Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • km 3/13 kur. 4-7
  • Jinsi ya Kutumia Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kutumia Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!
  • Huduma ya Ufalme—2013
  • Habari Zinazolingana
  • Tangaza Habari Njema za Ufalme Ukitumia Broshua
    Huduma Yetu ya Ufalme—1996
  • Tumia Broshua Mbalimbali Katika Huduma Yako
    Huduma Yetu ya Ufalme—1995
  • Mwige Yehova kwa Kujali Wengine Kikweli
    Huduma Yetu ya Ufalme—1996
  • Kusitawisha Kupendezwa na Ujumbe wa Ufalme
    Huduma Yetu ya Ufalme—1992
Pata Habari Zaidi
Huduma ya Ufalme—2013
km 3/13 kur. 4-7

Jinsi ya Kutumia Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu!

Broshua Mpya Iliyokusudiwa Kutusaidia Kufanya Ziara za Kurudia na Kuanzisha Mafunzo ya Biblia

1. Ni broshua gani mpya iliyotolewa kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Linda Moyo Wako!” ambayo imekusudiwa kutusaidia kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia?

1 Kwenye Kusanyiko la Wilaya la “Linda Moyo Wako!,” tulifurahi kupata broshua mpya ya kutusaidia kufanya ziara za kurudia na kuanzisha mafunzo ya Biblia. Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! inayochukua nafasi ya broshua Anataka, inafanana nayo kwa kuwa ina masomo mafupi. Jambo hilo litatusaidia tutumie broshua hiyo vizuri tunapoongoza mafunzo ya Biblia mlangoni. Hata hivyo, ingawa broshua Anataka ilizungumzia mambo ambayo Mkristo anapaswa kutimiza ambayo yanaweza kuwa vigumu kwa mwanafunzi kukubali, broshua hii mpya hukazia habari njema zinazopatikana katika Biblia.—Mdo. 15:35.

2. Kwa nini broshua Habari Njema ilichapishwa?

2 Kwa nini ilichapishwa? Ndugu ulimwenguni pote wamekuwa wakiulizia kifaa rahisi kinachoweza kuwafanya watu wavutiwe na kweli na kuwaelekeza kwenye kitabu Biblia Inafundisha, ambacho ni kifaa chetu cha msingi tunachotumia kuongoza mafunzo ya Biblia. Watu wanaoogopa kusoma vitabu mara nyingi huwa tayari kujifunza Biblia kwa kutumia broshua. Kwa kuongezea, ni rahisi zaidi kutafsiri broshua katika lugha nyingi.

3. Broshua hii inatofautianaje na machapisho mengine ya funzo?

3 Jinsi Ilivyo: Mengi ya machapisho yetu ya funzo yameandikwa ili mtu aweze kuyasoma na kuelewa kweli hata bila kusaidiwa na mtu mwingine. Broshua hii ni tofauti. Imechapishwa ili mtu ajifunze Biblia akiwa pamoja na mwalimu. Kwa hiyo, unapomtolea mtu broshua hiyo, ni vyema kusoma na kuzungumzia fungu moja au mawili. Mafungu ni mafupi, hivyo yanaweza hata kuzungumziwa mlangoni mwa mwenye nyumba au mahali anapofanyia kazi. Ingawa inafaa kuanza na somo la 1, tunaweza kuanzisha funzo kwa kutumia somo lolote katika broshua hiyo.

4. Broshua Habari Njema hutusaidiaje kufundisha moja kwa moja kutoka katika Biblia?

4 Katika mengi ya machapisho yetu, majibu ya maswali yaliyochapwa yanaweza kupatikana kwenye mafungu. Hata hivyo katika chapisho hili, majibu yanapatikana hasa kwenye Biblia. Watu wengi hutaka kujifunza kutoka kwenye Biblia badala ya machapisho yetu. Hivyo, maandiko mengi hayajanukuliwa. Yanapaswa kusomwa moja kwa moja kutoka kwenye Biblia. Hilo huwasaidia wanafunzi kutambua kwamba mambo wanayojifunza yanatoka kwa Mungu.—Isa. 54:13.

