Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Utaona Mambo Gani Katika Mikutano Yetu ya Kikristo?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 5

      Utaona Mambo Gani Katika Mikutano Yetu ya Kikristo?

      Mashahidi wa Yehova wakiwa katika Jumba la Ufalme nchini Argentina

      Argentina

      Mkutano wa Mashahidi wa Yehova Nchini Sierra Leone

      Sierra Leone

      Mkutano wa Mashahidi wa Yehova Nchini Ubelgiji

      Ubelgiji

      Mkutano wa Mashahidi wa Yehova Nchini Malasia

      Malasia

      Watu wengi wameacha kwenda katika dini zao kwa sababu hawapati mwongozo au faraja ya kiroho. Kwa nini basi uhudhurie mikutano ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova? Utaona mambo gani huko?

      Shangwe ya kuwa miongoni mwa watu wenye upendo na wanaojali. Katika karne ya kwanza, Wakristo walipangwa katika makutaniko, nao walikutanika ili kumwabudu Mungu, kujifunza Maandiko, na kutiana moyo. (Waebrania 10:24, 25) Wakiwa wamekusanyika pamoja na watu wenye upendo, walihisi kwamba wako miongoni mwa marafiki wa kweli, ndugu zao wa kiroho. (2 Wathesalonike 1:3; 3 Yohana 14) Tunafanya vivyo hivyo leo, nasi tunapata shangwe kama yao.

      Faida ya kujifunza jinsi ya kutumia kanuni za Biblia. Kama ilivyokuwa katika nyakati za Biblia, leo pia, wanaume, wanawake, na watoto hukutanika pamoja. Walimu wanaostahili huitumia Biblia kutusaidia kuelewa jinsi ya kutumia kanuni za Biblia maishani. (Kumbukumbu la Torati 31:12; Nehemia 8:8) Wote wanaweza kushiriki katika mazungumzo na kuimba. Kufanya hivyo hutupa nafasi ya kutangaza tumaini letu la Kikristo.—Waebrania 10:23.

      Imani yako katika Mungu itaimarishwa. Mtume Paulo aliliambia hivi kutaniko moja: “Ninatamani kuwaona ninyi ili . . . tutiane moyo, kila mmoja kupitia imani ya mwenzake, yenu na yangu pia.” (Waroma 1:11, 12) Tunaposhirikiana kwa ukawaida na waamini wenzetu katika mikutano, imani yetu na azimio letu la kuendelea kuishi kulingana na kanuni za Kikristo huimarika.

      Tunakualika uhudhurie mikutano yetu ili ujionee mwenyewe mambo hayo. Utakaribishwa kwa uchangamfu. Hakuna kiingilio katika mikutano yetu wala sadaka hazitolewi.

      • Mikutano yetu inafuata mfano gani?

      • Tunawezaje kufaidika kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Ikiwa ungependa kuona jinsi Jumba la Ufalme lilivyo ndani kabla ya kuanza kuhudhuria mikutano, mwombe mmoja wa Mashahidi wa Yehova akutembeze na kukuonyesha jinsi lilivyo.

  • Tunafaidikaje kwa Kushirikiana na Wakristo Wenzetu?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 6

      Tunafaidikaje kwa Kushirikiana na Wakristo Wenzetu?

      Mashahidi wa Yehova wakifanya tafrija

      Madagaska

      Mashahidi wa Yehova wakishirikiana mkutanoni

      Norway

      Shahidi wa Yehova akimsaidia Mkristo mwenzake

      Lebanoni

      Wazee Wakristo wamemtembelea Mkristo mwenzao

      Italia

      Hata ikitulazimu kusafiri kupitia msitu mkubwa au hali ya hewa ikiwa mbaya, tunahudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanajitahidi sana kushirikiana na waamini wenzao, licha ya kwamba huenda wakawa na hali ngumu maishani au uchovu baada ya kufanya kazi siku nzima?

      Ni kwa faida yetu. Paulo, alipokuwa akizungumzia wale tunaoshirikiana nao katika kutaniko, alisema “tufikiriane.” (Waebrania 10:24) Neno hilo linamaanisha ni lazima tujuane vizuri. Hivyo, tunatiwa moyo tuwajali wengine. Tunapoendelea kuwafahamu Wakristo wenzetu, tunatambua kwamba baadhi yao wamekabili na kushinda hali fulani ngumu kama yetu na wanaweza kutusaidia ili sisi pia tufaulu.

      Hufanya tuwe na urafiki wa kudumu. Akina ndugu na dada ambao tunakutanika pamoja nao katika mikutano yetu ni rafiki zetu wa karibu, si watu tunaowafahamu tu. Pindi nyingine, tunashirikiana nao katika tafrija. Tunapata faida gani kwa kushirikiana nao kwa njia hizo? Tunajifunza kuwathamini wengine hata zaidi, na jambo hilo linaimarisha upendo kati yetu. Kisha, wenzetu wanapokumbwa na matatizo, tunakuwa tayari kuwasaidia kwa sababu tayari tumejenga urafiki wenye upendo kati yetu. (Methali 17:17) Kwa kushirikiana na wote kutanikoni, tunaonyesha kwamba ‘tunatunzana.’—1 Wakorintho 12:25, 26.

      Tunakutia moyo uchague marafiki wanaofanya mapenzi ya Mungu. Utapata marafiki hao miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Usiruhusu kitu chochote kikuzuie kushirikiana nasi.

      • Kwa nini ni muhimu kwetu kushirikiana pamoja kwenye mikutano?

      • Ungependa kuanza lini kuhudhuria mikutano yetu?

  • Mikutano Yetu Hufanywaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 7

      Mikutano Yetu Hufanywaje?

      Mkutano wa Mashahidi wa Yehova nchini New Zealand

      New Zealand

      Mkutano wa Mashahidi wa Yehova nchini Japani

      Japani

      Mvulana akisoma Biblia nchini Uganda

      Uganda

      Mashahidi wawili wakifanya onyesho kuhusu habari fulani ya Biblia nchini Lithuania

      Lithuania

      Sehemu kuu ya mikutano ya Wakristo wa karne ya kwanza ilikuwa kuimba, kusali, hali kadhalika kusoma na kuzungumzia Maandiko. Nayo haikuhusisha desturi za kidini. (1 Wakorintho 14:26) Hivyo ndivyo tunavyofanya mikutano yetu leo.

      Mafundisho yanategemea Biblia na yanatunufaisha. Mwishoni mwa juma, kila kutaniko hukutana ili kusikiliza hotuba ya Biblia kuhusu jinsi Maandiko yanavyohusiana na maisha yetu na nyakati tunamoishi. Sote tunahimizwa kuambatana na msemaji anapokuwa akisoma Maandiko. Baada ya hotuba, kuna Funzo la “Mnara wa Mlinzi” kwa muda wa saa moja. Funzo hilo hutegemea makala ya toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi, na wote wako huru kutoa maelezo. Mazungumzo hayo yanatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kutumia mwongozo wa Biblia katika maisha yetu. Makutaniko zaidi ya 110,000 ulimwenguni hujifunza habari ileile.

      Tunasaidiwa kuboresha ustadi wa kufundisha. Pia, katikati ya juma sisi hukusanyika kwa ajili ya mkutano wenye sehemu tatu unaoitwa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo ambao hutegemea habari zinazochapishwa kila mwezi katika Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu. Sehemu ya kwanza ya mkutano huo, Hazina za Neno la Mungu, hutusaidia kuelewa sura kadhaa za Biblia ambazo wote katika kutaniko wamezisoma mapema. Kisha, sehemu ya pili, Boresha Huduma Yako, huwa na maonyesho ya jinsi ya kuzungumzia Biblia na wengine. Mshauri hutoa maelezo mafupi yanayotusaidia kuboresha ustadi wetu wa kusoma au kuzungumza. (1 Timotheo 4:13) Sehemu ya mwisho, Maisha ya Mkristo, huzungumzia jinsi tunavyoweza kutumia kanuni za Biblia maishani. Ni sehemu ya mazungumzo ya maswali na majibu ambayo huboresha uelewaji wetu wa Biblia.

      Utakapoanza kuhudhuria mikutano yetu, utafurahia kuona kwamba unaweza kujifunza mengi kuhusu Biblia.—Isaya 54:13.

      • Unaweza kutazamia kusikia mambo gani katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova?

      • Ni mkutano gani unaofanywa kila juma ambao ungependa kuhudhuria?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Soma baadhi ya habari zitakazozungumziwa katika mikutano michache inayofuata. Unaposoma, chunguza mambo unayojifunza katika Biblia ambayo yanaweza kukusaidia maishani.

  • Kwa Nini Tunavalia Vizuri Tunapohudhuria Mikutano?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 8

      Kwa Nini Tunavalia Vizuri Tunapohudhuria Mikutano?

      Baba na mvulana wakivaa kwa ajili ya kuhudhuria mkutano

      Iceland

      Mama na binti wakijitayarisha kuhudhuria mkutano

      Mexico

      Mashahidi wa Yehova wamevaa nguo nadhifu nchini Guinea-Bissau

      Guinea-Bissau

      Familia ikienda kwenye mkutano nchini Filipino

      Filipino

      Katika picha za broshua hii, je, umeona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyovalia vizuri wanapohudhuria mikutano? Kwa nini tunachukua kwa uzito jinsi tunavyovalia na kujipamba?

      Ili kuonyesha kwamba tunamheshimu Mungu wetu. Ni kweli kwamba Mungu hakazii fikira jinsi tulivyo kwa nje. (1 Samweli 16:7) Hata hivyo, tunapokutanika pamoja, tamaa yetu kuu ni kumwonyesha Mungu heshima na pia waabudu wenzetu. Ikiwa ungemtembelea mfalme au rais, bila shaka ungevalia kwa heshima kwa sababu ya cheo chake. Vivyo hivyo, tunapovalia vizuri katika mikutano, tunamheshimu “Mfalme wa mataifa,” Yehova Mungu, na pia mahali tunapomwabudia.—Yeremia 10:7.

      Ili kuonyesha viwango tunavyofuata maishani. Biblia inawatia moyo Wakristo wavalie kwa “kiasi na utimamu wa akili.” (1 Timotheo 2:9, 10) Kuvalia kwa “kiasi” kunamaanisha kuepuka mavazi ambayo yanaweza kuwafanya watu watukazie fikira kama vile mavazi ya kujionyesha, yanayoamsha tamaa mbaya, au yanayoonyesha uchi. Pia, kuwa na “utimamu wa akili” kunatusaidia kuchagua mavazi yenye kupendeza ambayo si ya kizembe au yanayopita kiasi. Kanuni hizi hazitubani, bado tuna uhuru wa kuchagua mavazi yanayotupendeza. Tunapovalia vizuri, ‘tunalipamba fundisho la Mwokozi wetu,’ na ‘kumtukuza Mungu.’ (Tito 2:10; 1 Petro 2:12) Hivyo, wengine wanaiheshimu ibada ya Yehova.

      Si lazima mtu avae mavazi rasmi ili ahudhurie mikutano katika Jumba la Ufalme. Mavazi ya kawaida yanaweza kuwa safi, nadhifu, na yenye kufaa.

      • Kwa nini ni muhimu kuvalia vizuri tunapomwabudu Mungu?

      • Ni kanuni gani zinazotuongoza tunapochagua jinsi tunavyovalia na kujipamba?

  • Ni Njia Gani Bora ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 9

      Ni Njia Gani Bora ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano?

      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni

      Kambodia

      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni
      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni

      Ukrainia

      Ikiwa unajifunza Biblia na Shahidi wa Yehova, huenda wewe husoma mapema habari ambazo mtajifunza. Ili ufaidike na mikutano pia, ni vizuri ufanye vivyo hivyo kabla ya kuhudhuria. Ukiwa na ratiba nzuri, utafanikiwa.

      Amua wakati na mahali pa kujifunzia. Ni wakati gani unapoweza kukaza fikira? Je, ni asubuhi na mapema kabla ya kuanza kazi za kila siku au ni usiku baada ya watoto kulala? Hata ikiwa huwezi kujifunza kwa muda mrefu, amua wakati unaoweza kutenga kwa ajili ya kujifunza, nawe usiruhusu chochote kivuruge ratiba yako. Tafuta mahali patulivu, na uepuke vitu vinavyokengeusha fikira kwa kuzima redio, televisheni, na hata simu ya mkononi. Kusali kabla ya kujifunza kutakusaidia upunguze mahangaiko ili uweze kukazia fikira Neno la Mungu.—Wafilipi 4:6, 7.

      Tia alama mambo makuu, na ujitayarishe kushiriki katika mikutano. Kwanza, jaribu kuelewa wazo kuu la habari unayojifunza. Fikiria kichwa kikuu cha makala au sura hiyo, chunguza jinsi kila kichwa kidogo kinavyohusiana na kichwa kikuu, na uchunguze picha na maswali yanayokazia mambo makuu. Kisha, usome kila fungu, na utafute majibu ya maswali yaliyochapishwa. Fungua na usome maandiko ambayo yametajwa, na ufikirie jinsi yanavyounga mkono kichwa kikuu. (Matendo 17:11) Unapopata majibu ya maswali, tia alama au upige mstari chini ya maneno makuu machache yatakayokusaidia kukumbuka majibu. Kwenye mikutano, unaweza kuinua mkono na kutoa maelezo mafupi ukitumia maneno yako mwenyewe.

      Ukichanganua habari tofauti-tofauti ambazo zinazungumziwa kila juma katika mikutano, utaongeza “hazina” yako ya ujuzi wa Biblia.—Mathayo 13:51, 52.

      • Ni maamuzi gani unayohitaji kufanya ili kuwa na ratiba nzuri ya kujitayarisha kwa ajili ya mikutano?

      • Unaweza kujitayarishaje ili uweze kutoa maelezo katika mikutano?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Kwa kutumia mapendekezo yaliyotajwa hapa, jitayarishe kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Biblia la Kutaniko. Ukisaidiwa na yule anayejifunza Biblia pamoja nawe, tayarisha maelezo mafupi unayoweza kutoa katika mkutano unaofuata.

  • Ibada ya Familia Ni Nini?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 10

      Ibada ya Familia Ni Nini?

      Familia ikifurahia ibada ya familia

      Korea Kusini

      Wenzi wa ndoa wakijifunza Biblia

      Brazili

      Shahidi wa Yehova akijifunza Biblia

      Australia

      Familia ikijadili habari fulani katika Biblia

      Guinea

      Tangu nyakati za kale, Yehova alitaka kila familia iwe na wakati wa kuwa pamoja ili kuimarisha hali yao ya kiroho na vilevile kujenga uhusiano wa karibu miongoni mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanatenga wakati kila juma kwa ajili ya ibada ya familia. Katika pindi hizo, wakiwa wamestarehe, wanazungumzia mambo ya kiroho yanayohusu familia zao. Hata ikiwa unaishi peke yako, unaweza kutumia wakati huo pamoja na Mungu kwa kujifunza jambo fulani katika Biblia.

      Ni wakati wa kumkaribia Yehova. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Tunaweza kumjua Yehova vizuri hata zaidi tunapojifunza mambo hususa kuhusu utu wake na matendo yake kupitia Neno lake. Ikiwa hamna ibada ya familia, njia rahisi ya kuianzisha ni kusoma Biblia kwa sauti mkiwa pamoja. Labda mnaweza kutumia ratiba ya kila juma ya Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Mnaweza kusoma kwa zamu, kisha mzungumzie mambo mliyojifunza katika Maandiko.

      Ni wakati wa kuimarisha uhusiano katika familia. Waume na wake, na vilevile wazazi na watoto, wanaweza kuimarisha uhusiano wao wanapojifunza Biblia pamoja wakiwa familia. Huo unapaswa kuwa wakati wa furaha na utulivu ambao kila mtu anatazamia kwa hamu kila juma. Ikitegemea umri wa watoto, wazazi wanaweza kuchagua habari zinazoifaa familia, labda makala ya Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Mnaweza kuzungumzia matatizo ambayo watoto wenu walikabili shuleni na jinsi ya kuyashughulikia. Kwa nini msitazame Programu kwenye JW Broadcasting (tv.jw.org) na kisha muizungumzie pamoja? Mnaweza kufanya mazoezi ya nyimbo zitakazoimbwa katika mikutano na hata kuwa na viburudisho baada ya ibada ya familia.

      Wakati huo wa pekee mnaotumia pamoja kila juma katika kumwabudu Yehova utamsaidia kila mmoja katika familia afurahie kujifunza Neno la Mungu, naye atabariki jitihada zenu.—Zaburi 1:1-3.

      • Kwa nini tunatenga wakati kwa ajili ya ibada ya familia?

      • Wazazi wanawezaje kufanya pindi hiyo iwe yenye kufurahisha?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Waulize wengine kutanikoni mambo wanayofanya katika ibada ya familia. Pia, tafuta machapisho yanayopatikana katika Jumba la Ufalme ambayo unaweza kutumia kuwafundisha watoto wako kumhusu Yehova.

  • Kwa Nini Tunahudhuria Makusanyiko?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 11

      Kwa Nini Tunahudhuria Makusanyiko?

      Kusanyiko la eneo la Mashahidi wa Yehova nchini Mexico

      Mexico

      Chapisho likitolewa kwenye kusanyiko la eneo nchini Ujerumani

      Ujerumani

      Mashahidi wa Yehova wakiwa katika kusanyiko la eneo nchini Botswana

      Botswana

      Kijana akibatizwa nchini Nikaragua

      Nikaragua

      Drama ikiigizwa kwenye kusanyiko la eneo nchini Italia

      Italia

      Kwa nini watu hawa wana furaha? Wamehudhuria mojawapo ya makusanyiko yetu. Kama watumishi wa Mungu wa wakati uliopita ambao waliagizwa wakusanyike mara tatu kwa mwaka, sisi pia hutazamia kwa hamu kukusanyika pamoja katika makusanyiko. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kila mwaka tuna makusanyiko matatu: makusanyiko mawili ya mzunguko, kila kusanyiko kwa siku moja, na kusanyiko la eneo linalofanywa kwa siku tatu. Tunafaidika jinsi gani kwa kuhudhuria makusanyiko hayo?

      Yanaimarisha ushirika wetu wa Kikristo. Kama vile Waisraeli walivyoshangilia kumsifu Yehova katika “makusanyiko,” sisi pia hushangilia kumwabudu Yehova katika makusanyiko. (Zaburi 26:12, maelezo ya chini; 111:1) Makusanyiko hutuwezesha kukutana na kushirikiana na Mashahidi wenzetu wa makutaniko mengine au hata nchi nyingine. Wakati wa mchana, tunafurahia kula pamoja mahali pa kusanyiko, jambo linalochangia mazingira ya kirafiki katika pindi hizo za kiroho. (Matendo 2:42) Katika makusanyiko tunajionea upendo unaotuunganisha tukiwa “ushirika mzima wa akina ndugu” ulimwenguni pote.—1 Petro 2:17.

      Yanatusaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Waisraeli walifaidika pia kwa ‘kuelewa maneno’ ya Maandiko yaliyokuwa yakifafanuliwa mbele yao. (Nehemia 8:8, 12) Sisi pia tunathamini mafundisho ya Biblia tunayopokea katika makusanyiko yetu. Kila programu hutegemea habari za Kimaandiko. Kupitia hotuba zenye kusisimua, mifululizo, na maigizo, tunafundishwa jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu katika maisha yetu. Tunatiwa moyo tunaposikia masimulizi ya wale ambao wamefaulu kubaki waaminifu licha ya hali ngumu. Kwenye makusanyiko ya eneo, drama hutusaidia kuona kihalisi masimulizi ya Biblia na kutufundisha masomo muhimu. Katika kila kusanyiko, wale ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu na wangependa kubatizwa, hubatizwa.

      • Kwa nini makusanyiko ni pindi zenye furaha?

      • Unaweza kufaidika jinsi gani kwa kuhudhuria kusanyiko?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Ikiwa ungependa kutujua vizuri zaidi, tafadhali hudhuria kusanyiko letu lijalo. Yule anayejifunza Biblia pamoja na wewe anaweza kukuonyesha programu ya kusanyiko ili uone habari zitakazozungumziwa. Tia alama kwenye kalenda yako tarehe na mahali ambapo kusanyiko lijalo litafanywa, na ujitahidi kuhudhuria.

  • Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 12

      Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?

      Mashahidi wa Yehova wakihubiri nyumba kwa nyumba

      Hispania

      Shahidi wa Yehova akihubiri katika bustani

      Belarus

      Shahidi wa Yehova akihubiri kupitia simu

      Hong Kong

      Mashahidi wa Yehova wakihubiri hadharani

      Peru

      Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisema: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Lakini kazi hiyo ya kuhubiri ulimwenguni pote ingetimizwa jinsi gani? Ingetimizwa kwa kufuata kielelezo ambacho Yesu aliweka alipokuwa duniani.—Luka 8:1.

      Tunajitahidi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba. (Mathayo 10:11-13; Matendo 5:42; 20:20) Wanafunzi hao walipewa maeneo hususa ya kuhubiri. (Mathayo 10:5, 6; 2 Wakorintho 10:13) Vivyo hivyo leo, kazi yetu ya kuhubiri inafanywa kwa utaratibu, na kila kutaniko huwa na eneo lake la kuhubiri. Utaratibu huo hutuwezesha kutimiza amri ya Yesu ya ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’—Matendo 10:42.

      Tunajitahidi kuwafikia watu mahali popote walipo. Yesu alituwekea mfano kwa kuwahubiria watu katika maeneo mbalimbali yenye watu wengi kama vile kwenye ufuo wa bahari au kisimani. (Marko 4:1; Yohana 4:5-15) Sisi pia huzungumza na watu kuhusu Biblia popote walipo—iwe ni barabarani, katika maeneo ya biashara, kwenye mabustani, au kupitia simu. Pia, tunawahubiria majirani, wafanyakazi, wanafunzi, na watu wetu wa ukoo tunapopata fursa. Jitihada zote hizo zimefanya iwezekane kwa mamilioni ya watu ulimwenguni pote kusikia “habari njema za wokovu.”—Zaburi 96:2.

      Je, kuna mtu yeyote ambaye ungependa kuzungumza naye kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu, na jinsi anavyoweza kufaidika wakati ujao? Zungumza naye mara tu upatapo fursa!

      • Ni “habari njema” zipi zinazohitaji kutangazwa?

      • Mashahidi wa Yehova wanaigaje mbinu ya Yesu ya kuhubiri?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Mwombe yule anayejifunza Biblia pamoja nawe akuonyeshe jinsi unavyoweza kuzungumza kwa busara pamoja na mtu unayemfahamu kuhusu jambo ambalo umejifunza katika Biblia.

  • Painia Ni Nani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 13

      13 Painia Ni Nani?

      Mhubiri wa wakati wote akihubiri hadharani

      Kanada

      Wahubiri wa wakati wote wakihubiri

      Nyumba kwa nyumba

      Wahubiri mapainia wakiongoza funzo la Biblia

      Funzo la Biblia

      Painia akijifunza Biblia

      Funzo la kibinafsi

      Mara nyingi, “painia” ni mtu anayevumbua maeneo mapya na njia ambayo wengine wanaweza kufuata. Tunaweza kusema kwamba Yesu alikuwa painia kwa sababu alitumwa duniani ili kuhudumu na kuwafungulia watu njia ya kupata wokovu. (Mathayo 20:28) Leo, wafuasi wake wanamwiga kwa kutumia muda mwingi iwezekanavyo katika kazi ya ‘kufanya wanafunzi.’ (Mathayo 28:19, 20) Wengine wamejiunga na utumishi unaoitwa upainia.

      Painia ni mhubiri wa habari njema wa wakati wote. Mashahidi wote wa Yehova ni wahubiri wa habari njema. Hata hivyo, wengine wamepanga mambo yao ili wawe mapainia wa kawaida, wakitumia saa 70 kila mwezi katika kazi ya kuhubiri. Wengi wao wanachagua kufanya kazi ya muda. Huenda wengine wakachaguliwa kuwa mapainia wa pekee katika maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, wakitumia saa 130 au zaidi katika huduma kila mwezi. Mapainia wanaridhika na mahitaji ya msingi, nao wana hakika kwamba Yehova atawaandalia mambo ya lazima maishani. (Mathayo 6:31-33; 1 Timotheo 6:6-8) Wale ambao hawawezi kuwa mapainia wa wakati wote wanaweza kuwa mapainia wasaidizi wanapoweza. Wanafanya hivyo kwa kuongeza utendaji wao wakihubiri saa 30 au 50 kwa mwezi.

      Painia anachochewa na upendo wake kwa Mungu na watu. Kama Yesu, tunatambua kwamba watu wengi leo wana uhitaji mkubwa wa kiroho. (Marko 6:34) Lakini tuna ujuzi ambao unaweza kuwasaidia sasa, na kuwapa tumaini hakika la wakati ujao. Kumpenda jirani kunamchochea painia atumie kwa hiari wakati na nguvu zake kuwasaidia wengine kiroho. (Mathayo 22:39; 1 Wathesalonike 2:8) Anapofanya hivyo, imani yake inaimarishwa, anamkaribia zaidi Mungu, naye anakuwa na furaha nyingi.—Matendo 20:35.

      • Painia ni nani?

      • Ni nini kinachowachochea wengine wawe mapainia wa wakati wote?

  • Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 14

      Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?

      Watumishi wa wakati wote wakihubiri hadharani

      Marekani

      Wanafunzi wakiwa katika Shule ya Gileadi
      Wanafunzi wakijitayarisha kwa ajili ya utumishi

      Shule ya Gileadi, Patterson, New York

      Wenzi wa ndoa wamishonari wakihubiri nchini Panama

      Panama

      Kwa miaka mingi elimu ya kitheokrasi imekaziwa sana na Mashahidi wa Yehova. Shule za pekee huandaliwa kwa ajili ya wale wanaotumikia wakiwa wahubiri wa wakati wote wa Ufalme ili ‘watimize kikamili huduma yao.’—2 Timotheo 4:5.

      Shule ya Utumishi wa Painia. Mwaka mmoja baada ya kuwa painia wa kawaida, mapainia huhudhuria shule ya siku sita ambayo hufanywa kwenye Jumba la Ufalme. Kusudi la shule hiyo ni kumsaidia painia amkaribie zaidi Yehova, aboreshe uwezo wake katika sehemu mbalimbali za huduma, na aendelee kutumikia kwa uaminifu.

      Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Shule hii ya miezi miwili imekusudiwa kuwazoeza mapainia wenye uzoefu ambao wako tayari kuhama nyumbani na kwenda kokote wanakohitajiwa. Ni kana kwamba wanasema, “Mimi hapa! Nitume mimi!” kwa kumwiga Mweneza-Injili mkuu zaidi, Yesu Kristo. (Isaya 6:8; Yohana 7:29) Baada ya kuhamia eneo lingine, huenda wakalazimika kuishi maisha rahisi. Huenda utamaduni, hali ya hewa, na vyakula vikawa tofauti na walivyozoea. Huenda pia wakahitaji kujifunza lugha mpya. Shule hii huwazoeza ndugu na dada waseja pamoja na wenzi wa ndoa, wenye umri kati ya miaka 23 na 65, wasitawishe sifa za kiroho watakazohitaji katika migawo yao na ustadi utakaowasaidia kumtumikia Yehova na tengenezo lake kikamili zaidi.

      Shule ya Gileadi. Katika Kiebrania neno “Gileadi” linamaanisha “Rundo la Ushahidi.” Tangu mwaka wa 1943, zaidi ya wamishonari 8,000 waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametumwa ili kutoa ushahidi “mpaka miisho ya dunia” na hiyo imeleta mafanikio makubwa. (Matendo 13:47) Wamishonari wetu walipofika nchini Peru, hakukuwa na kutaniko lolote huko. Sasa kuna zaidi ya makutaniko 1,000. Wamishonari wetu walipoanza kutumikia nchini Japani, kulikuwa na Mashahidi wasiozidi kumi. Sasa kuna zaidi ya Mashahidi 200,000. Mazoezi ya Gileadi yanayofanywa kwa miezi mitano yanatia ndani kujifunza Neno la Mungu kwa undani. Wale wanaotumikia wakiwa mapainia wa pekee au wamishonari, wale wanaotumikia kwenye ofisi za tawi, au wanaofanya kazi ya kuzungukia makutaniko hualikwa kwenye shule hii ili wajifunze kwa kina na hivyo kusaidia kuimarisha kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

      • Shule ya Utumishi wa Painia inatimiza kusudi gani?

      • Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme iliandaliwa kwa ajili ya akina nani?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki