Ratiba ya Familia—Andiko la Siku
1 Kila siku, wazazi wenye upendo hujitahidi sana kuwaandalia watoto wao chakula kizuri. Kuwaandalia chakula cha kiroho kutoka katika neno la Mungu ni muhimu zaidi. (Mt. 4:4) Njia moja ya kuwasaidia watoto wako kusitawisha hamu ya chakula cha kiroho ili ‘wakue kufikia wokovu’ ni kuchunguza andiko la siku na maelezo yake kila siku mkiwa familia. (1 Pet. 2:2) Mnaweza kuchunguza andiko la siku wakati gani?
2 Wakati wa Mlo: Kuanza siku kwa kuzungumzia andiko la siku kutaiwezesha familia yenu kumfikiria Yehova mchana kutwa. (Zab. 16:8) Mama mmoja alizoea kusoma na kuzungumzia andiko la siku na maelezo yake pamoja na mwana wake alipokuwa akila kiamsha kinywa na kusali naye kabla mwana huyo hajaondoka kwenda shuleni. Hilo lilimwimarisha kusimama imara alipokabili suala la uzalendo, kupinga vishawishi vya ukosefu wa maadili, na kuwahubiria kwa ujasiri wanafunzi na walimu. Hakuhisi upweke licha ya kuwa Shahidi pekee katika shule hiyo.
3 Ikiwa hamwezi kulichunguza andiko la siku asubuhi mkiwa familia, mnaweza kulichunguza baadaye, pengine mnapokula chakula cha jioni siku hiyo. Wengine huzungumzia mambo yaliyoonwa katika huduma ya shambani na mambo waliyofurahia katika usomaji wao wa Biblia. Wengi hukumbuka pindi kama hizo nao huziona kuwa pindi walizofurahia zaidi wakiwa pamoja na familia zao.
4 Usiku: Familia fulani huona kwamba muda mfupi kabla ya kwenda kulala ndio wakati bora wa kulichunguza andiko la siku. Hiyo inaweza pia kuwa pindi nzuri ya kusali pamoja. Watoto wenu humwona Yehova kuwa mtu halisi wanapowasikia mkiongea kumhusu na kusali kwake kila siku.
5 Yehova na abariki jitihada zenu za kuwafundisha watoto wenu kweli mnapotumia vizuri kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku.