Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 1 kur. 6-12
  • “Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Nendeni Mkafanye Wanafunzi”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kazi Ambayo Ingefanywa Ulimwenguni Pote
  • Muhtasari wa Kitabu cha Matendo
  • Kitabu Kitakachotusaidia Kujifunza Biblia
  • Kitabu Cha Biblia 44—Matendo
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • “Mpaka Sehemu ya Mbali Zaidi ya Dunia”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Mashahidi Wajasiri wa Yehova Wafanya Vitendo!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Mashahidi wa Kikristo wa Yehova Katika Karne ya Kwanza
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 1 kur. 6-12

SURA YA 1

“Nendeni Mkafanye Wanafunzi”

Muhtasari wa kitabu cha Matendo ya Mitume na jinsi tunavyoweza kunufaika kutokana na habari zilizomo

1-6. Simulia jambo lililoonwa linaloonyesha Mashahidi wa Yehova wakihubiri katika hali mbalimbali.

MSICHANA mmoja nchini Ghana, anayeitwa Rebecca, aliiona shule yao kuwa eneo lake la kuhubiri. Sikuzote alibeba vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia alipoenda shuleni. Aliwahubiria wanafunzi wenzake wakati wa mapumziko, na alijifunza Biblia na wanafunzi kadhaa wa darasa lake.

2 Kwenye kisiwa cha Madagaska chenye joto jingi, mapainia wawili walitembea kilomita 25 kwenda kuwafundisha Biblia watu kadhaa waliopendezwa ambao waliishi katika kijiji fulani kilicho mbali.

3 Wakiwa na lengo la kuwahubiria watu wanaoishi kandokando ya mto Paraguai na mto Paraná, Mashahidi nchini Paraguai pamoja na Mashahidi wengine 15 kutoka katika nchi nyingine walitengeneza mashua. Mashua hiyo inaweza kubeba watu 12. Wahubiri wa Ufalme wenye bidii walitumia mashua hiyo kutangaza habari njema kwenye maeneo yasiyofikika kwa urahisi.

4 Kwa kawaida, Alaska hupata watalii wengi wakati wa kiangazi. Mashahidi walitumia wakati huo kuwahubiria. Meli zilizobeba watalii kutoka katika nchi mbalimbali zinapotia nanga bandarini, Mashahidi wenyeji huwa tayari kuwapa wageni hao vitabu na magazeti ya Biblia ya lugha mbalimbali. Katika eneo hilohilo, akina ndugu husafiri kwa ndege hadi vijiji vya mbali kwenda kuwatangazia habari njema watu wa jamii za Aleut, Athabascan, Tsimshian, na Tlingit.

5 Larry aliishi katika jimbo la Texas nchini Marekani. Aliyaona makao aliyoishi ya kuwatunzia wazee kuwa eneo lake la kuhubiri. Alikuwa na bidii sana licha ya kutumia kiti cha magurudumu tangu alipopata aksidenti. Aliwahubiria wengine habari njema ya Ufalme, kutia ndani tumaini lake la kutembea tena wakati ujao, Ufalme wa Mungu utakapotawala.​—Isa. 35:5, 6.

6 Akina ndugu na dada walifunga safari ya siku tatu kwa meli kwenda kuhudhuria kusanyiko katika eneo la kaskazini nchini Myanmar. Wakiwa na lengo la kuhubiri habari njema, walibeba vitabu na magazeti yanayotegemea Biblia na kuwapa abiria wenzao. Kila mara meli hiyo ilipotia nanga katika bandari ya mji au kijiji fulani, wahubiri hao wenye bidii walishuka na bila kupoteza wakati walienda popote watu walipokuwa na kuanza kuwapa vitabu na magazeti. Wakati wa kuondoka ulipofika, kulikuwa na abiria wapya katika meli waliofanyiza “eneo jipya.”

7. Ni njia gani mbalimbali zinazotumiwa na waabudu wa Yehova kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu, nao wana lengo gani?

7 Kama ndugu na dada waliotajwa katika mafungu yaliyopita, waabudu wenye bidii wa Yehova ulimwenguni pote, ‘wanatoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.’ (Mdo. 28:23) Wanahubiri nyumba kwa nyumba, barabarani, kwa njia ya barua, na kupitia simu. Iwe wanasafiri, wanatembea katika bustani, au wanapumzika, wao hutumia kila nafasi wanayopata kuhubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Huenda njia wanazotumia zikatofautiana, lakini wana lengo moja, kuhubiri habari njema popote ambapo watu wanaweza kupatikana.​—Mt. 10:11.

8, 9. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba ongezeko katika kazi ya kuhubiri Ufalme ni muujiza? (b) Ni swali gani linalojitokeza, na tunaweza kupata jibu jinsi gani?

8 Msomaji mpendwa, je, wewe ni mmoja wa wahubiri hao wanaotangaza Ufalme katika nchi zaidi ya 235? Ikiwa ndivyo, unachangia ongezeko lenye kusisimua katika kazi hiyo ya kuhubiri Ufalme! Kile ambacho kimetimizwa ulimwenguni pote ni muujiza. Ingawa wanakabili upinzani na hali nyingine ngumu, kutia ndani marufuku na mateso ya moja kwa moja, Mashahidi wa Yehova wanaendelea kuwatolea watu wa mataifa yote ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu.

9 Huenda mtu akauliza hivi: Kwa nini hakuna kizuizi wala upinzani wowote ambao umezuia kazi ya kuhubiri Ufalme? Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova leo wanaendeleza kazi iliyoanzishwa katika karne ya kwanza, kuchunguza jinsi hali ilivyokuwa wakati huo kunaweza kutusaidia kupata jibu la swali hilo.

Kazi Ambayo Ingefanywa Ulimwenguni Pote

10. Kazi kuu katika maisha ya Yesu ilikuwa nini, naye alijua nini?

10 Yesu Kristo, Mwanzilishi wa kutaniko la Kikristo, alihubiri kwa bidii habari njema ya Ufalme wa Mungu; hiyo ilikuwa kazi kuu maishani mwake. Alisema hivi: “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Yesu alijua kwamba kazi aliyoianzisha hangeweza kuimaliza peke yake. Muda mfupi kabla ya kufa, Yesu alitabiri kwamba ujumbe wa Ufalme utahubiriwa “katika mataifa yote.” (Marko 13:10) Kazi hiyo ingefanywa jinsi gani, na ingefanywa na nani?

Yesu akiongea na kikundi cha wanafunzi wake.

“Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”​—Mathayo 28:19

11. Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi gani muhimu, na wangetegemezwa jinsi gani?

11 Alipofufuka, Yesu aliwatokea wanafunzi wake na kuwapa kazi muhimu: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru. Na tazama! mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mt. 28:19, 20) Maneno hayo, “nipo pamoja nanyi,” yanaonyesha kwamba Yesu angewategemeza wanafunzi wake katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Walihitaji utegemezo huo kwa sababu, kama Yesu alivyokuwa ametabiri, ‘wangechukiwa na mataifa yote.’ (Mt. 24:9) Pia, wanafunzi hao wangepata utegemezo kutoka katika chanzo kingine. Kabla tu ya kurudi mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba roho takatifu ingewapa nguvu, nao wangekuwa mashahidi wake “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”​—Mdo. 1:8.

12. Ni maswali gani yanayozuka, na kwa nini majibu yake ni muhimu?

12 Hata hivyo, maswali muhimu yanajitokeza: Je, mitume wa Yesu na wale wanafunzi wengine wa karne ya kwanza waliuchukua mgawo wao kwa uzito? Je, walitoa ushahidi kikamili kuhusu Ufalme wa Mungu hata walipoteswa vikali? Je, kweli walitegemezwa na Yehova, Yesu Kristo, na malaika katika kazi yao ya kufanya wanafunzi? Maswali hayo na mengine mengi yanajibiwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo. Majibu ya maswali hayo ni muhimu kwetu. Kwa nini? Yesu alisema kwamba kazi aliyowapa wanafunzi wake ingeendelea “mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Hivyo, kazi hiyo ingefanywa na Wakristo wote wa kweli, kutia ndani sisi tunaoishi wakati huu wa mwisho. Ndiyo maana tunapendezwa sana na masimulizi hayo ya kihistoria yaliyo katika kitabu cha Matendo.

Muhtasari wa Kitabu cha Matendo

13, 14. (a) Kitabu cha Matendo kiliandikwa na nani, naye alipata habari hizo jinsi gani? (b) Kitabu cha Matendo kinazungumzia nini?

13 Ni nani aliyeandika kitabu cha Matendo? Kitabu hicho hakisemi kiliandikwa na nani, hata hivyo, mistari michache ya kwanza inaonyesha kwamba mwandikaji wa kitabu hicho ndiye aliyeandika pia Injili ya Luka. (Luka 1:1-4; Mdo. 1:1, 2) Hivyo, tangu zamani, wengi wameamini kwamba kitabu cha Matendo kiliandikwa na Luka, yule “daktari mpendwa” ambaye pia alikuwa mwanahistoria makini. (Kol. 4:14) Kitabu hicho kinazungumzia matukio ya kipindi cha miaka 28 hivi, tangu Yesu aliporudi mbinguni mwaka wa 33 W.K., mpaka karibu mwaka wa 61 W.K. Paulo alipokuwa kifungoni huko Roma. Inaonekana kwamba katika mengi ya matukio anayosimulia katika kitabu cha Matendo, Luka alikuwapo kwa kuwa anatumia maneno yanayomhusisha. (Mdo. 16:8-10; 20:5; 27:1) Kwa sababu alipenda kufanya utafiti wake kwa uangalifu, bila shaka Luka alipata habari moja kwa moja kutoka kwa Paulo, Barnaba, Filipo, na wengine wanaotajwa kwenye masimulizi yake.

14 Ni mambo gani yanayozungumziwa katika kitabu cha Matendo? Katika Injili aliyoiandika mapema, Luka aliandika kuhusu mambo ambayo Yesu alisema na kufanya. Hata hivyo, katika kitabu cha Matendo, Luka anaandika kuhusu mambo ambayo wafuasi wa Yesu walisema na kufanya. Hivyo, kitabu cha Matendo kinazungumzia watu waliotimiza kazi kubwa, ijapokuwa wengi wao walionwa kuwa watu “wasio na elimu na wa kawaida tu.” (Mdo. 4:13) Kwa ufupi, kitabu hicho kinasimulia mwanzo na ukuzi wa kutaniko la Kikristo. Kinaeleza jinsi Wakristo wa karne ya kwanza walivyohubiri na mtazamo waliokuwa nao. (Mdo. 4:31; 5:42) Pia, kinaonyesha jinsi roho takatifu ilivyowasaidia Wakristo hao kueneza habari njema. (Mdo. 8:29, 39, 40; 13:1-3; 16:6; 18:24, 25) Kitabu cha Matendo kinakazia kichwa kikuu cha Biblia, kinachohusu kutakaswa kwa jina la Mungu kupitia Ufalme wake chini ya Kristo, na pia kinaonyesha jinsi habari njema kuhusu Ufalme huo ilivyohubiriwa licha ya upinzani mkali.​—Mdo. 8:12; 19:8; 28:30, 31.

15. Tutapata manufaa gani kwa kuchunguza kitabu cha Matendo?

15 Kwa kweli, habari zilizo katika kitabu cha Matendo zinavutia na kujenga imani! Kutafakari ujasiri na bidii ambayo wafuasi wa Kristo walionyesha katika karne ya kwanza, kutatuchochea. Tutachochewa kuiga imani yao, nasi tutakuwa tayari kutimiza kazi tuliyopewa ya kufanya wanafunzi. Kitabu hiki kitakusaidia kunufaika na habari zilizo katika kitabu cha Matendo.

Kitabu Kitakachotusaidia Kujifunza Biblia

16. Kitabu hiki kitatimiza mambo gani matatu?

16 Kitabu hiki kitatimiza nini? Kusudi la kitabu hiki ni (1) kutusadikisha kwamba Yehova anatumia roho yake takatifu kutegemeza kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, (2) kutuchochea kuwaiga wafuasi wa Kristo wa karne ya kwanza kwa kuwa na bidii katika kazi yetu ya kuhubiri, na (3) kulithamini zaidi tengenezo la Yehova na wale wanaoongoza makutaniko na kusimamia kazi ya kuhubiri.

17, 18. Eleza mpangilio wa kitabu hiki, na jinsi kitakavyoboresha funzo la Biblia la kibinafsi.

17 Kitabu hiki kimegawanywa katika sehemu nane zinazozungumzia sehemu mbalimbali za kitabu cha Matendo. Sura zinazofuata hazizungumzii kitabu cha Matendo mstari kwa mstari, badala yake zinazungumzia mambo mbalimbali tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi ya kitabu hicho cha Biblia na kutusaidia kuona jinsi tunavyoweza kuyatumia maishani. Mwanzoni mwa kila sura kuna maelezo mafupi yanayoonyesha mambo yanayozungumziwa katika sura hiyo na mistari ya kitabu cha Matendo inayozungumziwa.

18 Kitabu hiki kina mengi yanayoweza kuboresha funzo letu la Biblia la kibinafsi. Kina picha nzuri zinazoonyesha matukio yenye kusisimua katika kitabu cha Matendo. Picha hizo zitakusaidia kuwazia akilini masimulizi hayo ya Biblia. Sura kadhaa zina masanduku yenye habari za ziada. Masanduku fulani yanazungumzia watu mbalimbali wanaotajwa katika Biblia ambao tunaweza kuiga imani yao. Mengine yana habari za ziada kuhusu maeneo, matukio, desturi, au watu wengine wanaotajwa katika kitabu cha Matendo.

Ndugu akiwaonyesha wenzi wa ndoa eneo la kuhubiri.

Unapohubiri kumbuka kwamba maisha ya watu yako hatarini

19. Mara kwa mara tunaweza kujiuliza maswali gani yatakayotusaidia kujichunguza?

19 Kitabu hiki kinaweza kukusaidia kujichunguza. Hata iwe umekuwa mhubiri wa Ufalme kwa muda gani, ni vizuri mara kwa mara kutua na kuchanganua mambo unayotanguliza maishani na jinsi unavyoiona huduma ya Kikristo. (2 Kor. 13:5) Jiulize: ‘Bado ninaiona huduma yangu kuwa muhimu maishani? (1 Kor. 7:29-31) Ninahubiri habari njema kwa usadikisho na bidii? (1 The. 1:5, 6) Ninafanya yote niwezayo ili kuhubiri na kufanya wanafunzi?’​—Kol. 3:23.

20, 21. Kwa nini kazi yetu ni ya maana sana, nasi tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Sikuzote, tusisahau kwamba tunafanya kazi muhimu sana, kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Muda wa kufanya kazi hiyo unazidi kupungua. Mwisho wa mfumo huu unakaribia sana. Maisha ya watu wengi yako hatarini. Hatujui ni watu wangapi wenye mwelekeo unaofaa watakaoitikia ujumbe wetu. (Mdo. 13:48) Tuna daraka la kuwasaidia watu hao kabla ya mwisho kufika.​—1 Tim. 4:16.

21 Basi na tuige bidii ya wahubiri wa Ufalme wa karne ya kwanza. Unapozidi kusoma kitabu hiki na uchochewe kuhubiri kwa bidii na kwa ujasiri zaidi. Na uazimie kuendelea “kutoa ushahidi kamili kuhusiana na Ufalme wa Mungu.”​—Mdo. 28:23.

MIAKA YA MATUKIO MUHIMU KATIKA KUENEA KWA UKRISTO KATIKA KARNE YA KWANZA

  1. Mwaka wa 33

    Yesu afufuliwa

    Yesu awapa wafuasi wake agizo la kufanya wanafunzi

    Wanafunzi wapokea roho takatifu siku ya Pentekoste

    Kutaniko la Kikristo laanzishwa

  2. Mwaka wa 33-34 hivi

    Stefano auawa

    Towashi Mwethiopia abatizwa

  3. Mwaka wa 34 hivi

    Sauli wa Tarso awa Mkristo

  4. Mwaka wa 34-36 hivi

    Sauli ahubiri Damasko

  5. Mwaka wa 36 hivi

    Paulo awa mfuasi wa Kristo, aenda Yerusalemu

    Paulo amtembelea Petro huko Yerusalemu (Gal. 1:18)

  6. Mwaka wa 36

    Kornelio awa Mkristo

    Watu wa kwanza wa mataifa waanza kuwa Wakristo

  7. Mwaka wa 41 hivi

    Injili ya Mathayo yaandikwa

    Paulo anaona “mbingu ya tatu” katika maono (2 Kor. 12:2)

  8. Mwaka wa 44 hivi

    Agabo atabiri kuhusu njaa

    Yakobo (mwana wa Zebedayo) auawa

    Petro afungwa, afunguliwa kimuujiza

  9. Mwaka wa 44

    Herode Agripa wa Kwanza anakufa

  10. Mwaka wa 46 hivi

    Njaa iliyotabiriwa yatokea

    Paulo apeleka huduma ya misaada Yerusalemu

  11. Mwaka wa 47-48 hivi

    Safari ya kwanza ya umishonari ya Paulo

  12. Mwaka wa 49 hivi

    Suala la tohara lazuka Antiokia

    Mkutano wafanywa Yerusalemu

    Paulo ampinga Petro (Gal. 2:11-14)

  13. Mwaka wa 49-52 hivi

    Safari ya pili ya umishonari ya Paulo

    Barnaba na Marko wahubiri Kipro

  14. Mwaka wa 49-50 hivi

    Klaudio awafukuza Wayahudi waliokuwa Roma

  15. Mwaka wa 50 hivi

    Luka ajiunga na Paulo huko Troa

    Paulo amwona mwanamume Mmakedonia katika maono

    Paulo anatembelea Filipi

    Kutaniko la Filipi laanzishwa

    Kutaniko la Thesalonike laanzishwa

    Paulo anatembelea Athene

  16. Mwaka wa 50-52 hivi

    Paulo anatembelea Korintho

    Kitabu cha Kwanza cha Wathesalonike chaandikwa

    Kitabu cha Wagalatia chaandikwa

  17. Mwaka wa 51 hivi

    Kitabu cha Pili cha Wathesalonike chaandikwa

  18. Mwaka wa 52-56 hivi

    Safari ya tatu ya umishonari ya Paulo

  19. Mwaka wa 52-55 hivi

    Paulo anatembelea Efeso

  20. Mwaka wa 55 hivi

    Kitabu cha Kwanza cha Wakorintho chaandikwa

    Tito atumwa Korintho

    Kitabu cha Pili cha Wakorintho chaandikwa

  21. Mwaka wa 56 hivi

    Kitabu cha Waroma chaandikwa

    Paulo amfufua Eutiko huko Troa

    Paulo na Luka wakaa nyumbani kwa Filipo huko Kaisaria

    Paulo akamatwa huko Yerusalemu

  22. Mwaka wa 56-58 hivi

    Paulo afungwa Kaisaria

    Injili ya Luka yaandikwa

  23. Mwaka wa 58 hivi

    Festo awa gavana badala ya Feliksi

  24. Mwaka wa 58

    Herode Agripa wa Pili amsikiliza Paulo

  25. Mwaka wa 59-61 hivi

    Paulo afungwa Roma kwa mara ya kwanza

  26. Mwaka wa 60-61 hivi

    Kitabu cha Wakolosai chaandikwa

    Kitabu cha Waefeso chaandikwa

    Kitabu cha Filemoni chaandikwa

    Kitabu cha Wafilipi chaandikwa

  27. Mwaka wa 60-65 hivi

    Injili ya Marko yaandikwa

  28. Mwaka wa 61 hivi

    Kitabu cha Matendo chaandikwa

    Kitabu cha Waebrania chaandikwa

  29. Mwaka wa 61-64 hivi

    Kitabu cha Kwanza cha Timotheo chaandikwa

    Tito abaki Krete (Tito 1:5)

    Kitabu cha Tito chaandikwa

  30. Kabla ya mwaka wa 62

    Kitabu cha Yakobo chaandikwa

  31. Mwaka wa 62-64 hivi

    Kitabu cha Kwanza cha Petro chaandikwa

  32. Mwaka wa 64 hivi

    Kitabu cha Pili cha Petro chaandikwa

  33. Mwaka wa 65 hivi

    Paulo afungwa Roma kwa mara ya pili

    Kitabu cha Pili cha Timotheo chaandikwa

    Tito aenda Dalmatia (2 Tim. 4:10)

    Paulo auawa

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki