Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 49 uku. 255-uku. 257 fu. 3
  • Kutoa Sababu Zenye Kusadikisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoa Sababu Zenye Kusadikisha
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kutoa Utangulizi Mzuri wa Maandiko
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kuwaelimisha Wasikilizaji
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 49 uku. 255-uku. 257 fu. 3

SOMO LA 49

Kutoa Sababu Zenye Kusadikisha

Unahitaji kufanya nini?

Toa uthibitisho mzuri unaounga mkono mambo unayosema.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Wasikilizaji hawataamini yale unayosema wala hawatayafuata mpaka wasadiki kwamba ni ya kweli.

UNAPOTAJA jambo, wasikilizaji wana haki ya kuuliza: “Kwa nini jambo hilo ni kweli? Ni nini kinachothibitisha jambo ambalo msemaji anasema?” Ukiwa mwalimu, una daraka la kujibu maswali hayo au kuwasaidia kupata majibu hayo. Ikiwa jambo unalosema ni muhimu sana, hakikisha unawapa wasikilizaji sababu zenye kusadikisha ili walikubali. Hiyo itafanya hotuba yako iwe yenye kuvutia.

Mtume Paulo aliwasihi watu katika mazungumzo yake. Alitumia sababu zenye kusadikisha, alisababu kwa njia inayofuatana vizuri, na kuwasihi watu kwa bidii ili wabadili maoni yao. Alituwekea mfano mzuri. (Mdo. 18:4; 19:8) Ni kweli kwamba wasemaji wengine stadi huvutia watu na kuwapotosha. (Mt. 27:20; Mdo. 14:19; Kol. 2:4) Wanaweza kuanza kuzungumzia dhana potovu, kutegemea habari zinazopendelea upande mmoja, kutumia sababu zisizo na msingi, kupuuza mambo yanayopingana na maoni yao, au kuchochea hisia za watu badala ya kuwafanya wafikiri. Tujihadhari tusitumie mbinu hizo.

Sababu Zitegemee Kabisa Neno la Mungu. Tusifundishe kamwe mambo yetu wenyewe. Sisi hujitahidi kuwaeleza wengine mambo ambayo tumejifunza katika Biblia. Tumesaidiwa sana na vichapo vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Vichapo hivyo vinatusaidia kuchunguza Maandiko kwa makini. Sisi huwaelekeza watu katika Biblia, si kwa kusudi la kuthibitisha kuwa tunasema ukweli, bali kwa unyenyekevu tunataka wajionee wenyewe kile ambacho Biblia inasema. Tunakubaliana na Yesu Kristo, aliyemwambia Baba yake hivi katika sala: “Neno lako ni kweli.” (Yn. 17:17) Hakuna mtu mwenye mamlaka kuliko Yehova Mungu, Muumba wa mbingu na dunia. Sababu zetu zitasadikisha ikiwa zinategemea Neno lake.

Nyakati nyingine unaweza kuzungumza na watu ambao hawafahamu Biblia au hawaioni kuwa Neno la Mungu. Tambua kwa busara wakati wa kutumia maandiko ya Biblia na jinsi unavyoweza kuyatumia. Lakini unapaswa kujitahidi kuwaonyesha upesi kwamba mazungumzo yako yanategemea mamlaka fulani.

Je, kunukuu tu andiko fulani kunatoa sababu ambayo haiwezi kukanushwa? Si lazima. Huenda ukahitaji kuonyesha muktadha wa andiko ili kuthibitisha kwamba linaunga mkono jambo unalosema. Ikiwa unaonyesha kanuni fulani katika andiko na muktadha hauzungumzii habari hiyo, unahitaji kutoa uthibitisho zaidi. Unaweza kutumia maandiko mengine yanayohusiana na jambo hilo ili wasikilizaji waridhike kwamba jambo unalosema linategemea Maandiko.

Epuka kuongezea maana ambayo andiko halisemi. Lisome kwa makini. Huenda andiko hilo linataja kwa ujumla habari ambayo unazungumzia. Lakini ili sababu zako ziweze kuvutia, ni lazima msikilizaji aone kwamba zinathibitisha jambo unalosema.

Sababu Ziwe na Uthibitisho. Nyakati nyingine inaweza kufaa kutumia uthibitisho ambao hautokani na Biblia lakini unaotegemeka ili kusaidia watu waone sababu za Maandiko.

Kwa mfano, unaweza kutaja kwamba ulimwengu wote mzima ni uthibitisho wa kwamba kuna Muumba. Unaweza kutaja sheria za asili, kama vile nguvu za uvutano, na kwamba kuwapo kwa sheria hizo kunathibitisha kwamba kuna Yule aliyezitunga. Sababu yako inaweza kusadikisha mtu ikiwa inapatana na Neno la Mungu. (Ayu. 38:31-33; Zab. 19:1; 104:24; Rom. 1:20) Uthibitisho kama huo unasaidia kwa sababu unaonyesha kwamba jambo ambalo Biblia inasema linalingana na mambo halisi.

Je, unajaribu kumsaidia mtu kutambua kwamba kwa kweli Biblia ni Neno la Mungu? Unaweza kunukuu wasomi wanaosema hivyo, lakini je, hilo linathibitisha kwamba hiyo ni Neno la Mungu? Kunukuu mambo kama hayo huwasaidia wale tu wanaoheshimu wasomi hao. Je, unaweza kutumia sayansi kuthibitisha kama Biblia ni kweli? Kutumia maoni ya wanasayansi wasiokamilika ni kujenga kwenye msingi dhaifu. Lakini ukianza na Neno la Mungu kisha utaje mambo ambayo sayansi imegundua yanayokazia usahihi wa Biblia, sababu zako zitakuwa na msingi thabiti.

Hata iwe unajaribu kuthibitisha nini, toa uthibitisho wa kutosha. Kiasi cha uthibitisho unaohitaji kutoa kinategemea wasikilizaji. Kwa mfano, kama unazungumzia siku za mwisho zinazotajwa katika 2 Timotheo 3:1-5, unaweza kuwatajia wasikilizaji habari inayojulikana sana inayothibitisha kwamba watu hawana “shauku ya asili.” Mfano huo mmoja unaweza kuthibitisha kwamba sehemu hii ya ishara ya siku za mwisho inatimizwa wakati huu.

Mara nyingi inaweza kufaa kulinganisha mambo mawili ambayo yanafanana. Ulinganifu huo peke yake hauthibitishi jambo, lakini ukweli wake ni lazima ulinganishwe na maoni ya Biblia. Lakini ulinganifu huo unaweza kumsaidia mtu aone sababu ya jambo unalosema. Kwa mfano unaweza kutumia ulinganifu unapoeleza kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali. Unaweza kutaja kwamba Ufalme wa Mungu una watawala, raia, sheria, mfumo wa kutekeleza sheria, na mfumo wa elimu kama tu serikali za wanadamu.

Mambo halisi yaliyotokea yanaweza kutumiwa kuthibitisha kwamba ni hekima kutumia shauri la Biblia. Mambo ambayo umejionea pia yanaweza kutumiwa kuunga mkono habari unayozungumzia. Kwa mfano, unapomwambia mtu umuhimu wa kusoma na kujifunza Biblia, unaweza kumweleza jinsi ambavyo kufanya hivyo kumeboresha maisha yako. Mtume Petro alizungumzia mgeuko-umbo, ambao yeye mwenyewe alijionea, ili kuwatia moyo ndugu zake. (2 Pet. 1:16-18) Paulo pia alitaja mambo aliyojionea. (2 Kor. 1:8-10; 12:7-9) Usitumie sana mambo uliyojionea maishani usije ukajielekezea fikira mno.

Kwa kuwa watu wana malezi tofauti na wanafikiri kwa njia tofauti, uthibitisho unaomsadikisha mtu mmoja huenda usimsadikishe mwingine. Basi, fikiria maoni ya wasikilizaji unapoamua hoja ambazo utatumia na jinsi utakavyozitoa. Mithali 16:23 inasema: “Moyo wake mwenye hekima hufundisha kinywa chake; huzidisha elimu ya midomo yake.”

JINSI YA KUFAULU

  • Badala ya kusisitiza tu mambo, toa uthibitisho unaosadikisha ili kuunga mkono mambo muhimu.

  • Sababu zako zitegemee kabisa Maandiko.

  • Tumia mambo yanayothibitisha kusudi lako na kusadikisha wasikilizaji.

MAZOEZI: (1) Fungua kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko kwenye kichwa kikuu, “Yesu Kristo.” Ona jinsi maswali yanayojibiwa yanavyotegemea Biblia. (2) Chunguza makala za kwanza za Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Chagua mambo makuu kadhaa ambayo yanazungumziwa. Tia mstari maandiko makuu, na utie alama mambo yanayoyathibitisha.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki