Fanya Bidii ili Kuihifadhi Familia Yako Iingie Ndani ya Ulimwengu Mpya wa Mungu
“Wewe, BWANA [Yehova, NW], ndiwe utakayetuhifadhi, utatulinda na kizazi hiki milele.”—ZABURI 12:7.
1, 2. (a) Familia nyinginezo zinakabilianaje na mibano ya siku za mwisho? (b) Familia za Kikristo zenye nguvu zaweza kujitahidije ili kuokoka?
“LEO moyo wangu umejaa shangwe!” akapaaza sauti mzee mmoja Mkristo wa kundi aitwaye John. Sababu ya msisimuko wake ilikuwa nini? “Mwana wangu mwenye umri wa miaka 14 na binti yangu mwenye umri wa miaka 12 walibatizwa,” yeye asimulia. Lakini shangwe yake haikuishia hapo. “Mwana wangu mwenye umri wa miaka 17 na binti yangu mwenye umri wa miaka 16 wote wawili wamekuwa mapainia wasaidizi katika mwaka uliopita,” yeye aongeza.
2 Familia nyingi miongoni mwetu zina matokeo mazuri kama hayo zinapotumia kanuni za Biblia. Hata hivyo, baadhi yazo zinapatwa na matatizo. “Tuna watoto watano,” waandika wenzi wawili wa ndoa Wakristo, “na imeendelea kuwa vigumu kushughulika nao. Tayari tumempoteza mtoto mmoja kwa mfumo huu wa kale. Matineja wetu wachanga waonekana kuwa eneo hasa la shambulio la Shetani wakati huu.” Pia kuna wenzi wa ndoa walio na magomvi makali ya kindoa, nyakati nyingine yakitokeza mtengano au talaka. Hata hivyo, familia za Kikristo zenye nguvu zitaokoka “dhiki kubwa” na kuhifadhiwa kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja. (Mathayo 24:21; 2 Petro 3:13) Lakini, unaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba familia yako itahifadhiwa?
Kufanyia Maendeleo Mawasiliano
3, 4. (a) Mawasiliano yana maana gani katika maisha ya familia, na kwa nini matatizo yanayoyahusu hutokea mara nyingi? (b) Kwa nini waume wanapaswa wajitahidi kuwa wasikilizaji wazuri?
3 Mawasiliano mazuri ndiyo jambo linalodumisha afya njema ya familia; yanapokosekana, uvutano na mkazo huongezeka. “Pasipo mashauri makusudi hubatilika,” Mithali 15:22 husema. Kwa kupendeza, mshauri wa ndoa aripoti hivi: “Lalamiko la kawaida sana ninalosikia kutoka kwa wake ambao nimeshauri ni ‘Mume wangu haongei na mimi,’ na ‘Mume wangu hanisikilizi.’ Na mimi ninapowaambia waume zao lalamiko hilo, waume zao vilevile hawanisikii.”
4 Ni nini kinachosababisha ukosefu wa mawasiliano? Kwanza, wanaume na wanawake wako tofauti, na mara nyingi wana njia tofauti kabisa za kuwasiliana. Makala moja ilionyesha kwamba mume “huelekea kusema moja kwa moja na kwa njia yenye mafaa” katika mazungumzo yake, hali “lile ambalo [mke] ataka kuliko jambo jingine lolote ni msikilizaji mwenye hisia-mwenzi.” Ikiwa hilo hutokeza tatizo katika ndoa yako, jitahidi kufanya maendeleo. Mume Mkristo huenda akahitaji kujitahidi kuwa msikilizaji bora. “Kila mtu,” asema Yakobo, “na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema.” (Yakobo 1:19) Jifunze kuepukana na kuamuru-amuru, kuonya-onya, au kukemea-kemea wakati mke wako anapotaka tu kuonyeshwa “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8, NW) “Azuiaye maneno yake ni mwenye maarifa,” Mithali 17:27 husema.
5. Ni zipi baadhi ya njia ambazo waume wanaweza kufanya maendeleo katika kuonyesha mawazo na hisia zao?
5 Kwa upande ule mwingine, kuna “wakati wa kunena,” na huenda ukahitaji kujifunza kuwa mwenye kueleza mawazo na hisia zako vema zaidi. (Mhubiri 3:7) Kwa mfano, je, wewe ni mwenye ukarimu katika kumpongeza mke wako juu ya mambo ambayo ametimiza? (Mithali 31:28) Je! wewe huonyesha shukrani kwa ajili ya kazi ngumu anayofanya ya kukusaidia na kutunza nyumba? (Linganisha Wakolosai 3:15.) Au labda unahitaji kufanya maendeleo katika kutumia “maneno ya upenzi.” (Wimbo Ulio Bora 1:2, NW) Kufanya hivyo huenda kukaonekana mwanzoni kuwa jambo gumu lakini kwaweza kusaidia sana kumfanya mke wako ahisi usalama katika upendo wako kwake.
6. Wake wanaweza kufanya nini ili kufanyia maendeleo mawasiliano ya familia?
6 Namna gani wake Wakristo? Mke mmoja anukuliwa akisema kwamba mume wake ajua kwamba anamthamini, kwa hiyo si lazima amwambie. Hata hivyo, wanaume hufurahia wanapothaminiwa, kupongezwa, na kusifiwa. (Mithali 12:8) Je! unahitaji kujieleza zaidi juu ya mambo hayo? Kwa upande ule mwingine, labda unahitaji kuwa mwangalifu zaidi juu ya jinsi unavyosikiliza. Ikiwa mume wako huona kuwa vigumu kuzungumza matatizo, hofu, au mahangaiko yake waziwazi, je, umejifunza jinsi ya kumfanya awasiliane na wewe, kwa fadhili na kwa busara?
7. Ni mambo gani yanayoweza kusababisha magombano ya kindoa, nayo yaweza kuzuiwaje?
7 Bila shaka, hata wenzi wa ndoa ambao kwa kawaida hupatana vizuri huenda mara kwa mara wakapatwa na mvunjiko katika mawasiliano. Hisia-moyo huenda ikazuia kusababu kuzuri, au mazungumzo yenye upole huenda yakageuka upesi yakawa magombano makali. (Mithali 15:1) “Twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi”; hata hivyo, gombano la kindoa halimaanishi kwa vyovyote mwisho wa ndoa hiyo. (Yakobo 3:2) Lakini “kelele na matukano” hayafai na ni yenye kuharibu uhusiano wowote. (Waefeso 4:31) Mwe haraka kufanya amani wakati ambapo mmetupiana maneno yenye kudhuru. (Mathayo 5:23, 24) Magomvi yaweza mara nyingi kuzuiwa mwanzoni iwapo nyote wawili mnatumia maneno ya Paulo kwenye Waefeso 4:26: “Jua lisichwe na uchungu wenu bado haujawatoka.” Naam, suluhisheni mambo yanapokuwa madogo na rahisi kusuluhisha; msingojee mpaka hisia-moyo zenu zilete matokeo mabaya. Kutumia dakika chake kila siku ili kuzungumzia mambo yanayohangaisha kwaweza kufanyia maendeleo mawasiliano na kuzuia kutoelewana.
‘Rekebisho la Akilini la Yehova’
8. Kwa nini baadhi ya vijana huenda wakapeperuka na kuiacha kweli?
8 Yaonekana kwamba wazazi wengine wameridhika na kuwaruhusu watoto wao wakue tu bila mwongozo mwingi. Watoto huhudhuria mikutano na hushiriki sehemu fulani katika utumishi wa shambani, lakini mara nyingi hawajajijengea uhusiano wao wenyewe na Mungu. Baadaye “tamaa ya mwili, na tamaa ya macho” yaweza kuwaongoza wengi wa vijana hao mbali na kweli. (1 Yohana 2:16) Lingekuwa jambo la kuhuzunisha kama nini kwa wazazi kuokoka Har–Magedoni lakini wawaache watoto wao nyuma wakiwa wamekufa kwa sababu hawakuwajali wakati uliopita!
9, 10. (a) Kuwalea watoto “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova” kunatia ndani nini? (b) Kwa nini ni jambo la maana kuwaruhusu watoto waonyeshe hisia zao kwa uhuru?
9 Hivyo Paulo aliandika: “Akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Ili kufanya hivyo, ni lazima wewe mwenyewe ufahamu kikamili viwango vya Yehova. Wapaswa uweke mfano ufaao kwa habari ya mambo kama vile vitumbuizo unavyochagua, funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na utumishi wa shambani. Maneno ya Paulo hudokeza pia kwamba ni lazima mzazi (1) awe mtazamaji mwenye akili chapuchapu wa watoto wake na kwamba (2) adumishe mawasiliano mazuri pamoja nao. Kwa kufanya hivyo tu ndipo utajua mahali wanapohitaji “rekebisho la akilini.”
10 Ni jambo la asili kwa wabalehe kujitahidi kupata kadiri fulani ya kujitegemea. Hata hivyo, ni lazina uwe macho kuona ishara za waziwazi za uvutano wa kilimwengu katika usemi, fikira, mavazi na mapambo, na chaguo lao la marafiki. Baba mwenye hekima alisema kama ilivyorekodiwa kwenye Mithali 23:26: “Mwanangu, nipe moyo wako.” Je! watoto wako huhisi huru kushiriki mawazo na hisia zao pamoja na wewe? Watoto wasipohofu hasira ya mara hiyo, huenda wakaelekea zaidi kufunua jinsi wanavyohisi hasa juu ya mambo kama vile utendaji wa baada ya shule, matembezi pamoja na mtu wa jinsia tofauti, elimu ya juu, au kweli ya Biblia yenyewe.
11, 12. (a) Nyakati za mlo zaweza kutumiwaje ili kuendeleza mawasiliano ya familia? (b) Ni nini laweza kuwa tokeo la jitihada zisizokoma za mzazi za kuendeleza mawasiliano pamoja na watoto wake?
11 Katika nchi nyingi limekuwa jambo la kidesturi kwa familia kula pamoja. Hivyo mlo mkubwa wa kutwa waweza kuandaa nafasi nzuri kwa washiriki wa familia kushiriki katika mazungumzo yenye kujenga. Mara nyingi sana televisheni na mambo mengine huchukua mahali pa mlo wa familia. Lakini, kwa muda mrefu watoto wako kwa kweli huwa wamefungwa shuleni na hufunuliwa waingiwe na mawazo ya kilimwengu. Nyakati za mlo ni wakati mzuri wa kuwasiliana na watoto wako. “Sisi hutumia wakati wa mlo kuongea juu ya mambo yaliyotukia wakati wa mchana,” asema mzazi mmoja. Bado, nyakati za mlo hazihitaji kuwa vipindi vyenye kutahayarisha, vya kutia-tia nidhamu au kuhoji-hoji. Acha pindi hiyo iwe ya pumziko na yenye kufurahisha.
12 Kufanya watoto wawasiliane na wewe kwa uhuru ni jambo gumu na huenda likahitaji subira isiyo na kikomo. Lakini baadaye, huenda ukaona matokeo yenye kuchangamsha moyo. “Mwana wetu mwenye umri wa miaka 14 alikuwa ameshuka moyo na kuwa mwenye kujitenga na watu,” akumbuka mama mwenye kuhangaika. “Kupitia sala na udumifu wetu, anaanza kuwasiliana na kuongea tena!”
