustaafu-Mlango Ulio Wazi Kuelekea Utendaji wa Kitheokrasi?
USTAAFU—kwa walio wengi huo hufunga mlango wa kipindi kirefu cha mkazo na hali zenye kuudhi. Baada ya kufungiwa katika kawaida yenye kuchosha au ya wasiwasi, watu wengi hutazamia ustaafu uwafungulie mlango kuelekea kwenye miaka ya starehe na uhuru wa kibinafsi. Lakini, mara nyingi sana mlango huo huongoza kwenye uchovu na utepetevu. Tafrija na mambo ya kupisha wakati haziandai kwa vyovyote hali ya kujistahi ambayo kufanya kazi huandaa.
Kwa Mashahidi wa Yehova, ustaafu waweza kufungua “mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.” (1 Wakorintho 16:9, NW) Ingawa umri unaoongezeka una matatizo na vizuizi vyao, watu fulani wenye umri mkubwa wamegundua kwamba kwa msaada wa Yehova wao waweza kuongeza utumishi wao kwake. Fikiria mambo yaliyoonwa na Wakristo fulani wenye umri mkubwa katika katika Uholanzi. Mwaka wa utumishi wa 1995, 269 wa wale mapainia (wapiga-mbiu wa Ufalme wa wakati wote) zaidi ya 1,223 walikuwa na umri wa miaka 50 au zaidi. Kati yao, 81 walikuwa na umri wa miaka 65 au zaidi.
Watu fulani wanaweza kupainia kwa kuendelea na ule mwendo wenye shughuli waliositawisha walipokuwa wakifanya kazi za kimwili. (Linganisha Wafilipi 3:16.) Mkristo mmoja mstaafu aitwaye Karel akumbuka: “Nilipokuwa nikifanya kazi kwenye kazi yangu ya kimwili, nilikuwa nikianza kazi saa 1:30 asubuhi. Nilipoanza kupata malipo yangu ya uzeeni, niliamua kudumisha kawaida hiyohiyo. Nilikuwa nikianza siku kwa kutoa ushahidi wa barabarani nikiwa na magazeti mbele ya kituo cha gari-moshi kila asubuhi saa moja kamili.”
Pia kupanga kwa uangalifu ni ufunguo wa mafanikio. (Mithali 21:5) Kwa kielelezo, watu fulani wameweza kuweka kando fedha za kujitegemeza wenyewe katika huduma yao. Wengine wameamua kupunguza gharama za kibinafsi na kupata kazi ya kuajiriwa isiyo ya wakati wote. Wafikirie Theodore na Ann. Walianza maisha ya ndoa wakiwa mapainia hadi wajibu mbalimbali wa familia ulipowalazimu kuacha kupainia. Lakini roho yao ya upainia iliendelea! Mabinti wao walipokuwa wakikua, walitiwa moyo daima kupainia. La maana hata zaidi, Theodore na Ann waliweka kielelezo chema, wakitumika mara nyingi wakiwa mapainia-wasaidizi. Hao wasichana walipozidi kukua, Theodore na Ann walianza kupunguza kazi ya kimwili ili wawe na wakati zaidi kwa ajili ya utumishi wa shambani.
Baada ya mabinti wao kuingia katika utumishi wa wakati wote na kuondoka nyumbani, Ann akaanza kupainia. Siku moja alimtia moyo Theodore aache kazi yake. “Sote wawili twaweza kupainia,” Ann akadokeza. Theodore akamjulisha mwajiri wake makusudio yake. Kwa mshangao wake tajiri wake alijitolea kusaidia kwa kumpa kazi isiyo ya wakati wote, akisema: “Naamini kwamba wataka kumfanyia kazi wakati wote tajiri wako wa huko juu [mbinguni].” Theodore na Ann sasa hufurahia kupainia pamoja.
Watu fulani walianza kupainia kufuatia hali zilizotokea maishani mwao. Vifo vyenye kuhuzunisha vya binti yao na mjukuu wao wa kike viliwafanya mume na mke fulani wenye umri mkubwa wafikirie kwa uzito jinsi walivyokuwa wakitumia miaka yao iliyosalia. (Mhubiri 7:2) Badala ya kushindwa na huzuni, walianza utumishi wa wakati wote, ambao kufikia sasa wameufurahia kwa zaidi ya miaka minane!
Yakubalika kwamba, kubaki katika huduma ya wakati wote hutaka azimio halisi. Kwa mfano, Ernst na mke wake, Riek, walianza kupainia mara tu watoto wao walipoondoka nyumbani. Muda mfupi baadaye aliyekuwa mfanyabiashara mwenzake hapo awali alimtolea Ernst kazi yenye faida kubwa. Ernst akajibu: “Sisi tuna mwajiri bora zaidi, nasi hatuko tayari kuacha kumtumikia!” Kwa kuwa Ernst na mke wake waliendelea katika “kazi ya kuajiriwa” ya Yehova, walifunguliwa mapendeleo mengine ya utumishi. Walitumikia katika kazi ya mzunguko kwa zaidi ya miaka 20 nao waendelea wakiwa mapainia hata leo. Je, wao wanajuta mwendo wao wa kujidhabihu? Wakati fulani uliopita mume na mke hao waliandika hivi: “Ikiwa ni mapenzi ya Yehova, baada ya miezi mitatu twatarajia kuadhimisha miaka yetu 50 ya ndoa, mwadhimisho uonwao kuwa wenye thamani sana. Lakini tukiwa na usadikisho kamili twasema kwamba miaka yetu yenye thamani kikweli ilianza tulipoanza kupainia.”
Watu wengi hugundua kwamba mlango uelekezao kwenye utendaji ulioongezeka huelekeza pia kwenye shangwe iliyoongezeka! Ndugu mmoja aliyeanza kupainia majuma mawili baada ya kufikia umri wa miaka 65 asema hivi: “Ni lazima niseme kwamba sijawahi kujionea kipindi kingine maishani mwangu kilichojawa sana na baraka kama hii miaka kumi iliyopita ya kupainia.” Mume na mke ambao wamepainia kwa zaidi ya miaka saba wasema hivi: “Mume na mke wa umri wetu na wenye hali zetu wapaswa kuwa wakifanya nini kingine? Mara nyingi sisi huona watu walio na hali sawa na zetu katika eneo—wakiwa wamestarehe nyumbani, wakinenepa tu, kuzeeka, na kukauka mwili. Utumishi hudumisha afya yetu ya kiakili na ya kimwili. Sisi tuko pamoja sikuzote. Sisi hucheka sana na kufurahia maisha.”
Bila shaka, si wote wenye umri mkubwa walio na hali zinazowaruhusu kupainia. Wakristo hao waweza kuhakikishiwa kwamba Yehova huthamini lolote wawezalo kufanya katika utumishi wake. (Linganisha Marko 12:41-44.) Kwa kielelezo, dada mmoja asiyejiweza amelazwa katika makao ya kutunzia wagonjwa. Hata hivyo, mlango wa utendaji ungali wazi kwa ajili yake! Daktari fulani alimuuliza jinsi atumiavyo wakati wake. Yeye asimulia hivi: “Nilimwambia kuwa sikuzote mimi huwa sina wakati wa kutosha. Hakuweza kuelewa hilo. Nilimwambia kuwa hilo ni kwa kuwa siku zangu zinajawa na utendaji mbalimbali wenye kuridhisha. Mimi si mpweke, lakini mimi hutafuta wengine walio wapweke na hujaribu kuwaambia yale ambayo Mungu amewawekea wanadamu kwa wakati ujao.” Yeye atoa muhtasari wa mambo hayo kwa kusema: “Mtu hawezi kutarajia mengi sana kutoka kwa mtu akaribiaye miaka 80. Salini kwa ajili yangu ili niweze bado kuwaongoza watu wengi kwa Yehova.”
Je, wewe umefikia umri wa kustaafu? Mlango kuelekea kwenye starehe huenda ukawa wenye kuvutia sana, lakini huo si mlango kuelekea kwenye baraka za kiroho. Fikiria hali zako kwa sala. Huenda ikawa kwamba waweza kuingia kupitia mlango kuelekea kwenye utendaji mwingi zaidi katika utumishi wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 25]
Ustaafu waweza kuongoza kwenye utendaji ulioongezeka katika huduma