Moyo Wake Uliguswa
“Tulikuwa familia ya watoto 13,” aandika Gloria Adame, “wavulana 4 na wasichana 9. Ulikuwa mwaka wa 1984. Baba alirudi nyumbani Mexico na akapata kwamba alipokuwa ameenda kufanya kazi Marekani, familia yetu ilikuwa imeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Hakupendezwa hata kidogo, akaanza kutupinga. Ilionekana kana kwamba kila siku iliyopita, moyo wake ulizidi kuwa mgumu.
“Tulimpenda baba yetu sana, na tulitaka afaidike kutokana na ujuzi utoao uhai tuliokuwa tukiupata. Siku baada ya siku tulisali kwa bidii kwa Yehova, tukimwomba kwa kusihi sana atufungulie njia ili tuseme na Baba kuhusu makusudi ya Yehova. Yehova alisikia ombi letu kwa sababu alitupa moyo mkuu wa kukusanyika kila jioni kwenye sebule, ambapo Baba alitumia kila usiku akitazama televisheni. Hapo mama yangu na sisi wasichana tulikuwa tukikutana ili kusoma andiko la Biblia la kila siku.
“Mama aliongoza mazungumzo, na baada ya kusoma maelezo, tulikuwa tukichukua zamu kusali. Wakati dada yetu mdogo zaidi Marie, ambaye alikuwa na umri wa miaka mitano tu, aliposali, angeomba kwa bidii: ‘Yehova, tafadhali fanya moyo wa Baba uwe mwororo ili pia yeye aje kuwa Shahidi wako.’ Ilionekana kana kwamba Baba hakuwa akisikiliza, kwani angeongeza sauti ya televisheni. Hata hivyo, kadiri muda ulivyopita, alianza kupunguza sauti, mpaka usiku mmoja aliizima kabisa.
“Jioni hiyo, kama ilivyokuwa desturi yetu, Mama aliuliza ilikuwa zamu ya nani kusoma andiko. Kwa mshangao mkubwa, Baba alisema: ‘Ni zamu yangu.’ Tulishangaa lakini hatukusema lolote. Mama hakukinza wala kuuliza maswali lakini alimpa kile kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Baada ya yeye kuongoza mazungumzo ya andiko la Biblia, Mama aliuliza ilikuwa zamu ya nani kusali. ‘Ni zamu yangu,’ Baba akasema.
“Tulipigwa na bumbuazi. Sala ikiwa katikati, hatukuweza tena kuzuia machozi. Baba pia alianza kulia, akamuuliza Yehova amsamehe kwa Kumkufuru. Pia alimwomba Mama amsamehe kwa vile alikuwa ametupinga.
“Kwa hiyo katika mwaka wa 1986 upinzani wa baba ulikoma. Katika mwaka wa 1990 familia yetu ilihamia Texas katika Marekani. Halafu, Baba akaweka maisha yake wakfu kwa Yehova akafananisha hilo kwa ubatizo wa maji, kama tulivyofanya saba kati ya sisi dada. Katika Aprili mwaka wa 1997, Baba aliwekwa rasmi kuwa mzee Mkristo. Kufikia siku hii, kuchunguza andiko la Biblia la kila siku tukiwa familia ni jambo la maana sana kwetu, na sala kwa Yehova ni msingi wa maisha ya familia yetu.”
[Picha katika ukurasa wa 31]
1. Binti wanne wanaofanya upainia huko Mexico. Marie yuko mbele
2. Juanita na Isaac Adame, wakiwa na baadhi ya watoto wao. Gloria yuko mwisho kulia