Funzo la Familia Linalojenga
13. Kwa nini mazoezi ya watoto mapema ni ya maana sana, na yanaweza kutimizwaje?
13 “Rekebisho la akilini” latia ndani pia mafunzo rasmi katika Neno la Mungu. Sawa na Timotheo, mazoezi hayo yanapaswa yaanze “tangu utoto.” (2 Timotheo 3:15) Mazoezi ya mapema huimarisha watoto dhidi ya mitihani ya imani ambayo huenda yakatokea wakati wa miaka ya shule—miadhimisho ya siku ya kuzaliwa, sherehe za kizalendo, au sikukuu za kidini. Bila matayarisho kwa ajili ya mitihani hiyo, imani ya mtoto yaweza kuvunjwa kabisa. Kwa hiyo tumia kwa faida yako vichapo ambavyo Watch Tower Society imetayarisha kwa ajili ya watoto wadogo, kama vile vitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu na Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia.a
14. Funzo la familia laweza kudumishwaje likiwa la kawaida, na wewe umefanya nini ili kuwa na funzo la familia la kawaida?
14 Jambo jingine la kuangaliwa ni funzo la familia, ambalo laweza kwa urahisi kufikia hatua ya kutokuwa la kawaida au lisilopendeza, la kidesturi tu lenye kuwajaribu wazazi na watoto pia. Waweza kufanyaje maendeleo? Kwanza, ni lazima ‘ununue wakati’ kwa ajili ya funzo, kutoliruhusu lisongwe na vipindi vya televisheni au mambo mengine. (Waefeso 5:15-17, NW) “Ilikuwa vigumu kwetu kudumisha funzo la familia la kawaida,” chaungama kichwa kimoja cha familia. “Tulijaribu nyakati tofauti-tofauti mpaka hatimaye tukapata wasaa jioni baadaye kidogo uliotufaa. Sasa funzo letu ni la kawaida.”
15. Waweza kupatanishaje funzo lako la familia kulingana na mahitaji ya familia yako?
15 Halafu, fikiria mahitaji mahususi ya familia yako. Familia nyingi hufurahia kutayarisha pamoja somo lao la Mnara wa Mlinzi la kila juma. Hata hivyo, mara kwa mara, familia yako huenda ikawa na masuala mahususi yanayohitaji kuzungumziwa, kutia ndani matatizo yanayokabiliwa shuleni. Kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi na makala kutoka Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zaweza kutimiza mahitaji hayo. “Tukiona mitazamo yoyote kwa upande wa wavulana wetu inayohitaji kurekebishwa,” asema baba mmoja, “tunakazia sura moja katika kitabu Vijana Huuliza inayozungumzia mtazamo huo.” Mke wake aongeza hivi: “Tunajaribu kuwa wenye kubadilika. Ikiwa tuna jambo fulani lililopangwa kwa ajili ya funzo letu, na uhitaji watokea kuzungumzia jambo jingine, basi twabadilika kulingana na uhitaji.”
16. (a) Unaweza kuhakikishaje kwamba watoto wako wanaelewa yale wanayojifunza? (b) Ni nini kipaswacho kuepukwa kwa kawaida katika kuongoza funzo la familia?
16 Unaweza kuhakikishaje kwamba watoto wako wanaelewa kweli kweli kile wanachojifunza? Mwalimu Mstadi, Yesu, aliuliza maulizo ya maoni, kama vile, “Waonaje?” (Mathayo 17:25) Kwa kufanya vivyo hivyo, jaribu kupata kujua lile ambalo watoto wako wanafikiri kweli kweli. Mtie moyo kila mtoto ajibu kwa maneno yake mwenyewe. Bila shaka, ukiitikia maelezo yao ya unyoofu kwa hasira au kwa kushtuka, huenda wakasita kuongea waziwazi na wewe tena. Kwa hiyo baki ukiwa mtulivu. Epuka kugeuza funzo la familia kuwa kipindi cha kuwaadhibu. Lapaswa liwe la kufurahisha, lenye kujenga. “Ninapogundua kwamba mmoja wa watoto wangu ana tatizo,” asema baba mmoja, “nitalishughulikia wakati mwingine.” “Mtoto anaposhughulikiwa akiwa peke yake,” aongeza mama mmoja, “hatahayaki sana na aweza kuongea kwa uhuru zaidi ya vile angeongea ikiwa angeshauriwa wakati wa funzo la familia.”
17. Ni nini kiwezacho kufanywa ili kulifanya funzo la familia liwe lenye kupendeza, na ni nini linalofaa zaidi katika familia yako?