5. Kwa nini ni muhimu kwa mwalimu kujiandaa vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo?

5 Broshua hiyo haifafanui maandiko yote. Kwa nini? Imekusudiwa kumtia moyo mwanafunzi aulize maswali na kumpa mwalimu nafasi ya kutumia uwezo wake wa kufundisha. Kwa hiyo, ni muhimu kujitayarisha vizuri kwa ajili ya kila kipindi cha funzo. Tahadhari: Usiongee kupita kiasi. Tunapenda kufafanua Maandiko. Lakini kwa kawaida tunatimiza mengi zaidi kwa kumwomba mwanafunzi aeleze maoni yake kuhusu maana ya andiko fulani. Kwa kutumia maswali kwa busara, tunaweza kumsaidia apate maana ya kila andiko.—Mdo. 17:2.

6. Tunaweza kuitumiaje broshua hiyo (a) watu wanapotilia shaka Biblia na kuwapo kwa Mungu? (b) katika huduma ya nyumba kwa nyumba? (c) kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa njia ya moja kwa moja? (d) tunapofanya ziara za kurudia?

6 Kama machapisho mengine yanayotumika kuongoza mafunzo, broshua hii inaweza kutolewa wakati wowote, bila kuzingatia toleo la machapisho la mwezi. Wengi watafurahia kuitumia kuanzisha mafunzo mlangoni kwa njia ya moja kwa moja. Kwa kuongezea, kama ilivyotajwa katika kusanyiko la wilaya, kutumia broshua hiyo tunapowarudia wale waliopendezwa “kwa kweli kunaweza kufanya kazi hiyo isisimue sana!”—Ona masanduku kwenye ukurasa wa 5-7.

7. Unaweza kuongozaje funzo la Biblia kwa kutumia broshua hiyo?

7 Jinsi ya Kuongoza Funzo: Tunaweza kuanza mazungumzo kwa kusoma maswali yenye wino mzito yaliyoorodheshwa. Kisha, soma fungu na andiko au maandiko yaliyoandikwa kwa herufi za mlazo. Tumia maswali kwa busara kumsaidia mwenye nyumba aelewe maana ya maandiko. Halafu, kabla ya kuendelea na sehemu inayofuata, mwombe mwenye nyumba ajibu swali lililoandikwa kwa wino mzito, ili kuhakikisha kwamba ameelewa. Katika ziara chache za kwanza, huenda ikawa vyema kuzungumzia swali moja tu lililoandikwa kwa wino mzito. Baada ya muda, huenda tukaweza kurefusha mazungumzo kwa kuzungumzia somo lote.

8. Utangulizi wa maandiko unapaswa kutolewa kwa njia gani, na kwa nini?

8 Maandiko yanayotanguliwa na neno “soma” ndiyo hasa yanayojibu moja kwa moja maswali yaliyoandikwa kwa wino mzito. Unapoanza kuzungumzia andiko, epuka kusema, “Mtume Paulo aliandika” au, “Ona kile ambacho Yeremia alitabiri.” Huenda mwenye nyumba akafikiri kwamba tunasoma maneno ya wanadamu tu. Itakuwa vizuri zaidi tukisema, “Neno la Mungu linasema” au, “Ona kile ambacho Biblia ilitabiri.”

9. Je, maandiko yote yanapaswa kusomwa wakati wa funzo?

9 Je, tunapaswa kusoma maandiko yote au yale tu yaliyoandikwa “soma”? Itategemea hali. Maandiko yote yaliyopo yana kusudi fulani. Kila andiko lina habari muhimu ya kuzungumzia. Lakini, katika visa fulani huenda tukahitaji kusoma tu maandiko yaliyoandikwa “soma” ikiwa mwanafunzi anakosa wakati, hapendezwi, au ana uwezo mdogo wa kusoma.

10. Ni wakati gani tunaweza kuanza kutumia kitabu Biblia Inafundisha?

10 Wakati wa Kuanza Kutumia Kitabu Biblia Inafundisha: Baada ya pindi kadhaa za mazungumzo na kujifunza kwa ukawaida na mwanafunzi wa Biblia, tunaweza kuanza kutumia kitabu Biblia Inafundisha au kuendelea na broshua Habari Njema hadi tutakapoimaliza. Wahubiri wanaweza kuamua wakati watakapoanza kutumia kitabu hicho. Punde tu baada ya kuanza kutumia kitabu Biblia Inafundisha, je, ni lazima tuanze mwanzo wa kitabu? Hakuna sheria kuhusiana na hilo. Kila mtu ni tofauti. Hata hivyo, wanafunzi wengi watanufaika kwa kupitia tena habari zilezile zinazofafanuliwa kwa undani katika kitabu Biblia Inafundisha.

11. Kwa nini tunapaswa kutumia vizuri broshua hiyo mpya?

11 Katika ulimwengu ambao habari njema ni haba, tuna pendeleo kubwa sana la kutangaza habari bora kuliko zote—kwamba Ufalme wa Mungu unatawala na hivi karibuni utaleta ulimwengu mpya ambamo uadilifu utakaa! (Mt. 24:14; 2 Pet. 3:13) Tuna uhakika kwamba wengi wanaosikia ujumbe huo watakubaliana na maneno haya yaliyoongozwa na roho: “Jinsi inavyopendeza juu ya milima miguu ya yeye anayeleta habari njema, yeye anayetangaza amani, yeye anayeleta habari njema za jambo bora, yeye anayetangaza wokovu, yeye anayeuambia Sayuni: ‘Mungu wako amekuwa mfalme!’” (Isa. 52:7) Na tutumie broshua hii mpya kuwapelekea habari njema kutoka kwa Mungu wale wenye kiu katika eneo letu!

[Picha katika ukurasa wa 5]

Watu Wanapotilia Shaka Biblia na Kuwapo kwa Mungu:

● Katika baadhi ya maeneo, wahubiri wameona kwamba watu hukataa kuwasikiliza wanapotumia maneno “Mungu” na “Biblia.” Katika hali hiyo, kwenye ziara ya kwanza, huenda ikafaa sana kuzungumzia habari zinazowahangaisha watu katika eneo lenu, kama vile uhitaji wa serikali nzuri, chanzo cha msaada kwa familia, na mambo yatakayotendeka wakati ujao. Labda tunaweza kuanza kutumia broshua Habari Njema baada ya kuwa na pindi kadhaa za mazungumzo ya kuthibitisha kwamba Mungu yuko na kwamba Biblia inategemeka.

[Picha katika ukurasa wa 6]

Unapohubiri Nyumba kwa Nyumba:

● “Nimekutembelea ili kukuonyesha jinsi inavyoweza kuwa rahisi kujua mambo ambayo Mungu amekusudia kuwafanyia wanadamu wakati ujao. Je, umewahi kujiuliza ikiwa Mungu atatuondolea mateso? [Mruhusu ajibu.] Broshua hii inaonyesha ni wapi katika Biblia unapoweza kupata jibu la swali hilo. [Mpe broshua, na usome fungu la kwanza katika somo la 1 na vilevile andiko la Yeremia 29:11.] Kutokana na mambo tuliyoona, je, unaona ni jambo linalopatana na akili kwamba Mungu anataka tuwe na wakati ujao mzuri zaidi? [Mruhusu ajibu.] Ikiwa ungependa, ninaweza kukuachia broshua hii. Wakati ujao, tunaweza kuzungumzia fungu la pili ili tuone jinsi Biblia inavyojibu swali hili, ‘Mungu ataondoaje mambo yanayosababisha wanadamu wateseke?’” Ikiwa mwenye nyumba anaonekana kuwa na wakati mwingi zaidi katika ziara ya kwanza, huenda ukasoma na kuzungumzia fungu la pili na maandiko matatu ya Biblia kwenye fungu hilo. Fanya mipango ya kurudi ili mzungumzie swali la pili katika somo hilo.

