SOMO LA 25
Kutumia Muhtasari
WATU wengi huogopa kutumia muhtasari. Wao hufurahia zaidi ikiwa wameandika au kukariri kila jambo wanalotaka kusema.
Lakini ukweli ni kwamba kila siku sisi huzungumza bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza na jamaa zetu na marafiki bila kutumia muhtasari. Sisi huzungumza bila muhtasari tunapokuwa katika huduma. Hatutumii muhtasari tunaposali kutoka moyoni, iwe tunasali binafsi au kwa niaba ya wengine.
Unapotoa hotuba, je, kuna tofauti yoyote kati ya kusoma hotuba yako na kutumia muhtasari? Ingawa kusoma hotuba kunaweza kufanya utumie maneno yanayofaa na yaliyo sahihi, kufanya hivyo hakugusi mioyo. Mara nyingi ukisoma sentensi chache, utaanza kufuata mtindo fulani ambao ni tofauti na kawaida yako ya kuzungumza. Akili yako ikizama katika maandishi yako na kusahau wasikilizaji, huenda wengi wasisikilize kwa makini kama ambavyo wangesikiliza iwapo wangeona kwamba unawajali kweli na habari unayozungumzia inawahusu. Njia bora zaidi ya kutoa hotuba inayochochea kabisa ni kuitoa bila kutazama sana maandishi.
Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni kutusaidia katika maisha ya kawaida. Tunapokutana na marafiki, je, sisi hutoa karatasi na kuwasomea mambo tunayotaka kuwaeleza eti kuhakikisha tunatumia maneno yanayofaa zaidi? Tunapokuwa katika utumishi wa shambani, hatubebi maandishi ya kusoma, eti kwa sababu tunaogopa tutasahau mambo fulani ambayo tungependa kuwaeleza watu. Unapotoa onyesho katika shule kuhusu kutoa ushahidi katika hali hizo, jizoeze kuzungumza kwa njia ya kawaida kwa kadiri iwezekanavyo. Ukitayarisha vizuri, utaona kwamba muhtasari ambao umeandika au umeshika akilini hutosha kukukumbusha mambo makuu ambayo unataka kuzungumzia. Lakini unawezaje kufaulu kutumia muhtasari?
Panga Mambo Unayotaka Kuzungumzia. Ili uweze kutumia muhtasari, unahitaji kupanga mambo unayotaka kuzungumzia. Hiyo haimaanishi kuchagua maneno ambayo unapanga kutumia. Inamaanisha tu kufikiri kabla ya kuzungumza.
Kwa kawaida, mtu ambaye huzungumza bila kufikiri hushtukia amesema mambo ambayo baadaye anajutia. Mwingine naye anaweza kuzungumza bila mpango, akitangatanga kutoka jambo moja hadi jingine. Unaweza kusuluhisha matatizo hayo vizuri kwa kutua na kupanga kwa ufupi mawazo yako akilini kabla ya kuzungumza. Kwanza kumbuka kusudi lako, kisha chagua mambo ambayo unahitaji kufanya ili kutimiza kusudi hilo, kisha uzungumze.
Je, unajitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani? Panga mkoba wako na ufikirie mambo utakayosema. Ukiamua kutumia mmojawapo wa utangulizi katika Huduma Yetu ya Ufalme, uusome mara kadhaa ili ukumbuke vizuri mambo makuu. Taja mambo hayo katika sentensi moja au mbili. Tumia maneno ya utangulizi huo kwa kupatana na hali zako na hali za eneo lenu. Inafaa kuwa na muhtasari fulani akilini. Muhtasari huo unaweza kuwa na nini? (1) Kwenye utangulizi, unaweza kutaja jambo ambalo linawahangaisha watu wengi katika eneo lenu. Mpe nafasi mwenye nyumba atoe maoni yake. (2) Fikiria jambo fulani hususa ambalo unaweza kuzungumza naye kuhusu habari hiyo, pamoja na andiko moja au maandiko mawili yanayoonyesha ahadi ya Mungu ya kusuluhisha tatizo hilo. Ukipata fursa, kazia kwamba Yehova atatatua tatizo hilo kupitia Ufalme wake, serikali yake ya mbinguni. (3) Mtie moyo mwenye nyumba achukue hatua juu ya jambo ambalo umezungumzia. Unaweza kumtolea kichapo au Funzo la Biblia na kufanya mipango hususa ya kuendeleza mazungumzo.
Katika hali hizo utahitaji tu muhtasari ambao umeshika akilini. Ukitaka kuangalia muhtasari ulioandika kabla ya kufanya ziara ya kwanza, muhtasari huo uwe na utangulizi mfupi tu, andiko moja au mawili, na umalizio mfupi. Kutayarisha muhtasari kama huo na kuutumia hutusaidia tusitangetange katika mazungumzo. Pia kunatusaidia kumwachia mwenye nyumba ujumbe ulio wazi ambao anaweza kukumbuka kwa urahisi.
Ikiwa swali fulani au kipingamizi fulani huzushwa katika eneo lenu, inaweza kufaa kufanya utafiti kulihusu. Kwa kawaida, unahitaji tu mambo makuu mawili au matatu pamoja na maandiko yanayoyaunga mkono. “Vichwa vya Biblia vya Mazungumzo” au vichwa vidogo vyenye maandishi mazito vinavyopatikana katika kitabu Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko vinaweza kuwa na muhtasari hususa unaohitaji. Unaweza kupata mnukuo mzuri katika kichapo kingine ambao unaweza kutumia pia. Tayarisha muhtasari mfupi, ambatanisha nakala ya mnukuo huo, kisha uziweke pamoja na vifaa unavyotumia katika utumishi wa shambani. Mwenye nyumba anapozusha swali lile au kipingamizi kile, mjulishe kwamba ungefurahi kumwambia sababu zinazokufanya uamini jambo hilo. (1 Pet. 3:15) Tumia muhtasari huo kumjibu.
Ikiwa utatoa sala mbele ya familia, kikundi cha funzo, au kutaniko, ni vizuri kupanga mambo utakayosema. Kulingana na Luka 11:2-4, Yesu aliwapa wanafunzi wake muhtasari rahisi wa sala yenye maana. Na wakati wa kuweka hekalu wakfu huko Yerusalemu, Solomoni alitoa sala ndefu. Bila shaka alifikiria kimbele jambo la kusema. Kwanza alitaja Yehova na ahadi yake kwa Daudi; kisha akataja hekalu; kisha akataja hali hususa na makundi hususa ya watu. (1 Fal. 8:22-53) Mifano hiyo inaweza kutufaidi.
Muhtasari Wako Uwe Rahisi. Je, muhtasari wako ni wa kutoa hotuba? Muhtasari huo uwe na habari gani?
Kumbuka kwamba kusudi la muhtasari ni kukusaidia kukumbuka mawazo unayotaka kuwasilisha. Labda ungependa kuandika utangulizi wenye sentensi chache. Lakini baada ya hapo kazia akili mawazo unayotaka kuwasilisha na wala si maneno unayotaka kutumia. Tumia sentensi fupi-fupi unapoandika mawazo hayo. Mambo makuu machache ambayo unapanga kutumia yawe dhahiri katika muhtasari wako. Unaweza kuyafanya yawe dhahiri kwa kuyaandika kwa herufi kubwa, kuyapiga mstari, au kuyatia alama kwa rangi tofauti. Chini ya kila jambo kuu, orodhesha mambo ambayo unataka kutumia ili kulifafanua jambo kuu. Andika maandiko ambayo unapanga kusoma. Mara nyingi ni afadhali kusoma maandiko hayo katika Biblia. Andika mifano ambayo unataka kutumia. Pia unaweza kuwa na mnukuo mzuri uliopata katika vichapo vya kilimwengu ambao unafaa kutumiwa. Maandishi yako yawe na mambo hususa unayotaka kutaja. Ni rahisi zaidi kutumia muhtasari nadhifu.
Wengine hutumia mihtasari ambayo ina mambo machache kabisa. Muhtasari unaweza kuwa na maneno machache makuu, maandiko ambayo msemaji atayanukuu kutoka akilini, na michoro au picha zinazomwezesha kukumbuka mambo anayotaka kusema. Kwa maandishi hayo tu, msemaji anaweza kutoa hotuba inayofuatana vizuri na kwa njia ya mazungumzo. Na hilo ndilo lengo la somo hili.
Kuna mazungumzo yanayohusu “Kutayarisha Muhtasari” katika ukurasa wa 39 hadi 42 wa kitabu hiki. Kuna faida kubwa ya kusoma habari hiyo unaposhughulikia somo hili la “Kutumia Muhtasari.”
Jinsi ya Kutumia Muhtasari. Wakati huu kusudi lako si kutayarisha muhtasari wa hotuba, bali ni kuutumia muhtasari vizuri.
Hatua ya kwanza ya kutumia muhtasari ni matayarisho ya kuutoa. Chunguza kichwa kikuu, soma kila jambo kuu, na utambue uhusiano uliopo kati ya mambo hayo makuu na kichwa kikuu. Tazama muda ambao unaweza kutumia kwa kila jambo kuu. Kisha chunguza jambo kuu la kwanza. Pitia sababu zinazoonyeshwa, maandiko, na mifano ambayo unataka kutumia katika sehemu hiyo. Pitia sehemu hiyo mara kadhaa mpaka uielewe vizuri. Fanya hivyo na kila mojawapo ya mambo mengine makuu. Fikiria mambo ambayo unaweza kukosa kutaja hali ikikulazimu ili umalize kwa wakati. Kisha pitia hotuba yote. Kazia mambo makuu, na wala si maneno. Usikariri hotuba hiyo.
Unapotoa hotuba, unapaswa kuwatazama wasikilizaji kwa njia nzuri. Mara nyingi baada ya kusoma andiko, unapaswa kusababu juu ya andiko hilo ukitumia Biblia bila kurudia maandishi yako. Vilevile ukitoa mfano, uutoe kama ambavyo ungewaeleza marafiki wako badala ya kusoma mfano huo katika maandishi yako. Unapozungumza, usitazame-tazame maandishi yako na kusoma kila sentensi. Zungumza kwa hisia, nawe utagusa mioyo ya wale wanaokusikiliza.
Utakapokuwa stadi wa kutoa hotuba ukitumia muhtasari, utakuwa umepiga hatua kubwa ya kuwa msemaji mzuri unapohutubia watu.