Watangazaji wa Ufalme Waripoti
Ukamilifu Chini ya Marufuku
KWA miaka 11 kazi ya kuhubiri katika nchi moja ya Kiesia ya Kusini-mashariki imekuwa chini ya marufuku rasmi ya serikali. Hata hivyo, katika miaka ya majuzi akina ndugu wamekuwa na sababu ya kuitikadi kwamba watu fulani wenye madaraka katika serikali wangependa kutuliza hali hiyo. Inaonekana marufuku ilichochewa na uvutano imara wa dini za Jumuiya ya Wakristo katika sehemu za kiserikali.
Nyakati nyingine akina ndugu wamekuwa wakichunguliwa-chunguliwa, kukamatwa, na kuulizwa sana maswali. Wale wanaofanyia kazi taasisi za serikali wametishwa juu ya kushushwa cheo au juu ya kulazimishwa kustaafu kazi ikiwa hawatajiunga na chama cha kisiasa cha Nchi. Kikundi kimoja cha wahubiri kilipigwa vikali.
Mashahidi wamenyang’anywa pia haki za kisheria, kama vile utumishi unaotokana na mahakama za kiraia na haki ya kuendesha maziko. (Wenye mamlaka wanaweka rasmi kiongozi wa kidini ndiye afanye hivi.) Katika mahali fulani fulani, Mashahidi hata wananyimwa uandikishaji wa ndoa!
Hata hivyo, wenye kufanya uangalizi wa kazi huko wanaripoti hivi: “Nyakati zote, mahali ambako akina ndugu wanaelekeana na suala hilo kwa ujasiri, wakitoa ushuhuda kwa staha kutokana na Biblia, mwishowe maulizo-ulizo yale hukoma na kuchunguliwa-chunguliwa kunapungua, hiyo ikiwezesha akina ndugu kuendesha kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa matokeo mazuri.”—Mathayo 28:19, 20, NW.
Mathalani, dada mmoja mwenye kuulizwa-ulizwa maswali aliulizwa ni wapi sisi tunapata jina Yehova. Kwa ushujaa akafungua Biblia yake kwenye Kutoka 15:3, ambako jina hilo huonekana. Mwulizaji, ambaye ni amiri wa kijeshi, alifuatana naye katika kuangalia Biblia, akisema: “Ndiyo, kweli kweli. Limo katika Biblia.” Halafu, akigeukia kiongozi mmoja wa kidini aliyekuwa pia akishiriki katika kuuliza-uliza maswali, yeye akamwuliza: “Kwa nini ninyi hamwarifu watu juu ya jina hili?” Huyo kiongozi wa kidini alijibu hivi bila kujua la kusema: “Oh, ndiyo, jina hilo limo katika Agano la Kale. Lakini kwa sababu nchi hii haina mahusiano ya kibalozi pamoja na Israeli, sisi hatutumii jina hilo.” Dada aliachiliwa mara hiyo!
Kwa kutenda kulingana na kidokezo walichopata kutoka kwa mtu “mwenye kupendezwa,” polisi walifuta wa kwanza wa mikusanyiko mitatu ya wilaya usiku uliotangulia kuanza kwao! Hata hivyo, watu kadhaa wenye akili ya mwelekeo mzuri katika kani ya polisi walisaidia kukomesha maulizo-ulizo yaliyofuata. Bila kuogopa, akina ndugu wakafanya mikusanyiko ile mingine miwili.
Ijapokuwa upinzani wa kidini ni imara katika nchi hii, kungali kuna wale wanaopenda uadilifu. Mathalani, mwajiri-kazi mmoja alipokuwa amekwisha kuona ushikamanifu wa akina ndugu kwa kanuni zao na itikadi, amekuwa na itibari nyingi zaidi katika akina ndugu. Wao wanapewa madaraka zaidi kazini.
Mambo yanayofanana na hayo yanapata watoto wa shule. Walimu wenye mioyo ya kufuata haki wanavutiwa nao kwa sababu ya msimamo wao thabiti wanaouchukua kwa ajili ya itikadi yao.
Ingawa hali katika shamba imekuwa ikirahisika kidogo kwa akina ndugu, bado makanisa yanaendeleza usumbuaji wao na kujaribu kila njia inayowezekana ili yakomeshe kazi ya ushuhuda. Nyakati fulani yanajaribu kuwadhuru kimwili wale wanaojifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Hata hivyo, bado watu wenye kupendezwa wanamiminika makundi-makundi kuingia kwenye tengenezo la Yehova. Jambo moja lililoonwa ni lile la nyanya mmoja aliye katika umri wa miaka 70 na kitu. Baada ya moja la macho yake kufanyiwa upasuaji, yeye alieleza alitaka upainia msaidizi. Kwa sababu ya umri wake, kwanza yeye alihisi kwamba lile takwa la saa 60 lilikuwa kubwa mno kwake, lakini baada ya kujaribu, yeye akagundua angeweza kufaulu. Kwa uhakika, katika siku kumi za kwanza, aliingiza saa 38 katika utumishi wa shambani; akaangusha vitabu viwili, vijitabu vitatu, na magazeti mawili katika eneo gumu; na alianza mafunzo mawili ya Biblia. Yeye alikuwa mwenye furaha!
Kwa ujumla, hali ya utumishi wa shambani katika nchi ni nzuri sana. Hasa baada ya uchaguzi mkuu, akina ndugu wameweza kufuatia sehemu mbalimbali za kutoa ushuhuda. Hii imechocheleza kweli kweli mwendo wa ile kazi. Mhubiri mmoja wa kawaida anaweza kuwa na mafunzo saba mpaka kumi ya Biblia. Hapo kwanza, wenye nyumba walikuwa wauliziaji sana juu ya sisi ni akina nani, tulitoka wapi, na kadhalika. Sasa ni mara chache akina ndugu wanapolazimika kujulisha wao ni akina nani. Watu wana njaa ya chakula cha kiroho chenye kutosheleza. Shamba liko tayari kweli kweli kwa ajili ya mavuno.—Mathayo 9:37, 38.
Kweli kweli, akina ndugu katika nchi hii wameshika ukamilifu chini ya jaribu, hivi majuzi wakifurahia ongezeko la asilimia 7 katika wahubiri! Wao wanachukua msimamo ule ule ambao mtunga zaburi Daudi alichukua aliposema: “Kwa habari yangu mimi, katika ukamilifu wangu mimi nitatembea.”—Zaburi 26:11, NW.