Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g17 Na. 5 kur. 12-13
  • Je, Inafaa Kujihatarisha Kwa Kusudi la Kujisisimua?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Inafaa Kujihatarisha Kwa Kusudi la Kujisisimua?
  • Amkeni!—2017
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • CHANGAMOTO
  • MAMBO UNAYOPASWA KUJUA
  • MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA
  • Michezo ya Kusisimua—Je! Niijasirie?
    Amkeni!—1994
  • “Michezo Hatari”—Je, Ujihatarishe?
    Amkeni!—2000
  • Wataka Rafiki za Namna Gani?
    Kupata Faida Zote za Ujana Wako
  • Jinsi ya Kuepuka Kushinikizwa na Marafiki
    Amkeni!—2014
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—2017
g17 Na. 5 kur. 12-13
Vijana wawili wakitazama kwenye Intaneti mchezo wa watu wanaojihatarisha

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Je, Inafaa Kujihatarisha Kwa Kusudi la Kujisisimua?

CHANGAMOTO

“Nilisimama kando ya treni iliyokuwa inapita chini ya ardhi kwa mwendo kasi. Msisimuko niliopata ulifanya nihisi kana kwamba matatizo yangu yote yameisha.”—Leon. a

“Kujirusha kwenye maji kutoka juu sana kulifanya nijihisi huru kabisa kwa sekunde chache. Kwa kawaida nilifurahia kufanya hivyo, lakini nyakati fulani niliogopa.”—Larissa.

Kama Leon na Larissa, vijana wengi husisimuka wanapojaribu kupima mipaka ya uwezo wao, nyakati fulani kwa kufanya mambo hatari sana. Je, unatamani kufanya hivyo? Ikiwa ndivyo, basi makala hii itakusaidia.

MAMBO UNAYOPASWA KUJUA

Zoea la kujisisimua kwa kujihatarisha linaweza kuwa uraibu. Huenda utasisimuka kwa muda mfupi, lakini utatamani kujisisimua zaidi. Marco, ambaye alikuwa na zoea la kwenda kwenye njia za treni kama Leon, alisema hivi: “Ilikuwa ni hali ya kujirudia. Nilipata furaha kwa muda mfupi. Lakini bado, nilitamani kujisisimua zaidi.”

Justin, ambaye alikuwa akiteleza kwa kasi kwa kutumia viatu vyenye magurudumu akiwa ameshikilia gari, alisema hivi: “Hisia nilizopata zilinichochea nitake kufanya hivyo tena. Nilitaka watu wanitambue, lakini niliishia hospitalini.”

Kushinikizwa na marafiki kunaweza kukufanya upuuze hatari. Kijana anayeitwa Marvin, alisema: “Rafiki zangu walinishinikiza kupanda jengo fulani refu bila kutumia kifaa chochote, wakisema: ‘Endelea. Utafanikiwa.’ Niliogopa sana. Nilikuwa nikitetemeka nilipokuwa ninapanda ukuta.” Larissa, aliyetajwa mapema, anasema: “Nilifanya mambo ambayo wengine walifanya. Nilifuata tu umati.”

Baadhi ya watu wametumia Intaneti kuwashinikiza wengine kwa kuwasifu wale wanaojihatarisha na kutoonyesha hatari zinazohusika. Kwa kweli, baadhi ya video za kujihatarisha zinapowekwa kwenye mitandao ya kijamii zinatazamwa na watu wengi kwa muda mfupi tu, na hivyo kufanya watu wanaojihatarisha wajulikane na kusifiwa.

Kwa mfano, video kadhaa maarufu zimeonyesha watu wakijaribu kupita maeneo yenye vizuizi (kama vile kuta, nyumba, na ngazi) ili tu wafike mahali wanapotaka, kwa kukimbia, kukwea, au kuruka kwa kasi bila kutumia vifaa vyovyote vya usalama. Hilo linaweza kukufanya ufikiri kimakosa kwamba: (1) Hatari si kubwa sana. (2) Hilo ni jambo linalofanywa na kila mtu. Matokeo ni kwamba, huenda ukashawishika kujaribu kufanya mambo yanayohatarisha uhai wako.

Kuna njia bora na salama za kupima mipaka ya uwezo wako. Biblia inasema: “Mazoezi ya kimwili ni yenye faida kidogo.” (1 Timotheo 4:8) Lakini pia inatutia moyo “tuishi kwa utimamu wa akili.” (Tito 2:12) Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Tathmini hatari zinazohusika. Biblia inasema hivi: “Mwerevu atatenda kwa ujuzi, lakini mjinga ataeneza upumbavu kila mahali.” (Methali 13:16) Kabla ya kujihusisha na utendaji wowote, chunguza hatari zinazohusika. Jiulize, ‘Je, utendaji huu unaweza kunigharimu uhai wangu au kusababisha niumie vibaya?’—Kanuni ya Biblia: Methali 14:15.

Chagua marafiki wanaoheshimu uhai. Marafiki wa kweli hawawezi kukuchochea uhatarishe uhai wako au kukushinikiza ufanye jambo ambalo hauko tayari kulifanya. Larissa anasema: “Marafiki wazuri na wenye kutegemeka walinisaidia kufanya maamuzi yanayofaa kuhusu utendaji ambao ningeshiriki. Maisha yangu yalibadilika nilipochagua marafiki wanaofaa.”—Kanuni ya Biblia: Methali 13:20.

Jiulize, ‘Je, utendaji huu unaweza kunigharimu uhai wangu au kusababisha niumie vibaya?’

Furahia ustadi wako bila kuhatarisha uhai. Kitabu Adolescent Risk Behaviors kinasema kwamba, “kujifunza jinsi ya kujiwekea mipaka na kanuni zako mwenyewe” ni sehemu ya ukuaji. Unaweza kupima mipaka ya uwezo wako katika mazingira salama, ukitumia vifaa vya usalama na kuwa mwangalifu.

Jijengee heshima ya kweli. Watu watakuheshimu unapotumia ustadi kushughulika na changamoto za maisha na si kwa kujihatarisha ili kujisisimua. Larissa anasema: “Zoea la kujirusha kwenye maji kutoka juu lilikuwa mwanzo wa mazoea mengi ya kujihatarisha niliyofanya. Laiti ningekataa kushawishiwa.”

Jambo kuu ni hili: Badala ya kujihatarisha bila sababu ili kujisisimua, tumia busara unapochagua burudani.—Kanuni ya Biblia: Methali 15:24.

a Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAANDIKO MUHIMU

  • “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

  • “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” —Methali 13:20.

  • “Kwa yule anayetenda kwa ufahamu njia ya uzima inaelekea juu, ili kuliepuka Kaburi lililo chini.”—Methali 15:24.

Peter

PETER

“Usifikirie tu raha utakayopata, unapaswa kujua pia hatari zinazohusika. Kwa vyovyote vile, hakuna kijana ambaye angependa aishie kuwa mlemavu.”

Rio

RIO

“Ikiwa rafiki zako wanakwenda kufanya jambo usilotaka kufanya, ni bora tu usiende nao. Itakuwa kuchelewa mno kusema hapana au kubadili maoni yako ikiwa tayari umefika huko.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki