Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • od sura 6 kur. 53-58
  • Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu
  • Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SIFA ZA KIMAANDIKO ZA WATUMISHI WA HUDUMA
  • JINSI WANAVYOTUMIKIA
  • Watumishi wa Huduma Ni Baraka kwa Watu wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Watumishi wa Huduma Dumisheni Msimamo Mzuri!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
  • Kudumisha Upatano Kati ya Wazee na Watumishi wa Huduma
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
Pata Habari Zaidi
Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
od sura 6 kur. 53-58

SURA YA 6

Watumishi wa Huduma Hufanya Utumishi Muhimu

MTUME Paulo aliliandikia kutaniko la Filipi hivi: “Paulo na Timotheo, watumwa wa Kristo Yesu, kwa watakatifu wote katika muungano na Kristo Yesu walio huko Filipi, pamoja na waangalizi na watumishi wa huduma.” (Flp. 1:1) Ona kwamba aliwataja pia watumishi wa huduma. Wanaume hao kwa kweli walitimiza jukumu muhimu sana ili kuwasaidia wazee wakati huo. Ndivyo ilivyo leo. Watumishi wa huduma hufanya utumishi muhimu ambao unawasaidia wazee na kuchangia utaratibu mzuri katika kutaniko.

2 Je, unawajua watumishi wa huduma katika kutaniko lenu? Je, unajua kazi wanazofanya kwa faida yako na kutaniko zima? Bila shaka Yehova anathamini sana jitihada za wanaume hao. Paulo aliandika hivi: “Wanaume wanaohudumu vizuri wanajipatia sifa nzuri na uhuru mwingi wa kusema katika imani iliyo katika Kristo Yesu.”—1 Tim. 3:13.

SIFA ZA KIMAANDIKO ZA WATUMISHI WA HUDUMA

3 Watumishi wa huduma wanatarajiwa kuishi maisha ya Kikristo, wawe wanaume wenye kutegemeka wanaoshughulikia migawo yao kwa njia nzuri. Jambo hilo ni wazi tunapochunguza yale ambayo Paulo alisema kuhusu sifa zao katika barua yake kwa Timotheo: “Vilevile watumishi wa huduma wanapaswa kuchukua mambo kwa uzito, si wenye ndimi mbili, si wenye kunywa divai nyingi, si wenye pupa ya mapato yasiyo ya haki, wakiishika siri takatifu ya imani kwa dhamiri safi. Pia, wanapaswa kwanza kujaribiwa kama wanafaa; ndipo watumike wakiwa wahudumu, kwa kuwa hawana shtaka. Watumishi wa huduma wanapaswa kuwa waume wa mke mmoja, wanaosimamia vizuri watoto wao na nyumba zao wenyewe.” (1 Tim. 3:8-10, 12) Watumishi wa huduma wakishika viwango vya juu kutaniko litalindwa dhidi ya shutuma zinazoweza kutokea kuhusu wanaume wanaopewa majukumu ya pekee.

4 Iwe wao ni vijana au wana umri mkubwa watumishi wa huduma wanashiriki katika huduma kila mwezi. Wanamwiga Yesu kwa kuwa na bidii katika huduma. Kupitia bidii hiyo, wana maoni kama ya Yehova, ambaye anapenda watu waokolewe.—Isa. 9:7.

5 Wanaume wanaotumika wakiwa watumishi wa huduma huweka mfano mzuri kupitia mavazi, kujipamba, usemi, mtazamo, na mwenendo wao. Wana utimamu wa akili, sifa ambayo huwafanya waheshimiwe na wengine. Kwa kuongezea, wanachukua kwa uzito uhusiano wao na Yehova na mapendeleo yao ya utumishi kutanikoni.—Tito 2:2, 6-8.

6 Wanaume hao ‘wamejaribiwa kama wanafaa.’ Hata kabla ya kuwekwa rasmi, wamethibitika kuwa wanaume wenye bidii. Wameonyesha kwamba wanatanguliza masilahi ya Ufalme katika maisha yao na wanajitahidi kufikia mapendeleo yoyote ya utumishi wanayoweza kufikia. Kwa kweli wao huweka mfano mzuri kutanikoni.—1 Tim. 3:10.

JINSI WANAVYOTUMIKIA

7 Watumishi wa huduma hufanya utumishi mbalimbali kwa ajili ya ndugu na dada zao, na hivyo kuruhusu waangalizi kuwa na wakati wa kukazia fikira ufundishaji na majukumu ya uchungaji. Baraza la wazee linapowapa migawo watumishi wa huduma, hufikiria uwezo wa kila mmoja na mahitaji ya kutaniko.

Watumishi wa huduma hufanya utumishi mbalimbali kwa ajili ya ndugu na dada zao, na hivyo kuruhusu waangalizi kuwa na wakati wa kukazia fikira ufundishaji na majukumu ya uchungaji

8 Hebu fikiria baadhi ya kazi zao: Mtumishi wa huduma mmoja anaweza kupewa mgawo wa kushughulikia machapisho ili tupate machapisho kwa ajili yetu na kwa ajili ya huduma. Wengine hupewa mgawo wa kutunza hesabu za kutaniko au kutunza rekodi za maeneo. Baadhi yao hushughulikia maikrofoni, mfumo wa sauti, hutumikia wakiwa wakaribishaji na kuwasaidia wazee kwa njia mbalimbali. Kuna kazi nyingi inayohitaji kufanywa ili kudumisha na kusafisha Jumba la Ufalme, hivyo kwa kawaida watumishi wa huduma huombwa wasaidie kutimiza majukumu hayo.

9 Katika makutaniko fulani, huenda ikawezekana kumkabidhi kila mtumishi wa huduma mojawapo ya migawo hiyo. Katika makutaniko mengine huenda mtumishi mmoja wa huduma akapewa migawo kadhaa. Nyakati nyingine, watumishi wa huduma kadhaa wanaweza kushughulikia mgawo fulani. Ikiwa hakuna watumishi wa huduma wa kutosha, baraza la wazee linaweza kupanga ndugu waliobatizwa ambao ni mfano mzuri washughulikie migawo hiyo muhimu. Hivyo wanaweza kupata uzoefu utakaowasaidia baadaye watakapostahili kuwa watumishi wa huduma. Ikiwa hakuna akina ndugu, dada ambaye ni mfano mzuri anaweza kuombwa kushughulikia mambo fulani, ingawa hatapendekezwa kuwa mtumishi wa huduma. Mtu ambaye ni mfano mzuri anaweka kielelezo kizuri katika mambo ya kimwili na ya kiroho. Anapaswa kuwa mfano mzuri kwa wengine katika mazoea yake ya kuhudhuria mikutano, kushiriki katika huduma, maisha ya familia, burudani anazochagua, mavazi na kujipamba, na mambo mengine.

10 Katika makutaniko yenye wazee wachache, watumishi wa huduma wenye uwezo wanaweza kuombwa kupitia na wale wanaotaka kubatizwa maswali yanayohusu mafundisho. Maswali hayo yanapatikana katika Nyongeza “Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo.” Kwa kuwa “Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo” inahusu mambo mazito ya kibinafsi, mzee anapaswa kushughulikia sehemu hiyo.

11 Ikiwa kuna sababu zinazofaa, mara kwa mara huenda baraza la wazee likaona inafaa kubadili baadhi ya migawo ya watumishi wa huduma. Hata hivyo, kuna faida kubwa kuwaacha akina ndugu waendelee kufanya migawo ileile kwa kipindi fulani ili wapate uzoefu na ustadi.

12 Ikitegemea hali ya kutaniko, watumishi wa huduma wanaweza kupewa migawo mingine ikiwa ‘maendeleo yao yanaonekana wazi kwa watu wote.’ (1 Tim. 4:15) Ikiwa hakuna wazee wa kutosha, mtumishi wa huduma anaweza kuwekwa kuwa msaidizi wa mwangalizi wa kikundi au katika visa fulani, kuwa mtumishi wa kikundi, akifanya kazi chini ya uangalizi wa wazee. Watumishi wa huduma wanaweza kupewa migawo fulani kwenye Mkutano wa Huduma na Maisha kutia ndani kuongoza Funzo la Biblia la Kutaniko kunapokuwa na uhitaji, na kutoa hotuba za watu wote. Watumishi wa huduma wanaweza kupewa mapendeleo mengine kunapokuwa na uhitaji hususa na ikiwa wanastahili kutimiza migawo hiyo. (1 Pet. 4:10) Wanapowasaidia wazee, watumishi wa huduma wanapaswa kujitoa wenyewe kwa hiari.

13 Ingawa kazi yao ni tofauti na kazi ya wazee, bado ni sehemu ya utumishi mtakatifu kwa Mungu unaofaidi kutaniko. Baada ya muda, ikiwa watumishi wa huduma wanatimiza vizuri majukumu yao na wanastahili kuwa wachungaji na walimu, wanaweza kupendekezwa kuwa wazee.

14 Ikiwa wewe ni ndugu kijana au umebatizwa karibuni, je, unajitahidi kustahili kuwa mtumishi wa huduma? (1 Tim. 3:1) Kwa kuwa watu wengi wanakuja katika kweli kila mwaka, wanaume wanaostahili kiroho wanahitajiwa ili washughulikie majukumu kutanikoni. Unaweza kustahili kwa kusitawisha tamaa ya kuwatumikia wengine. Unaweza kufanya hivyo kwa kutafakari mfano mzuri wa Yesu. (Mt. 20:28; Yoh. 4:6, 7; 13:4, 5) Tamaa yako itaongezeka unapoona shangwe inayotokana na kuwatumikia wengine. (Mdo. 20:35) Kwa hiyo, jitolee kuwasaidia wengine, saidia kudumisha Jumba la Ufalme, au kujitolea kutoa hotuba za wanafunzi katika Mkutano wa Huduma na Maisha. Pia, ili ustahili unapaswa kusitawisha sifa za kiroho na kuwa na funzo la kibinafsi kwa ukawaida. (Zab. 1:1, 2; Gal. 5:22, 23) Isitoshe, ndugu anayejitahidi kufikia mapendeleo anaonyesha kuwa anategemeka na ni mwaminifu anapopewa migawo kutanikoni.—1 Kor. 4:2.

15 Watumishi wa huduma wanawekwa rasmi na roho takatifu kwa manufaa ya kutaniko. Wote kutanikoni wanaweza kuonyesha kwamba wanathamini bidii ya watumishi wa huduma kwa kushirikiana nao wanapotimiza migawo yao. Kwa njia hiyo, kutaniko litaonyesha kwamba linathamini mpango wa Yehova wa kudumisha utaratibu kutanikoni.—Gal. 6:10.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki