Tulinufaika na Mikusanyiko ya “Njia ya Mungu ya Maisha”
1 Miezi michache tu iliyopita, tulikuwa tukifanya mipango ya kuhudhuria Mikusanyiko ya Wilaya na Mkusanyiko wa Kimataifa wa 1998 wa “Njia ya Mungu ya Maisha.” Sasa mikusanyiko hiyo imekuwa kumbukumbu lenye kupendeza katika nchi zetu. Tulifurahia kabisa chakula cha kiroho tulichopokea kwenye mikusanyiko hiyo yenye kutokeza.
2 Jambo la kwamba mikusanyiko ya mwaka huu ilikuwa ya kimataifa lilikuwa lenye kusisimua kwelikweli. Iwe wamishonari au wajumbe wa kutoka nchi za kigeni walikuwepo mahali tulipohudhuria au la, sisi sote tulisikia mambo mazuri yaliyoonwa Ijumaa alasiri katika sehemu iliyokuwa na kichwa “Utumishi Katika Shamba la Kimishonari.” “Ripoti za Jinsi Kazi ya Mavuno Inavyoendelea” zilizotolewa kila siku kutoka ulimwenguni kote zilikuwa zenye kutia moyo sana.
3 Vitolewaji Vipya Vizuri Ajabu: Hotuba ya mwisho Ijumaa ilitegemea swali ambalo watu wengi zaidi wasioijua kweli wameuliza: “Je, Kuna Uhai Baada ya Kifo?” Hotuba yenye kupendeza zaidi ilimalizia kwa kutolewa kwa broshua mpya, Ni Nini Hutupata Tunapokufa? Kufikia sasa bila shaka tumeisoma na twaweza kuona jinsi itakavyokuwa yenye thamani katika kusaidia watu wafahamu kweli kuhusu hali ya wafu na kuwafariji waliofiwa kwa tumaini la ufufuo.
4 Programu ya Jumamosi alasiri ilimalizika kwa hotuba “Utu wa Muumba na Njia Zake.” Ilituongoza tufikie mkataa wenye kupatana na akili wa kwamba lazima kuwe na Muumba. Ili kututayarisha tusaidie wengine wathamini jambo hili, kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kilitolewa. Ingawa kitabu hicho chazidisha imani yetu katika Yehova na uthamini wa utu wake na njia zake, kimekusudiwa hasa wale ambao ijapokuwa wana elimu ya juu ya kilimwengu, huenda ikawa hawamwamini Mungu.
5 Azimio la Moyoni: Hotuba ya mwisho ya mkusanyiko ilikazia uhitaji wa sisi sote ‘Kuendelea Kutembea Katika Njia ya Yehova.’ Ilifaa kama nini kutangaza waziwazi azimio la kibinafsi la kuamua kushikamana, kutetea, na kuendeleza sikuzote ubora wa njia ya Mungu ya maisha! (Isa. 30:21) Tulipokea kitia-moyo kizuri kama nini kwa kuhudhuria Mkusanyiko wa “Njia ya Mungu ya Maisha”!