● “Watu wengi hupenda kusali, hasa wanapokuwa na matatizo. Je, nyakati nyingine wewe husali? [Mruhusu ajibu.] Je, unafikiri Mungu husikiliza sala zote, au huenda hapendezwi na sala zingine? [Mruhusu ajibu.] Hapa nina broshua inayoonyesha jinsi Biblia inavyojibu maswali hayo. [Mpe broshua, na mzungumzie pamoja fungu la kwanza katika somo la 12 na msome maandiko yaliyoandikwa “soma.”] Je, haipendezi sana kwamba Mungu yuko tayari kutusikiliza? Lakini ili tufaidike kikamili kutokana na sala, tunahitaji kumjua Mungu vizuri. [Fungua somo la 2 na umwonyeshe vichwa vidogo.] Ikiwa ungependa, naweza kukuachia broshua hii, na wakati mwingine tunaweza kuona jinsi Biblia inavyojibu kwa njia nzuri maswali hayo yenye kupendeza.”

● “Niko hapa kwa sababu watu wengi wana wasiwasi kuhusu mahali ambapo ulimwengu huu unaelekea. Je, unafikiri hali zitawahi kuwa nzuri? [Mruhusu ajibu.] Watu wengi wanashangaa kujifunza kwamba Biblia ina habari njema zinazoweza kutupa tumaini. Haya ni baadhi ya maswali ambayo Biblia hujibu.” Mpe broshua, na umwombe achague swali katika ukurasa wa mwisho ambalo linampendeza sana. Kisha fungua somo alilochagua, na umwonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyofanywa. Fanya mipango ya kurudi ili mzungumzie swali linalofuata katika somo hilo.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Jaribu Njia ya Moja kwa Moja:

● “Nimekutembelea kifupi ili kukueleza kuhusu mtaala mpya wa kujifunza Biblia. Broshua hii ina masomo 15 yanayoonyesha ni wapi katika Biblia unapoweza kupata majibu ya maswali muhimu sana. [Mwonyeshe ukurasa wa kwanza na wa mwisho.] Je, umewahi kujaribu kuielewa Biblia? [Mruhusu ajibu.] Acha nikuonyeshe jinsi masomo haya yalivyo rahisi. [ Zungumzia fungu la kwanza la swali la 3 katika somo la 3, na usome Ufunuo 21:4, 5. Ikiwa inafaa, zungumzia fungu linalofuata na maandiko yaliyoandikwa “soma.”] Ukipenda, ninaweza kukuachia broshua hii. Tunapendekeza ujaribu kujifunza Biblia angalau mara moja kwa kutumia njia hii. Ukipenda, unaweza kuendelea. Wakati ujao, tunaweza kuchunguza somo la kwanza. Ona kwamba somo hilo liko katika ukurasa mmoja tu.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Itumie Katika Ziara ya Kurudia:

● Tunapomrudia mtu aliyependezwa, tunaweza kusema: “Ninafurahi kukuona tena. Nimekuletea broshua hii inayojibu maswali mengi yenye kupendeza ya Biblia. [Mpe broshua, na umwombe atazame ukurasa wa nyuma.] Ni habari gani kati ya hizi inayokuvutia zaidi? [Mruhusu ajibu. Kisha fungua kwenye somo alilochagua.] Acha nikuonyeshe jinsi broshua hii inavyoweza kutumiwa kupata majibu ya Biblia.” Mwonyeshe jinsi funzo linavyofanywa kwa kuzungumzia fungu moja au mawili na maandiko yaliyoandikwa “soma.” Hebu wazia jinsi ilivyo rahisi kuanzisha Funzo la Biblia! Mwachie mwenye nyumba broshua na ufanye mipango ya kurudi. Unapomaliza somo hilo, unaweza kuzungumzia somo lingine ambalo mwenye nyumba amechagua au uanze mwanzoni mwa broshua.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki