Chakula cha Kiroho cha Kila Siku —Cha Lazima kwa Familia ya Kikristo
1 “Mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu [Yehova, NW].” (Mt. 4:4) Jinsi maneno hayo yalivyo ya kweli! Kama vile tunavyohitaji chakula cha kimwili kila siku, ndivyo tunavyohitaji kula chakula cha kiroho kila siku. Ili kutusaidia katika kula kwa kawaida kutokana na Neno la Mungu, Sosaiti imechapisha kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Mkiwa familia ya Kikristo, je! mnaweka wakati kando kila siku ili kuchunguza andiko la siku?
2 Ni Lazima Wazazi Waweke Mfano: Kukiwa na shughuli nyingi za kawaida, ni rahisi kukosa kuchunguza andiko, kwa kufikiri kwamba hilo laweza kufanywa wakati mwingine. Lakini ikiwa wazazi wanaona uhitaji wa kiroho wa familia yao, watapata wakati, naam, watafanya wakati, kila siku kufanya hivyo familia inapokuwa pamoja. (Mt. 5:3) Wao watachukua hatua ya kwanza si kwa kusoma tu andiko la siku na watoto wao bali pia kukazia mambo yaliyo katika maelezo ya Mnara wa Mlinzi na kuzungumzia jinsi habari na shauri hilo liwezavyo kutumika kihalisi. Ni kweli, huenda ikataka jitihada na mazoezi ili kuwa na kawaida ya kufanya hivyo, lakini faida zinazopatikana zinastahili jitihada hizo. (Linganisha Matendo 17:11, 12.) Kwa hiyo, wazazi, jitahidini kuweka mfano mzuri!
3 Tafuta Wakati Unaofaa: Ni wakati gani unaofaa zaidi kwa familia nzima kuja pamoja kwa mazungumzo ya andiko, bila kufanya hilo liwe jambo la kushtukia? Kuna faida katika kuanza siku kwa kuchunguza andiko la Biblia. Katika Betheli na makao ya wamishonari kuzunguka ulimwengu, siku huanza na ibada ya asubuhi, ambayo hutia ndani mazungumzo mafupi ya andiko la siku. Hilo husaidia akina ndugu kuanza siku vyema, wakifikiria makumbusho ya Yehova kila siku.—Zab. 1:1, 2; Flp. 4:8.
4 Familia za Kikristo zaweza kufaidika vilevile na mazungumzo ya Biblia ya asubuhi. Watoto wanaweza kusaidiwa kukabiliana na vitisho dhidi ya hali yao ya kiroho wanavyoona shuleni. Ikiwa kwa muda fulani haiwezekani kwa familia nzima kuketi pamoja kwa mazungumzo ya andiko la siku, wazazi wanaweza kufikiria mipango ya badala ili kwamba ulishaji huo wa kiroho wenye maana usikosekane. Kwa mfano, baba anapolazimika kwenda kazini kabla ya watoto kuamka asubuhi, labda mama aweza kutumia wakati fulani kuzungumza andiko na watoto. Kwa upande mwingine, familia nyingine hupanga kuzungumzia andiko jioni kwa sababu wakati huo wanakuwa pamoja. Kila familia yaweza kupanga ratiba inayofaa zaidi hali yayo.
5 Ulishaji wa kiroho wa kila siku ni wa lazima kwa familia ya Kikristo. Tanguliza uchunguzi wa andiko la kila siku mbele ya mambo mengine. (Flp. 1:10) Kuzungumzia andiko la Biblia kila siku kutatusaidia tushikamane na sheria na kanuni za haki za Yehova. Ushirikiano kwa upande wa kila mshiriki wa familia utafanya mpango huo uwafaidi wote.