Fundisha kwa Njia Rahisi
1. Taja jambo moja lililo muhimu katika kufundisha kwa njia inayoeleweka wazi.
1 Ni muhimu sana kurahisisha mambo tunapowafundisha watu. Tunaweza kufanya maendeleo katika ‘ufundi wetu wa kufundisha’ kwa kuzingatia jinsi Yesu, yule Mwalimu Mkuu, alivyofundisha.—2 Tim. 4:2; Yoh. 13:13.
2. Kufundisha kwa njia rahisi kunahusisha nini, na matokeo ni nini?
2 Eleza Mambo kwa Njia Rahisi: Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alieleza kwa njia rahisi sana baadhi ya kweli muhimu ambazo wanadamu wamewahi kufundishwa. (Mt., sura ya 5-7) Umati uliomsikiliza ‘ulishangazwa na njia yake ya kufundisha.’ Maofisa waliotumwa kumkamata Yesu waliguswa sana na maneno yake hivi kwamba walisema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Mt. 7:28, 29; Yoh. 7:46) Hatuhitaji kutumia maneno magumu au sentensi na mifano tata, ili kuwasadikisha watu kuhusu kweli. Kweli za Biblia zinaweza kuelezwa waziwazi kwa kutumia maneno ya kawaida ambayo watu wanaelewa.
3. Kwa nini baadhi ya wahubiri wanawafundisha watu mambo mengi mno, na tunaweza kuepukaje kufanya hivyo?
3 Usizungumzie Habari Nyingi Mno: Yesu aliwafikiria wasikilizaji wake alipoamua kiasi cha habari ambacho angewafundisha kwa wakati mmoja. (Yoh. 16:12) Tunahitaji kutambua uhitaji wa wale tunaoongea nao na kubadili mazungumzo kupatana na hali yao. Hili ni muhimu hasa tunapowahubiria watu wa ukoo, watoto, au wale ambao wameanza kupendezwa majuzi. Hatupaswi kuwafundisha mambo mengi mno, hata wanapoonekana kusikiliza kwa makini. Wale walio na moyo mweupe wataendelea kujifunza kumhusu Mungu wa kweli, Yehova.—Yoh. 17:3; 1 Kor. 3:6.
4. Kwa nini ni muhimu kukazia mambo makuu badala ya kuzungumzia mambo mengi madogo-madogo?
4 Kazia Mambo Makuu: Yesu hakufanya mambo aliyofundisha yawe magumu kueleweka kwa kuzungumzia habari nyingi mno. Aliposema: ‘Wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watatoka,’ hakueleza kwa undani kuhusu tumaini la waliotenda mema, au hukumu ya waliotenda mabaya, ambao watafufuliwa. (Yoh. 5:28, 29) Tunapoongoza mafunzo ya Biblia, tunapaswa kukazia mambo makuu na kujizuia tusizungumzie habari zisizo muhimu ambazo hazimo katika kitabu cha funzo.
5. Huenda tukapata baraka gani tukifundisha kwa njia rahisi?
5 Tunashukuru sana kwamba Yehova ametufundisha kwa njia rahisi yote tunayohitaji kujua! (Mt. 11:25) Na tujitahidi sana kufundisha kwa njia rahisi na hivyo kupata shangwe inayotokana na kuwa na matokeo mazuri katika huduma.