Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ct sura 11 kur. 184-191
  • Fanya Maisha Yako Yawe na Maana Daima Dawamu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Fanya Maisha Yako Yawe na Maana Daima Dawamu
  • Je, Kuna Muumba Anayekujali?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kumwendea Muumba
  • Maana ya Maisha Yategemea Ujuzi
  • Muumba Aweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Muumba Wako—Jifunze Jinsi Alivyo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kwa Sababu Gani Ushukuru Muumba?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Ni Nini Hufanya Maisha Yawe na Kusudi Halisi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Je, Kuna Muumba Anayekujali?
ct sura 11 kur. 184-191

Sura Ya Kumi Na Moja

Fanya Maisha Yako Yawe na Maana Daima Dawamu

MAHALI popote tuishipo, sisi husikia juu ya ugunduzi wa sayansi. Wataalamu wa viumbe na wa bahari, na wengine huendelea kuongezea ujuzi wa mwanadamu mambo yanayohusu dunia na uhai uliopo. Mbali na dunia, wataalamu wa anga na fizikia wanajifunza mengi zaidi kuhusu mfumo wetu wa jua, nyota, na hata makundi ya mbali ya nyota. Mambo haya yanaonyesha nini?

Watu wengi wenye kufikiri kwa makini hukubaliana na Mfalme Daudi wa kale: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.” (Zaburi 19:1) Ni kweli kwamba huenda wengine wakakataa kuamini kwamba kuna Muumba au wasiwe na uhakika juu ya jambo hilo. Lakini baada ya kufikiria uthibitisho ambao umetolewa katika kitabu hiki, je, huwezi kuona sababu ya kutosha ya kuamini kwamba kuna Muumba na ndiye mwanzilishi wa ulimwengu na uhai wetu?

Mtume Paulo alisema: “Watu hawawezi kusema kwamba hawajui lolote juu ya Mungu. Tangu mwanzo wa ulimwengu, watu waliweza kuona jinsi Mungu alivyo kupitia vitu ambavyo Yeye amefanyiza. Hilo laonyesha uwezo Wake wenye kudumu milele. Laonyesha kwamba Yeye ni Mungu.” (Waroma 1:20, Holy Bible—New Life Version) Habari tulizozungumzia katika sura zilizotangulia kuhusu uumbaji zilifanya iwe rahisi “kuona jinsi Mungu alivyo,” na kuthamini “sifa zake zisizoonekana.” (NW) Lakini, kujua tu kwamba uumbaji halisi waonyesha jinsi Muumba alivyo hakutoshi. Kwa nini?

Wanasayansi wengi wamejitoa kuchunguza ulimwengu, lakini bado maisha zao hazina kusudi, wakikosa maana yenye kudumu. Kwa mfano, mtaalamu wa fizikia Steven Weinberg aliandika: “Kadiri ulimwengu uonekanavyo kuwa wenye kueleweka zaidi, ndivyo inavyozidi kuonekana kuwa hatuelewi ni kwa nini ulimwengu upo.” Kuhusu maoni ya mtaalamu wa nyota Alan Dressler, gazeti Science lilisema: “Watafiti wasemapo kwamba ulimwengu wafunua ‘akili’ au ‘kazi’ za Mungu, wao wamsifu Mungu kwa mambo ambayo si muhimu sana ulimwenguni—yaani muundo wake uonekanao.” Dressler alionyesha kwamba jambo kuu zaidi ni maana ya maisha ya wanadamu. Alisema: “Watu wameacha kuamini ile itikadi ya zamani ya kwamba wanadamu ndio kitovu cha ulimwengu [uonekanao], lakini ni lazima warudie kuamini kwamba wanadamu ndio muhimu zaidi katika maana ya maisha.”

Kwa wazi, kila mmoja wetu apaswa kupendezwa sana na maana ya maisha yetu. Kukiri tu kwamba kuna Muumba, au Mbuni, na kwamba tunamtegemea huenda kusifanye maisha yetu yawe na maana. Hiyo ni kweli hasa kwa sababu uhai huonekana kuwa mfupi. Wengi wamehisi kama Mfalme Macbeth katika mojawapo ya tamthilia za William Shakespeare:

“Maisha ni ya punde tu, ni mwigizaji asiye na ujuzi

Mwenye madaha na uchungu akiwa jukwaani

Na kisha atoweka kabisa. Ni hadithi

Isimuliwayo na mpumbavu, iliyojaa kelele na ghadhabu,

Na isiyo na maana.”—Macbeth, Onyesho la Tano, Mandhari ya Tano.

Watu duniani kote waweza kukubaliana na maneno hayo; lakini wao binafsi wanapokabili tatizo kubwa, bado wanaweza kumlilia Mungu wakimwomba msaada. Elihu, mtu mmoja wa zamani mwenye hekima, alisema: “Kwa sababu ya wingi wa jeuri wao hulia; walilia msaada . . . Wala hapana asemaye, Yuko wapi Mungu Muumba wangu? . . . Atufundishaye zaidi ya hayawani wa nchi, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege za angani.”—Ayubu 35:9-11.

