Toa Ushahidi Katika Eneo la Biashara kwa Ujasiri
1. Kwa nini hatupaswi kukata tamaa ikiwa tunaogopa kutoa ushahidi katika eneo la biashara?
1 Je, wewe huogopa kutoa ushahidi katika eneo la biashara? Ikiwa ndivyo, usikate tamaa, kwa sababu hata Paulo aliyekuwa mhubiri hodari, alihitaji ‘kujipa ujasiri’ ili ahubiri. (1 The. 2:2) Katika makala hii, tutachunguza hali mbalimbali zinazoweza kufanya tuwe na wasiwasi, na mapendekezo yatakayotusaidia kukabiliana nazo.
2. Kwa nini tusiogope kuwakatiza wafanyakazi?
2 Je, Wafanyabiashara au Wafanyakazi Wataudhika Nikiwakatiza? Katika maeneo mengi ya biashara, wafanyakazi wanaowahudumia watu wamezoea kukatizwa. Mara nyingi, watakuwa wenye urafiki, kwa kuwa huenda wakafikiri wewe ni mteja. Iwapo wewe ni nadhifu, mchangamfu na mwenye urafiki, kwa kawaida watakutendea kwa heshima.
3. Tutaepuka kuwaudhi wateja jinsi gani?
3 Je, Itanibidi Kutoa Ushahidi Wateja Wengi Wakiwepo? Ikiwezekana, chagua wakati ambapo maduka hayana wateja wengi, kwa mfano, baada tu ya duka kufunguliwa. Ili usiwazuie wateja wasipate huduma, subiri mpaka msimamizi au mwuzaji anapokuwa peke yake kabla ya kumhubiria, na useme kifupi sana.
4. Tunaweza kusema nini tunapotoa ushahidi katika eneo la biashara?
4 Niseme Nini? Ikiwa kuna wafanyakazi kadhaa, ongea na msimamizi wa biashara. Unaweza kusema: “Ni vigumu kuwapata wafanyabiashara nyumbani, ndiyo sababu tunakutembelea hapa kazini. Ninajua una shughuli nyingi, kwa hiyo nitasema kifupi sana.” Ili wasifikiri kwamba sisi ni wafanyabiashara, ni bora tusitaje mpango wa kutoa michango, isipokuwa wakiuliza jinsi kazi yetu inavyogharimiwa. Ikitegemea aina ya biashara, unaweza kumwomba msimamizi ruhusa ya kuzungumza kifupi na wafanyakazi. Unapoongea nao unaweza kutumia utangulizi uleule unaoonyeshwa hapa juu. Ikiwa mfanyakazi ana shughuli nyingi, fupisha mazungumzo na umwachie trakti. Kama haiwezekani kuzungumza na wafanyakazi, huenda ukaomba ruhusa ya kuacha machapisho mahali ambapo wote wanaweza kuyaona.
5. Tuna sababu gani za kutoa ushahidi katika eneo la biashara kwa ujasiri?
5 Yesu na Paulo waliwahubiria watu katika maeneo yao ya biashara kwa ujasiri, na wewe unaweza kufanya hivyo pia. (Mt. 4:18-21; 9:9; Mdo. 17:17) Mwombe Yehova akusaidie uwe na moyo mtulivu na uwe mwenye ujasiri. (Mdo. 4:29) Jitahidi kutoa ushahidi katika eneo la biashara kwa maana hutakosa watu katika eneo hilo.