Jinsi Ambavyo Washiriki wa Familia Hushirikiana Kikamili—Katika Funzo la Biblia
1 Kweli huongezea maana na kusudi halisi katika maisha ya familia, lakini mafanikio katika kumtumikia Yehova hayaji yenyewe tu. Huhitaji wakati na jitihada ili kujenga familia iliyo na nguvu kiroho. Kuna uhitaji mkubwa wa washiriki wa familia kushirikiana kwa ukaribu katika jitihada hii. Makala hii ya kwanza katika mfululizo wenye sehemu tatu itakazia jinsi familia zinavyoweza kushirikiana kusitawisha mazoea mazuri ya funzo.
2 Kwa Kusoma Biblia Kila Siku: Mithali 24:5 husema kwamba “mtu mwenye maarifa [“ujuzi,” NW] huongeza uwezo.” Ujuzi unaopatikana kutokana na kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida humpa mtu nguvu ya ndani inayohitajiwa kukinza mashambulizi ya Shetani kwa hali yake ya kiroho. (Zab. 1:1, 2) Je, nyinyi husoma Biblia pamoja mkiwa familia kila siku? Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inaorodhesha “Ratiba ya Kuongezea ya Usomaji wa Biblia” wa kila juma katika mwaka. Kuifuata hutaka dakika kumi hivi za familia kila siku. Chagueni wakati ufaao, kama vile wakati wa kiamsha-kinywa, baada ya mlo wa jioni, au kabla ya kwenda kulala, kusoma Biblia na kuchunguza andiko la siku kutoka katika Kuyachunguza Maandiko. Fanyeni hiyo iwe sehemu ya kawaida ya kila siku ya familia.
3 Kwa Kujifunza Pamoja Kila Juma: Funzo la Biblia la familia lapaswa kuwa jambo kuu la familia katika juma. Kila mshiriki apaswa kuliunga mkono kwa kushiriki kwa hamu katika funzo. Kichwa cha familia atataka kufikiria kwa uangalifu mahitaji ya familia anapoteua habari ya funzo na siku, wakati, na urefu wa funzo. Tanguliza funzo la familia katika ratiba ya juma. Usiruhusu mambo mengine yasiyo ya maana sana yaliingilie.—Flp. 1:10, 11.
4 Baba ambaye sikuzote alipata simu za shughuli za biashara nyumbani kwake alikuwa akiondoa kiunganisho cha simu wakati wa funzo la familia. Wateja walipokuja nyumbani kwake, walikaribishwa kujiunga na funzo au kungoja hadi limalizike. Baba huyo alikuwa ameamua kwamba hakuna chochote ambacho kingeingilia funzo la familia. Hilo lilikuwa na uvutano mkubwa sana kwa watoto wake, na kuhusu biashara yake, ilisitawi.
5 Inapendeza kama nini washiriki wa familia wanaposhirikiana katika shughuli za kiroho! Uaminifu katika jitihada zetu za kushiriki kikamili katika funzo la Biblia la familia utaleta baraka za Yehova.—Zab. 1:3.