17 Kufanya watoto washiriki katika funzo la familia kwaweza kuwa jambo gumu, hasa wakati unaposhughulika na watoto wa umri tofauti-tofauti. Watoto wachanga zaidi huenda wakawa wenye kucheza-cheza, wasiweze kutulia, au wasiweze kukazia fikira habari kwa muda mrefu. Waweza kufanya nini? Jaribu kudumisha hali ya funzo likiwa lenye ustarehe. Ikiwa watoto wako hawawezi kukazia fikira habari kwa muda mrefu, jaribu vipindi vifupi-vifupi lakini vya kawaida zaidi. Inasaidia pia kuwa mwenye idili. “Msimamizi na asimamie kwa bidii.” (Warumi 12:8, HNWW) Husisha kila mtu. Watoto wadogo zaidi wanaweza kueleza juu ya vielezi au kujibu maswali sahili. Labda matineja wanaweza kuombwa wafanye utafiti zaidi au kuonyesha jinsi habari hiyo inavyoweza kutumiwa ifaavyo.
18. Wazazi wanaweza kukaziaje kikiki Neno la Mungu kwenye kila pindi, kukiwa na tokeo gani?
18 Hata hivyo, usifanye kutoa maagizo ya kiroho kuwe kwa muda wa saa moja kila juma na basi. Kazia kikiki Neno la Mungu ndani ya mioyo ya watoto wako kila pindi. (Kumbukumbu la Torati 6:7) Chukua wakati kuwasikiliza. Wahimize na kuwafariji inapohitajiwa. (Linganisha 1 Wathesalonike 2:11.) Uwe mwenye huruma na mwenye rehema. (Zaburi 103:13; Malaki 3:17) Kwa kufanya hivyo, ‘utafurahishwa’ na watoto wako na utategemeza uhifadhi wao ili waingie ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu.—Mithali 29:17.
“Wakati wa Kucheka”
19, 20. (a) Tafrija ina fungu gani katika maisha ya familia? (b) Ni baadhi ya njia zipi ambazo kwazo wazazi wanaweza kupangia tafrija kwa ajili ya familia yao?
19 Kuna “wakati wa kucheka . . . , wakati wa kuruka-ruka.” (Mhubiri 3:4, NW) Neno la Kiebrania linalotumiwa kwa ‘-cheka’ huenda pia likatafsiriwa kwa kutumia maneno kama vile “-sherehekea,” “-cheza,” “-chezea,” au hata “furahia.” (2 Samweli 6:21; Ayubu 41:5; Waamuzi 16:25; Kutoka 32:6; Mwanzo 26:8) Kucheza kwaweza kuwa na kusudi lenye mafaa, na ni kwa maana kwa watoto na vijana. Katika nyakati za Biblia wazazi walipanga vitumbuizo na tafrija kwa ajili ya familia zao. (Linganisha Luka 15:25.) Je! wewe hufanya vivyo hivyo?
20 “Sisi hutumia kwa faida yetu bustani za umma,” asema mume Mkristo mmoja. “Twaalika baadhi ya ndugu vijana na kuwa na mchezo wa mpira na kufanya mandari. Wanafurahia na kuonea shangwe ushirika ufaao.” Mzazi mwingine aongeza hivi: “Sisi hupanga mambo ya kufanya pamoja na wavulana wetu. Twaenda kuogelea, kucheza mpira, kwenda likizoni. Lakini tunadumisha vitumbuizo vyetu kuwa vile vinavyofaa. Ninakazia uhitaji wa kudumisha usawaziko.” Tafrija yenye kujenga, kama vile vikusanyiko vifaavyo au visafari vya kwenda mahali pa kuhifadhia wanyama na majumba ya kuhifadhia vitu vya kale, yaweza kusaidia sana kumzuia mtoto asivutiwe na anasa za ulimwengu.
21. Wazazi wanaweza kuwazuiaje watoto wao wasihisi wananyimwa jambo fulani kwa sababu hawasherehekei sikukuu za kilimwengu?