Maneno ya Elihu yakazia kwamba sisi wanadamu si muhimu katika maana ya maisha. Muumba wetu Mtukufu ndiye muhimu, na kwa kufaa maana yoyote ya maisha yahusika naye na kumtegemea. Ili kupata maana kama hiyo na uradhi wa ndani ambao maana hiyo huleta, tunahitaji kujua Muumba na kupatanisha maisha yetu na mapenzi yake.

Kumwendea Muumba

Musa alimwendea Muumba. Yeye alikiri hivi kwa wazi: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini, na kiburi chake ni taabu na ubatili.” Kutambua jambo hilo hakukumfanya Musa awe mwenye huzuni au mwenye kutazamia mabaya; kulimsaidia kuthamini mafaa ya kumwendea Muumba. Musa alisali hivi: “Basi, utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima. Utushibishe asubuhi kwa fadhili zako, nasi tutashangilia na kufurahi siku zetu zote. Na uzuri wa BWANA, Mungu wetu, uwe juu yetu.”—Zaburi 90:10, 12, 14, 17.

‘Kushiba asubuhi.’ ‘Kushangilia siku zetu zote.’ ‘Uzuri wa BWANA kwetu.’ Je, maneno kama hayo hayadokezi kwamba mtu amepata maana ya maisha—maana ambayo watu kwa ujumla hawana?

Twaweza kuchukua hatua kubwa ya kuwa na maana maishani kwa kutambua mahali petu mbele za Muumba. Kwa njia fulani, ujuzi unaoongezeka kuhusu ulimwengu unaweza kutusaidia. Daudi aliuliza: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?”—Zaburi 8:3, 4.

Tunahitaji kufanya zaidi ya kukiri tu ya kwamba Yehova aliumba jua, mwezi, na nyota kisha akasababisha viumbe vijae duniani pamoja na vitu vyote vya dunia. (Nehemia 9:6; Zaburi 24:2; Isaya 40:26; Yeremia 10:10, 12) Kama tulivyojifunza mapema, jina la kipekee la Yehova laonyesha kwamba yeye ni Mungu wa kusudi na ni yeye peke yake anayeweza kutekeleza mapenzi yake kabisa.

Isaya aliandika: “Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; hakuiumba ukiwa, aliiumba ili ikaliwe na watu.” Kisha Isaya akanukuu maneno ya Yehova: “Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine.” (Isaya 45:18) Na baadaye Paulo alisema hivi kuhusu Wakristo wenzake: “Sisi ni tokeo la kazi yake na tuliumbwa katika muungano na Kristo Yesu kwa ajili ya kazi zilizo njema.” Jambo kuu kuhusu “kazi zilizo njema” ni kujulisha “hekima ya Mungu ya namna nyingi, kulingana na kusudi [lake] la milele.” (Waefeso 2:10; 3:8-11) Inawezekana kuwa na uhusiano na Muumba na tunapaswa kufanya hivyo, tukijitahidi kujifunza kusudi lake na kushirikiana nalo.—Zaburi 95:3-6.

Kutambua kwamba kuna Muumba mwenye upendo na mwenye kujali kwapasa kutusukuma tutende. Kwa mfano, ona uhusiano uliopo kati ya kutambua jambo hilo na jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. “Amwoneaye maskini humsuta Muumba wake; bali yeye awahurumiaye wahitaji humheshimu.” “Mungu aliyetuumba siye mmoja tu? Basi, mbona kila mmoja anamtenda ndugu yake mambo ya hiana?” (Mithali 14:31; Malaki 2:10) Kwa hiyo, kutambua kwamba kuna Muumba ambaye anajali kunapasa kutusukuma tujali zaidi viumbe vyake vingine.

Hatujaachwa peke yetu kutimiza jambo hilo. Muumba aweza kutusaidia. Hata ingawa sasa Yehova hatokezi viumbe vipya vya dunia, inaweza kusemwa kwamba bado anaumba kwa njia nyingine. Yeye huwasaidia sana wanadamu kwa njia yenye matokeo watafute mwongozo wake. Baada ya kutenda dhambi, Daudi aliomba: “Ee Mungu, uniumbie moyo safi, uifanye upya roho iliyotulia ndani yangu.” (Zaburi 51:10; 124:8) Na Biblia huwahimiza Wakristo ‘waweke mbali utu wa hapo zamani’ uliofanyizwa kwa kupatana na ulimwengu uliowazunguka na ‘kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.’ (Waefeso 4:22-24) Ndiyo, Yehova aweza kuumba moyo mpya wa mfano katika watu, akiwasaidia kusitawisha utu ambao unaonyesha jinsi yeye alivyo.

