Vijana—Miradi Yenu ya Kiroho Ni Ipi?
1 Yehova ajua jinsi kazi ifaayo na miradi iwezayo kufikiwa, ilivyo na maana katika kuleta furaha. (Ona Mwanzo 1:28; 2:15, 19.) Leo, Yehova amewapa watu wake mgawo wa kuhubiri na kufundisha. Pia tuna mradi wa mwisho wa kufikia uhai udumuo milele katika Paradiso. Kwa wakati uleule, twahitaji kuweka miradi ya kiroho yenye maendeleo ikiwa tutaepuka kuelekeza vibaya nishati na mali zetu.—1 Kor. 9:26.
2 Miradi Halisi kwa Vijana: Vijana wapaswa kuwa na miradi ya kitheokrasi ambayo yaweza kufikiwa kulingana na uwezo wao binafsi. (1 Tim. 4:15) Baadhi ya walio wachanga zaidi wamefikia miradi ya kukariri vitabu vya Biblia hata kabla ya kujua kusoma. Kupitia funzo la familia, watoto wanajifunza kutayarisha kwa ajili ya mikutano ili waweze kufikia miradi ya kutoa maelezo yafaayo na kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Watoto wanapoandamana na wazazi wao katika utumishi wa shambani, wanajifunza kuwa na sehemu ya kutoa ushahidi huku wakifanya maendeleo kuelekea mradi wa kuwa watangazaji wasiobatizwa. Wazazi wanapaswa kukazia watoto wao mradi wa wakfu na ubatizo.
3 Ikiwa wewe ni tineja, miradi yako ya kiroho yatia ndani nini? “Mkumbuke Muumba wako” kwa kukazia miradi iliyo ya maana sana maishani. (Mhu. 12:1; Zab. 71:17) Kwa nini usifanye upainia msaidizi wakati wa miezi ya likizo ya shule? Je, umepata kufikiria kuchukua huduma ya wakati wote ukiwa painia wa kawaida? Vipi kujifunza lugha mpya ili wakati ujao uweze kusaidia kikundi au kutaniko la lugha tofauti katika eneo lako au mahali penginepo? Wengi ambao sasa wanatumikia wakiwa Betheli au wakiwa waangalizi wasafirio au wamishonari waliweka miradi ya utumishi wa pekee wa wakati wote walipokuwa wangali shuleni. Kwa nini usifanye vivyo hivyo?
4 Maadamu ungali mwenye umri mchanga, jitahidi kuiga kielelezo cha Yesu. Hata akiwa mwenye umri mchanga wa miaka 12, alisema kwa utayari juu ya mambo ya kiroho. (Luka 2:42-49, 52) Kujiwekea miradi yenye manufaa ya kufanya funzo la kibinafsi, kusoma Biblia kila siku, na kushirikiana kwa ukawaida na Wakristo wakomavu kwenye mikutano na katika utumishi kutakusaidia ujipatie stadi za kufundisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu kwa njia ambayo Yesu alifanya.