Kustaafu—Je, Ni Mlango Uongozao Kwenye Utendaji Zaidi?
1 Watu wengi ambao hufanya kazi kwa bidii hutazamia wakati ambapo kustaafu kutawapumzisha kutokana na taabu na mahangaiko ya kazi ya kimwili. Hata hivyo, mara nyingi kustaafu hutokeza kutojali, uchovu, na kuzeeka mapema. Kukosa kazi yenye kusudi kwaweza kumfanya mtu awe na mahangaiko mengi. Gazeti moja la Brazili liliripoti kwamba wafanyakazi wa umma waliostaafu walilalamika kwamba walikuwa na matatizo kama vile ‘kutoridhika, kukasirika-kasirika, kukosa usalama, na kukosa kusudi maishani, kushuka moyo na kuhisi kwamba ulimwengu umeenda mrama.’
2 Kinyume chake, Wakristo wengi huona maisha hayo mapya kuwa mlango uongozao kwenye utendaji zaidi wa kiroho. Ndugu mmoja aliyeanza kupainia majuma mawili baada ya kufikia umri wa miaka 65 alisema hivi: “Sijawahi kamwe kuwa na baraka nyingi maishani mwangu kama zile ambazo nimepata katika miaka kumi ambayo nimekuwa nikifanya upainia.” Wenzi wa ndoa waliandika hivi: “Miaka yetu iliyo bora zaidi ilianza tulipoanza upainia.” Naam, kwa walio wengi, kustaafu huwapa fursa nzuri ya kupanua huduma yao na kupata baraka nyingi sana kutoka kwa Yehova.
3 Kuwa Mwenye Shughuli na Mwenye Matokeo: Walipokuwa wakikua, wengi ambao sasa wamestaafu hawakuwa na vifaa vya kisasa nao walijifunza kufanya kazi kwa bidii tangu mapema maishani. Ingawa huenda wasiwe na nguvu za ujana sasa, bado wao ni wafanyakazi wenye matokeo. Katika eneo la ofisi moja ya tawi, asilimia 22 ya mapainia, yaani, ndugu na dada wapatao 20,000, wana umri wa angalau miaka 60. Mapainia hao wazee huchangia sehemu kubwa ya kazi ya kuhubiri. Uzoefu wao na sifa zao za kimungu hutajirisha makutaniko wanayoshirikiana nayo.—Yak. 3:17, 18.
4 Kuwa na shughuli katika huduma ya Kikristo huchangia afya na maisha bora zaidi. Dada mwenye umri wa miaka 84 aliyeanza upainia alipostaafu alisema: “Kujifunza Biblia pamoja na watu wengi wanaopendezwa kumenisaidia kuwa na utimamu wa akili. Sina gari, kwa hiyo mimi hutembea sana. Hilo hunifanya niwe na afya nzuri.” Wenzi wa ndoa wazee walio mapainia walisema: “Utumishi hutufanya tuwe na afya nzuri ya akili na ya kimwili. Sikuzote sisi huwa pamoja. Sisi hucheka sana na kufurahia maisha.”
5 Kutumikia Mahali Penye Uhitaji: Wakristo fulani waliostaafu wenye hali nzuri ya kifedha, wamehama ili kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Wengine wamepanua huduma yao ili watumikie katika eneo la lugha ya kigeni. Kama mtume Paulo, wahubiri hao wenye bidii ‘hufanya mambo yote kwa ajili ya habari njema, ili wapate kuwa washiriki wayo pamoja na wengine.’—1 Kor. 9:23.
6 Wenzi fulani wa ndoa walianza kufanya upainia baada ya kulea wana wao wawili. Baada ya miaka kadhaa ya kufanya upainia, walianza kujifunza Kichina. Sasa wakiwa na umri wa zaidi ya miaka 70, hivi karibuni walishangilia kuona kikundi cha Kichina ambacho wamekuwa wakishirikiana nacho kikiwa kutaniko. Wenzi kama hao wamekuwa baraka kama nini!
7 Hakuna Kustaafu Kutoka Katika Huduma: Ingawa watu wengi hustaafu kutoka katika kazi zao za kimwili, Wakristo hawastaafu kutoka katika utumishi wa Mungu. Lazima wote waendelee kuwa waaminifu “hadi mwisho.” (Mt. 24:13, 14) Bila shaka, kadiri miaka inavyozidi kusonga, wengine hawawezi tena kutimiza mengi katika utumishi wa Yehova kama awali. Lakini ni jambo lenye kutia moyo kama nini kuwaona wakifanya yale wawezayo kwa moyo wao wote! Neno la Mungu huwahakikishia kwamba Yehova hatasahau kazi yao na upendo wanaoonyesha kwa ajili ya jina lake.—Luka 21:1-4; Ebr. 6:10.
8 Ikiwa unakaribia umri wa kustaafu, mbona usisali na kufikiria jinsi unavyoweza kutumia ifaavyo hali yako itakayobadilika? Kwa msaada wa Mungu, unaweza kuona kwamba kustaafu hukufungulia mlango uongozao kwenye utendaji zaidi ambao humsifu Yehova na kuleta baraka nyingi.—Zab. 148:12, 13.