Lakini, hizo ni hatua za kwanza tu. Tunahitaji kuingia ndani zaidi. Paulo aliwaambia Waathene fulani wenye elimu: ‘Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyo katika huo aliagiza nyakati zilizowekwa ili watu wamtafute, ikiwa wangeweza kupapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ijapokuwa yeye hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.’—Matendo 17:24-27.

Maana ya Maisha Yategemea Ujuzi

Kutokana na mambo ambayo tumezungumzia, inapasa kuwa wazi kwamba Muumba ameandaa habari nyingi kupitia uumbaji wake halisi na kupitia Neno lake lililopuliziwa, Biblia. Yeye atuhimiza tukuze ujuzi na ufahamu wa ndani, hata akitabiri wakati ambapo “dunia itajawa na kumjua BWANA.”—Isaya 11:9; 40:13, 14.

Si mapenzi ya Muumba kwamba uwezo wetu wa kujifunza na kufanya maendeleo uwe tu kwa muda wa maisha wa miaka 70 au 80. Unaweza kuona jambo hilo katika mojawapo ya taarifa za Yesu zilizo mashuhuri zaidi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:16.

“Uhai udumuo milele.” Hiyo si ndoto tu. Badala yake, wazo la kuishi daima dawamu linapatana na kile ambacho Muumba aliwapa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa. Linapatana na mambo ya hakika ya sayansi kuhusu mfanyizo na uwezo wa ubongo wetu. Na linapatana na yale ambayo Yesu Kristo alifundisha. Jambo kuu la ujumbe wa Yesu lilikuwa ni mwanadamu kupata uhai udumuo milele. Kwenye jioni yake ya mwisho duniani akiwa na mitume, alisema: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’—Yohana 17:3.

Kama ilivyozungumzwa katika sura iliyotangulia, ahadi ya Yesu ya uhai udumuo milele itakuwa halisi hapahapa duniani kwa mamilioni ya watu. Kwa wazi, kuwa na tazamio hilo kwaweza kuongeza sana maana ya maisha ya mtu. Kunamaanisha kusitawisha uhusiano pamoja na Muumba. Uhusiano kama huo sasa unaweka msingi wa kupata uhai wa milele. Ebu wazia mambo ambayo maisha kama hayo yatakuwezesha kufanya: kujifunza, kuvumbua, na kuona—yote bila kikomo ambacho sasa kimewekwa na ugonjwa na kifo. (Linganisha Isaya 40:28.) Ungefanya nini na maisha kama hayo? Wewe mwenyewe wajua vizuri zaidi mapendezi yako, vipawa ambavyo unatamani kusitawisha, na majibu ambayo ungetaka kupata. Uwezo wako wa kuweza kuzifuatia hata utaongezea zaidi maana ya maisha yako!

Paulo alikuwa na sababu nzuri ya kutazamia wakati ambapo “viumbe vyenyewe pia vitawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Wale ambao watapata uhuru huo watafurahia maana halisi ya maisha sasa nao wataishi milele, kwa utukufu wa Mungu.—Ufunuo 4:11.

Mashahidi wa Yehova duniani pote wamejifunza habari hiyo. Wao wamesadiki ya kwamba kuna Muumba na kwamba anawajali na anakujali pia. Wanafurahi kuwasaidia wengine kupata maana hiyo yenye msingi thabiti katika maisha. Tafadhali uwe huru kuchunguza jambo hili pamoja nao. Kufanya hivyo kutafanya maisha yako yawe na maana daima dawamu!

[Sanduku katika ukurasa wa 185]

Mungu Katika Maana Gani?

“Wanasayansi na wengine nyakati nyingine hutumia neno ‘Mungu’ kumaanisha kitu ambacho ni cha kuwaziwa sana na kisichohusika sana hivi kwamba Yeye hawezi kutofautishwa na sheria za asili,” akasema Steven Weinberg, mshindi wa tuzo la Nobeli kwa kazi yake ya kani za msingi. Aliongezea hivi:

“Naona ya kwamba ili neno ‘Mungu’ liwe na manufaa yoyote, lapaswa kueleweka kumaanisha Mungu mwenye kupendezwa, muumba na mpaji-sheria ambaye hajaanzisha tu sheria za asili na ulimwengu bali pia ameanzisha viwango vya mema na uovu, utu fulani ambao unahangaikia matendo yetu, kwa ufupi kitu kinachostahili kuabudiwa nasi. . . . Huyo ndiye Mungu wa maana kwa wanaume na wanawake katika historia yote.”—Dreams of a Final Theory.

[Picha katika ukurasa wa 187]

Musa alitambua kwamba hata tuishi muda mrefu kadiri gani, maana halisi ya maisha yamtegemea Muumba

[Picha katika ukurasa wa 190]

Kupata maana yenye kudumu maishani hutokeza mambo mengi tuwezayo kufanya

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki