“Hatuwezi Kukoma Kusema”
1 Yesu Kristo anasimamia kwa ukaribu kazi ya kuhubiri. (Mt. 28:20; Mr. 13:10) Ijapokuwa kuna watangazaji karibu milioni sita wanaotoa ushahidi katika nchi 234, tusidhani kwamba kazi yetu ya kutoa ushahidi imekwisha. Mungu asipotangaza kwamba kazi imekwisha, “hatuwezi kukoma kusema” juu ya mambo ambayo tumejifunza.—Mdo. 4:20.
2 Tegemea Roho ya Mungu: Shetani huongeza mkazo mwingi ili kutuvunja moyo. (Ufu. 12:17) Mwili wetu wenyewe usio mkamilifu pia hutuletea shida nyingi. Mambo hayo yanaweza kukengeusha fikira zetu kutoka katika kazi ya maana zaidi ya kuhubiri. Hata hivyo, tukimtumaini Yehova, roho yake itatusaidia tukabiliane na kizuizi chochote.
3 Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza liliponyanyaswa vibaya, akina ndugu walimwomba Mungu awasaidie waendelee kusema neno lake kwa ujasiri wote. Yehova alijibu sala yao, akiwajaza roho yake na kuwapa bidii na azimio lililohitajiwa ili kuendelea kuhubiri. Tokeo likawa kwamba waliendelea bila kuacha kutangaza kwa ujasiri habari njema.—Mdo. 4:29, 31; 5:42.
4 Usihofu Mazungumzo Yenye Kuvunja Moyo: Maoni ya watu kwa ujumla au uchongezi wa hadharani huenda ukatuogofya. Hata hivyo, kumbuka walivyosema kwa ujasiri Petro na mitume wale wengine mbele ya Sanhedrini, kama ilivyorekodiwa kwenye Matendo 5:29-32. Kama vile alivyokubali Gamalieli mwalimu wa Sheria, kazi ya Mungu haiwezi kupinduliwa. Haitimizwi kwa nguvu zetu wenyewe. Kazi hii kuu inategemezwa na Mungu, na ni yeye tu awezaye kuitimiza!—Zek. 4:6.
5 Na tumwombe sana Yehova kila siku atupe roho yake itusaidie tutangaze habari njema kwa bidii. Na tuseme kama Yeremia, kwamba ujumbe wa Ufalme ni kama moto uwakao ndani ya mifupa yetu. (Yer. 20:9) Hatuwezi kunyamaza!