SOMO LA 11
Zungumza kwa Hisia
HISIA ni sehemu ya msingi ya maisha ya wanadamu. Mtu anapoongea kwa hisia, anafunua yaliyo moyoni mwake, utu wake wa ndani, na maoni yake kuhusu hali na watu. Watu wengi huficha hisia zao kwa sababu ya magumu ambayo wamepata maishani na nyakati nyingine kwa sababu ya malezi yao. Lakini Yehova anatuhimiza tukuze sifa njema katika utu wetu wa ndani kisha tuonyeshe hisia zinazolingana na sifa hizo.—Rom. 12:10; 1 The. 2:7, 8.
Tunapoongea, maneno yetu yanaweza kuonyesha hisia zetu za kweli. Lakini ikiwa maneno yetu hayaambatani na hisia inayofaa, wale wanaotusikiliza wanaweza kutilia shaka unyofu wetu. Kwa upande mwingine, maneno yakiandamana na hisia inayofaa, usemi wetu unaweza kuvutia sana na kujaa hisia zinazoweza kugusa mioyo ya wale wanaotusikiliza.
Kuonyesha Huruma. Mara nyingi huruma huhusiana na mawazo kuhusu watu. Basi, tunapoongea juu ya sifa za Yehova zenye kupendeza na tunapoonyesha jinsi tunavyothamini wema wa Yehova, sauti yetu ionyeshe huruma hiyo. (Isa. 63:7-9) Na tunapoongea na watu wengine, njia yetu ya kuongea ionyeshe huruma.
Mtu fulani mwenye ukoma amjia Yesu ili aponywe. Ebu wazia sauti ya Yesu anaposema: “Nataka. Fanywa safi.” (Mk. 1:40, 41) Pia wazia hali hii: Mwanamke fulani ambaye ametoka damu kwa miaka 12 amjia Yesu kimya-kimya kutoka nyuma na kugusa upindo wa vazi lake la nje. Mwanamke huyo anapotambua kwamba amegunduliwa, yuaja mbele akitetemeka, aanguka miguuni pa Yesu, na kufichua hadharani sababu ambayo imemfanya aguse vazi lake na jinsi ambavyo ameponywa. Wazia jinsi Yesu anavyomwambia: “Binti, imani yako imekufanya upone; shika njia yako uende katika amani.” (Luka 8:42b-48) Huruma ambayo Yesu alionyesha pindi hizo inagusa mioyo yetu hadi leo hii.
Tukiwahurumia watu kama Yesu na iwapo kweli tunataka kuwasaidia, tutaongea nao kwa njia ya huruma. Huruma kama hiyo ni ya kweli, na si yenye kupita kiasi. Huruma tunayoonyesha inaweza kusaidia sana wengine wasikilize. Mambo mengi tunayosema katika huduma ya shambani ni yale ambayo hutajwa kwa njia ya wororo, hasa tunaposababu na wengine, tunapowatia moyo, tunapowahimiza, na tunapowahurumia.
Ikiwa unapenda wengine, basi uso wako uonyeshe hivyo. Unapoonyesha uchangamfu, wasikilizaji wanavutiwa kama ambavyo watu huvutiwa na moto katika usiku wenye baridi. Ikiwa uso wako hauonyeshi uchangamfu, wasikilizaji wanaweza kufikiri kwamba huwajali. Huwezi kujifanya eti wewe ni mchangamfu—ni lazima uchangamfu utoke moyoni.
Pia sauti yako inapasa kuonyesha hisia. Kama una sauti kali yenye kukwaruza, inaweza kuwa vigumu kuonyesha hisia unapoongea. Lakini unaweza kufaulu ukitia bidii kwa muda fulani. Jambo moja ambalo linaweza kusaidia ni kukumbuka kwamba maneno mafupi-mafupi ya haraka-haraka hufanya usemi usiwe na hisia. Jifunze kuvuta zaidi sauti nyororo katika maneno. Hiyo itakusaidia kuonyesha hisia unapoongea.
Lakini jambo muhimu hata zaidi ni kile unachokazia akili. Ikiwa kweli unakazia akili wasikilizaji na kutamani kuwaambia jambo linaloweza kuwafaidi, maneno yako yataonyesha hisia hiyo.
Hotuba changamfu huchochea, lakini inahitaji hisia ya upendo. Haitoshi tu kuchochea akili; ni lazima tuchochee moyo pia.
Kuonyesha Hisia Nyinginezo. Mtu anayesononeka anaweza kuonyesha hisia kama wasiwasi, woga, na kushuka moyo. Shangwe ni hisia ambayo tunapaswa kuonyesha sana katika maisha yetu na tunapoongea na wengine. Lakini kuna hisia ambazo tunahitaji kudhibiti. Hisia hizo hazifai utu wa Kikristo. (Efe. 4:31, 32; Flp. 4:4) Maneno tunayotumia, sauti tunayotumia, mkazo tunaotumia tunapozungumza, uso wetu, na ishara zetu zinaweza kuonyesha hisia mbalimbali.
Biblia inataja hisia nyingi za wanadamu. Nyakati nyingine inataja hisia hizo moja kwa moja. Na nyakati nyingine inasimulia matukio au kunukuu maneno yanayoonyesha hisia hizo. Sauti yako ikionyesha hisia hizo unaposoma kwa sauti, habari hiyo itakuvutia zaidi na kuwavutia wasikilizaji. Ili ufaulu, jiweke katika hali za wale unaosoma habari zao. Hata hivyo jihadhari usipite kiasi unaposoma kwa sababu hotuba si tamasha. Fanya maandiko unayosoma yawe halisi akilini mwa wasikilizaji.
Hisia Ifae Habari Unayozungumzia. Kama ilivyo na shauku, hisia unazoonyesha hutegemea sana mambo unayosema.
Ebu fungua Mathayo 11:28-30, utazame maneno yake. Kisha soma jinsi Yesu alivyowashutumu waandishi na Mafarisayo katika Mathayo sura ya 23. Haiwezekani kwamba aliwashutumu vikali kwa sauti dhaifu na nyonge.
Unafikiri ni hisia ipi inayofaa kutumiwa kusoma masimulizi kama ya Mwanzo sura ya 44 kuhusu sihi ya Yuda kwa niaba ya ndugu yake Benyamini? Ebu ona hisia inayoonyeshwa katika mstari wa 13, na jinsi inavyoonekana Yuda alihisi katika mstari wa 16 kuhusu sababu ya msiba huo, na jinsi Yosefu mwenyewe alivyohisi katika Mwanzo 45:1.
Basi, ili tufaulu tunapoongea au kusoma, mbali na kufikiria maneno tutakayotumia ni lazima pia tufikirie hisia tunazopaswa kuonyesha.