Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 41 uku. 226-uku. 229 fu. 1
  • Usemi Unaoeleweka

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Usemi Unaoeleweka
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Habari Inayoeleweka
    Boresha Uwezo Wako wa Kusoma na Kufundisha
  • Kuwaelimisha Wasikilizaji
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kutayarisha Hotuba za Watu Wote
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Fundisha kwa Njia Rahisi
    Huduma ya Ufalme—2009
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 41 uku. 226-uku. 229 fu. 1

SOMO LA 41

Usemi Unaoeleweka

Unahitaji kufanya nini?

Zungumza kwa njia inayoeleweka kwa urahisi.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Kadiri usemi wako unavyoeleweka kwa urahisi ndivyo wasikilizaji wanavyofaidika.

KUZUNGUMZA si kutoa tu habari. Jaribu kufanya usemi wako ueleweke. Hiyo inaweza kufanya maneno yako yaeleweke vizuri iwe unahutubia kutaniko au unazungumza na watu ambao si Mashahidi.

Kuna mambo mengi yanayohusiana na usemi unaoeleweka. Baadhi ya mambo hayo yako katika Somo la 26 “Habari Inayofuatana Vizuri.” Mambo mengine yako katika Somo la 30 “Kupendezwa na Wengine.” Tutazungumzia mambo mengine machache katika somo hili.

Tumia Maneno Rahisi, Zungumza kwa Njia Rahisi. Maneno rahisi na sentensi fupi-fupi hufanya mtu aeleweke kwa urahisi. Mahubiri ya Yesu ya Mlimani ni mfano mzuri sana wa hotuba ambayo mtu yeyote anaweza kuelewa hata iwe anaishi wapi. Huenda Yesu alitaja mambo mapya. Lakini waliyaelewa kwa sababu alizungumzia mambo yanayotuhusu sisi sote. Alitaja jinsi ya kuwa mwenye furaha, jinsi ya kuboresha mahusiano na wengine, jinsi ya kukabiliana na mahangaiko, na jinsi ya kufanya maisha yawe na maana zaidi. Na alitumia lugha rahisi sana. (Mt., sura ya 5-7) Biblia ina mifano mingi ya sentensi za aina mbalimbali na zenye urefu tofauti-tofauti. Basi kusudi lako kuu liwe kuzungumza kwa njia inayoeleweka vizuri.

Hata kama unazungumzia habari ngumu, inaweza kueleweka kwa urahisi ukizungumza kwa njia rahisi. Unawezaje kueleweka kwa urahisi? Usiwalemee wasikilizaji kwa mambo madogo-madogo yasiyo muhimu. Panga habari kwa njia inayoingiana vizuri na mambo makuu. Chagua kwa makini maandiko makuu ambayo utatumia. Badala ya kukimbia kutoka andiko moja hadi jingine, soma maandiko na kuyafafanua. Usifunike wazo zuri kwa maneno mengi mno.

Tumia kanuni hizo hata unapoongoza funzo la Biblia la nyumbani. Usijaribu kuelezea kila jambo dogo. Msaidie mwanafunzi aelewe vizuri mawazo makuu. Baadaye, anaweza kujazia mambo mengine katika funzo la kibinafsi na mikutano ya kutaniko.

Ili utoe hotuba kwa njia iliyo rahisi kueleweka, unahitaji kujitayarisha vizuri. Kwanza, ni lazima uelewe vizuri jambo unalozungumzia ikiwa utawasaidia wengine walielewe. Unapoelewa jambo fulani vizuri, unaweza kutoa sababu zinazolithibitisha. Pia unaweza kufafanua jambo hilo kwa maneno yako mwenyewe.

Fafanua Maneno Yasiyoeleweka. Nyakati nyingine tunahitaji kueleza maana ya maneno ambayo wasikilizaji hawaelewi. Usidhani wasikilizaji wanajua mambo mengi sana, wala usidhani hawajui jambo lolote. Kwa sababu ya kujifunza Biblia, huenda ukatumia maneno ambayo watu wengine hawaelewi vizuri. Wale ambao hawashirikiani na Mashahidi wa Yehova hawawezi kuelewa kwamba maneno kama “mabaki,” “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” “kondoo wengine,” na “umati mkubwa” yanarejelea vikundi fulani vya watu usipoyafafanua. (Rom. 11:5; Mt. 24:45; Yn. 10:16; Ufu. 7:9) Hali kadhalika, mtu asiyejua tengenezo la Mashahidi wa Yehova huenda asielewe maneno kama “mhubiri,” “painia,” “mwangalizi wa mzunguko,” na “Ukumbusho.”