21 Pia ni jambo la maana kwamba watoto wako wasihisi kuwa wananyimwa jambo fulani kwa sababu hawasherehekei siku za kuzaliwa au sikukuu zisizo za Kikristo. Kwa kupanga kwako mambo kwa kadiri fulani, wanaweza kutazamia nyakati nyingi zenye kufurahisha muda wote wa mwaka. Kwani mzazi mwema hahitaji sikukuu fulani iwe udhuru wa kuonyesha upendo wake kwa njia ya kimwili. Sawa na Baba yake wa kimbingu, yeye ‘ajua jinsi ya kuwapa watoto wake zawadi nzuri’—kwa hiari.—Mathayo 7:11, NW.
Kusalimishia Familia Yako Wakati Ujao wa Milele
22, 23. (a) Dhiki kubwa inapokaribia, familia zinazomcha Mungu zinaweza kuhakikishiwa nini? (b) Familia zaweza kufanya nini zinapojitahidi kuhifadhiwa kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu?
22 Mtunga zaburi alisali hivi: “Wewe, BWANA [Yehova, NW], ndiwe utakayetuhifadhi, utatulinda na kizazi hiki milele.” (Zaburi 12:7) Mbano kutoka kwa Shetani hakika utazidi kuongezeka—hasa dhidi ya familia za Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, inawezekana kustahimili shambulio hilo linaloongezeka daima. Kwa msaada wa Yehova na azimio thabiti na jitihada kwa upande wa waume, wake, na watoto, familia—kutia na familia yako—zaweza kuwa na tumaini la kuhifadhiwa zikiwa hai wakati wa dhiki kubwa.
23 Waume na wake, leteeni ndoa yenu amani na upatano kwa kutimiza madaraka yenu mliyogawiwa na Mungu. Wazazi, endeleeni kuwawekea watoto wenu mifano ifaayo, mkinunua wakati ili kuwapa mazoezi na nidhamu wanayohitaji sana. Ongeeni nao. Wasikilizeni. Maisha zao zimo hatarini! Watoto, wasikilizeni na kuwatii wazazi wenu. Kwa msaada wa Yehova mwaweza kufanikiwa na kujisalimishia wenyewe wakati ujao wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja.
[Maelezo ya Chini]
a Kaseti-sauti zapatikana katika lugha nyinginezo.
Je! Wakumbuka?
◻ Waume na wake wanaweza kufanyiaje maendeleo mawasiliano yao?
◻ Wazazi wanaweza kuwaleaje watoto wao katika “rekebisho la akilini la Yehova”? (Waefeso 6:4, NW)
◻ Ni zipi baadhi ya njia za kufanya funzo la familia liwe lenye kujenga na lenye kupendeza zaidi?
◻ Wazazi wanaweza kufanya nini katika kuzipangia familia zao tafrija na vitumbuizo?
[Sanduku katika ukurasa wa 16]
MUZIKI—UVUTANO WENYE NGUVU
Mtungaji mmoja wa kitabu juu ya malezi ya mtoto asema hivi: “Ikiwa ningalisimama mbele ya wasikilizaji . . . na kuunga mkono karamu za ulevi, kulewa kwa kutumia kokeni, bangi, au dawa za kulevya nyinginezo zinazogeuza akili, wangalinitazama kwa mshangao wenye mshtuo. . . . [Hata hivyo] wazazi mara nyingi huwapa watoto wao pesa za kununua rekodi au sahani zinazounga mkono mambo hayo waziwazi.” (Raising Positive Kids in a Negative World, cha Zig Ziglar) Kwa mfano, katika United States, maneno ya muziki wa maongezi yanayotaja ngono waziwazi hurudiwa-rudiwa na vijana wengi. Je! unawasaidia watoto wako waepuke mitego hiyo ya kishetani kwa kuwa wenye kuchagua kwa uangalifu muziki wao?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nyakati za mlo zaweza kuwa pindi zenye kufurahisha zinazoendeleza umoja na mawasiliano ya familia