Waalike Waje
1 Mwaliko uliotolewa karne nyingi zilizopita watolewa sasa katika nchi 233 ulimwenguni pote: “Njoni, twende juu mlimani kwa BWANA, . . . naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake.” (Isa. 2:3) Kuelekeza watu kwenye tengenezo la Yehova ni mojawapo ya njia bora zaidi tunazoweza kuwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho yaongozayo kwenye uhai udumuo milele.
2 Huenda wahubiri fulani wakasitasita kualika watu kwenye Jumba la Ufalme hadi baada ya watu hao kufanya maendeleo makubwa katika funzo lao la Biblia la nyumbani. Hata hivyo, nyakati nyingine watu wataanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko hata kabla ya kuanza kujifunza Biblia. Hatupaswi kuchelewa kutoa mwaliko mchangamfu na kuwatia moyo watu waje mikutanoni.
3 Jambo la Kufanya: Tumia vizuri vikaratasi vya kukaribisha watu vilivyopo kujulisha watu juu ya mikutano ya kwetu. Taja kwamba mikutano si ya malipo na kwamba hakuna sadaka zinazokusanywa. Eleza jinsi mikutano inavyoongozwa. Taja kwamba mikutano hiyo hasa ni mitaala ya kujifunza Biblia na kwamba vichapo vya kujifunzia vyapewa wote ili wafuatie funzo linapoendelea. Elekeza fikira kwenye malezi mbalimbali na watu wa kila namna wanaohudhuria. Taja kwamba ni watu kutoka eneo hilo na kwamba watoto wa kila umri wanakaribishwa kuja. Twapaswa kualika wale ambao tunajifunza nao, tukiwapa msaada kwa njia yoyote ile ili wahudhurie.
4 Mojawapo ya mambo ya mwisho yaliyorekodiwa katika Biblia ni mwaliko mchangamfu wa kushiriki maandalizi ya Yehova kwa ajili ya uhai: “Na roho na bibi-arusi hufuliza kusema: ‘Njoo!’ . . . Na acha yeyote anayeona kiu aje; acha yeyote atakaye achukue maji ya uhai bure.” (Ufu. 22:17) Hakuna jambo liwezalo kuchukua mahali pa kualika watu wahudhurie mikutano yetu.
5 Isaya 60:8 hufafanua kiunabii mamia ya maelfu ya wasifaji wapya wanaokuja sasa katika makutaniko ya watu wa Mungu kama njiwa “warukao kama wingu, na kama njiwa waendao madirishani kwao.” Sote twaweza kualika wapya kwenye mikutano yetu na kuwafanya wahisi wamekaribishwa. Kwa njia hiyo, tutakuwa tukishirikiana na Yehova aharakishapo kazi ya kukusanya.—Isa. 60:22.