Mapendekezo Matatu ya Kuboresha Ufundishaji Wako
1. Kwa nini tunapaswa kutafuta njia za kuboresha ufundishaji wetu?
1 Wahudumu wote Wakristo ni walimu. Tunafundisha watu tunapowahubiria watu kwa mara ya kwanza, tunaporudi ili kuendeleza upendezi, au tunapoongoza funzo la Biblia. Na ujumbe tunaofundisha ni wa pekee. Tunaangaza nuru ya “maandishi matakatifu,” yanayoweza kuwafanya watu wawe wenye “hekima kwa ajili ya wokovu.” (2 Tim. 3:15) Hilo ni pendeleo kubwa kama nini! Yafuatayo ni mapendekezo matatu yatakayotusaidia kuboresha ufundishaji wetu.
2. Tunawezaje kufundisha kwa njia rahisi?
2 Rahisisha Habari: Tunapoielewa vizuri habari fulani, ni rahisi kusahau kwamba inaweza kuwa vigumu kwa mtu mwingine kuelewa habari hiyohiyo. Kwa hiyo, unapoongoza funzo la Biblia, usiongeze habari nyingi zisizo za lazima. Badala yake, kazia mambo makuu. Kuongea sana hakumaanishi unafundisha vizuri. (Met. 10:19) Kwa kawaida, ni vizuri zaidi kusoma tu maandiko yanayokazia jambo kuu. Baada ya kusoma andiko, kazia sehemu ya andiko inayohusiana na habari mnayozungumzia. Mahubiri ya Mlimani ambayo yamerekodiwa kwenye Mathayo sura ya 5 hadi ya 7, yanatia ndani kweli muhimu sana, na bado Yesu alifundisha kwa njia rahisi na alitumia maneno machache yaliyochaguliwa vizuri.
3. Mifano ina faida gani, na ni mifano ya aina gani iliyo bora zaidi?
3 Tumia Mifano: Mifano inachochea kufikiri, inasisimua, na hata inasaidia kukumbuka habari. Si lazima uwe msimuliaji wa hadithi ili ufundishe kwa kutumia mifano mizuri. Mara nyingi Yesu alitumia mifano mifupi iliyo rahisi kueleweka. (Mt. 7:3-5; 18:2-4) Kuchora picha kunaweza pia kusaidia sana. Kufanya matayarisho mapema kunaweza kukusaidia kufikiria mifano mizuri.
4. Tunaweza kutumiaje mifano kwa njia yenye mafanikio?
4 Tumia Maswali: Maswali yatamfanya mwanafunzi wako afikiri. Kwa hiyo, uwe mwenye subira baada ya kuuliza swali. Ikiwa utatoa jibu mara moja bila kumpa mwanafunzi nafasi ya kujibu, hutajua kabisa kile ambacho ameelewa. Iwapo atatoa jibu lisilo sahihi, huenda ikawa afadhali kutumia maswali ya ziada kumwongoza kwenye jibu sahihi, badala ya kumrekebisha. (Mt. 17:24-27) Bila shaka, hakuna yeyote kati yetu aliye mwalimu mkamilifu. Ndiyo sababu Biblia inatuhimiza tujiangalie daima jinsi tunavyofundisha. Kufanya hivyo kutaleta manufaa ya milele kwetu, na kwa wale wanaotusikiliza.—1 Tim. 4:16.