Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb09 kur. 66-141
  • Samoa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Samoa
  • 2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • NURU YA KWELI YAWASILI
  • MIKUTANO YA KWANZA-KWANZA
  • MSAADA KUTOKA NG’AMBO
  • MAENDELEO MJINI APIA
  • MAENDELEO NCHINI SAMOA YA MAREKANI
  • WAMISHONARI WA GILEADI WAWASILI
  • “SINEMA YA BURE LEO”
  • BIDII KATIKA KAZI YA KUHUBIRI YAGUSA MIOYO
  • UTAMADUNI WA KISAMOA
  • MATOKEO YA VICHAPO VYA KISAMOA
  • MAKUSANYIKO YATUIMARISHA
  • UASI-IMANI WAINGIA APIA
  • USHIRIKA WENYE KUTIA MOYO
  • SAMOA YA MAREKANI YASONGA MBELE
  • WAMISHONARI WARUHUSIWA KUINGIA SAMOA
  • KUZOEA MAISHA YA KISIWANI
  • KISIWA CHA SAVAII CHAPOKEA HABARI NJEMA
  • KUSHINDA MATATIZO YA AFYA ILI KUMTUMIKIA YEHOVA
  • MAJARIBU VISIWANI TOKELAU
  • YEHOVA ABARIKI UKUZI WA KIROHO
  • KAZI YA KUTAFSIRI YAPAMBA MOTO
  • OFISI YA TAWI YAHITAJI KUPANULIWA
  • MSIBA WATOKEA!
  • “BARAKA ZISIZO NA KIFANI”
  • KWELI HUBADILI MAISHA
  • VIJANA WANAOMSIFU MUUMBA WAO
  • ELIMU KUPITIA REDIO
  • MAJUMBA YA UFALME YAHITAJIWA
  • KUKABILIANA NA MABADILIKO
  • KUSONGA MBELE PAMOJA NA TENGENEZO LA YEHOVA
2009 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb09 kur. 66-141

Samoa

VISIWA vyenye kupendeza vya Samoa vyaonekana viking’aa katika maji yenye rangi ya bluu yenye joto kiasi katika Bahari ya Pasifiki, katikati ya Hawaii na New Zealand. Ijapokuwa visiwa hivyo vilitokana na milipuko ya volkano, vina mandhari yenye kupendeza sana, vilele vya milima yake hufika mawinguni, na kuna misitu ya kitropiki na fukwe zenye mitende. Nyangwa zenye kumeremeta zina viumbe wa kupendeza chungu nzima. Kuna aina 200 tofauti-tofauti za matumbawe na aina tofauti za samaki zipatazo 900. Basi haishangazi kwamba wamishonari wa kwanza kutoka bara Ulaya waliofika katika visiwa hivyo vyenye maua yenye harufu nzuri, walisema kwamba visiwa hivyo ni kati ya visiwa vyenye kupendeza zaidi walivyopata kuona katika Bahari ya Pasifiki!

Karne kumi hivi kabla ya Kristo, Walapita walikuwa wakikaa katika visiwa vya Samoa, na yaaminika kwamba ndio watu wa kwanza kukaa katika visiwa hivyo.a Yaonekana kwamba Wapolinesia hao waliokuwa wasafiri wajasiri na stadi wa kuabiri walihamia visiwani humo kutoka kusini mashariki mwa Asia. Wakifuata pepo na mikondo ya bahari, walikuwa watu wa kwanza kufunga safari ndefu za baharini wakitumia mitumbwi miwili-miwili iliyounganishwa pamoja. Katika bahari kuu ya Pasifiki Kusini, waligundua kikundi kidogo cha visiwa ambacho walikiita Samoa.

Kadiri miaka ilivyopita, wazao wao walienea kuelekea mashariki ng’ambo ya Pasifiki hadi Tahiti, kisha Hawaii kuelekea kaskazini, New Zealand upande wa kusini magharibi, na pia kusini mashariki katika kisiwa kinachoitwa Easter Island. Sasa, eneo hilo kubwa linaitwa Polinesia, jina linalomaanisha “Visiwa Vingi,” nao wakazi wake wanaitwa Wapolinesia. Ndiyo sababu Samoa huitwa “Chimbuko la Polinesia.”

Leo, kikundi fulani cha Wasamoa wenye ujasiri kimekuwa katika safari tofauti. Kama mababu zao waliokuwa wakisafiri baharini, wamekuwa wakitafuta maisha bora. Hata hivyo, badala ya kufunga safari halisi, Wasamoa hao wamekuwa “wakisafiri” kutoka katika giza la kiroho na kuingia katika nuru ya kiroho. Wamekuwa wakitafuta ibada inayokubaliwa na Mungu wa kweli, Yehova.—Yoh. 4:23.

Masimulizi haya yanahusu Mashahidi wa Yehova katika Samoa,b Samoa ya Marekani, na Tokelau. Mwaka wa 1962, Samoa Magharibi ilipata uhuru na kuwa taifa, nayo Samoa ya Marekani bado ingali chini ya utawala wa Marekani. Hivyo basi, visiwa vya Samoa vimegawanyika katika sehemu mbili—Samoa na Samoa ya Marekani.

NURU YA KWELI YAWASILI

Habari njema ya Ufalme wa Mungu ilifika nchini Samoa kwa mara ya kwanza mwaka wa 1931. Wakati huo, mgeni aliyezuru sehemu mbalimbali katika visiwa hivyo aliwaachia watu wenye kupendezwa vitabu na vijitabu zaidi ya 470. Huenda mgeni huyo ni Sydney Shepherd, Shahidi mwenye bidii aliyezuru sehemu mbalimbali za Polinesia akieneza habari njema wakati huo.

Miaka saba baadaye, ujumbe wa Ufalme ulifika Samoa ya Marekani, J. F. Rutherford, kutoka makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, alipotua katika kisiwa cha Tutuila, akisafiri kwa meli kutoka Australia kwenda Marekani. Muda huo mfupi alipokuwa katika kisiwa hicho, Rutherford na wenzake walitumia nafasi hiyo kuwagawia watu vitabu katika jiji la bandari hiyo linaloitwa Pago Pago.

Miaka miwili baadaye, mwaka wa 1940, Harold Gill, aliyekuwa painia katika sehemu mbalimbali za Asia na Pasifiki, alifika Samoa ya Marekani. Alikuwa na nakala 3,500 za kijitabu Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?), ambacho ndicho kitabu cha kwanza kabisa cha Mashahidi wa Yehova kuchapishwa katika lugha ya Kisamoa.c

Kisha Harold akavuka na kuingia kisiwa cha Upolu, Samoa, safari inayochukua kati ya saa nane hadi kumi hivi kwa mashua. “Inaonekana kwamba tayari walikuwa na habari kwamba niko njiani,” aliandika baadaye, “kwa kuwa nilipofika tu, polisi mmoja aliniambia kwamba siruhusiwi kukanyaga kisiwa hicho. Nilimtolea hati yangu ya kusafiria na kumsomea utangulizi unaomwomba yeyote yule anayehusika, amruhusu mwenye hati hiyo, ambaye ni raia wa Milki ya Mfalme wa Uingereza, ‘kuingia pasipo shida wala kizuizi chochote na kumpa usaidizi anaohitaji na ulinzi.’ Kisha nikaruhusiwa kuongea na Gavana, aliyeniruhusu kukaa humo hadi kutakapokuwa na mashua inayoondoka kisiwani humo, siku tano hivi baadaye. Nilikodi baiskeli na kusafiri kwa mapana na marefu katika kisiwa hicho, nikiwaachia watu vijitabu nilivyokuwa navyo.”

Baada ya safari hiyo yenye mafanikio nchini Samoa, Harold, alilazimika kurudi Australia. Hata hivyo, kijitabu kimoja alichoacha hatimaye kilifika mikononi mwa mfanyakazi mmoja anayeitwa Pele Fuaiupolu.d Ujumbe wa kijitabu hicho ulibaki moyoni mwa Pele, hadi Mashahidi waliporudi na kutilia maji kweli zenye thamani zilizokuwa zimepandwa.—1 Kor. 3:6.

Mwaka wa 1952, miaka 12 baadaye, John Croxford, Shahidi kutoka Uingereza, alifika Apia, jiji kuu la Samoa, kwenye kisiwa cha Upolu. Aliajiriwa katika ofisi ambayo Pele alikuwa akifanya kazi. John alikuwa mwenye urafiki naye alikuwa na hamu ya kuwahubiria wengine. Alipogundua kwamba Pele anapendezwa na Biblia, John aliamua kumtembelea nyumbani kwake. Pele aandika: “Tuliongea mpaka karibu mapambazuko ya Jumapili. Nilimwuliza maswali mengi, naye akanijibu yote kwa kutumia Biblia. Nilisadikishwa kabisa kwamba huu ndio ukweli niliokuwa nikiutafuta kwa muda mrefu.” Baadaye, mwaka huohuo, Pele na mke wake, Ailua, wakawa Wasamoa wa kwanza kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

Pele alijua kwamba hangeweza kuiacha dini ya mababu zake hivihivi tu. Kwa hiyo akajifunza mambo mengi awezavyo na kumwomba Yehova kwa bidii amsaidie. Alipoagizwa na chifu mkuu wa familia afike kwenye mkutano uliofanyiwa Faleasiu, kijiji cha nyumbani kwa akina Pele kilichokuwa kilomita 19 kutoka Apia, Pele na mtu mwingine wa familia yao ambaye pia alikuwa akipendezwa na kweli walijikuta mbele ya machifu sita, wasemaji watatu, mapadri kumi, walimu wawili wa masuala ya kidini, chifu mkuu aliyekuwa mwenyekiti katika kikao hicho, na wanaume na wanawake wazee wa familia.

“Walitulaani na kutushutumu kwa kuliaibisha jina la familia na kanisa la mababu zetu,” akumbuka Pele. Kisha chifu mkuu akapendekeza kuwe na mjadala, mjadala ambao uliendelea hadi saa 10 alfajiri.

“Ijapokuwa wengine walipiga kelele wakisema, ‘Mnyang’anyeni Biblia! Usitumie Biblia!’ niliitumia kujibu maswali yote na kukanusha madai yao,” asema Pele. “Mwishowe, wakabaki kimya, wakiinamisha vichwa vyao chini kwa aibu. Kisha chifu mkuu akasema kwa sauti hafifu: ‘Umeshinda, Pele.’”

“Samahani, Chifu,” Pele akumbuka akimwambia chifu mkuu, “hayakuwa mashindano. Furaha yangu ni kwamba usiku wa leo mmesikia ujumbe wa ufalme. Ni matumaini yangu kwamba mtaufikiria kwa uzito.”

Kwa sababu ya unyenyekevu wa Pele, na kumtegemea Yehova na Neno Lake, Biblia, mbegu ya kweli ya Ufalme ilikuwa imeanza kutia mizizi Upolu.

MIKUTANO YA KWANZA-KWANZA

Habari kuhusu dini mpya ya Pele zilienea kama moto katika jamii hiyo yenye uhusiano wa karibu. Kama Waathene wa karne ya kwanza ambao Paulo aliwahuburia, baadhi yao walikuwa na hamu ya kujua mengi zaidi kuhusu ‘fundisho hilo jipya.’ (Mdo. 17:19, 20) Kijana mmoja anayeitwa Maatusi Leauanae, alipata fununu kwamba watu wanaopendezwa na dini hiyo mpya walikuwa wakikutana kila juma katika nyumba ya daktari fulani aliyekuwa akiishi katika uwanja wa hospitali, naye akaamua kupeleleza. Lakini alipofika kwenye lango la hospitali hiyo, akalemewa na wasiwasi, akageuka aende zake. Hata hivyo, wakati huohuo John Croxford akafika na kumwalika ajiunge na kikundi hicho jioni hiyo. Maatusi alifurahia kwelikweli funzo hilo la kitabu “Let God Be True,” naye akataka kuhudhuria tena siku nyingine. Ijapokuwa mwanzoni alikuwa akihudhuria mikutano mara mojamoja, baadaye kweli ilitia mizizi moyoni mwake, naye akabatizwa mwaka wa 1956.

Muda si muda, wapya waliokuwa wakishirikiana na kikundi hicho wakaona umuhimu wa kuzungumza na wengine mambo waliyokuwa wamejifunza. Baada ya miezi mitano tu, tangu Ndugu Croxford alipofika Apia, watu kumi walikuwa wamejiunga naye katika kazi ya kuhubiri. Miezi minne baadaye, idadi hiyo ilikuwa imeongezeka kufikia watu 19. Wapya hao walipata matokeo mazuri kwa kuwahubiria marafiki na watu wa ukoo.

Mmoja wao alimhubiria binamu yake, Sauvao Toetu, aliyekuwa akiishi Faleasiu. Muda si muda, Sauvao na shemeji yake, Finau Feomaia, wakaanza kuhudhuria mikutano pamoja na familia zao na kuchukua msimamo upande wa kweli.

Mwezi wa Januari, 1953, ibada ya kweli nchini Samoa ilipiga hatua kubwa. Kwa kuwa tayari watu 40 hivi walikuwa wakihudhuria mikutano kufikia wakati huo, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Australia iliidhinisha kuundwa kwa kutaniko la kwanza nchini Samoa, katika mji wa Apia. Ndugu Croxford aliporudi Uingereza, Pele aliyekuwa amebatizwa karibuni akaanza kusimamia kutaniko. Wahubiri wa kutaniko hilo walikuwa wenye ujasiri na bidii, hata hivyo, walikuwa wangali wachanga kiroho. Wengi wao walihitaji kujifunza kutangaza ujumbe wa Ufalme kwa busara na njia yenye kuvutia zaidi. (Kol. 4:6) Wengine walihitaji kujivika utu mpya kikamili zaidi. (Efe. 4:22-24) Jambo la kupendeza ni kwamba msaada ulikuwa njiani.—Efe. 4:8, 11-16.

MSAADA KUTOKA NG’AMBO

Mnamo Mei (Mwezi wa 5), 1953, mapainia wawili kutoka Australia, Ronald na Olive (Dolly) Sellars walifika ili kulisaidia Kutaniko la Apia. “Kwa muda fulani, mawasiliano kati ya Kutaniko la Apia na ofisi ya tawi ya Australia yalikuwa yamekatika, nayo ofisi ya tawi ilikuwa na hamu ya kujua hali ya kutaniko hilo,” aandika Ron. “Kwa kuwa tulikuwa tayari kutumikia katika Pasifiki, ofisi ya tawi ilituomba twende Samoa na kutumikia katika kutaniko hilo jipya tukiwa mapainia wa pekee.”

Wakiwa kwenye ndege kuelekea Samoa, Ron na Dolly walijitayarisha kiakili kukabili hali ngumu mbalimbali ambazo kwa kawaida watu hukumbana nazo katika migawo yao ya umishonari sehemu za mbali. “Tulishangaa kama nini,” akumbuka Ron, “kuona miti na mimea mingi kila sehemu ya kisiwa hicho. Kila mahali, tuliona watu wenye furaha, wenye kutabasamu, na wenye afya. Watoto walikuwa wakichezacheza kuzunguka nyumba zilizoezekwa na zenye sakafu nzuri ya matumbawe, ijapokuwa hazikuwa na kuta. Kila kitu kilikuwa kikifanywa polepole, bila haraka yoyote. Ni kana kwamba tulikuwa katika paradiso.”

Baada ya kupewa mahali pa kukaa na familia ya Pele, akina Sellars walianza kazi mara moja. “Nilipanga kukutana na akina ndugu kila jioni ili kuwajibu maswali yao mengi,” asema Ron. “Ijapokuwa walijua mafundisho ya msingi ya Biblia, muda si muda niliona kwamba wanahitaji kufanya mabadiliko mbalimbali ili kupatanisha maisha yao na viwango vya Mungu. Ili kuwasaidia kufanya hivyo, Dolly nami tulijitahidi sana kuwa na subira na kuwaonyesha upendo mwingi sana.” Hata hivyo, kwa kusikitisha, wengine walikataa marekebisho hayo ya upendo yaliyotokana na Maandiko na baada ya muda wakaacha kushirikiana na kutaniko. Lakini, wengine walikuwa wanyenyekevu nao walikubali mafundisho na mahimizo hayo. Baadaye, wakafanya maendeleo ya kiroho, na kwa sababu hiyo, kutaniko likasafishwa na kuimarishwa.

Ron na Dolly waliongoza katika kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba pia. Kabla ya hapo, ndugu wengi walikuwa wakiwahubiria marafiki na majirani tu. Sasa, walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba pamoja na akina Sellars, walipata watu wengi wanaopendezwa. “Pindi moja,” aandika Ron, “tulialikwa kwenda katika kijiji cha chifu anayependezwa, ambaye alitaka kujua mengi zaidi kuhusu habari njema ya Ufalme. Baada ya kula, tukawa na mazungumzo mazuri ya Biblia. Baada ya saa moja hivi, mazungumzo hayo yalikuwa yamebadilika na kuwa hotuba ya watu wote kwa sababu watu walikuwa wameongezeka kufikia 50, nasi hatukuwa tumemwalika yeyote!” Mara nyingi, wahubiri walipoanza kujifunza Biblia na watu 2 au 3, muda si muda kikundi hicho kilivutia watu wengine 10 hadi 40, waliotaka kujua utendaji wa Mashahidi wa Yehova.

Mapadri pia walikuwa wakiona yaliyokuwa yakiendelea. Wenye mamlaka walipokataa kuwaongezea Ron na Dolly muda wa kuendelea kukaa nchini humo, Ron alimwendea kamishna mkuu na kumuuliza ni kwa nini. Ron akumbuka: “Alitujibu kwamba makasisi fulani waliilalamikia serikali kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. Kwa hiyo, akasema kwamba tukiahidi kwamba tutaacha kusaidia kutaniko hilo katika kazi ya kuhubiri, atatuongezea muda kwenye vibali vyetu. Nilikataa. Pia, nikamwambia asisahau kamwe kwamba hakuna mtu anayeweza kuzuia kazi ya Mungu. Alicheka na kusema, ‘Tutaona, mkishaondoka!’”

Tangu wakati huo wenye mamlaka wakawa wakiwazuia Mashahidi wa Yehova kutoka nchi za kigeni wasiingie nchini humo. Ijapokuwa hayo yote, mwaka wa 1953, Theodore Jaracz, aliyekuwa akitumikia katika ofisi ya tawi ya Australia, na ambaye sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, aliingia kimya-kimya nchini humo kuwatia moyo akina ndugu wa kutaniko hilo. “Ziara yake ilitutia moyo kwelikweli na kutuhakikishia kwamba tulikuwa tukienda sambamba na tengenezo la Yehova,” asema Ron.

Muda mfupi baadaye, muda wa Ron na Dolly kukaa nchini humo ukamalizika, nao wakahamia Samoa ya Marekani. Hata hivyo, kwa muda wa miezi minane waliyokaa Samoa, walikuwa wameliimarisha na kulitia nguvu kutaniko hilo. Ijapokuwa wenye mamlaka hawakujua, Mashahidi wengine walikuwa njiani kuja kuchukua mahali pa akina Sellars.

MAENDELEO MJINI APIA

Richard Jenkins, Mwaustralia mwenye umri wa miaka 23 aliyekuwa ametoka tu kubatizwa, alifika Apia Mei 1954. Anasimulia: “Kabla ya kuondoka Australia, nilishauriwa nisichangamane na ndugu wenyeji hadi nipate kazi ya kudumu. Hata hivyo, baada ya miezi kadhaa, nikaanza kuhisi upweke na kujiona dhaifu kiroho. Basi nikaamua kuwasiliana kwa busara na Pele Fuaiupolu.” Wawili hao walikutana usiku mmoja.

“Pele aliniambia hatatumia jina langu halisi, ili wenye mamlaka wasianze kushuku kwamba nashirikiana na kutaniko na kunitimua nchini humo,” akumbuka Richard. “Kwa hiyo akanibandika jina la mwana wake aliyezaliwa karibuni, Uitinese, yaani, ‘witness’ (shahidi) katika matamshi ya Kisamoa. Hadi leo hii, ndugu na dada wa Samoa huniita hivyo.”

Akitumia jina lake jipya, Richard aliendelea kuwasiliana na akina ndugu kwa busara. Pia, alihubiri kwa njia isiyo rasmi na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Mwanafunzi wake mmoja wa Biblia, Mufaulu Galuvao, kijana aliyekuwa mkaguzi wa afya, baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Samoa. Mwanafunzi mwingine pia, Falema‘a Tuipoloa, akawa Shahidi, pamoja na watu wengine kadhaa wa familia yake.

Mwanafunzi mmoja, aliyekuwa akijifunza Biblia na Richard, kijana Siemu Taase, alikuwa kiongozi wa genge la wezi waliokuwa wakiiba bidhaa za wizara ya ujenzi. Hata hivyo, kabla hajafanya maendeleo ya kiroho, alinaswa na mkono mrefu wa serikali na kutupwa gerezani. Richard hakuchoka. Alimwomba msimamizi wa gereza aendelee kujifunza na Siemu chini ya mwembe uliokuwa mita 100 hivi nje ya jela. Baada ya muda, wafungwa wengine kadhaa wakaanza kushiriki funzo hilo.

“Ijapokuwa hatukuwa tukilindwa,” akumbuka Richard, “hakuna mfungwa yeyote aliyejaribu kutoroka, na baadhi yao waliikubali kweli.” Alipofunguliwa, hatimaye Siemu alitumikia akiwa mzee wa kutaniko.

Mwaka wa 1955, Richard alimwoa painia Mwaustralia, Gloria Green. Walikaa miaka 15 nchini Samoa na kuwasaidia watu 35 kujifunza kweli kabla ya kurudi Australia. Sasa wanaishi Brisbane, Australia, ambako Richard anatumikia akiwa mzee katika kutaniko la Kisamoa.

Wenzi wengine wa ndoa kutoka Australia waliosadia katika miaka hiyo ya kwanza-kwanza, ni Bill na Marjorie (Girlie) Moss. Bill, mzee wa kutaniko mwenye ujuzi, na Girlie, aliyekuwa amefanya upainia kwa miaka 24, walifika Apia mwaka wa 1956. Wakati huo kulikuwa na wahubiri 28 katika Kutaniko la Apia. Pia kulikuwa na mafunzo ya kitabu Apia na Faleasiu. Kwa miaka tisa iliyofuata, Bill na Girlie walifanya kazi bega kwa bega na kutaniko. Kufikia wakati ambapo afya ya Girlie ilipokuwa mbaya hivi kwamba wakalazimika kurudi Australia mwaka wa 1965, kikundi cha Faleasiu tayari kilikuwa kutaniko.

Miaka hiyo, maombi yote yaliyotolewa ya kuwaruhusu wamishonari kuingia nchini yalikataliwa na serikali ya Samoa. Ni wazi kwamba wenye mamlaka na makasisi walitumaini kwamba Mashahidi wa Yehova wataisha. Hata hivyo, mambo yakawa kinyume. Mashahidi walizidi kuongezeka, wakiwa watendaji na wenye bidii—hawakwisha!

MAENDELEO NCHINI SAMOA YA MAREKANI

Kabla ya muda wa akina Sellars kukaa nchini Samoa kumalizika katika mwaka wa 1954, Ron aliamua kutuma maombi yao ya kuwa wakazi nchini Samoa ya Marekani badala ya kurudi Australia. Ron anaandika: “Nilipozungumza na mwanasheria mkuu wa Samoa ya Marekani na kumweleza kwamba serikali ya Samoa ilikuwa imekataa maombi yetu kwa sababu za kidini, aliniambia, ‘Bwana Sellars, tuna uhuru wa kidini nchini Samoa ya Marekani, nitafanya juu chini mpaka mpate vibali hivyo.’”

Ron na Dolly waliwasili mji wa Pago Pago, nchini Samoa ya Marekani mnamo Januari 5, 1954. Mwanasheria huyo aliwapa vibali vya kuingia kwa sharti moja, kwamba Ron awe akiripoti ofisini kwake mara kwa mara na kumweleza mengi zaidi kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Hivyo, wakawa na mazungumzo mengi mazuri ya Biblia.

Baadaye mwezi huo, mwanasheria huyo aliwaalika Ron na Dolly nyumbani kwake kwa ajili ya chakula. Kwa kuwa padri wa Katoliki na padri wa London Missionary Society walikuwa wamealikwa pia, kukawa na mazungumzo ya Biblia yenye kusisimua. Ron anakumbuka: “Tulipokaribia kuondoka, mwanasheria huyo alitushukuru sote kwa kufika na kusema, ‘Nafikiri Bwana na Bibi Sellars ndio washindi katika mazungumzo yetu leo.’ Muda si muda, tukapata vibali vyetu vya kuwa wakazi wa kudumu. Mwanasheria mkuu aliponijulisha baadaye kwamba serikali ingekubali maombi zaidi ya wamishonari Mashahidi nchini, niliijulisha ofisi ya tawi ya Australia bila kukawia.”

Ualesi (Wallace) Pedro, Mtokelau mwenye umri wa miaka 19, ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza nchini Samoa ya Marekani kujiweka wakfu kwa Yehova. Lydia Pedro, mtu wao wa ukoo aliyekuwa painia wa pekee huko Fiji, alikuwa amemwachia ndugu ya Wallace kitabu “Let God Be True,” alipowatembelea mwaka wa 1952. Wallace alikipata kitabu hicho nyumbani kwa ndugu yake na kukisoma kwa makini.

Baada ya kukutana na familia ya Pedro mwaka wa 1954, Ron na Dolly walijifunza na dada na ndugu mkubwa wa Wallace. Wallace alimwamini Yehova Mungu, lakini kwa sababu ya kushuku dini, mwanzoni aliogopa kujiunga na wengine katika funzo. Muda si muda, alisadiki kwamba Mashahidi wa Yehova wanafundisha kweli, naye akaanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida Fagatogo. Alifanya maendeleo ya haraka ya kiroho na mnamo Aprili 30, 1955, Wallace akabatizwa katika Bandari ya Pago Pago.

Kufikia Januari 1955, mwaka mmoja tu baada ya Ron na Dolly kufika, watu saba walikuwa wakihudhuria mikutano katika nyumba ndogo ya painia katika kijiji cha Fagatogo. Kwa sababu ya uhaba wa viti, watu waliketi sakafuni. Muda si muda, watatu kati yao walianza kuandamana na Ron na Dolly katika huduma ya shambani. Ijapokuwa ilikuwa siku ya mambo madogo, kulikuwa na mengi akibani.

WAMISHONARI WA GILEADI WAWASILI

Mnamo Februari 4, 1955, wamishonari Paul na Frances Evans, na pia Gordon na Patricia Scott kutoka Marekani, walifika Samoa ya Marekani. Waliishi katika makao ya wamishonari ya Fagatogo. Kutoka katika makao hayo, mtu angeweza kuona watu na pilikapilika zao za kila siku kijijini. Leonard (Len) Helberg, mwangalizi wa mzunguko aliyetembelea Pago Pago mwaka huo asimulia mambo aliyojionea:

“Wamishonari walikuwa wakikaa katika nyumba kubwa iliyokuwa juu ya duka kubwa la zamani. Upande mmoja, ng’ambo ya kijito, kulikuwa na baa, nao mabaharia walipenda kujiburudisha humo wakati wa jioni. Walipolewa na kuanza kusababisha vurugu barabarani, polisi wa kijiji hicho, ambaye alikuwa mfupi lakini ngangari, angejipenyeza katikati ya umati huo akiwa na sigara yake mdomoni huku akivurumisha makonde huku na huku ili kutenganisha pande mbili zinazozozana. Upande wa nyuma wa nyumba hiyo, kutoka katika kanisa lililokuwa likipakana na nyumba yetu kulikuwa na kelele za mahubiri ya kuwatisha watu kuhusu moto wa mateso. Tukiwa kwenye varanda upande wa mbele, tulikuwa tukiona umati wa watu ukikusanyika karibu na benki mara moja kwa mwezi siku ya mshahara. Wamishonari kutoka katika makanisa, walikuja kutoka pande zote za kisiwa hicho ili kukusanya fungu la kumi kutoka kwa waumini wao kabla hawajatumia mishahara yao.”

Katika mazingira hayo yenye vituko, watu wengi walipendezwa na mambo ya kiroho. Len anaeleza: “Mmishonari mmoja alikuwa akianza mahubiri saa 12 asubuhi kwa kuongoza funzo la Biblia katika kibanda cha kunyolea kilichokuwa karibu na nyumba yao, kabla kinyozi huyo kufungua kazi. Baada ya hapo, angejifunza na mwokaji mikate, kabla ya kununua mkate ambao angerudi nao nyumbani kwa ajili ya kiamsha-kinywa. Baadaye siku hiyo, ndugu huyohuyo alijifunza na kikundi cha wafungwa katika jela iliyokuwa katika kijiji hicho.” Kufikia mwisho wa mwaka huo, wamishonari hao walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia 60 hivi yaliyokuwa yakihudhuriwa na watu zaidi ya 200.

“SINEMA YA BURE LEO”

Mojawapo ya sababu zilizochochea watu wengi kupendezwa na kweli ni ile filamu The New World Society in Action.e Filamu hiyo ya kwanza kutayarishwa na tengenezo miaka 40 baada ya ile filamu ya “Photo-Drama of Creation,” ilionyesha kazi ulimwenguni pote ya kuhubiri na kuchapisha, hali kadhalika utendaji wa tengenezo la Mashahidi wa Yehova. Katika ziara yake ya majuma manne nchini Samoa ya Marekani mwaka wa 1955, Len alionyesha jumla ya watu 3,227 filamu hiyo katika maonyesho 15 tofauti-tofauti, wastani wa watu 215 hivi kwa kila onyesho.

Len akumbuka: “Kabla ya kila onyesho, tulizunguka kwa gari kijiji kizima tukitawanya vikaratasi vilivyokuwa na matangazo kuhusu filamu hiyo. Wakati huohuo tulipaaza sauti, ‘Kuna sinema ya bure leo,’ na kutaja mahali ambapo sinema hiyo itaonyeshwa.”

Filamu hiyo iliwavutia watu wengi. Baada ya kila onyesho, watazamaji walitaka kujua mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova na mafundisho yao. Watu waliopendezwa hawakungoja watembelewe nyumbani na Mashahidi, badala yake walijileta wenyewe katika makao ya wamishonari, ambapo wamishonari waliongoza mafunzo kadhaa sehemu tofauti-tofauti katika makao hayo wakati uleule. Kikundi kimoja kilipoondoka kingine kiliingia. “Miaka kadhaa baadaye,” Ron Sellars anasema, “bado watu walikuwa wakihusianisha mambo waliyoona katika filamu ile na Mashahidi wa Yehova.”

BIDII KATIKA KAZI YA KUHUBIRI YAGUSA MIOYO

Miezi miwili baada ya ziara ya Len Helberg, kutaniko la kwanza la Mashahidi wa Yehova nchini Samoa ya Marekani lilianzishwa katika kijiji cha Fagatogo. Katika kipindi cha mwaka mmoja tu idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka 14 mpaka 22. Karibu wakati huohuo mapainia wa pekee wawili, Fred na Shirley Wegener, kutoka Australia walikuja kulisaidia kutaniko hilo. Sasa Fred ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Samoa.

Wahubiri, mapainia, na wamishonari hao walikuwa ‘wakiwaka roho.’ (Rom. 12:11) Len anasema: “Kwa sababu ya bidii yao na kwa kuwa watu wengi katika eneo hilo walipendezwa na Biblia, kufikia katikati ya miaka ya 1960, katika karibu kila nyumba kijijini Fagatogo kulikuwa mtu anayejifunza Biblia. Pia, katika kipindi hicho, kila nyumba katika kisiwa hicho ilihubiriwa angalau mara moja kila mwezi.”

Kampeni hiyo kubwa ya kuhubiri iliwachochea watu wa eneo hilo kupatanisha maoni yao na mafundisho ya Biblia. Len asema: “Kila mtu akapata kujua kwamba watu wataishi milele duniani, hakuna moto wa mateso, na kwamba wafu hawajui lolote. Watu walijifunza mambo hayo ya msingi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova bali si kutoka katika makanisa yao. Sababu ni kwamba tulizungumza nao kibinafsi na kujadiliana nao kwa kutumia Biblia zao wenyewe.”

Hata hivyo, dini na uhusiano wa kifamilia uliwafanya wengi wasichukue hatua. Baadhi yao waliendelea kuishi maisha mapotovu yaliyoendekezwa na makanisa badala ya maadili mazuri ya Wakristo wa kweli. Lakini kuna wengine waliokuwa wanyoofu kama yule mfanyabiashara katika mfano wa Yesu, ambao waliiona kweli kuwa lulu yenye thamani kubwa. Watu wengi wanyoofu kama hao walisimama imara upande wa kweli.—Mt. 13:45, 46.

UTAMADUNI WA KISAMOA

Caroline Pedro, painia kutoka Kanada ambaye aliolewa na Wallace Pedro mwaka wa 1960, anasema: “Tulifurahia sana kuhubiri zamani hizo. Karibu katika kila nyumba kulikuwa na mtu aliyependezwa na ujumbe wa Biblia. Ilikuwa rahisi kuanzisha mafunzo ya Biblia, na mara nyingi familia nzima-nzima ziliketi kusikiliza.

“Hatuwezi kusahau jinsi ilivyokuwa tulipokuwa tukihubiri vijijini. Kwa kawaida watoto wadogo walikuwa wakitufuata kutoka nyumba moja hadi nyingine wakisikiliza kwa makini mahubiri yetu. Kisha wangekimbia hadi nyumba iliyofuata na kuwaambia kwamba tunakuja. Hata waliwaeleza wenye nyumba ujumbe wetu na maandiko tuliyokuwa tukitumia! Ili kuwaweza watoto hao, tulitayarisha aina mbalimbali za utangulizi.”

Walipokuwa wakihubiri, akina ndugu walijitahidi kuheshimu utamaduni wa eneo hilo. (1 Kor. 9:20-23) Charles Pritchard, aliyekuwa mmishonari na ambaye sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya New Zealand, anasema: “Kwa sababu ya joto, nyumba za vijijini hazina kuta, hivyo tungeweza kuona kwa urahisi ikiwa kuna mtu au la. Kulingana na utamaduni wa Samoa, kuzungumza na mwenye nyumba ukiwa tumesimama au kabla ya kukaribishwa, ni kukosa adabu. Hivyo, tulipoikaribia nyumba, tulisubiri mwenye nyumba atukaribishe. Kisha, angetandika mkeka safi sakafuni ndani ya nyumba. Hiyo ilikuwa ishara tuvue viatu, tuingie na kuketi kwenye mkeka huo tukiwa tumepishanisha miguu yetu.” Haikuwa rahisi kwa wamishonari wengi kuketi hivyo sakafuni kwa muda mrefu. Hata hivyo, waliruhusiwa kunyoosha miguu na kuifunika kwa mkeka. Kwa kufanya hivyo, waliepuka kumwelekezea mwenye nyumba miguu jambo ambalo Wasamoa huliona kuwa ukosefu mkubwa wa adabu.

John Rhodes, ambaye kwa miaka 20 alikuwa mmishonari nchini Samoa na Samoa ya Marekani anasema: “Wenye nyumba walitukaribisha na kusema kwamba tumewaonyesha heshima kubwa kwa kuwapelekea ujumbe wa Biblia katika nyumba zao duni. Kisha wangetusalimu kwa kutuuliza maswali kama vile: Mmetoka wapi? Mna watoto? Kwenu ni wapi?”

Helen, mke wa John, anasema: “Sikuzote tulizungumza na wenye nyumba tukitumia maneno ya heshima ambayo kwa kawaida yalitumiwa wakati wa pindi rasmi. Kufanya hivyo kulionyesha kwamba tunamheshimu mwenye nyumba na kuufanya ujumbe wetu wa Biblia uheshimiwe.”

Caroline Pedro anasema: “Salamu hizo zilitusaidia kufahamiana na watu mbalimbali na familia zao. Hivyo tungeweza kuwasaidia vizuri zaidi kiroho.”

Baada ya salamu, wahubiri wangeweza kutoa ujumbe wa Ufalme. Robert Boies ambaye aliwahi kuwa mmishonari anakumbuka hivi: “Kwa kawaida wenye nyumba walitusikiliza kwa makini haidhuru mazungumzo hayo yalichukua muda gani. Kisha, wangerudia mambo mbalimbali tuliyozungumzia ili kuonyesha kwamba wanauona ujumbe wetu kuwa muhimu.”

Ilikuwa kawaida kuwa na mazungumzo marefu ya Biblia kwa sababu watu wengi walikuwa wameisoma Biblia. Caroline Pedro anasema: “Mazungumzo hayo yalinisaidia kuelewa vizuri zaidi habari mbalimbali za Biblia.” Wenye nyumba wengi walikubali vitabu na magazeti yetu. Baada ya muda, wahubiri wangeweza kutofautisha kati ya wadadisi tu na wale wanaopendezwa kikweli na mambo ya kiroho.

Wapya wengi waliopendezwa ambao walianza kuhudhuria mikutano, walitamani sana kuhubiri. John Rhodes anasema: “Kiasili, Wasamoa huzungumza kwa ufasaha, na wapya wengi wangeweza kuzungumza na wengine kuhusu imani yao kwa usadikisho hata pasipo mazoezi mengi. Hata hivyo, tuliwatia moyo watumie mapendekezo yaliyochapishwa na kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko badala ya kutegemea tu uwezo wao wa kiasili wa kusema.” Mazoezi hayo mazuri hatimaye yaliwasaidia wengi kuwa wahubiri stadi.

MATOKEO YA VICHAPO VYA KISAMOA

Ingawa Wasamoa wengi huzungumza Kiingereza kwa ufasaha, wengine kati yao hawakijui. Ili kuifikia mioyo ya watu hao wanaopenda kweli, Pele Fuaiupolu alitafsiri trakti nne katika lugha ya Kisamoa mwaka wa 1954. Kwa miaka mingi, Pele hasa ndiye aliyekuwa akitafsiri vichapo katika lugha ya Kisamoa. Akitumia taa ya kandili, mara nyingi alifanya kazi mpaka usiku sana akipiga chapa kwa kutumia mashini ya zamani ya kupigia chapa.

Mbali na kufanya kazi hiyo ya kutafsiri, Pele alikuwa na mke na watoto nane waliomtegemea, alisimamia mambo mbalimbali kutanikoni, naye alifanya kazi siku tano na nusu kila juma akikagua mashamba ya kakao kotekote kisiwani. Len Helberg anasema: “Ijapokuwa alitimiza mengi katika miaka hiyo, Pele hakujitafutia umaarufu wala sifa. Badala yake, aliliona kuwa pendeleo kubwa kutumiwa na Yehova. Kwa sababu ya ushikamanifu, unyenyekevu, na bidii yake, Pele alikuwa Shahidi mwenye sifa za pekee, nasi sote tulimpenda sana.”

Mwaka wa 1955, wahubiri waligawa nakala 16,000 za kijitabu cha Kisamoa chenye kurasa 32, “Habari Njema Hizi za Ufalme.” Kijitabu hicho kilikuwa na lugha rahisi na kilizungumzia mafundisho ya msingi ya Biblia kwa njia inayoeleweka kwa urahisi, na hivyo kukifanya kuwa kifaa muhimu cha kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Richard Jenkins, anaandika: “Baada ya kukisoma kijitabu hicho mara kadhaa, wapya wangeweza kubatizwa. Tulikipenda sana!” Baadaye vijitabu vingine vya Kisamoa vilichapishwa.

Gazeti la kwanza la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Kisamoa lilichapishwa mwaka wa 1958. Fred Wegener, aliyekuwa akifanya kazi ya uchapishaji, alitengeneza gazeti hilo kwa kubana pamoja karatasi zilizorudufishwa. Baadaye matoleo mengine yalichapishwa nchini Marekani na kisha Australia. Vitabu kadhaa vilitafsiriwa na makala mbalimbali kutokea kila mwezi katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kisamoa. Kuanzia mapema miaka ya 1970 kutolewa kwa vitabu vizima vya Kisamoa kulichangia sana katika kazi ya kuhubiri.

Vitabu vya tengenezo vimegawanywa sana katika visiwa vya Samoa. Mwaka wa 1955, wahubiri walipokuwa wakigawanya kitabu You May Survive Armageddon Into God’s New World, watu wengi wa Samoa ya Marekani walipata nakala. Wallace Pedro anasema: “Ingawa watu walikuwa wakisoma Biblia zao, wengi hawakuwa wamesikia kuhusu Har–Magedoni. Lakini, baada ya familia kukisoma kitabu hicho, hata watoto walipotuona tukiingia kijijini walipiga kelele, ‘Har–Magedoni, Har–Magedoni!’ Hata wazazi fulani waliwaita watoto wao Har–Magedoni.”

Ndivyo ilivyokuwa pia kuhusu kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele kilichotolewa mwaka wa 1972 katika lugha ya Kisamoa. Mwanzoni, kwa kuwa wengi walipenda kukisoma, wamishonari wengi waligawanya katoni mbili au zaidi kila mwezi. Fred Wegener anasema: “Watu walitujia sokoni, huku wengine wakichungulia madirishani katika mabasi wakiomba nakala za kitabu Kweli.”

MAKUSANYIKO YATUIMARISHA

Mnamo Juni 1957, akina ndugu walikuwa na msisimko mkubwa wakitazamia kusanyiko la kwanza la mzunguko ambalo lingefanywa Pago Pago, nchini Samoa ya Marekani. Kulikuwa na wahubiri waliotumia boti kutoka Samoa kuja kufurahia programu. Kwa kuwa walitaka kuwakaribisha watu wengi, akina ndugu walitangaza kotekote kuhusu kusanyiko hilo katika lugha ya Kiingereza na Kisamoa. Wahubiri hao 60 wa Samoa na Samoa ya Marekani, walifurahi kuona watu 106 katika kipindi cha kwanza siku ya Ijumaa (Siku ya 5).

Wakati wa kusanyiko hilo, wapita-njia walikuwa wakitukodolea macho, na kwa sababu ya utamaduni wa Kisamoa, wakati wa mapumziko kulikuwa na mambo fulani yasiyo ya kawaida. Ron Sellars anasema: “Wasamoa hupenda kula pamoja, na kwa kawaida watu huwaalika wapita-njia wale pamoja nao. Lakini akina ndugu walipowaalika wapita-njia wengi kwa ajili ya chakula cha mchana katika kusanyiko hilo, idara ya chakula ilikuwa na kibarua kigumu kwa sababu ilikuwa imetayarisha chakula kwa ajili ya akina ndugu na dada waliohudhuria tu.”

Hata hivyo, ushahidi mzuri ulitolewa katika pindi hizo. Katika utamaduni wa Kisamoa, wanaume hula kabla ya wanawake na watoto. Kwa kawaida wageni na viongozi wa kidini hutengewa mahali pao pa kuketi nao hula chakula maalum. Lakini kwenye kusanyiko hilo watazamaji waliwaona wamishonari na wenyeji wakila pamoja. Wote walishuhudia upendo na umoja uliokuwapo kati ya watu wa Yehova.

Mbali na kuwatia moyo na kuwazoeza wahubiri hao, makusanyiko kama hayo yaliwatayarisha kukabiliana na majaribu mengi yaliyokuwa mbele yao.

UASI-IMANI WAINGIA APIA

Pamoja na ukuzi uliokuwa ukishuhudiwa katika visiwa hivyo, wimbi la matatizo lilianza kujikusanya nchini Samoa. Watu kadhaa wakiongozwa na mtu mmoja aliyekuwa matai (chifu wa familia), walikuwa wakipinga mwongozo wa tengenezo na hivyo kuchochea matatizo katika Kutaniko la Apia. Kwa kuwa mikutano ilikuwa ikifanywa katika nyumba ya mtu huyo, wasiwasi uliongezeka kutanikoni.

Mwishowe mwaka 1958, waasi hao walijitenga na kuanzisha kikundi chao. Douglas Held kutoka ofisi ya tawi ya Australia na ambaye alikuwa akitembelea Fiji wakati huo, alienda Samoa ili kujaribu kuwasaidia ndugu waliokuwa wametatanika. Ingawa shauri lake la Kimaandiko liliwatia moyo sana waliokuwa waaminifu kutanikoni, robo ya wale waliokuwa wakihudhuria mikutano, walijiunga na kikundi hicho cha waasi. Baadhi ya watu hao walitengwa na ushirika kwa sababu ya kiburi chao.

Muda si muda ilionekana wazi roho ya Yehova inaunga mkono kikundi gani. Hatimaye kikundi hicho cha waasi kilisambaratika. Kwa upande mwingine, Kutaniko la Apia lilipata ongezeko la asilimia 35 ya wahubiri mwaka huo. Baada ya kufanyia mikutano kwa muda katika nyumba ya Richard na Gloria Jenkins iliyokuwa karibu na hospitali ya Apia, hatimaye kutaniko hilo lilihamia katika nyumba ya Maatusi Leauanae aliyekuwa akiishi Faatoia, mjini Apia. Wakiwa huko, kutaniko lilikuwa na upendo na ushirikiano wa kweli. Jumba la Ufalme la kwanza la Apia lilijengwa katika shamba la Maatusi, baada ya kupokea msaada wa kifedha kutoka kutaniko moja la Sydney nchini Australia.

USHIRIKA WENYE KUTIA MOYO

Kutaniko la Apia liliimarishwa zaidi mnamo 1959, serikali ya Samoa ilipowaruhusu wamishonari watano kutoka Samoa ya Marekani kuhudhuria kusanyiko la kwanza la mzunguko lililofanyiwa Apia. Ilikuwa furaha kama nini kuona watu 288 wakihudhuria na 10 wakibatizwa! Miaka miwili baadaye, kutaniko hilo lilipata pendeleo la kuwa na kusanyiko la wilaya la kwanza katika eneo lao. Kusanyiko hilo lilifanyiwa katika jengo la zamani la hospitali ya Wajerumani karibu na nyumba ya wageni iitwayo White Horse Inn. Waliohudhuria kusanyiko hilo walitoka sehemu za mbali kama vile New Zealand.

Makusanyiko hayo, yaliwapa akina ndugu uzoefu wa kuendesha makusanyiko. Hivyo, baadaye serikali ya Samoa ilipowanyima waangalizi wanaosafiri na wamishonari vibali vya kuingia nchini humo, akina ndugu walipanga makusanyiko yao. Mwaka wa 1967, walitayarisha na kuigiza drama ya kwanza ya nyakati za Biblia—ya kwanza kabisa nchini Samoa. Drama hiyo, iliyohusu uandalizi wa Mungu wa majiji ya makimbilio katika Israeli la kale, ilikumbukwa kwa muda mrefu na wale waliohudhuria.

Kwenye pindi hizo wahubiri kutoka Samoa walifurahia kuhudhuria makusanyiko yaliyohudhuriwa na akina ndugu kutoka visiwa mbalimbali, yaliyofanyiwa Samoa ya Marekani na Fiji, ijapokuwa walihitaji kujidhabihu. Kwa mfano, ili kuhudhuria makusanyiko hayo huko Fiji, mbali na pesa za nauli na chakula, walilazimika pia kukaa ugenini kwa muda wa mwezi mmoja hivi.

SAMOA YA MAREKANI YASONGA MBELE

Mwaka wa 1966, akina ndugu nchini Samoa ya Marekani walifurahi sana Kusanyiko la Wilaya la “Wana wa Mungu wa Uhuru” lilipofanyiwa Pago Pago. Kusanyiko hilo la kihistoria lilihudhuriwa na wajumbe 372 na vikundi vya lugha nane kutoka Australia, Fiji, New Caledonia, New Zealand, Niue, Samoa (iliyokuwa ikiitwa Samoa Magharibi awali), Tahiti, Tonga, na Vanuatu (iliyokuwa ikiitwa New Hebrides awali). Umati huo wa watu kutoka nchi mbalimbali uliinua uwiano kati ya Mashahidi na wakaaji katika jiji la kusanyiko kufikia shahidi 1 kwa watu 35, ijapokuwa wakati huo kulikuwa na wahubiri 28 tu katika kutaniko hilo!

Wahubiri wachache hivyo katika nchi hiyo wangewezaje kuwapa makao wageni wengi hivyo? “Hatukuwa na shida kupata makao kwa ajili ya idadi hiyo kubwa ya wajumbe,” asema Fred Wegener. “Wenyeji wa eneo hilo ni wakarimu nao walikuwa tayari kuwapokea akina ndugu, jambo ambalo liliwaudhi sana viongozi wa kidini.”

Kusanyiko hilo lilikuwa na matokeo mazuri sana kwa Kutaniko la Pago Pago. Katika kipindi cha miezi sita, hudhurio la kutaniko liliongezeka kwa asilimia 59 na wapya wengi wakastahili kuwa wahubiri wa habari njema. “Pia, hilo lilichochea kutaniko kujenga mahali panapofaa kwa ajili ya mikutano,” asema Ron Sellars. Katika kisiwa cha Tutuila, lilipo jiji la Pago Pago, kulikuwa kiwanja kidogo ambacho tungeweza kutumia. Hata hivyo, kwa fadhili mhubiri fulani aliyekuwa na shamba katika kijiji cha Tafuna, upande wa magharibi wa jiji, alitoa sehemu ya shamba lake itumiwe na kutaniko kwa miaka 30.

“Kiwanja hicho kilikuwa chini ya usawa wa bahari,” asema Fred Wegener, “kwa hiyo, kwa miezi mitatu, kutaniko lilifanya kazi ngumu sana ya kukusanya mawe ili kuinua msingi wa jengo.”

Walipokuwa tayari kuweka sakafu, padri wa kanisa Katoliki, ambaye alikuwa akisoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kwa ukawaida, aliwaruhusu akina ndugu watumie mashini ya kanisa ya kukorogea zege. Ron Sellars aandika: “Baadaye padri huyo alisoma makala ya Amkeni! kuhusu ndoa, akaacha upadri na kufunga ndoa.”

Akina ndugu kutoka ng’ambo walitegemeza ujenzi huo wa Jumba la Ufalme. Gordon na Patricia Scott, waliokuwa miongoni mwa wamishonari wa kwanza kutumikia Samoa ya Marekani, na walikuwa wamerudi Marekani, walichanga viti kutoka katika kutaniko lao ili vitumiwe katika jumba hilo jipya. “Kisha, tukauzia ukumbi wa sinema viti vya ziada, na kutumia pesa tulizopata kulipia gharama ya kusafirisha viti hivyo!” Jumba hilo jipya la Tafuna linaloweza kutoshea watu 130 lilikamilika na kuwekwa wakfu mwaka wa 1971. Baadaye makao ya wamishonari yalijengwa juu ya Jumba hilo.

WAMISHONARI WARUHUSIWA KUINGIA SAMOA

Kabla ya mwaka 1974, haikuwa rahisi kuhubiri nchini Samoa kwa kuwa serikali iliweka vizuizi vingi vilivyowazuia wamishonari kuingia nchini humo. Mwaka huo, akina ndugu wenyeji wenye kuongoza walimwendea waziri mkuu kuzungumzia jambo hilo. Mmoja wa ndugu hao, Mufaulu Galuvao, anaandika: “Wakati wa mazungumzo hayo tuligundua kwamba ofisa mmoja wa serikali alikuwa ameunda tume isiyo halali ya kukagua maombi yote ya wamishonari. Tume hiyo ya watu wa dini wasiopenda kazi yetu, ilikataa kuidhinisha maombi ya akina ndugu ya kuomba vibali vya kukaa nchini bila hata kumwarifu waziri mkuu.

“Waziri mkuu hakuwa na habari yoyote kuhusu hila hiyo; hivyo, akaamuru mara moja ofisa mkuu wa uhamiaji amletee faili la Mashahidi wa Yehova. Papo hapo mbele yetu akavunjilia mbali tume hiyo bandia, na kuwapa Paul na Frances Evans, vibali vya kukaa nchini kwa miaka mitatu wakiwa wamishonari, na muda huo ungeweza kuongezwa ukimalizika.” Habari zenye kusisimua kama nini! Baada ya kusubiri kwa miaka 19, hatimaye waliingia rasmi Samoa wakiwa wamishonari!

Mwanzoni, Paul na Frances waliishi pamoja na familia ya Mufaulu Galuvao, lakini John na Helen Rhodes walipofika mwaka wa 1977, walihamia makao mapya ya wamishonari yaliyokuwa yamekodiwa huko Vaiala, Apia. Wamishonari wengine ni Robert na Betty Boies waliokuja mwaka wa 1978, David na Susan Yoshikawa waliokuja mwaka wa 1979, na Russell na Leilani Earnshaw waliokuja mwaka wa 1980.

KUZOEA MAISHA YA KISIWANI

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa nchi nyingine waliohamia Samoa walitambua kwamba hata kisiwa hicho maridadi kina matatizo yake. Mojawapo ya matatizo hayo ni usafiri. John Rhodes anasema: “Miaka miwili ya kwanza tuliyokaa Apia, mara nyingi tulitembea kwa muda mrefu ili kuhudhuria mikutano na kwenda kuhubiri. Nyakati nyingine tulisafiri kwa mabasi ya umma yenye madoido.”

Kwa kawaida mabasi huwa na kichwa cha lori na bodi za mbao. Abiria hujazana ndani pamoja na mizigo yao, nao hubeba kila kitu, iwe ni majembe, au vyakula. Muziki unaofunguliwa kwa sauti ya juu na nyimbo zinazoimbwa kwa sauti ni mambo ya kawaida wakati wa safari. Vituo vya mabasi, ratiba, na barabara ambazo mabasi hayo hupitia hubadilika-badilika sana. “Basi la kwenda Vava‘u,” asema kiongozi mmoja wa safari, “halichelewi kamwe, saa zake za kufika ni wakati wowote ambapo litafika.”

“Tulipotaka kununua kitu njiani,” asema John, “tulimwambia dereva asimamishe basi. Kisha baada ya kununua tulichotaka, tulipanda basi tena na kuendelea na safari yetu. Ajabu ni kwamba hakuna yeyote aliyejali.”

Basi lilipojaa, abiria waliokuwa wameketi waliwapakata abiria wapya. Hivyo, akina ndugu wamishonari wakajifunza kuwapakata wake zao. Safari ilipofika mwisho, abiria wote, watoto kwa wakubwa walibandua sarafu ndogo iliyokuwa sikioni na kulipa nauli yao—pochi ya ajabu!

Wamishonari walisafiri toka kisiwa kimoja hadi kingine kwa ndege na mashua ndogo. Safari zilikuwa zenye kuchosha; na mara nyingi walichelewa kufika. “Tulilazimika kujifunza kuwa wenye subira na kuwa wacheshi,” asema Elizabeth Illingworth, ambaye kwa miaka mingi aliandamana na mume wake, Peter, katika kazi ya kuzungukia makutaniko kotekote katika Pasifiki ya Kusini.

Haikuwa rahisi kusafiri kwa barabara wakati wa mvua—hasa msimu wa tufani. Alipokuwa akijaribu kuvuka kijito kilichofurika akielekea kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, mmishonari Geoffrey Jackson aliteleza na kutumbukia katika kijito hicho. Aliibuka akiwa amelowa maji na matope, akaendelea na safari yake. Alipofika, wenye nyumba inayotumiwa kwa mkutano huo walimpangusa na kumvisha lavalava ndefu nyeusi (kikoi cha Kipolinesia ambacho wanaume hasa hujifunga kiunoni). Wenzake walishindwa kujizuia kucheka wakati ambapo mtu mmoja anayependezwa alimwona na kudhani kwamba ni padri wa Katoliki! Ndugu Jackson sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

Hali nyingine ngumu ambazo wageni kutoka nchi nyingine walikumbana nazo zinatia ndani kujifunza lugha mpya, kuzoea joto jingi, magonjwa mapya, ukosefu wa vifaa vingi vya kisasa, na wadudu wengi ambao huuma. “Wamishonari kwa kweli walijitoa kwa ajili yetu,” asema Mufaulu Galuvao, “na hivyo, wazazi wengi waliothamini jitihada zao waliwapa watoto wao majina ya ndugu hao wapendwa, waliokuwa wametusaidia kwa upendo.”

KISIWA CHA SAVAII CHAPOKEA HABARI NJEMA

Sasa, acheni tuzungumzie kisiwa kikubwa zaidi cha Samoa, ambacho kwa kiasi kikubwa mazingira yake yangali yalivyokuwa kiasili. Sehemu kubwa ya kisiwa hicho haikaliwi nacho kina milima mirefu, magenge ya volkano, na mabonde yapatayo 450 ya volkano, misitu mikubwa isiyopenyeka kwa urahisi, na nyanda zenye mawe-mawe ya lava. Wenyeji wengi hukaa katika vijiji vidogo-vidogo vilivyo kando ya bahari. Mwaka wa 1955 ndipo habari njema ilipofika Savaii. Len Helberg na kikundi cha wahubiri kutoka katika kisiwa cha Upolu walizuru kwa siku chache na kuonyesha ile filamu ya The New World Society in Action.

Miaka sita baadaye, dada wawili wamishonari—Tia Aluni, Msamoa wa kwanza kuhudhuria Shule ya Gileadi, na mwenzake Ivy Kawhe—waliombwa wahame kutoka Samoa ya Marekani na kwenda Savaii. Walipofika mwaka wa 1961, dada hao waliishi na mume na mke waliokuwa wazee kwa umri huko Fogapoa, kijiji kilicho upande wa mashariki wa kisiwa hicho. Baadaye, dada mwingine painia wa pekee, ambaye wakati mmoja alikuwa akiishi Savaii, akajiunga nao kwa muda. Ili kukitia moyo na kukitegemeza kikundi hicho kipya cha watu sita hadi nane hivi, akina ndugu kutoka Apia walizuru mara moja kwa mwezi na kutoa hotuba ya watu wote. Mikutano hiyo ilifanyiwa katika nyumba ndogo huko Fogapoa.

Tia na Ivy waliendelea kukaa Savaii hadi 1964, walipopewa mgawo wa kuhamia kisiwa kingine. Kwa miaka kumi iliyofuata, kazi ya kuhubiri katika kisiwa hicho cha Savaii ilifanywa kwa kiwango kidogo. Kisha, kuanzia mwaka wa 1974, familia kadhaa zilihamia Savaii ili kuchochea tena kazi hiyo. Waliohamia huko ni kutia ndani Risati na Mareta Segi, Happy na Maota Goeldner-Barnett, Faigaai Tu, Palota Alagi, Kumi Falema‘a (aliyeitwa Thompson baadaye), na Ron na Dolly Sellars, waliohama kutoka Samoa ya Marekani. Kikundi kidogo kilichoanzishwa Fogapoa kilikuwa kikikutanikia katika nyumba ya akina Segi, iliyokuwa kando ya bahari. Baadaye makao ya wamishonari na Jumba la Ufalme lilijengwa karibu na mahali hapo. Baada ya muda, kikundi kingine kikaanzishwa Taga, kijiji kilicho pwani, upande wa magharibi wa Savaii.

Kuanzia 1979, wamishonari zaidi walipewa mgawo wa kwenda Savaii kuwaunga mkono wahubiri wenyeji. Walitia ndani Robert na Betty Boies, John na Helen Rhodes, Leva na Tenisia Faai‘u, Fred na Tami Holmes, Brian na Sue Mulcahy, Matthew na Debbie Kurtz, na Jack na Mary Jane Weiser. Wamishonari hao walitoa mwongozo unaohitajika nayo kazi kisiwani Savaii ilisonga mbele.

Hata hivyo, katika kisiwa cha Savaii, utamaduni na masuala ya familia yalikuwa yamewafunga sana watu. Karibu theluthi moja ya vijiji vilikuwa vimewapiga marufuku Mashahidi wa Yehova wasihubiri katika jamii zao, vijiji fulani hata vikitangaza kupitia redio. Kwa hiyo, kuwasaidia wapya wafanye maendeleo kulihitaji wakati na subira. Hata hivyo, wengi, kutia ndani wengine waliokuwa na matatizo makubwa ya afya, walijifunza kweli.

KUSHINDA MATATIZO YA AFYA ILI KUMTUMIKIA YEHOVA

Mmoja wao ni Metusela Neru. Alipokuwa na umri wa miaka 12, alianguka alipokuwa akiendesha farasi na kuvunjika mgongo. “Baada ya kuanguka,” akumbuka mmishonari mmoja, “alitembea kana kwamba ana kibiongo, naye alikuwa na maumivu daima.” Metusela alipoanza kujifunza Biblia akiwa na umri wa miaka 19, aliamua kabisa kuvumilia upinzani wa familia yake. Kwa sababu ya ulemavu wake, safari ya kwenda kwenye mikutano ambayo kwa kawaida ingechukua dakika tano, ilimchukua dakika 45, tena kwa shida. Hata hivyo, Metusela alifanya maendeleo, akabatizwa mwaka wa 1990. Baadaye akawa painia wa kawaida na kustahili kuwa mzee kutanikoni. Tangu wakati huo, watu zaidi ya 30 kutoka katika familia yao wamehudhuria mikutano huko faga, na baadhi yao wamebatizwa. Leo, licha ya matatizo yake ya afya, Metusela anajulikana kuwa mtu mwenye tabasamu na furaha sikuzote.

Mwingine aliyeshinda matatizo makubwa ya afya na kufanya maendeleo ya kiroho ni Saumalu Taua‘anae. Saumalu alikuwa na sura isiyo ya kawaida kwa sababu ya ukoma, naye alikuwa akiishi katika kijiji cha Aopo. Kwa sababu kijiji alichoishi kilikuwa mbali, mwanzoni alijifunza Biblia kupitia barua walizokuwa wakiandikiana na Ivan Thompson. Kisha Asa Coe, painia wa pekee, akahamia Savaii na kuendeleza funzo hilo. Saumalu alipohudhuria mkutano wake wa kwanza mwaka wa 1991, alisafiri kwa gari kwa saa mbili hadi Taga, kijiji kilichokuwa upande wa pili wa kisiwa hicho.

Saumalu hakuwa huru kuchangamana na watu kwa sababu ya sura yake. Hivyo, alipohudhuria kusanyiko la pekee, alisikiliza programu akiwa ndani ya gari lake. Hata hivyo, aliguswa moyo sana kwamba wakati wa mapumziko ya mchana, ndugu na dada walimjia kwa upendo na kumkaribisha kwa moyo mkunjufu. Alikubali mwaliko wao na kusikiliza programu iliyosalia akiwa ameketi pamoja na wasikilizaji wengine.

Punde si punde, Saumalu na mke wake, Torise, wakaanza kuhudhuria mikutano katika kijiji cha Faga, wakisafiri umbali wa zaidi ya saa moja. Saumalu alibatizwa mwaka wa 1993, na baada ya muda akastahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Baadaye, hata madaktari walipoukata mguu wake, bado alikuwa akiendesha gari lake kwenda kwenye mikutano. Kijiji chao kimepiga marufuku kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova; kwa hiyo, Saumalu na Torise huwahubiria wengine kwa njia zisizo rasmi na kupitia simu.

Leo, wanaishi Apia, ambapo Saumalu hupata matibabu mbalimbali anayohitaji mara kwa mara. Badala ya kuwa na uchungu moyoni, anajulikana kuwa mtu mwenye matumaini na shangwe maishani. Yeye na mke wake wanaheshimiwa sana kwa sababu ya imani yao yenye nguvu.

MAJARIBU VISIWANI TOKELAU

Visiwa vitatu vya matumbawe vinavyofanyiza Tokelau vilipata ujumbe wa Ufalme kwa mara ya kwanza mwaka wa 1974. Mwaka huo, Ropati Uili, aliyekuwa daktari, alirudi Tokelau baada ya kufuzu kutoka katika shule ya kitiba nchini Fiji. Emmau, mke wa Ropati, alikuwa Shahidi aliyebatizwa, naye Ropati alikuwa amejifunza na Mashahidi wa Yehova kwa muda mfupi akiwa Fiji.f

Akiwa Tokelau, Ropati aligundua kwamba daktari mwingine pamoja na mke wake, Iona na Luisa Tinielu, walikuwa Mashahidi waliobatizwa. Pia alikutana na mtu mwingine anayependezwa, Nanumea Foua, ambaye watu wake wa ukoo walikuwa Mashahidi wa Yehova. Wanaume hao watatu walipanga kufanya kwa ukawaida mikutano ya Biblia na hotuba za watu wote na muda si muda hudhurio likafikia 25. Pamoja na familia zao walianza kuwahuburia wengine kwa njia zisizo rasmi.

Hata hivyo, si kila mtu aliyependezwa na utendaji huo wa kitheokrasi. Kufuatia uchochezi wa padri wa London Missionary Society, baraza la wazee wa kijiji liliwaita wanaume hao watatu. “Walituamuru tuache kufanya mikutano yetu,” akumbuka Ropati, “na kusema kwamba tusipoacha, watatuteketeza tukiwa hai katika nyumba zetu au kutuingiza katika mtumbwi na kutufukuza twende zetu. Tulijaribu kujadiliana nao kwa kutumia Maandiko, lakini hawakutaka kusikia lolote. Walitazamia tutii mamlaka yao hata iweje.” Baada ya kusikia uamuzi wao wa mwisho, familia hizo ziliamua kufanya mikutano yao kisiri ili kuepuka matatizo.

Hata hivyo, upinzani huo ulikuwa mwanzo tu. Miaka 12 baadaye, wakati ambapo dadake Ropati na mume wake walipoikubali kweli na kujiuzulu kutoka katika kanisa lao, wazee wa kijiji waliwafukuza Mashahidi wote kijijini humo. “Usiku huo,” aandika Ropati, “kila familia ilifunga virago vyake na kuvipakia kwenye mashua ndogo, na kutafuta makimbilio katika kijiji kikubwa zaidi kisiwani humo. Nyumba zao na mashamba yao yaliporwa na jirani zao.”

Licha ya minyanyaso hiyo, wahubiri hao waliendelea kukutanika pamoja ili kuabudu. “Wakijifanya kana kwamba walikuwa wakienda matembezi mwishoni mwa juma,” Ropati aeleza, “Jumamosi asubuhi familia hizo zilikuwa zikisafiri kwa mtumbwi kwenda katika kisiwa kidogo kisicho na watu wengi na kurudi Jumapili jioni baada ya kufanya mikutano yao.” Wakati huo, familia kadhaa pia zilifunga safari ndefu kwa mashua kutoka Tokelau hadi Samoa kuhudhuria makusanyiko ya wilaya ya kila mwaka.

Hatimaye, kwa sababu ya upinzani huo usiokoma, familia hizo ziliamua kuhamia New Zealand. Kwa hiyo, kufikia mwaka wa 1990, hakukuwa na Mashahidi wowote katika visiwa hivyo. Hata hivyo, Ivan Thompson, aliyekuwa akifanya upainia huko Apia, alijifunza kupitia barua na Lone Tema, kijana aliyekuwa akiishi Tokelau. Lone alifanya maendeleo kiroho naye sasa anatumikia akiwa mzee wa kutaniko nchini Australia.

Baada ya muda, wahubiri kadhaa walirudi Tokelau. Geoffrey Jackson, ambaye wakati huo alikuwa akitumikia katika ofisi ya tawi ya Samoa, alijaribu pasipo mafanikio kuwasiliana na kamishna wa New Zealand anayeshughulikia masuala ya Tokelau ili ajadiliane naye kuhusu matatizo ambayo Mashahidi wa Yehova wanakumbana nayo katika visiwa hivyo. “Hata hivyo, nilipewa kibali cha kuzuru Tokelau kama mwana-isimu,” asema Geoff, “na tukiwa safarini, kapteni wa meli hiyo alinikaribisha nijiunge naye pamoja na mwanamume mwingine katika sebule ya maofisa wa meli ili kupata kinywaji. Kumbe mwanamume huyo ndiye yuleyule kamishna wa masuala ya Tokelau ambaye tulikuwa tukijaribu kuwasiliana naye! Tulizungumza kwa zaidi ya saa nzima. Mwishoni mwa mazungumzo yetu, alinishukuru na kuahidi kwamba atafanya kila awezalo ili kuwasaidia ndugu zetu walio Tokelau.”

Leo, kungali upinzani dhidi ya kazi ya Mashahidi wa Yehova huko Tokelau. Kitinda-mimba wa Fuimanu na Hatesa Kirifi alipokufa mwaka wa 2006 na Fuimanu akatoa hotuba ya Kimaandiko kwenye maziko, baraza la wazee wa kijiji lilitisha kuifukuza familia Fuimanu kutoka katika kisiwa hicho. Baadaye, Fuimanu alitishwa alipokataa kufanya kazi katika kanisa fulani, naye pamoja na mke wake walikumbwa na hali ngumu walipokataa kushiriki katika mambo ya kisiasa. Hata hivyo, yeye pamoja na familia yake walisimama imara katika imani yao nayo imani yao ikawa yenye nguvu hata zaidi. Fuimanu asema, “Tumejifunza kumtegemea Yehova tunapojaribiwa.” (Yak. 1:2-4) Walijionea wenyewe kwamba Yehova hawaachi kamwe watumishi wake waaminifu.—Kum. 31:6.

YEHOVA ABARIKI UKUZI WA KIROHO

Tangu habari njema ilipofika Samoa mara ya kwanza, ofisi nyingi za tawi zimesimamia kazi ya Ufalme katika visiwa hivyo. Kwa sasa, Halmashauri ya Nchi yenye ndugu wanne wenye bidii inafanya kazi chini ya ofisi ya tawi ya Australia ikisimamia kazi katika visiwa vya Samoa. Kadiri ambavyo miaka imepita, akina ndugu wa Samoa wamejitahidi sana kufikisha ujumbe wa Ufalme hata sehemu za mbali zaidi. Kampeni za mara kwa mara za kuhubiri Samoa ya Marekani zimefikisha ujumbe huo katika visiwa vya mbali kama vile Kisiwa cha Swains na Visiwa vya Manu‘a, vilivyo umbali wa kilomita 320 upande wa kaskazini na kilomita 100 upande wa mashariki wa Kisiwa cha Tutuila. Wakati wa ziara hizo, wahubiri waliwaachia watu wanaopendezwa vitabu na magazeti mengi na kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia pamoja nao. Wahubiri wengine wamepanua eneo lao kwa kuwahubiria watu wanaozungumza lugha za kigeni.

KAZI YA KUTAFSIRI YAPAMBA MOTO

Kadiri idadi ya wahubiri ilivyoongezeka, ndivyo pia uhitaji wa vitabu katika lugha ya Kisamoa ulivyoongezeka. Ili kutosheleza uhitaji huo, mwaka wa 1985, Geoffrey Jackson na mke wake, Jenny, walihamishwa kutoka Tuvalu, walipokuwa wakitumikia wakiwa wamishonari, na kwenda katika ofisi ya tawi ya Samoa. Geoff alipewa mgawo wa kusimamia timu yenye watafsiri wawili. “Mwanzoni,” anasema, “watafsiri walitumia meza zilizokuwa katika chumba cha kulia cha Betheli. Kila asubuhi, waliondoa vyombo mezani baada ya kiamsha-kinywa kabla ya kuanza kutafsiri. Kisha, kabla tu ya chakula cha mchana, waliondoa vifaa vyao na kutayarisha meza kwa ajili ya chakula cha mchana. Tena, baada ya chakula, waliondoa vyombo mezani na kuendelea na kazi yao.”

Shughuli hizo ziliathiri sana kazi yao. Kazi ya kutafsiri ilikuwa ngumu nayo ilichukua wakati mwingi. “Mara nyingi waliandika tafsiri zao kwa mkono kisha kuzichapa,” akumbuka Geoff. “Kila karatasi ilichapwa mara kadhaa, ili kufanyiwa masahihisho, kabla ya kuwa tayari kuchapishwa.” Mwaka wa 1986, kompyuta ya kwanza iliponunuliwa kwa ajili ya ofisi ya tawi, kazi hiyo ilipungua sana. Programu nyingine za kompyuta zimerahisisha sana kazi ya kutafsiri na kuchapisha.

Kazi hiyo ya kutafsiri na kuchapisha imezingatia hasa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Tangu Januari 1993, gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kisamoa limekuwa likichapishwa sambamba na chapa ya Kiingereza—tena likiwa na rangi nne. Halafu, mwaka wa 1996, gazeti la Amkeni! lilianza kuchapishwa mara nne kwa mwaka katika lugha ya Kisamoa. “Kutolewa kwa Amkeni!” akumbuka Geoff, “kulitangazwa, si katika magazeti ya kilimwengu na redio tu lakini pia kupitia televisheni.”

Kwa sasa, kikundi cha watafsiri wa Kisamoa kinajitahidi kutosheleza mahitaji ya lugha hiyo. Kama timu nyingine ulimwenguni pote, watafsiri hao pia walipata mazoezi ya kuboresha ufahamu wa lugha na pia mbinu za kutafsiri, mazoezi ambayo yanawasaidia kutafsiri vizuri zaidi na kwa usahihi zaidi.

OFISI YA TAWI YAHITAJI KUPANULIWA

Ndugu Milton G. Henschel alipotembelea Samoa akiwa mwangalizi wa eneo la dunia mwaka wa 1986, ilionekana wazi kwamba makao ya wamishonari ya Sinamoga yalikuwa madogo sana yasiweze kutosheleza mahitaji ya ofisi ya tawi yanayozidi kuongezeka. Hivyo, Baraza Linaloongoza likawapa mgawo akina ndugu katika Idara ya Miundo na Ujenzi iliyo Brooklyn na Ofisi ya Uhandisi ya Kimkoa nchini Australia watembelee Samoa ili kuangalia uhitaji wa mahali pakubwa zaidi. Walipendekeza nini? Uwanja wa ekari saba ununuliwe Siusega, umbali wa kilomita tano kutoka Sinamoga, ili makao mapya ya Betheli yajengwe. Kisha, ofisi ya tawi ikimalizika kujengwa, Betheli ya zamani inaweza kubomolewa na Jumba jipya la Kusanyiko lijengwe mahali hapo.

Ujenzi wa ofisi mpya ya tawi ulianza mwaka wa 1990, nayo ilijengwa na wajenzi kutoka katika nchi mbalimbali! Watumishi wa kimataifa 44, wajitoleaji wa kimataifa 69, na wajitoleaji wa wakati wote wenyeji 38, pamoja na wafanyakazi wengine wengi wa muda walifanya kazi bega kwa bega katika mradi huo. Hata hivyo, ujenzi ulipokuwa umesonga sana, ghafula msiba ukatokea.

MSIBA WATOKEA!

Kimbunga Val, mojawapo ya dhoruba kali zaidi ambazo zimepata kupiga Pasifiki ya Kusini, kilitokea Samoa Desemba 6, 1991. Pepo zilizokuwa zikivuma kwa mwendo wa kilomita 260 kwa saa zilishambulia kisiwa hicho kwa siku tano, ukikwanyua majani ya asilimia 90 ya mimea yote, na kusababisha hasara ya dola za marekani zipatazo milioni 380. Inasikitisha kwamba watu 16 walikufa.

“Ofisi ya tawi ilianzisha haraka shughuli za kutoa msaada,” akumbuka John Rhodes. Juma hilohilo, kontena lenye bidhaa mbalimbali lilifika kutoka katika ofisi ya tawi ya Fiji. Muda si muda, michango ya pesa kutoka katika ofisi nyingine za tawi katika eneo la Pasifiki zikaanza kuingia.

“Tulihangaikia mahitaji ya msingi kwanza,” aandika Dave Stapleton, mtumishi wa kimataifa aliyekuwa akishiriki katika ujenzi wa ofisi mpya ya tawi huko Siusega. “Mahitaji hayo yalitia ndani kuwagawia ndugu wenye uhitaji maji safi, mahema, mafuta ya taa, na dawa. Halafu tukakarabati Betheli ya Sinamoga na pia majengo yaliyoharibiwa ya ofisi mpya ya tawi. Baadaye, tukarekebisha na kujenga upya Majumba ya Ufalme, makao ya wamishonari, na nyumba za akina ndugu. Kazi hiyo ilichukua miezi kadhaa.”

Baadaye, serikali ilipotoa pesa za kusaidia dini zote—kutia ndani Mashahidi wa Yehova—kurekebisha majengo yao, akina ndugu walirudisha pesa hizo pamoja na barua iliyopendekeza kwamba kwa kuwa tayari tulikuwa tumerekebisha majengo yetu, pesa hizo zinaweza kutumiwa kurekebisha majengo ya serikali. Mawaziri wa serikali walithamini tendo hilo na kutupunguzia ushuru wa bidhaa za ujenzi zilizotoka ng’ambo, na hivyo, tukaokoa pesa nyingi.

“BARAKA ZISIZO NA KIFANI”

Baada ya marekebisho yote hayo, kazi ya kujenga ofisi mpya ya tawi ikasonga mbele haraka. Mwaka mmoja na nusu baadaye, Mei 1993, familia ya Betheli ikafunga safari iliyokuwa imesubiriwa kwa muda mrefu, safari ya kuhama Sinamoga kwenda Siusega katika makao yao mapya.

Kisha, September 1993, kikundi cha Mashahidi 85, wenye ufundi mbalimbali walikuja Samoa kutoka Australia, Hawaii, Marekani, na New Zealand, ili kujenga Jumba la Kusanyiko la Sinamoga. Wote hao walijilipia nauli zao. “Majina tofauti ya vifaa vya ujenzi, na vipimo tofauti-tofauti vilitumiwa wakati wa ujenzi,” aandika Ken Abbott, aliyeongoza mafundi kutoka Australia, “hata hivyo, roho ya Yehova ilitusaidia kushinda matatizo yoyote yaliyozuka.”

“Kujionea wenyewe undugu wa kimataifa,” asema Abraham Lincoln, aliyekuwa na kikundi kutoka Hawaii, “kuligusa moyo wa kila mmoja.”

Kutokana na jitihada za pamoja za kikundi hicho cha ujenzi cha kimataifa, Jumba hilo la Kusanyiko lilijengwa kwa siku kumi tu. Wahubiri wenyeji walijifunza ufundi mbalimbali kwa kufanya kazi pamoja na ndugu wageni, nao walijengwa kiroho pia. Hivyo, mradi huo ulipokamilika, wahubiri fulani walijiandikisha kuwa mapainia au kuingia katika utumishi wa Betheli.

Hatimaye, Novemba 20-21, 1993, ofisi ya tawi na Jumba la Kusanyiko zikawekwa wakfu. John Barr wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba za wakfu. Akieleza jinsi wengi walivyohisi katika pindi hiyo yenye furaha, mmishonari wa muda mrefu Paul Evans alisema: “Yehova ametupa baraka zisizo na kifani.”

KWELI HUBADILI MAISHA

Kweli ya Neno la Mungu inapogusa mioyo ya watu, huwachochea kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Wasamoa wengi wamejionea nguvu za Neno la Mungu maishani mwao.—Efe. 4:22-24; Ebr. 4:12.

Kwa mfano, Ngongo na Maria Kupu, kama Wasamoa wasemavyo, walikuwa “wakiishi gizani”—yaani, hawakuwa wamefunga ndoa. “Tulikuwa tumejifunza na Ngongo na Maria kwa muda fulani,” asema Fred Wegener, “lakini hatukujua kwamba hawakuwa wamefunga ndoa. Kisha siku moja wakatuonyesha cheti cha ndoa walichokuwa wamepata karibuni. Muda mfupi baadaye, wakabatizwa. Ijapokuwa Ngongo alikufa, Maria anaendelea kutumikia akiwa painia wa kawaida Samoa ya Marekani.”

Tatizo lingine lililowakabili wapya nchini Samoa ni suala la utakatifu wa damu. Wasamoa hunyonga nguruwe na kuku kabla ya kuwapika na kuwala, jambo ambalo linakatazwa katika Neno la Mungu. (Mwa. 9:4; Law. 17:13, 14; Mdo. 15:28, 29) Mwanamke mmoja nchini Samoa ya Marekani alishangaa kuona katika nakala yake mwenyewe ya Biblia amri hiyo ya Mungu iliyo wazi. “Ijapokuwa familia yake ilikuwa ikienda kanisani na kusoma Biblia kwa ukawaida,” asema Julie-Anne Padget, “alikuwa akila nyama za wanyama walionyongwa tangu alipokuwa mtoto. Hata hivyo, alikubali mara moja maagizo ya Biblia na kuamua kutokula tena kamwe nyama zenye damu.” Leo, msimamo wa Mashahidi wa Yehova kuhusu utakatifu wa damu unajulikana sana kotekote nchini Samoa. Isitoshe, kwa kawaida wataalamu wa kitiba nchini Samoa huwa tayari kuheshimu msimamo wetu kuhusu kutiwa damu mishipani.

VIJANA WANAOMSIFU MUUMBA WAO

Nchini Samoa, wazazi huwazoeza vijana wao kupika, kusafisha, kulima, na kulea wadogo zao. Huenda ndiyo sababu vijana wengi Wasamoa huchukua wajibu wa kiroho kwa uzito wakiwa wangali wachanga maishani, wengine wao hata wakijiamulia wenyewe pasipo kuungwa mkono au kuchochewa na familia zao.

Ane Ropati alikuwa na umri wa miaka 13 wazazi wake walipoacha kuhudhuria mikutano. Alikuwa akiwatayarisha ndugu zake wawili na dada yake mmoja na kutembea kilomita 8 hadi kwenye Jumba la Ufalme ili kuhudhuria mikutano. Baadaye akawa painia, naye alisaidia pia katika ujenzi wa ofisi ya tawi ya Siusega. “Wamishonari,” asema Ane, “walinichochea sana na kunisaidia kufanya maendeleo kiroho.” Wakati wa ujenzi, alikutana na Steve Gauld, mjitoleaji kutoka Australia. Walifunga ndoa na kutumikia wakiwa watumishi wa kimataifa katika miradi mbalimbali ya ujenzi barani Asia ya Kusini-Mashariki, Afrika, na Urusi kabla ya kurudi Betheli ya Samoa. Sasa wanatumikia katika ofisi ya tawi ya Australia.

ELIMU KUPITIA REDIO

Miaka nenda miaka rudi, Mashahidi wa Yehova wametumia njia mbalimbali kueneza habari njema ya Ufalme. Njia moja ambayo imekuwa na matokeo mazuri ni kupitia redio. Tangu Januari 1996, kituo kimoja cha redio ya FM mjini Apia kiliwaomba Mashahidi wa Yehova wawe na kipindi cha redio cha kila juma kinachoitwa “Maswali Yako ya Biblia Yajibiwa.”

Vipindi hivyo vilihaririwa na kutangazwa na Leva Faai‘u na Palota Alagi kutoka katika ofisi ya tawi ya Samoa. “Katika kipindi chetu cha kwanza,” asema Leva, “Ndugu Alagi aliuliza maswali kadhaa, kama vile: Je, kulikuwa na furiko katika siku za Noa? Maji yote hayo yalitoka wapi? Maji hayo yalienda wapi? Wanyama wengi hivyo walitosheaje ndani ya safina? Niliyajibu maswali hayo kwa kutumia sehemu mbalimbali kutoka katika vichapo vyetu. Mwishoni mwa kipindi hicho, tulitaja mada ya juma linalofuata na kuwaomba wasikilizaji walio na maswali wawasiliane na Mashahidi wa Yehova walio karibu nao. Vipindi vingine vilijibu maswali kama vile: Kwa kuwa Wakristo wanapaswa kuwa na mke mmoja tu, kwa nini Sulemani alikuwa na wake wengi? Mungu mwenye upendo anawezaje kuwatesa watu milele katika moto wa mateso? Je, Biblia ni kitabu cha wanadamu au cha Mungu?”

Kipindi hicho cha redio kilirushwa hewani kwa zaidi ya mwaka mmoja na watu wengi walipendezwa na habari hizo. “Watu wengi walituambia kwamba walifurahia kipindi hicho nao walikuwa wakikisikiliza sikuzote,” asema Ivan Thompson. “Wengine walituambia kwamba hawakujua kamwe kwamba wangeweza kupata majibu ya masuala yenye kupendeza hivyo katika Biblia.”

MAJUMBA YA UFALME YAHITAJIWA

Katika miaka ya 1990 makutaniko mengi nchini Samoa na Samoa ya Marekani yalikutana katika nyumba za faragha au katika majengo yaliyojengwa kutokana na vifaa duni. “Sehemu hizo za kukutanikia zilidharauliwa na watu katika jamii,” asema Stuart Dougall, aliyetumika katika Halmashauri ya Nchi kati ya mwaka wa 2002 na 2007. Hata Jumba la Ufalme la Tafuna, nchini Samoa ya Marekani lililojengwa miaka 25 iliyopita lilikuwa limechakaa. Wakati wa kujenga jumba jipya ulikuwa umefika.

Hata hivyo, ili kujenga Jumba la Ufalme jipya tulihitaji kiwanja kikubwa, ambacho hakingeweza kupatikana kwa urahisi katika kisiwa hicho kidogo cha Tutuila. Akina ndugu waliwasiliana na mwanamke fulani Mkatoliki ambaye alikuwa na kiwanja sehemu za Petesa, karibu na mahali ambapo Jumba la Ufalme tulilokuwa tukitumia wakati huo lilikuwa. Mwanamke huyo alipojua kwamba akina ndugu wanahitaji kiwanja cha kujenga nyumba ya ibada, alisema atazungumza na binti yake ambaye alikuwa amepanga kujenga nyumba za biashara katika kiwanja hicho. Sala za akina ndugu zilijibiwa siku tatu baadaye mwanamke huyo alipowaambia kwamba atawauzia kiwanja hicho kwa sababu, kama alivyosema, “Mungu anapaswa kutangulizwa.”

Wallace Pedro anasema: “Alitupatia hati ya kumiliki uwanja huo hata kabla ya kumlipa, naye akasema, ‘Ninajua ninyi ni wanyoofu na mtalipa pesa zote.’ Bila shaka, hivyo ndivyo tulivyofanya.” Jumba la Ufalme maridadi linaloweza kutoshea watu 250, lenye mfumo wa kusafisha hewa, lilijengwa katika kiwanja hicho, na likawekwa wakfu mwaka wa 2002.

Mwaka wa 1999, programu mpya ya kusaidia nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha kujenga Majumba ya Ufalme, ilianzishwa na Mashahidi wa Yehova. Jumba la kwanza katika visiwa vya Samoa lilijengwa Lefaga, kijiji kilicho mbali katika pwani ya kusini ya kisiwa cha Upolu. Mwanzoni, kutaniko la Mashahidi kumi katika kijiji cha Lefaga lilikuwa likikutanika katika kibanda kisicho na kuta kilichoezekwa kwa makuti. Upande wa nyuma wa kibanda hicho kulikuwa na nyumba ya mhubiri fulani.

Ujenzi ulisimamiwa na Jack Sheedy, kutoka Australia, aliyekuwa ametumikia kwa miaka saba nchini Tonga, pamoja na mke wake, Coral. “Toka mbali,” asema, “kikundi hicho cha wajenzi kilichofanyizwa kwa wakulima, wavuvi, na wanawake, kilionekana kama mchwa wanaokimbia huku na huku kwenye kiwanja cha ujenzi.”

Wakati Jumba hilo la Ufalme linaloweza kutoshea watu 60 lilipokamilika mwaka wa 2001, wanakijiji walilisifu. Walisema: “Majumba yenu yanavutia kwa sababu ni nadhifu na sahili. Ni tofauti kabisa na makanisa yetu ambayo kwa sababu ya madoido na vikorokoro vingi, hayaonekani kuwa nadhifu.” Hudhurio la mikutano liliongezeka sana pia. Mwaka wa 2004, watu 205 walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo katika jumba hilo jipya.

Kufikia mwishoni mwa mwaka wa 2005, kupitia programu ya kujenga Majumba ya Ufalme katika nchi sisizo na uwezo mkubwa wa kifedha, Majumba ya Ufalme manne mapya yalikuwa yamejengwa na mengine matatu yakafanyiwa marekebisho katika visiwa vya Samoa. Pia, Jumba la Kusanyiko la Sinamoga, mjini Apia, Samoa, lilifanyiwa marekebisho. Kama ilivyo katika nchi nyingine sisizo na uwezo mkubwa wa kifedha, wahubiri nchini Samoa wanathamini sana msaada wenye upendo kutoka kwa akina ndugu na dada zao Wakristo ulimwenguni pote.—1 Pet. 2:17.

KUKABILIANA NA MABADILIKO

Wasamoa wengi wamehamia nchi za kigeni. Kwa mfano, jamii nyingi za Wasamoa zimehamia nchi ya Australia, Marekani, hasa eneo la Hawaii, na New Zealand. Katika nchi hizo, kuna Mashahidi zaidi ya 700 katika makutaniko 11 na vikundi 2 vya lugha ya Kisamoa. Wahubiri wengine Wasamoa hushirikiana na makutaniko ya Kiingereza katika nchi ambazo wamehamia.

Mashahidi kadhaa kutoka Samoa wamesafiri nchi za ng’ambo kuhudhuria shule mbalimbali za kitheokrasi na baadaye kurudi nchini Samoa au Samoa ya Marekani ili kutumia ujuzi waliopata kwa faida ya akina ndugu. Kwa mfano, katika miaka ya 1990, Talalelei Leauanae, Sitivi Paleso‘o, Casey Pita, Feata Sua, Andrew Coe, na SioTaua, walihudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Australia, kisha wakarudi Samoa ili kuendeleza kazi ya Ufalme. Leo, Andrew na mke wake, Fotuosamoa, wanatumikia Betheli ya Samoa. Sio na mke wake, Ese, wametumikia katika kazi ya mzunguko kwa miaka kadhaa wakiwa na mwana wao mchanga, El-Nathan. Sio, sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi. Wahitimu wengine wanatumikia kwa uaminifu wakiwa wazee, mapainia, au wahubiri katika makutaniko yao.

Kumekuwa na matokeo gani? Mwaka wa 2008, kulikuwa na kilele kipya cha wahubiri 620 katika makutaniko 12 nchini Samoa na Samoa ya Marekani. Zaidi ya watu 2,300 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2008. Hilo linaonyesha kwamba kuna matumaini makubwa ya ongezeko katika visiwa vya Samoa.

KUSONGA MBELE PAMOJA NA TENGENEZO LA YEHOVA

Kadiri ambavyo miaka imepita, watu wenye mioyo minyoofu wamekubali habari njema ya Ufalme wa Mungu nchini Samoa. (Mt. 24:14) Kama vile mababu zao waliokuwa mabaharia, wameshinda magumu mengi katika safari yao kutoka katika ulimwengu wa Shetani na kuingia katika tengenezo la Yehova linaloongozwa na roho. Vizuizi kama vile upinzani kutoka katika familia, kufukuzwa kutoka katika jamii, propaganda za viongozi wa kidini, vizuizi vya serikali, majaribu ya kimwili, na majaribu mengine hayajawazuia kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova. (1 Pet. 5:8; 1 Yoh. 2:14) Matokeo yamekuwa nini? Leo, wanafurahia usalama katika paradiso ya kiroho!—Isa. 35:1-10; 65:13, 14, 25.

Hata hivyo, bado wangali safarini. Hivi karibuni watafika mwisho wa safari yao, watakapoingia katika dunia itakayokuwa paradiso chini ya utawala wenye uadilifu wa Ufalme wa Mungu. (Ebr. 11:16) Wakishirikiana na ndugu zao wa ulimwenguni pote, na wakiongozwa na Neno la Mungu na roho yake takatifu, Mashahidi wa Yehova katika visiwa vya Samoa wanaendelea kusonga mbele, wakiwa wameazimia kufikia mwisho wa safari yao.

[Maelezo ya Chini]

a Jina Lapita larejelea mahali fulani huko New Caledonia ambako vyombo vya pekee vya udongo vilivyofinyangwa na watu hao viligunduliwa kwa mara ya kwanza.

b Samoa Magharibi ilibadili jina na kuanza kuitwa Samoa mwaka wa 1997. Katika masimulizi haya, tutatumia jina Samoa.

c Wajukuu kadhaa wa Bw. Taliutafa Young, aliyempa Harold mahali pa kukaa, baadaye walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova. Mjukuu wake mmoja, Arthur Young, sasa anashirikiana na Kutaniko la Tafuna, Samoa ya Marekani, ambako anatumikia akiwa mzee wa kutaniko na painia. Mojawapo ya vitu ambavyo Arthur anathamini sana ni Biblia ambayo Harold Gill aliipa familia yao.

d Wasamoa huwa na jina moja, kama vile Pele, halafu jina la familia. Jina la familia la Pele ni Fuaiupolu. Pia, kuna Wasamoa ambao hupewa jina linalowakilisha ukoo mzima. Baadhi ya Mashahidi wa Yehova huyakataa majina hayo, kwa kuwa wanayaona kuwa ya kisiasa au ya kilimwengu. Kwa sababu hiyo, katika masimulizi haya tutatumia jina la kwanza na jina la familia linalojulikana sana, kama vile Pele Fuaiupolu.

e Filamu hiyo ilitolewa upya katika kaseti ya video mwaka wa 1995 nayo inapatikana katika Kiarabu, Kicheki, Kichina (Kikantoni na Kimandarini), Kidachi, Kidenishi, Kifaransa, Kifini, Kigiriki, Kihispania, Kiingereza, Kiitaliano, Kijapani, Kijerumani, Kikorea, Kinorwei, Kireno (cha Brazili na Ulaya), na Kiswedi.

f Ropati alibatizwa baadaye alipozuru New Zealand.

[Blabu katika ukurasa wa 77]

“Usiku wa leo mmesikia ujumbe wa ufalme. Ni matumaini yangu kwamba mtaufikiria kwa uzito”

[Blabu katika ukurasa wa 98]

“Watoto walipotuona tukiingia kijijini walipiga kelele, ‘Har–Magedoni, Har–Magedoni!’”

[Blabu katika ukurasa wa 108]

“Basi la kwenda Vava‘u halichelewi kamwe: saa zake za kufika ni wakati wowote ambapo litafika”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 69, 70]

Dini Nchini Samoa—Zamani na Sasa

Wasamoa wengi wa zamani walikuwa na miungu mingi, kama vile viumbe, pepo, na mababu, ijapokuwa hawakuwa na majengo ya ibada, sanamu, wala mapadri. Dini ilikuwa muhimu sana maishani mwao. Mbona basi Wasamoa walikuwa tayari kukubali mabadiliko ya kidini wakati wamishonari wa London Missionary Society (LMS) walipofika huko mwaka wa 1830?

Hekaya ya Kisamoa ilitabiri kwamba dini mpya yenye nguvu ingekomesha utawala wa miungu ya zamani. Machifu (matai) wa Samoa walidai kwamba wamishonari hao ni wawakilishi wa dini hiyo mpya. Mfalme Malietoa aliamua kumwabudu Yehova, Mungu wa Wakristo, naye akawaamuru raia wake wafanye vivyo hivyo.

Wamishonari wa Kanisa Katoliki, Methodisti, Mormon, na LMS walipata wafuasi wengi sana, na leo hii karibu kila mtu katika visiwa vya Samoa ni mfuasi wa dini fulani. Wito wa serikali ya Samoa ni: “Samoa imejengwa juu ya Mungu.” Nao wito wa serikali ya Samoa ya Marekani ni: “Wasamoa, mtangulizeni Mungu.” Televisheni ina vipindi vingi vya kidini.

Vijijini hasa, kuna uvutano mkubwa wa kidini, ambapo mara nyingi ni machifu huamua dini ambayo wanakijiji watajiunga nayo. Wakaaji fulani hata hushurutishwa kuchanga zaidi ya asilimia 30 ya mapato yao ili kulipia gharama za mapadri na miradi ya kidini, jambo ambalo wengi wanalichukia sana na kuliona kuwa mzigo. Hata kuna mashindano ya kuona ni nani anayeweza kutoa pesa nyingi zaidi. Makanisa fulani hutangaza majina ya waliotoa pesa nyingi zaidi.

Katika vijiji vingi, watu huacha shughuli zao kwa dakika 10 hadi 15 hivi kwa ajili ya sala ya kijiji kizima inayoitwa sa. Vijana wenye fimbo husimama sehemu mbalimbali barabarani ili kuhakikisha desturi hiyo inafuatwa. Wanaokiuka desturi hiyo hukemewa, kutozwa faini ya dola 100 hivi, au kulazimishwa kulisha wazee wa baraza au kijiji kizima. Nyakati nyingine, adhabu huwa kali hata zaidi inayotia ndani kuchapwa au kufukuzwa kijijini.

Pindi moja, John Rhodes, mwangalizi wa mzunguko pamoja na mke wake, Helen, walifika kijijini Salimu, baada ya safari ndefu. Kwa kuwa ulikuwa wa wakati wa sa, walinzi waliwaambia wasubiri nje ya kijiji. Walisubiri mpaka kipindi hicho cha sala kilipoisha kisha wakaenda mahali walipopangiwa kukaa.

Chifu mkuu wa kijiji hicho aliposikia kwamba John na Helen walikuwa wamezuiliwa nje ya kijiji, alimwomba msamaha dada aliyewapa makao. Chifu huyo alisema kwamba Mashahidi ni wageni wanaostahili heshima, naye akawaagiza walinzi hao wasiwazuie Ndugu na Dada Rhodes kuingia kijijini wakati wowote, hata ikiwa ni wakati wa sa. Kwa sababu gani? Kwa kuwa Sio, mwana wa chifu, alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi naye alikuwa amefanya maendeleo ya kiroho. Leo, Sio Taua ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi ya Samoa.

[Picha]

John na Helen Rhodes

[Sanduku katika ukurasa wa 72]

Maelezo Mafupi Kuhusu Samoa, Samoa ya Marekani, na Tokelau

Nchi

Samoa inafanyizwa kwa visiwa viwili vikubwa—Upolu na Savaii, vinavyotenganishwa na mlango-bahari wenye upana wa kilomita 18—na visiwa vingine vidogo-vidogo. Samoa ya Marekani, iliyo kilomita 100 hivi upande wa kusini-mashariki wa Samoa, ni muungano wa visiwa kadhaa, kimoja kikubwa kinachoitwa Tutuila, na visiwa vidogo vya Manu‘a, Swains, ‘Aunu‘u, na kisiwa kingine cha matumbawe cha Rose kisichokaliwa na watu. Nayo Tokelau ni muungano wa visiwa vitatu vya matumbawe vilivyo kilomita 480 upande wa kaskazini wa Samoa.

Watu

Watu zaidi 214,000 wanaishi Samoa na 57,000 hivi wanaishi Samoa ya Marekani. Tokelau ina wakaaji 1,400 hivi. Zaidi ya asilimia 90 ni Wapolinesia, na wanaobaki ni watu wenye asili ya Asia, Ulaya, au machotara.

Lugha

Kisamoa ndiyo lugha kuu ingawa watu wengi huzungumza Kiingereza. Kitokelau, lugha inayofanana na Kisamoa, huzungumzwa Tokelau.

Kazi

Kilimo, utalii, uvuvi, na usindikaji wa samaki.

Chakula

Vyakula vyenye wanga, ndizi, na mikate iliyotengenezwa kwa matunda na tui la nazi, ndicho chakula cha msingi. Pia wao hula nyama ya nguruwe, kuku, au samaki. Kuna matunda mengi kama vile mapapai, mananasi, na maembe.

Hali ya hewa

Kwa kuwa visiwa hivyo viko karibu na ikweta, kwa kawaida kuna joto na unyevunyevu karibu mwaka mzima. Kila mwaka, jiji la Pago Pago, kisiwani Tutuila, katika Samoa ya Marekani hupokea mita 5 za mvua.

[Sanduku katika ukurasa wa 75]

“Kitabu Kizuri Sana”

Ndugu Harold Gill, alikuja na nakala 3,500 za kijitabu Wafu Wako Wapi? vya lugha ya Kisamoa ili aweze kuvigawanya nchini Samoa ya Marekani. Alipompa gavana nakala moja ya kijitabu hicho, gavana huyo alimwambia Harold awaonyeshe viongozi wote wa dini kijitabu hicho ili viongozi hao wamjulishe mwanasheria mkuu ikiwa ni sawa kukigawanya. Hata hivyo, viongozi hao wa dini waliitikiaje?

Padri wa London Missionary Society alikuwa mwenye urafiki na hakupinga. Wasabato (SDA) hawakujali, maadamu Harold hatawanyang’anya washiriki. Ijapokuwa padri wa jeshi la majini alionyesha dhihaka, hakumpinga. Hata hivyo, tukio lisilo la kawaida lilitokea kabla ya Harold kukutana na padri wa Katoliki. Harold alikuwa amempa kijitabu hicho polisi mmoja ambaye alimpeleka kwa gavana. Siku chache baadaye, Harold alimuuliza polisi huyo ikiwa alifurahia kukisoma kijitabu hicho.

Polisi huyo alimjibu: “Mkubwa wangu [mwanasheria mkuu] aliniambia: ‘Nenda kamuulize padri [wa Katoliki] ikiwa kitabu hicho ni kizuri.’ Niliketi chini ya mti na kukisoma. Nikajiambia, ‘Kitabu hiki ni kizuri sana, lakini nikimwonyesha padri, atasema, “Si kizuri.”’ Hivyo, nikaamua kumwambia mkubwa wangu, ‘Bwana Mkubwa, padri alisema, “Ni kitabu kizuri sana.”’”

Baadaye mwanasheria mkuu alimwalika Harold ofisini kwake. Mwanasheria huyo alipokuwa akifungua-fungua kijitabu hicho, Harold alikuwa akimweleza habari iliyomo. Kisha, mwanasheria mkuu akapiga simu kuagiza kijitabu kiruhusiwe kugawanywa. Hivyo, karibu nakala zote ambazo Harold alikuja nazo ziligawanywa katika kisiwa chote.

[Sanduku katika ukurasa wa 76]

Utamaduni wa Kale wa Wasamoa

Mwaka wa 1847, mmishonari wa London Missionary Society, anayeitwa George Pratt alisema kwamba, Wasamoa “ndio watu wenye adabu zaidi katika visiwa vya Polinesia, au hata ulimwenguni.” Utamaduni huo wa kale wa Wasamoa, unaoitwa faa Samoa (maisha ya Wasamoa), ni taratibu mbalimbali zinazofuatwa na watu Wasamoa wa kila tabaka.

Jambo la msingi katika utamaduni huo ni “kuwaheshimu na kuwastahi, walio ‘juu’ ya mtu,” chasema kitabu Samoan Islands. Heshima hiyo huonekana kupitia adabu, usemi unaofaa, na mtu kuwa mwaminifu kwa familia na kijiji chao. Wengi huliona kuwa jambo lisilowazika kuacha desturi na dini ya mababu zao.

Machifu wa familia (matai), walio na daraka la kuhakikisha kwamba utamaduni huo unafuatwa, huelekeza shughuli za kila siku za familia moja au zaidi na kuziwakilisha katika baraza la kijiji. Wao hudai utii kamili, na wasiotii hutozwa faini, huchapwa, au hata kufukuzwa kijijini. Kwa mfano, matai wa kijiji kimoja alimtoza faini padri mmoja aliyewaagiza wavulana wawatupie mawe Mashahidi wa Yehova.

Vijiji huwa na matai kadhaa, kuanzia 10 hadi 50. Wengi wao huchaguliwa na watu wa ukoo (aiga), na wengine hurithi vyeo hivyo. Cheo cha mtu hutegemea ngazi yake katika jamii. Kila kijiji kina chifu mkuu (alii), ambaye husimamia baraza la kijiji. Chifu-msemaji (tulafale), husimamia sherehe mbalimbali. Hata hivyo, si matai wote walio na wajibu wa kisiasa au wa kidini. Huenda baadhi yao wakaamua kushughulikia mambo ya familia tu, kama vile masuala ya mashamba, wakiwa na mamlaka ya kuamua jinsi yatakavyotumiwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 79]

“Mtu wa Yehova”

SAUVAO TOETU

ALIZALIWA 1902

ALIBATIZWA 1954

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mtu wa kwanza kukubali ukweli Faleasiu. Baadaye Jumba la Ufalme lilijengwa katika shamba lake. Limesimuliwa na mwana wake, Tafiga Sauvao

MWAKA wa 1952, binamu ya baba yangu aliyekuwa akiishi Apia alitutembelea katika kijiji cha Faleasiu. Binamu huyo, aliyekuwa akishirikiana na Mashahidi wa Yehova, alitaka kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja baba yangu. Watu kadhaa wa ukoo wetu waliokuwa wakiishi katika kijiji hicho wakaamua kusikiliza. Walizungumza mfululizo kuanzia Jumamosi asubuhi mpaka Jumatatu (Siku ya 1) alasiri, na kwa muda wote huo walipumzika kwa kulala kwa saa moja tu. Baada ya mazungumzo kama hayo miisho-juma minne iliyofuata, baba yangu alisema hivi hatimaye: “Maswali yangu yote yamejibiwa. Nimeupata ukweli.” Hivyo basi, baba yangu, na shemeji yake, Finau Feomaia, pamoja na familia zao wakaikubali kweli.

Baba yangu alianza kuhubiri mara moja. Hilo liliwashangaza watu wa ukoo, waliomwona kuwa mfuasi sugu wa dini ya Sabato. Walikuwa wakimdhihaki kwa kumwita mtu wa Yehova. Hata hivyo, ilikuwa sifa nzuri kama nini! Ingawa baba yangu hakuwa mtu mkubwa kimwili, alikuwa na moyo mkuu, naye alikuwa na akili nyingi na msemaji mwenye usadikisho. Hilo lilimwezesha kuitetea imani yake mpya kwa ustadi. Baada ya muda fulani kikundi chetu kidogo kikawa kutaniko la pili nchini Samoa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 83]

Uaminifu Licha ya Matatizo ya Afya

FAGALIMA TUATAGALOA

ALIZALIWA 1903

ALIBATIZWA 1953

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikataa kuwa matai, akawa painia wa kawaida.

IJAPOKUWA hangeweza kuona vizuri, naye alikuwa na mguu uliojipinda, Fagalima alitumikia kwa miaka mingi akiwa painia wa pekee sehemu mbalimbali za Samoa. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba na Fagalima, aliona kwamba alikuwa akisoma maandiko kwa usahihi bila kutumia miwani, kisha akamuuliza ikiwa ameanza kuona vizuri tena. Fagalima akamjibu kwamba alikuwa amepoteza miwani yake na alikuwa akinukuu maandiko hayo kutoka kichwani.

Akiwa na hamu ya kuhudhuria kusanyiko huko Fiji, kwa majuma manne, Fagalima alifanya kazi ya kukusanya nazi katika eneo la mbali la Upolu, akiwa peke yake. Licha ya ulemavu wake, alikuwa akibeba nazi 15 na kutembea umbali wa kilomita 3 hivi hadi mahali ambapo angeweza kuzifua makumbi, kutoa mbata na kuikausha. Kisha aliuza mbata hizo na kwenda hadi Apia akalipe nauli ya kwenda Fiji. Alipofika, aligundua kwamba hana pesa za kutosha kwa sababu nauli ilikuwa imepanda sana. Badala ya kulalamika, kukata tamaa, au kuomba-omba, alirudi kutengeneza mbata zaidi ili apate kiasi kinachohitajika. Alifanya yote hayo kusudi ahudhurie kusanyiko, tena ambalo alidhani litafanywa katika lugha mbili asizojua. Wazia furaha ya Fagalima alipofika Fiji na kugundua kwamba sehemu kubwa ya programu ya kusanyiko hilo itatolewa katika lugha yake mwenyewe!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 87]

“Nilifurahi Kila Siku”

RONALD SELLARS

ALIZALIWA 1922

ALIBATIZWA 1940

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na mke wake, Olive (Dolly), walifika Samoa wakiwa mapainia wa pekee mwaka wa 1953. Alihitimu shule ya wamishonari ya Gileadi mwaka wa 1961. Ron bado anatumikia akiwa painia wa pekee huko Samoa ya Marekani.

SERIKALI ya Samoa ilipokataa kuongeza muda wetu wa kukaa, mimi na Dolly tulihamia Samoa ya Marekani. Tulishushwa na meli kwenye gati la mji wa Pago Pago saa tisa alfajiri, wakati ambapo hakukuwa na watu. Hakukuwa na wahubiri wengine katika nchi hiyo nasi tulikuwa na dola 12 tu mfukoni. Baadaye asubuhi hiyo, baba ya mtu ambaye awali alikuwa akijifunza Biblia alitupa mahali pa kukaa. Alikuwa na chumba kimoja, nasi tulikuwa tukilala kwenye kona, iliyotengwa kwa pazia. Ingawa tulitaka kutafuta nyumba ya kukaa, tulianza kuhubiri nyumba ya jirani yake.

Majuma kadhaa baadaye, tulikodisha nyumba kubwa iliyokuwa juu ya duka la jumla katika kijiji cha Fagatogo. Ukiwa katika nyumba hiyo, ungeweza kuona vizuri Bandari ya Pago Pago hata hivyo ilikuwa tupu. Ndugu Knorr alikuwa ametuambia: “Mtakapoenda kwenye visiwa vya Pasifiki, huenda maisha yakawa magumu. Huenda mkalazimika kutandaza makatoni ya vitabu sakafuni na kuyatumia kama kitanda.” Hivyo ndivyo tulivyofanya! Miezi mingi ilipita kabla hatujapata pesa za kutosha kutengeneza kitanda, meza, na viti vinavyofaa. Hata hivyo, tulifurahi kuwa na nyumba yetu wenyewe.

Ingawa mke wangu mpendwa alikufa mwaka wa 1985, bado mimi huenda katika utumishi wa shambani siku nyingi. Ninapofikiria miaka zaidi ya 50 ambayo nimetumia katika utumishi wa upainia na umishonari, kwa kweli ninaweza kusema kwamba nilifurahi kila siku!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 88]

“Walinichochea Kumpenda Yehova”

WALLACE PEDRO

ALIZALIWA 1935

ALIBATIZWA 1955

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mtu wa kwanza kubatizwa nchini Samoa ya Marekani. Yeye na mke wake, Caroline, walifanya upainia, baadaye wakawa na familia. Sasa wanatumikia Seattle, Washington, Marekani.

NILIPOANZA kujifunza Biblia na kuanza kuhubiri, nilifukuzwa nyumbani nikiwa tu na nguo nilizokuwa nimevaa! Usiku huo nililala ufuoni. Nilimwomba Yehova anipe ujasiri wa kumtumikia hata iweje.

Siku iliyofuata, nilikuwa katika maktaba ya shule wakati ambapo Ndugu Paul Evans aliingia bila mimi kumtarajia. Alipoona kwamba kuna jambo linalonisumbua, aliniambia, “Twende kwenye makao ya wamishonari, tukazungumze.” Wamishonari walinikaribisha kwa fadhili, na mwaka huohuo nikabatizwa.

Baada ya kumaliza masomo yangu ya sekondari, nilianza kufanya upainia pamoja na wamishonari. Baadaye nikamwoa Caroline Hinsche, painia mwenye bidii kutoka Kanada aliyekuwa akitumikia nchini Fiji, nasi tukawa mapainia wa pekee nchini Samoa ya Marekani.

Hatua kwa hatua mtazamo wa wazazi wangu ulianza kubadilika. Baba yangu alijifunza Biblia kabla hajafa, na mama yangu alibatizwa alipokuwa na umri wa miaka 72. Ninathamini sana kielelezo cha wamishonari hao wa kwanza-kwanza. Walinichochea kumpenda Yehova, jambo ambalo limenitegemeza hadi leo hii!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 91, 92]

Subira Yavuta Heri

PAUL EVANS

ALIZALIWA 1917

ALIBATIZWA 1948

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na mke wake, Frances, walitumikia wakiwa wamishonari nchini Samoa na Samoa ya Marekani kwa zaidi ya miaka 40.

TULIPOANZA kazi ya kuzunguka mwaka wa 1957, haikuwa rahisi kwangu na mke wangu kuingia nchini Samoa kwa sababu serikali haikutaka Mashahidi nchini humo wapate msaada kutoka nje. Wageni na watalii walihitajika kutia sahihi mkataba wakiahidi kwamba kwa muda wote watakaokuwa huko, hawatamshawishi mtu yeyote kubadili dini yake. Hivyo, katika ziara yangu ya kwanza nchini Samoa nikiwa mwangalizi wa mzunguko, nilimuuliza ofisa wa uhamiaji walichomaanisha hasa. Nilipoona kuwa amechanganyikiwa, nikamuuliza:

“Tuseme wewe ni Mkatoliki, umetembelea nchi nyingine, na uamue kuenda kanisani. Ukiombwa kutoa hotuba, je, ungekubali?”

“Hakuna ubaya wowote,” akajibu.

“Kisha,” nikaendelea, “unajua kwamba Mashahidi wa Yehova huwatembelea watu nyumbani kwao wakiwa na ujumbe wa Biblia. Rafiki zangu wakiniomba niambatane nao wanapofanya kazi hiyo, kuna ubaya wowote nikiandamana nao?”

“Sidhani kama kuna ubaya,” akajibu.

“Vipi mwenye nyumba akiniuliza swali?” nikamuuliza. “Ninaweza kumjibu?”

“Sioni ubaya wowote kufanya hivyo,” akasema.

“Hiyo ni sawa. Angalau sasa ninajua ninachopaswa kufanya,” nikamwambia.

Nilipokuwa nikiondoka nchini baada ya ziara yenye mafanikio, nilimuuliza ofisa huyohuyo iwapo alikuwa amepata ripoti yoyote mbaya kuhusu ziara yetu.

“Sijasikia lolote,” akajibu. “Mambo yote sawa.”

“Namna gani tutakaporudi tena, tutapataje vibali?” nikamuuliza.

“Msiombe vibali kupitia idara ya uhamiaji,” akatushauri. “Niandikieni barua, nami nitahakikisha kwamba mmepata vibali.”

Hivyo ndivyo tulivyofanya katika ziara kadhaa.

Inasikitisha kwamba maofisa waliochukua mahali pake baadaye hawakuwa wenye ufikirio kama yeye nao waliwanyima vibali vya kuingia Samoa waangalizi wasafirio waliofuata. Hali hiyo iliendelea mpaka mwaka wa 1974, serikali ilipotupa, mimi na Frances, kibali cha kutumikia tukiwa wamishonari. Mwishowe tulibarikiwa kwa sababu ya kuwa wavumilivu na wenye bidii.

[Picha]

Frances na Paul Evans

[Sanduku katika ukurasa wa 97]

Lugha ya Wasemaji Wenye Ufasaha

Lugha ya Kisamoa huzungumzwa kwa uanana nayo ni tamu masikioni. Hata hivyo, “kwa kuwa maneno mengi huonekana kama mchanganyiko wa vokali tupu,” asema Fred Wegener, “wamishonari wanahitaji faata‘ita‘iga na faalaeiauina, yaani, wanahitaji mazoezi mengi na kutiwa moyo sana ili kuijua vizuri lugha hiyo.”

Ufasaha wa kusema na matumizi ya methali huchangia pakubwa katika utamaduni wa Kisamoa. Machifu (matai) na wasemaji (tulafale, yaani, machifu wasemaji), hupenda kunukuu Biblia na pia kutumia misamiati mingi hasa wakati wa shughuli rasmi. Utamaduni wa Wasamoa huonekana hasa katika njia yao ya kutumia lugha fasaha ikitegemea kama ni pindi rasmi au nyakati za sherehe. Wasamoa wana lugha rasmi inayoonyesha heshima (tautala lelei) ambayo hutumiwa wanapozungumza kumhusu Mungu, machifu, watu wenye mamlaka, au wageni. Kwa upande mwingine, Wasamoa wana lugha ya kawaida (tautala leaga) inayotumiwa katika mazungumzo ya kila siku, bila kuzingatia sana kanuni za lugha.

Ili kuepuka kuwaudhi watu wakati ambapo mambo rasmi na ya kisherehe au yanayohusu Biblia yanapozungumziwa, lugha rasmi ya Wasamoa yenye maneno hususa ya heshima hutumiwa. Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ambaye alikuwa mmishonari nchini Samoa anasema: “Kwa kuwa upole na heshima ni muhimu katika utamaduni wa Kisamoa, ni muhimu unapowahubiria utumie lugha ya upole inayotumiwa hasa unapozungumza na mtu mwenye mamlaka, na wakati huohuo utumie maneno ya kawaida yanayotumiwa kila siku unapozungumza juu yako mwenyewe ili kujishusha.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 99]

‘Tulihuzunika Sana Tulipoondoka’

ROBERT BOIES

ALIZALIWA 1942

ALIBATIZWA 1969

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na mke wake Elizabeth (Betty), walitumikia wakiwa wamishonari katika visiwa vya Samoa tangu mwaka wa 1978 mpaka 1986.

TANGU tulipofika, tulitambua kwamba watu wa Samoa ya Marekani walithamini jitihada zetu za kujifunza Kisamoa nao hawakuzingatia mara nyingi tulizokosea. Pindi moja nilitumia andiko la Ufunuo 12:9 kueleza uvutano wa Shetani ulimwenguni. Hata hivyo, neno ibilisi (tiapolo) katika Kisamoa linafanana sana na neno limau (tipolo). Nilichanganya maneno hayo nikieleza kwamba “limau” lilikuwa limetupwa kutoka mbinguni nalo linaipotosha dunia nzima inayokaliwa. Lakini hivi karibuni Yehova ataliangamiza “limau” na kuliondoa kabisa. Mwenye nyumba na mmishonari niliyekuwa naye walicheka sana.

Pindi nyingine, nilimkariria mwanamke Msamoa maneno niliyokuwa nimepanga kutumia katika kazi ya nyumba kwa nyumba. Baadaye nilikuja kujua kwamba alichoelewa katika mazunguzo yangu yote ni andiko la Ufunuo 21:4 tu. Kwa kuwa aliamini kwamba lazima ujumbe wangu ni muhimu, aliingia ndani ya nyumba, akasoma andiko hilo katika Biblia yake. Andiko hilo moja tu liligusa moyo wake sana hivi kwamba akakubali kujifunza Biblia, sasa yeye na watoto wake ni Mashahidi wa Yehova!

Hata hivyo, mwishowe tulijua vizuri lugha ya Kisamoa na tukafurahia mambo mengi mazuri katika kazi ya kuhubiri. Tulipolazimika kurudi Marekani kwa sababu ya matatizo ya afya, tulihuzunika sana tulipoondoka Samoa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 101, 102]

“Mji Mzima Ulikuja”

Mazishi ya Fred Williams yaliyofanywa miaka ya 1950 mjini Apia yalihudhuriwa na watu wengi isivyo kawaida. Mke wa baharia huyo mstaafu, ambaye wengi walipenda kumwita Kapteni, alikuwa Shahidi wa Yehova. Alikuwa ameabiri katika bahari zote kuu naye alijulikana sana katika Pasifiki ya Kusini. Mojawapo ya mambo yaliyoshangaza watu wengi aliyoyafanya yanatia ndani kuwaokoa wafanyakazi wenzake baada ya meli yao kuzama. Akitumia mashua ya kuokolea, aliwabeba watu hao maelfu ya kilomita hadi kwenye matumbawe yaliyokuwa mbali. Isitoshe walikuwa na chakula kidogo sana.

Kapteni aliona kwamba watu wengi wa dini ni wanafiki. Hata hivyo, mtu huyo aliyekuwa mnywaji wa pombe kali na mcheza-kamari awali alijifunza Biblia na Bill Moss na kuwa Shahidi mwenye bidii. Kufikia wakati alipobatizwa, uwezo wake wa kuona ulikuwa umepungua naye alikuwa mgonjwa sana. Hata hivyo, hakukosa kamwe kuwahubiria wageni wengi waliomtembelea, kutia ndani viongozi wa kidini.

Kapteni alipokufa, wosia wake ulisema kwamba azikwe baharini na mazishi yake yafanywe na Mashahidi wa Yehova. “Ilionekana kana kwamba mji mzima ulikuja kuhudhuria mazishi hayo,” aandika Girlie Moss. “Stesheni ya redio ilitangaza kifo chake, nayo makampuni ya biashara mjini Apia yakapeperusha bendera zao nusu-mlingoti kuonyesha heshima yao.” Mbali na Mashahidi, kulikuwa na wanasheria, walimu, viongozi mashuhuri wa kidini, na wafanyabiashara wengi.

Kila mtu alisikiliza kwa makini wakati msemaji, Bill Moss alipokuwa akisoma maandiko mengi ya Biblia, kufafanua tumaini la Kapteni kufufuliwa na kuishi katika dunia itakayokuwa paradiso. Girlie anasema: “Niliguswa moyo sana kwa sababu alikuwa amepanga ushahidi huo utolewe katika mazishi yake kwa watu wengi sana ambao kwa kawaida si rahisi kuwapata katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Nilimkumbuka Abeli ambaye, ‘ijapokuwa alikufa, bado anasema.’” (Ebr. 11:4) “Kapteni alitoa ushahidi mkubwa kupitia kifo chake.”

Baada ya hotuba ya mazishi iliyotolewa nyumbani kwa Kapteni, msafara wa magari zaidi ya 50 ukaelekea bandarini. Girlie aandika: “Gati lilikuwa limejaa watazamaji mpaka polisi wakalazimika kuwaondoa watu njiani ili tuweze kuingia ndani ya boti. Kisha, sisi na familia yake, balozi, na watu wengine mashuhuri, tukaingia ndani ya boti inayoitwa Aolele (Wingu Linaloruka) na kuabiri kuelekea baharini.” Jina hilo lilifaa sana kwa sababu Bill alilazimika kujishikilia kwenye mlingoti huku boti hilo likitupwa huku na huku baharini nao upepo ukivuma kwa nguvu na kupeperusha mavazi yake na kurasa za Biblia yake. Mwishowe, Bill alisoma ahadi ya Biblia ya kwamba ‘bahari itawatoa wale wafu walio ndani yake’ kisha akatoa sala. (Ufu. 20:13) Kisha, mwili wa Kapteni uliokuwa umefungwa na kuongezwa uzito ukatumbukizwa na kuzama katika maji yenye msukosuko ya Bahari ya Pasifiki, bahari aliyoipenda sana Kapteni. Mazishi hayo yalikumbukwa na watu kwa muda mrefu, yakitokeza nafasi nyingi za kutoa ushahidi.

[Picha]

“Kapteni” Fred Williams kabla ya kubatizwa

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 109, 110]

“Hatukuchoka Kurudi”

FRED WEGENER

ALIZALIWA 1933

ALIBATIZWA 1952

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye pamoja na mke wake Shirley, wanatumikia katika Betheli ya Samoa. Fred ni mshiriki wa Halmashauri ya Nchi.

BAADA ya kufunga ndoa mwaka wa 1956, tulihamia Samoa ya Marekani kutoka Australia ili kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Mgawo wetu wa kwanza ulikuwa Lauli‘i, kijiji kidogo kilicho upande wa mashariki wa Bandari ya Pago Pago. Huko, tulianza kuishi katika kibanda kibovu, ambacho hakikikuwa na milango, madirisha, paa, wala maji ya bomba. Baada ya kukikarabati kidogo, familia yetu ikaongezeka. Wallace Pedro, kijana mwenyeji aliyekuwa amefukuzwa nyumbani na wazazi wake, akaanza kuishi na kuhubiri pamoja nasi.

Miaka miwili baadaye, tulihudhuria Shule ya Gileadi na kutumwa Tahiti tukiwa wamishonari. Hata hivyo, hatukukaa huko kwa muda mrefu. Serikali ilikataa ombi letu la kuwa wamishonari na kutujulisha kupitia barua tuondoke nchini humo haraka iwezekanavyo. Baada ya kurudi Samoa ya Marekani, tulitumikia pamoja na Paul na Frances Evans na pia Ron na Dolly Sellars katika makao ya wamishonari ya Fagatogo huko Pago Pago. Nilichapa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Huduma Yetu ya Ufalme nikitumia mashini ya zamani ya kupiga chapa iliyokuwa katika chumba cha kulia. Mwaka wa 1962, tulipata mgawo wa kuzunguka. Mzunguko wetu wa kwanza ulitia ndani sehemu kubwa ya Pasifiki ya Kusini, kutia ndani Samoa ya Marekani, Visiwa vya Cook, Fiji, Kiribati, Niue, Samoa, Tonga, Tuvalu, na Vanuatu.

Miaka minane baadaye, mwana wetu Darryl alizaliwa, nasi tukaacha kuzunguka na kukaa Samoa ya Marekani. Nilitumikia nikiwa painia wa pekee, naye Shirley alitumia muda wake mwingi akitafsiri vitabu na magazeti ya Biblia katika Kisamoa.

Wakati huo pia, nilifanya kazi pamoja na Shahidi mzamia koa ili kukimu mahitaji ya familia. Mtambo wa mashua yake uliharibika, nasi tukakaa baharini kwa siku nne. Mawimbi yalitupeleka mamia ya kilomita, tukakumbwa na dhoruba kali, tukaona meli 32 zikipita, na hata karibu tugongwe na meli kubwa ya makontena kabla ya kuokolewa. Muda mfupi baadaye, Shirley nami tukagundua kwamba tunatarajia kupata mtoto mwingine. Kwa hiyo, mwaka wa 1974, tukaamua shingo upande kurudi Australia, ambako binti yetu, Tamari, alizaliwa.

Miaka iliyofuata, tulifikiria mara nyingi kurudi katika mgawo wetu wa umishonari tulioupenda sana. Wazia shangwe yetu wakati ambapo Shirley nami tulipoombwa turudi Samoa mwaka wa 1995 pamoja na Tamari, kutumikia Betheli. Mwaka mmoja baadaye, Shirley nami tuliombwa turudi katika kazi ya kuzunguka—miaka 26 baadaye! Tulishangilia kama nini kukutana na ndugu na dada wengi wa zamani tuliokuwa tumefanya kazi pamoja nchini Samoa, Samoa ya Marekani, na Tonga!—3 Yohana 4.

Leo, Shirley nami pamoja na Tamari na mume wake, Hideyuki Motoi, tunatumikia Betheli ya Samoa. Tunafurahi kama nini kwamba hatukuchoka kurudi!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 113, 114]

“Yehova Amejibu Sala Zangu”

FAIGAAI TU

ALIZALIWA 1932

ALIBATIZWA 1964

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuwa painia katika visiwa vya Upolu na Savaii tangu mwaka wa 1965 mpaka 1980. Sasa anaishi Savaii.

NILIZALIWA nikiwa na miguu iliyojipinda vibaya na kwa sababu hiyo ilikuwa vigumu sana kwangu kutembea.

Nilipoisikia kweli kwa mara ya kwanza, ilipenya moyoni mwangu. Nilitamani kuhudhuria mikutano ya kutaniko lakini ilikuwa vigumu kwangu kutembea kwa miguu mitupu katika barabara yenye mawe ili kufika huko. Mwishowe nikawa stadi wa kujitengenezea viatu vyangu mwenyewe kutokana na malapa nami ningeweza kutembea bila shida.

Nilianza upainia baada tu ya kubatizwa. Kisha baada ya kufanya upainia kwa miaka tisa katika kisiwa cha Upolu, mimi na dada yangu na mume wake tulihamia Savaii, palipokuwa na uhitaji wa wahubiri wa Ufalme. Mimi na mpwa wangu, Kumi Falema‘a, tulitumikia tukiwa mapainia wa pekee katika eneo hili.

Nikiwa pamoja na Kumi, tulisafiri kwa basi kila juma kutoka Faga mpaka Lata, kijiji kidogo kilicho upande wa pwani ya magharibi ya Savaii. Baada ya kujifunza na mwanamke mmoja kijijini Lata, tulitembea kilomita nane kwenda Taga kujifunza na mwanamke mwingine. Tulilala kwa mwanamke huyo na kurudi Faga siku iliyofuata kwa basi la asubuhi. Tulifanya hivyo kwa miaka miwili hivi. Inafurahisha kwamba wanawake hao wawili pamoja na familia zao ni Mashahidi wenye bidii.

Familia yetu ilipoondoka Savaii, nilibaki ili kushughulikia kikundi kidogo cha akina dada na wanawake fulani wenye kupendezwa kijijini Faga. Niliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko na kuhubiri pamoja na akina dada hao katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Mara moja kila mwezi mzee mmoja kutoka Apia alikuja kuongoza mikutano ya Jumapili. Kwa kuwa chifu wa kijiji alitukataza kuimba nyimbo za Ufalme katika mikutano yetu, tulisoma maneno ya nyimbo hizo kwa sauti. Miaka mitano baadaye, wamishonari wawili, Leva na Tenisia Faai‘u, walikuja kutoka New Zealand kusaidia kikundi chetu kidogo. Wengine wakafuata. Leo, kisiwa cha Savaii kina makutaniko mawili yenye maendeleo, moja liko Faga na lingine Taga.

Ingawa sikuwahi kuolewa, ninapenda watoto na kila wakati ninakuwa karibu nao. Watoto wengine hata waliishi nami kwa muda. Kuona “watoto” wangu wa kiroho wakifanya maendeleo na kubaki waaminifu kwa Yehova kunanipa shangwe.

Sasa nimezeeka na siwezi tena kutembea kutoka nyumba moja hadi nyingi. Mimi huongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwangu na kuwahubiria watu ninaokutana nao hospitalini. Hata hivyo, hali yangu ilinitamausha, nami nilisali kwa Yehova na kumwomba anisaidie nifanye mengi zaidi. Kisha, wamishonari katika kutaniko letu wakanifundisha jinsi ya kuhubiri kwa kutumia simu. Ninapotazama maisha yangu, ninaona kwamba kwa kweli Yehova amejibu sala zangu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 118]

Jana, Leo, na Kesho

Saa za wakaaji wa Samoa na Tonga hulingana, ijapokuwa kulingana na kalenda, Tonga iko mbele kwa siku moja! Kwa nini? Samoa na Tonga ziko pande mbili tofauti za mstari wa tarehe wa kimataifa—Tonga ikiwa upande wa magharibi nayo Samoa ikiwa upande wa mashariki. Hivyo, hata ingawa nchi hizo zinapakana, Tonga ni kati ya nchi za kwanza ulimwenguni kuadhimisha Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo, huku Samoa ikiwa kati ya nchi za mwisho kuuadhimisha.

[Mchoro]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

\

\

\

\

\ SAMOA

| Saa 1:00 jioni

| Jumatano

|

|

|

|

|

TONGA |

Saa 1:00 jioni | BAHARI YA PASIFIKI YA KUSINI

Alhamisi |

|

|

Mstari wa Tarehel | wa Kimataifa

|

| NIUE

|

|

|

|

|

|

|

|

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 123, 124]

Tafsiri ya Biblia Inayotumia Jina la Mungu

Mwaka wa 1884, wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo walichapisha tafsiri ya Biblia katika lugha ya Kisamoa ambayo ilitumia jina Yehova kotekote katika Maandiko ya Kiebrania. Pia, mara nne katika Maandiko ya Kigiriki jina la Mungu linapatikana likiwa limefupishwa katika neno Aleluia, linalomaanisha “Msifuni Yah.” (Ufu. 19:1-6) Hata hivyo, toleo la mwaka wa 1969 la tafsiri hiyo liliondoa kabisa jina Yehova katika mistari yote isipokuwa mstari mmoja tu—ambapo inaonekana watafsiri walilisahau! (Kut. 33:14) Viongozi wa makanisa pia waliliondoa jina la Mungu kutoka katika vitabu vyao vya nyimbo, na kuwaaambia waumini wao wasilitumie jina la Yehova.

Hata hivyo, mnamo Novemba 2007, watu wanaopenda Biblia nchini Samoa walifurahi kupokea Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Kisamoa. Tafsiri hiyo sahihi, inayoeleweka kwa urahisi imelirudisha jina la Mungu mahali pake. Geoffrey Jackson, aliyekuwa mmishonari chini Samoa na sasa ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitangaza kutolewa kwa Biblia hiyo mpya wakati wa kusanyiko la wilaya la pekee kwa ajili ya visiwa hivyo, lililofanywa jijini Apia, Samoa.

Ripoti ya kutolewa kwa Biblia hiyo iliyotangazwa kwenye televisheni ilivutia watu wengi. Watu fulani waliipigia simu Betheli ya Samoa wakiomba Biblia hiyo. Ofisa mkuu wa serikali aliomba nakala kumi ili awape wafanyakazi katika ofisi yake. Mkuu wa shule moja aliomba nakala tano ili awape wanafunzi bora mwishoni mwa muhula.

Watu wengi wamesifu tafsiri hiyo mpya kwa usahihi wake, jambo linalofanya iwe rahisi kuelewa kilichomaanishwa katika maandiko ya awali. Pia, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inawasaidia Wasamoa kujua umuhimu wa kulitumia jina la Mungu. Finau Finau, painia wa pekee huko Vailele, Upolu, alitumia sala ya kielelezo ya Yesu kumsaidia mwanamke fulani kuelewa umuhimu wa kulitumia jina la Mungu.

Baada ya kusoma Mathayo 6:9, Finau alimuuliza, “Unafikiri ni jina la nani linalopaswa kutakaswa?”

Mwanamke huyo akajibu, “La Bwana.”

“Lakini andiko la 1 Wakorintho 8:5 linasema kuna ‘miungu mingi’ na ‘mabwana wengi,’” Finau akaeleza. “Jina la Mungu linawezaje kuwa Bwana ilhali kuna miungu mingi ya uwongo inayoitwa hivyohivyo?”

Kisha akamwonyesha mwanamke huyo jina Yehova na kumweleza kwamba dini zinazodai kuwa za Kikristo zimeliondoa jina hilo katika Biblia zao. Ili kumsaidia aelewe hoja hiyo vizuri, aliongeza hivi: “Ikiwa mtu angejaribu kuondoa au kubadili jina la ukoo wenu, mngehisije?”

Akajibu, “Tungekasirika.”

“Kweli kabisa,” akajibu Finau, “na hivyo ndivyo Yehova anavyohisi watu wanapojaribu kuliondoa jina lake kutoka katika Neno lake.”

[Picha]

“Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo” katika Kisamoa

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 126, 127]

“Yehova Amenibariki Sana”

LUMEPA YOUNG

ALIZALIWA 1950

ALIBATIZWA 1989

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Ni binti ya aliyekuwa waziri mkuu, naye sasa ni painia wa kawaida jijini Apia.

NILILELEWA katika kisiwa cha Savaii, nikiwa binti ya mfanyabiashara na mwanasiasa mashuhuri. Kwa kuwa baba yangu alimiliki shamba kubwa la kakao naye alikuwa ameajiri wafanyakazi 200 hivi, magazeti ya Samoa yalikuwa yakimwita Bwana-Kakao, na kwa miaka mingi alikuwa waziri mkuu wa Samoa.

Nilikuwa mmoja kati wa watoto 11. Baba hakuwa mtu wa dini sana, lakini mama alitufundisha mambo ya msingi ya Biblia. Nilihuzunika sana alipokufa. Hivyo, Judy Pritchard, dada mmishonari, aliponihubiria kuhusu tumaini la ufufuo, wazo la kwamba ningeweza kumwona tena mama yangu lilinisisimua!

Nilimuuliza Judy maswali mengi, naye aliyajibu yote kwa kutumia Biblia. Muda si muda tukaanza kujifunza Biblia pamoja. Kisha nikaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi.

Mwanzoni, mume wangu, Steve, shemasi aliyejulikana sana katika kanisa letu la kijijini, alinipinga. Alinipeleka kwa viongozi mbalimbali wa kidini waliojaribu kunivunja moyo niache kuhudhuria mikutano ya Mashahidi. Lakini sikuwasikiliza. Kisha alinipeleka kwa baba yangu, ambaye alichofanya tu ni kupendekeza nijifunzie Biblia mahali pengine lakini si nyumbani. Hata hivyo, ndugu na dada zangu wa kimwili walinidhihaki kwa kubadili dini yangu. Lakini sikuacha kujifunza kweli ya Biblia.

Hatimaye, nilipostahili kuwa mhubiri wa Ufalme, nyumba ya kwanza tuliyofika ilikuwa ya waziri mmoja katika baraza la mawaziri la baba yangu. Alikuwa amehudhuria mikutano mingi ya kisiasa nyumbani kwetu, naye alinifahamu vizuri. Niliogopa sana, nami nikajificha nyuma ya mhubiri mwenzangu! Watu walishangaa kuniona nikihubiri, wakawa wakiniuliza, “Baba yako anaonaje kazi hii unayofanya?” Hata hivyo, Baba yangu alinielewa, naye aliitetea imani yangu mpya. Isitoshe, kufikia wakati huo alikuwa akisoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

Mwishowe, niliacha kuwaogopa wanadamu nami nikawa painia wa kawaida. Ninapenda sana kuongoza mafunzo ya Biblia, nami huweka orodha ya watu 50 hivi wanaopendezwa na ambao ninaweza kujifunza nao ninapopata nafasi katika ratiba yangu. Hata hivyo, shangwe yangu kubwa inatokana na kuwafundisha kweli watoto wangu wanne. Binti yangu Fotuosamoa na mwana wangu Stephen pamoja na wenzi wao wa ndoa, Andrew na Ana, sasa wanatumika Betheli ya Samoa. Pia, nilimsaidia dada yangu Manu kujifunza kweli. Hata mume wangu, Steve, aliyekuwa akinipinga, alianza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano. Kwa kweli, Yehova amenibariki sana.

[Picha]

Kushoto: Fotuosamoa na Andrew Coe; kulia: Ana na Stephen Young

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 129, 130]

Kuchagua Kati ya Yehova na Kuwa Mchezaji-Gofu wa Kulipwa

LUSI LAFAITELE

ALIZALIWA 1938

ALIBATIZWA 1960

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Aliamua kuwa painia badala ya kuwa mchezaji-gofu wa kulipwa.

NILIKUWA na umri wa miaka 18 nilipopata kujua kwamba familia moja iliyokuwa ikiishi ng’ambo ya barabara ilikuwa imejiunga na dini inayoitwa Mashahidi wa Yehova. Nikiwa na hamu ya kujua ni kwa nini wanamwita Mungu Yehova, nilimtembelea baba yao, Siemu Taase ili kumuuliza. Nilivutiwa na upole wake na jinsi alivyotumia Maandiko. Alianza kunifundisha Biblia nami nikaanza kuhudhuria mikutano. Baba yangu alipopata kujua nilichokuwa nikifanya, alinitisha. Nilimsihi aniruhusu nihudhurie mikutano, lakini akasisitiza kwamba niache kabisa kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, jambo la kushangaza ni kwamba siku iliyofuata alibadili nia yake. Baadaye, shangazi yangu aliniambia, “Usiku wa jana, ulikuwa ukisema-sema, ‘Yehova, tafadhali nisaidie!’” Haikosi nilikuwa nikiota huku nikuzungumza kwa sauti. Jambo la kupendeza ni kwamba maneno yangu yaliugusa moyo wa baba.

Pia, ng’ambo ya barabara ndipo kulipokuwa na uwanja wa pekee wa gofu nchini Samoa, na hapo ndipo nilifanya kazi ya kutafuta na kuuza mipira ya gofu ili kupata pesa kidogo. Baadaye, nilifanya kazi ya kumbebea Mfalme Malietoa vigoe vya gofu. Wakati huo, mfalme huyo ndiye alikuwa kiongozi wa serikali ya Samoa. Mfalme aliona kuwa ninaweza kuwa mchezaji mzuri wa gofu naye akanipa vigoe vyake vya zamani. Pia, alipanga wafanyabiashara wawili wanifadhili ili niwe mchezaji-gofu wa kulipwa. Aliamini kwamba uchezaji wangu wa gofu “ungeiletea Samoa sifa.” Nilifurahi wee! Lakini, punde si punde mchezo wa gofu ulianza kunikengeusha katika utumishi wangu kwa Yehova, nayo dhamiri yangu ikaanza kunisumbua.

Nilijikuta njia panda nilipowashinda wachezaji wa kulipwa wa kimataifa katika Mashindano ya Gofu ya Samoa. Mfalme alifurahi sana naye alitaka nikutane na mchezaji maarufu kutoka Marekani katika dhifa ya kukabidhiwa zawadi jioni hiyo. Nikiwa na wasiwasi, nilijiambia: ‘Huu ndio wakati wa kufanya uamuzi. Utachagua gofu au Yehova?’ Jioni hiyo nikaamua kwenda kwenye mazoezi ya kusanyiko la mzunguko badala ya kwenda kwenye dhifa hiyo.

Mfalme alikasirika sana. Baba yangu alipotaka kujua sababu ya uamuzi wangu, nilizungumza naye kwa muda mrefu na kumweleza kwa kutumia Biblia kwa nini kumtumikia Yehova ni muhimu sana kwangu. Nilishangaa alipoanza kutoa machozi. Kisha akaniambia: “Ulipokuwa na umri wa miaka mitano, ulikuwa mgonjwa sana nao madaktari wakasema kwamba umekufa. Tulipokuwa tukikushusha kaburini, nyuki alikuuma usoni. Ghafula, ukapiga kelele na kuanza kulia, kabla tu ya kukufukia! Sasa naamini kwamba uliokolewa ili uwe shahidi wa Yehova Mungu.” Tangu siku hiyo, hakunipinga tena kamwe.

Baada ya kuhamia New Zealand, nilitumikia kwa miaka kumi nikiwa painia wa kawaida kisha painia wa pekee, na nikamwoa Robyn, ambaye pia alikuwa painia wa pekee. Kisha tukapata watoto watatu na kuhamia Australia. Kwa miaka 30 iliyofuata, nilifanya kazi ya kimwili ya wakati wote ili kuitegemeza familia yangu. Katika kipindi hicho, tuliwasaidia watu wengi wa ukoo wetu kujifunza kweli. Mara nyingi nilimwomba Yehova anisaidie kurudia upainia. Wazia shangwe yangu nilipoutimiza mradi wangu hatimaye, baada ya kustaafu mwaka wa 2004. Nina furaha kama nini kwamba nilichagua kumtumikia Yehova badala ya kuwa mchezaji-gofu wa kulipwa!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 135]

Mazoezi ya Wazazi Yazaa Matunda

PANAPA LUI

ALIZALIWA 1967

ALIBATIZWA 1985

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na mke wake, Mareta, ni mapainia wa pekee nchini Samoa.

TULIPOMPELEKA mwana wetu, Sopa katika shule ya msingi, nilimpa mwalimu mkuu broshua ya Mashahidi wa Yehova na Elimu na kumweleza msimamo wetu kuhusu mambo ya kidini na masuala ya kitaifa.

Hata hivyo, siku iliyofuata Sopa alituambia kwamba mwalimu mkuu aliirarua-rarua broshua hiyo mbele ya wanafunzi wote na walimu, kisha akawaamuru watoto wa Mashahidi waimbe wimbo wa kidini. Walipokataa, akawaamuru wasimame mbele ya wanafunzi wote na kuimba wimbo wa dini yao. Alifikiri kwamba hilo lingewababaisha na kuwafanya wakubali kujiunga na wanafunzi wengine wanapoimba nyimbo za dini. Lakini Sopa aliwachochea watoto wenzake wa Mashahidi, “Tuwaimbie ‘Asante, Yehova,’” kisha akawaongoza wengine katika kuimba wimbo huo.

Mwalimu mkuu alivutiwa sana naye akampongeza Sopa kwa ujasiri huo. Baadaye, yeye na walimu wengine walipendezwa na kweli. Wakati wowote tunapokutana na mwalimu huyo, yeye hutusalimu na kutaka kujua Sopa anaendeleaje, naye hutuambia tumsalimu. Sopa alifanya maendeleo kiroho naye akabatizwa mwaka wa 2005.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 138, 139]

“Safari ya Kwenda Mikutanoni Si Ndefu”

VALU LOTONUU

ALIZALIWA 1949

ALIBATIZWA 1995

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Yeye na watoto wake sita walikuwa wakitembea kilomita 22, wakipita milima na mabonde ili kuhudhuria mikutano.

MWAKA wa 1993, tulipokuwa tukiishi Lefaga, Mashahidi wa Yehova walitutembelea nyumbani, nami nikakubali kujifunza Biblia. Muda mfupi baadaye, mimi na watoto wangu tukaanza kuhudhuria mikutano iliyokuwa ikifanyiwa Faleasiu, kilomita 22 upande wa pili wa kisiwa.

Siku za mikutano ya katikati ya juma, nilikuwa nikiwachukua watoto kutoka shuleni mapema. Walimu fulani walitishia kuwafukuza shuleni mpaka nilipowaeleza kwamba kuhudhuria mikutano ni muhimu kwetu kiroho. Kila mtoto alikuwa akibeba nguo zake za mikutano, Biblia, kitabu cha wimbo, na kitabu cha funzo katika mfuko wa plastiki. Nyakati nyingine tungepata lifti kwenye basi, lakini mara nyingi tulitembea kilomita zote 22 kwa miguu.

Tulipofika katika Jumba la Ufalme la Faleasiu baada ya safari hiyo ndefu, Mashahidi wenyeji walitukaribisha na kutupa chakula. Pia tulioga na kuvaa nguo safi kwa ajili ya mikutano. Baada ya mikutano tulianza tena safari ya kurudi nyumbani. Tulipofika juu ya mlima unaogawanya kisiwa hicho mara mbili, tulipumzika kidogo ili watoto wapate angaa usingizi kidogo. Walipokuwa wakipumzika, nilikaa macho kuona endapo gari lolote lingeweza kutupa lifti ya kurudi nyumbani. Mara nyingi tulifika nyumbani usiku wa manane. Asubuhi iliyofuata, saa 11 asubuhi, nilikuwa tayari nimeamka, nikisubiri basi la kwanza kwenda Faleasiu, ili kuhubiri.

Pindi moja, niliambiwa nifike mbele ya kikao cha matai wa kijiji. Kikao hicho kilisimamiwa na chifu mkuu wa kijiji. Walitaka kujua ni kwa nini ninasafiri mbali hivyo kwenda Faleasiu badala ya kushirikiana na kanisa lililo kijijini kwetu, hasa kanisa lililoanzishwa na babu yangu. Mwishowe wakaniamuru niache kwenda Faleasiu kuhudhuria mikutano. Hata hivyo sikukubali chochote kinizuie kuhudhuria mikutano. Niliazimia kumtii Mungu kuliko wanadamu.—Mdo. 5:29.

Punde si punde mambo yakaenda mrama. Nilipokosa kuhudhuria toonai (karamu ya Jumapili iliyohudhuriwa na wahudumu wa kanisa, mashemasi, na matai wa kijiji) baraza hilo lilinipiga faini ya nguruwe watano wakubwa. Huo ulikuwa mzigo mkubwa kwangu, hasa kwa sababu nilikuwa na watoto sita nami sikuwa na mume. Hata hivyo, mwishowe nililipa faini hiyo. Kadiri muda ulivyopita, watu kijijini waliheshimu msimamo wetu nao wakaacha kutupinga.

Kuhudhuria mikutano kwa miaka yote hiyo kulihitaji jitihada nyingi. Lakini haikuwa kazi bure. Watoto wangu wote ni Mashahidi wenye bidii, na mwana wangu mmoja ni mtumishi wa huduma.

Hadi leo hii, bado mimi na watoto wangu huenda mikutanoni kwa miguu. Hata hivyo, hatutembei kilomita 22 kwenda Faleasiu. Sasa Jumba la Ufalme liko karibu. Mwaka wa 2001, Jumba maridadi la Ufalme lilijengwa katika kijiji chetu, nalo kutaniko letu linazidi kukua. Kwa hiyo, hata sasa safari ya kwenda mikutanoni si ndefu!

[Chati/Grafu katika ukurasa wa 132, 133]

MFUATANO WA MATUKIO—Samoa

1930

1931 Habari njema yafika Samoa.

1940

1940 Harold Gill agawanya kijitabu Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?), kichapo cha kwanza kabisa cha Kisamoa.

1950

1953 Kutaniko la kwanza laanzishwa Apia.

1955 Wamishonari wa Gileadi wawasili Samoa ya Marekani.

1955 Filamu yenye kichwa The New World Society in Action yaonyeshwa kotekote nchini Samoa ya Marekani.

1957 Kusanyiko la kwanza la mzunguko lafanywa nchini Samoa ya Marekani.

1958 Gazeti la Mnara wa Mlinzi laanza kutafsiriwa katika Kisamoa.

1959 Kusanyiko la mzunguko la kwanza lafanywa Samoa ya Magharibi.

1960

1970

1974 Wamishonari wawasili Samoa. Kazi ya kuhubiri yaanza Tokelau.

1980

1984 Ofisi ya tawi yaanzishwa katika makao ya wamishonari ya Sinamoga, Apia.

1990

1991 Kimbunga Val chaharibu visiwa.

1993 Gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kisamoa lachapishwa sambamba na toleo la Kiingereza. Kuwekwa wakfu kwa makao mapya ya Betheli na Jumba la Kusanyiko.

1996 Kipindi kinachoitwa “Maswali Yako ya Biblia Yajibiwa” charushwa hewani kila juma kupitia redio ya FM.

1999 Kazi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme yasonga mbele haraka.

2000

2007 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yatolewa katika Kisamoa.

2010

[Grafu]

(See publication)

Jumla ya Wahubiri

Jumla ya Mapainia

700

400

100

1930 1940 1950 1960 1970 1980 1990 2000 2010

[Picha]

Frances na Paul Evans

[Ramani katika ukurasa wa 73]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

HAWAII

AUSTRALIA

NEW ZEALAND

TOKELAU

Kisiwa cha Swains

SAMOA

SAMOA YA MAREKANI

Visiwa vya Manu‘a

Kisiwa cha Rose

BAHARI YA PASIFIKI YA KUSINI

NIUE

Mstari wa Tarehe wa Kimataifa Jumatano (Siku ya 3)

‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐‐

Alhamisi (Siku ya 4)

TONGA

SAMOA YA MAREKANI

Tutuila

PAGO PAGO

Petesa

Tafuna

Fagatogo

Lauli‘i

‘Aunu‘u

SAMOA

Savaii

Aopo

Lata

Taga

Faga

Salimu

Fogapoa

Upolu

APIA

Faleasiu

Siusega

Vailele

Lefaga

Vava‘u

APIA

Vaiala

Faatoia

Sinamoga

[Picha katika ukurasa wa 66]

[Picha katika ukurasa wa 74]

Pele na Ailua Fuaiupolu, Wasamoa wa kwanza kujiweka wakfu kwa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 81]

Ron na Dolly Sellars walihamia Samoa mwaka wa 1953 kutumikia katika eneo lenye uhitaji

[Picha katika ukurasa wa 84]

Richard na Gloria Jenkins, siku ya harusi yao, Januari 1955

[Picha katika ukurasa wa 85]

Girlie na Bill Moss wakiwa njiani kuelekea Samoa

[Picha katika ukurasa wa 95]

Nyumba ya Kisamoa

[Picha katika ukurasa wa 100]

Jumba la Ufalme lililojengwa mjini Apia lilikuwa la kwanza nchini Samoa

[Picha katika ukurasa wa 107]

Jumba la Ufalme la kwanza la Tafuna, nchini Samoa ya Marekani

[Picha katika ukurasa wa 115]

Metusela Neru

[Picha katika ukurasa wa 116]

Saumalu Taua‘anae

[Picha katika ukurasa wa 131]

Ane Ropati (anayeitwa Gauld sasa) alichukua msimamo wake upande wa Yehova akiwa kijana

[Picha katika ukurasa wa 141]

Ofisi na Betheli ya Samoa

Halmashauri ya Nchi ya Samoa: Hideyuki Motoi, Fred Wegener, Sio Taua, na Leva Faai‘u

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki