SOMO LA 52
Kutoa Himizo Linalofaa
NI LAZIMA wazee Wakristo ‘wahimize kwa bidii kwa fundisho lenye afya.’ (Tito 1:9) Nyakati nyingine ni lazima wafanye hivyo japo hali ngumu sana. Ni muhimu kutoa mashauri kulingana na miongozo ya Maandiko. Kwa hiyo, ni lazima wazee watii shauri hili: “Endelea kujitahidi . . . kuhimiza kwa bidii.” (1 Tim. 4:13) Ingawa mazungumzo yetu yanalenga hasa wazee au wale ambao wanajitahidi kufikia pendeleo hili, kuna nyakati ambazo ni lazima wazazi wawahimize watoto wao au nyakati ambazo wale wanaoongoza mafunzo ya Biblia wanahitaji kuwahimiza wanafunzi wao wa Biblia. Miongozo iliyopo hapa inafaa hali hizo pia.
Hali Zinazohitaji Himizo. Ili kujua wakati unapohitaji kutoa himizo, inafaa kuchunguza pindi ambazo watu walihimizwa katika Biblia. Mtume Petro aliwahimiza wazee wakazie uangalifu daraka lao la kuchunga kutaniko la Mungu. (1 Pet. 5:1, 2) Paulo alimshauri Tito awahimize wanaume vijana wawe “timamu katika akili.” (Tito 2:6) Paulo aliwahimiza Wakristo wenzake ‘waseme kwa upatano’ na kuepuka wale waliojaribu kuleta migawanyiko miongoni mwa akina ndugu. (1 Kor. 1:10; Rom. 16:17; Flp. 4:2) Ingawa Paulo alilitia moyo kutaniko lililokuwa Thesalonike kwa ajili ya matendo yao mema, aliwahimiza watumie zaidi mafundisho waliyopokea. (1 The. 4:1, 10) Petro aliwasihi Wakristo wenzake ‘wafulize kujiepusha na tamaa za kimwili.’ (1 Pet. 2:11) Yuda aliwahimiza ndugu zake ‘wafanye pigano kali kwa ajili ya imani’ ili wasiathiriwe na watu wasiomcha Mungu wenye mwenendo mlegevu. (Yuda 3, 4) Kwa ujumla Wakristo waliombwa wahimizane ili hata mmoja asije akafanywa kuwa mgumu kwa nguvu ya udanganyifu ya dhambi. (Ebr. 3:13) Petro aliwahimiza hivi Wayahudi ambao hawakuwa wametia imani katika Kristo: “Pateni kuokolewa kutokana na kizazi hiki kilicho kombo.”—Mdo. 2:40.
Ni sifa gani zinazohitajiwa ili kuwahimiza watu katika hali hizo? Mtu anayewahimiza wengine anawezaje kuonyesha hali ya dharura bila kuwashurutisha wasikilizaji au bila kuwa mkali?
“Juu ya Msingi wa Upendo.” Ikiwa hatuwahimizi wengine “juu ya msingi wa upendo,” himizo letu laweza kuwa kali. (Flm. 9) Ni kweli kwamba ikiwa hatua ya mara moja inahitajika, msemaji anapaswa kuzungumza kwa hali inayoonyesha udharura huo. Lakini, kuzungumza kwa upole sana kunaweza kuwafanya wengine wafikiri msemaji anaomba radhi. Na bado tunapaswa kuwahimiza wengine kwa uzito na kwa hisia nyingi. Inaelekea kwamba wasikilizaji watachochewa na himizo linalotolewa kwa upendo. Paulo aliwaambia Wathesalonike hivi alipokuwa akizungumza kwa niaba yake na kwa niaba ya waandamani wake: “Mwajua vema jinsi, kama vile baba afanyiavyo watoto wake, tulifuliza kuhimiza kwa bidii kila mmoja wenu.” (1 The. 2:11) Waangalizi hao Wakristo waliwasihi ndugu zao kwa upendo. Zungumza kwa njia inayoonyesha kwamba kwa kweli unawahangaikia wasikilizaji.
Uwe na busara. Usiwachokoze wale ambao unajaribu kuwahimiza kutenda. Lakini pia usikose kuwaambia wasikilizaji “shauri lote la Mungu.” (Mdo. 20:27) Wale wanaothamini mashauri hayo hawataudhika au hawataacha kukupenda eti kwa sababu umewahimiza kwa fadhili kufanya lililo sawa.—Zab. 141:5.
Kwa kawaida, ni vizuri kutoa pongezi hususa kutoka moyoni kabla ya kutoa himizo. Fikiria mambo mazuri ambayo yanampendeza sana Yehova ambayo akina ndugu wanafanya kama vile imani wanayoonyesha katika kazi yao, upendo unaowachochea kutia bidii, na uvumilivu wao wanapokabili majaribu. (1 The. 1:2-8; 2 The. 1:3-5) Jambo hili litawasaidia akina ndugu waone unawathamini na kuwaelewa, na hilo litawafanya wawe tayari kiakili kukubali himizo ambalo utatoa.
“Kwa Ustahimilivu Wote.” Tunapaswa kuwahimiza wengine kwa “ustahimilivu wote.” (2 Tim. 4:2) Hiyo inahusisha nini? Ustahimilivu unatia ndani kuvumilia kwa subira unapokosewa au kuchokozwa. Mtu mstahimilivu hutumaini daima kwamba wasikilizaji watatii mambo anayosema. Ukiwahimiza wasikilizaji kwa njia hiyo hawatafikiri kwamba unatazamia tu mabaya kuwahusu. Ukiwa na hakika kwamba akina ndugu na dada wanataka kumtumikia Yehova kwa kadiri ya uwezo wao, watakuwa na hamu ya kufanya yaliyo mema.—Ebr. 6:9.
‘Kwa Fundisho Lenye Afya.’ Mzee anawezaje ‘kuhimiza kwa bidii kwa fundisho lenye afya’? Atafanya hivyo kwa “kushika kwa imara lile neno la uaminifu kwa habari ya usanifu wa kufundisha kwake.” (Tito 1:9) Badala ya kutumia maoni yako tu, wahimize kwa msingi wa Neno la Mungu. Yale unayosema na yategemee Biblia. Orodhesha faida za kutii maoni ya Biblia kuhusu jambo unalozungumzia. Kumbuka vizuri matokeo ya wakati huu na ya wakati ujao ya kutofuata Neno la Mungu, na uyatumie kusadikisha wasikilizaji juu ya uhitaji wa kuchukua hatua inayofaa.
Hakikisha unawaeleza wasikilizaji waziwazi yale wanayopaswa kufanya na jinsi wanavyopaswa kuyafanya. Iwe wazi kwamba sababu unazotoa zinategemea Maandiko. Maandiko yakiruhusu uhuru wa kiasi fulani wa uamuzi wowote unaohitaji kufanywa, taja kadiri wanavyoweza kutumia uhuru huo. Kisha unapomalizia hotuba yako, wahimize mwishowe kwa kuimarisha azimio lao la kutenda.
Kwa ‘Uhuru wa Usemi.’ Ili uwahimize wengine kwa njia inayofaa, ni lazima uwe na ‘uhuru wa usemi katika imani.’ (1 Tim. 3:13) Ni nini kinachomwezesha mtu aseme kwa uhuru? Ni kuwa “kielelezo cha kazi zilizo bora” kuhusu mambo anayowahimiza akina ndugu wafanye. (Tito 2:6, 7; 1 Pet. 5:3) Kwa njia hiyo, wale wanaohimizwa watatambua kwamba yule anayewahimiza hawatarajii wafanye jambo ambalo yeye mwenyewe hafanyi. Wataona kwamba wanaweza kuiga imani yake anapojaribu kumwiga Kristo.—1 Kor. 11:1; Flp. 3:17.
Himizo linalotegemea Neno la Mungu na linalotolewa kwa roho ya upendo linaweza kufaidi sana. Wale ambao wamepewa madaraka ya kuwahimiza wengine wanapaswa kujitahidi kuwahimiza kwa njia nzuri.—Rom. 12:8.