Huenda ikafaa kufafanua maneno mengine ya Biblia ambayo pia hutumiwa sana na hata watu ambao si Mashahidi. Watu wengi wanafikiri “Har-magedoni” inamaanisha maafa ya nyuklia. Wanaweza kufikiri “Ufalme wa Mungu” ni hali fulani iliyo ndani ya mtu au wafikiri unahusiana na mbingu wala si serikali. Wengine wakisikia neno “nafsi,” wanaweza kufikiria sehemu fulani ya kiroho ya binadamu ambayo huendelea kuishi baada ya mwili kufa. Mamilioni ya watu wamefundishwa kwamba “roho takatifu” ni mtu, sehemu ya Utatu. Na kwa sababu watu wengi sana hawafuati kanuni za Biblia, wanaweza kuhitaji kusaidiwa kuelewa Biblia inamaanisha nini inaposema: “Ukimbieni uasherati.”—1 Kor. 6:18.

Watu ambao hawasomi Biblia kwa kawaida huenda wasikuelewe unaposema, “Paulo aliandika . . . ” au “Luka alisema . . . ” Labda rafiki zao au majirani wao wanaitwa hivyo. Inaweza kufaa kufafanua kidogo kwamba huyo ni mtume Mkristo au ni mwandishi wa Biblia.

Mara nyingi watu wa siku zetu wanahitaji kusaidiwa kuelewa maandiko yanayotaja vipimo au desturi za nyakati za kale. Kwa mfano, huenda wasielewe maneno yanayosema kwamba safina ya Noa ilikuwa urefu wa mikono 300, upana wa mikono 50, na kwenda juu mikono 30. (Mwa. 6:15) Lakini ukifafanua vipimo hivyo kwa njia zilizo rahisi kueleweka kwenu, wasikilizaji wataelewa mara moja ukubwa wa safina.

Eleza Mambo Magumu. Kufafanua tu jambo hakutoshi kuwafanya wasikilizaji walielewe vizuri. Katika siku za Ezra kule Yerusalemu, Sheria ilisomwa na kufafanuliwa. Ili watu waelewe maana ya Sheria, Walawi waliifafanua na kuonyesha jinsi ilivyohusu hali za watu wakati huo. (Neh. 8:8, 12) Vivyo hivyo, eleza maandiko unayosoma na kuonyesha jinsi yanavyotumika maishani.

Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu aliwaeleza wanafunzi wake kwamba tukio hilo lilitimiza Maandiko. Pia alikazia daraka lao wakiwa mashahidi wa mambo hayo. (Luka 24:44-48) Ukiwasaidia watu waone jinsi mambo ambayo wamefundishwa yanahusu maisha yao, watayaelewa kwa urahisi zaidi.

Jinsi Moyo Unavyohusika. Hata kama unafafanua mambo kwa njia ya wazi, kuna mambo mengine yanayomfanya mtu akuelewe au asikuelewe. Mtu mwenye moyo mgumu hawezi kupata maana ya mambo yanayosemwa. (Mt. 13:13-15) Watu ambao wameshikilia sana maoni ya kimwili huona mambo ya kiroho kuwa upumbavu tu. (1 Kor. 2:14) Mtu akiwa na roho kama hiyo, huenda likawa jambo la hekima kumaliza mazungumzo hayo angalau kwa wakati huo.

Lakini mioyo ya wengine huwa migumu kwa sababu ya magumu ya maisha. Na moyo wa mtu kama huyo unaweza kukubali mambo akisikia kweli ya Biblia kwa kipindi fulani. Yesu alipowaambia mitume wake kwamba angechapwa na kuuawa, hawakuelewa. Kwa nini? Hawakutarajia mambo hayo wala hawakutaka yatukie! (Luka 18:31-34) Lakini baada ya muda, wale mitume 11 walionyesha kwamba wamemwelewa Yesu kwa kufuata mambo aliyowafundisha.

Matokeo ya Mfano Mzuri Tunaoweka. Mbali na kuwasaidia watu kuelewa mambo kupitia maneno yetu, matendo yetu vilevile yanasaidia. Watu wengi husema kwamba walipohudhuria Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza jambo wanalokumbuka zaidi ni upendo walioona wala si mambo waliyosikia. Hali kadhalika, furaha yetu imesaidia watu wengi kukubali kweli ya Biblia. Wengi wamekata kauli ya kwamba dini ya Mashahidi ndiyo ya kweli kwa sababu waliona upendo wenye fadhili ambao watu wa Yehova wameonyeshana na jinsi ambavyo wamewajali wale ambao wamepata misiba. Basi, unapojitahidi kuwasaidia watu waelewe kweli ya Biblia, fikiria jinsi unavyoifafanua na mfano ambao wewe mwenyewe unaweka.

JINSI YA KUFAULU

  • Tumia lugha rahisi; afadhali utumie sentensi fupi unapozungumzia mawazo makuu.

  • Kazia mambo machache makuu.

  • Fafanua maneno ambayo wasikilizaji hawaelewi vizuri.

  • Eleza maandiko na kuonyesha jinsi yanavyotumika.

  • Fikiria jinsi mfano wako unavyoweza kuwaathiri wasikilizaji.

MAZOEZI: Jaribu kumweleza mtu wa ukoo, jirani, mfanyakazi mwenzako, mwanafunzi mwenzako ambaye si Shahidi juu ya jambo ambalo ulifurahia juma hili kwenye mkutano wa kutaniko. Hakikisha unafafanua maneno ambayo huenda mtu haelewi.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki