Ni nani awezaye kukubali funzo la Biblia?
1 Nabii Amosi alitangaza kwamba kungekuwa njaa katika bara la Israeli, “si njaa ya chakula wala kiu cha maji lakini kwa kusikia maneno ya BWANA.” (Amo. 8:11) Kwa faida ya wale walio na njaa na kiu cha kiroho, tengenezo la Yehova linagawa kiasi kikubwa cha vichapo vya kibiblia ulimwenguni pote.
2 Mpaka sasa, tumechapa vitabu Ujuzi milioni 70 na broshua Anataka milioni 91. Katika kufundisha kweli, tunathamini urahisi na matokeo ya vichapo hivyo. Hata hivyo, kwa kweli, umati wa watu ambao wamepokea vichapo vyetu bado hawajajifunza Biblia pamoja nasi. Tunaweza kufanya nini kuhusu hilo?
3 Kila kichapo tunachoachia watu ni funzo linalowezekana! Fikiria jambo lililoonwa la mhubiri aliyependekeza funzo kwa mwanamke fulani mara ya kwanza alipozungumza naye kwenye mlango. Mwanamke huyo alikubali mara moja. Baadaye akamwambia mhubiri, “Wewe ndiwe mtu wa kwanza ambaye amewahi kupendekeza kujifunza Biblia pamoja nami.” Katika eneo lenu, ni watu wangapi wenye kuwa tayari na vichapo vyetu ambao wanaweza kusema jambo hilohilo? Kila kichapo tunachoachia watu kinatoa nafasi kwa ziara za kurudia na funzo la Biblia la nyumbani.
4 Kwa kuwa mara nyingi tunakuta watu ambao tayari wana vitabu vyetu, tunawezaje kuchochea kupendezwa kwao na kujifunza yale yaliyo katika vichapo vyetu? Shahidi mmoja aliuliza moja kwa moja msikilizaji ikiwa alikuwa na maulizo ya Biblia. Mwanamke huyo akajibu, “Hapana.” Dada akasisitiza, “Bila shaka una maulizo fulani.” Kwa kweli mwanamke huyo alikuwa nayo, na funzo likasitawishwa. Kwa nini usimuulize msikilizaji ikiwa angetaka kujifunza maoni ya Biblia kuhusu swali au jambo fulani linalomhusu? Uwe tayari kutokeza ulizo lenye kupendeza ikiwa yeye hawezi kufikiria jambo fulani. Mazungumzo kama hayo yanaweza kutoa nafasi kwa funzo la kawaida la kweli za Biblia za msingi.
5 Utendaji wa kuongoza mafunzo ya Biblia ndilo jambo la maana zaidi la huduma yetu. Kwa kuwa hatujui kamwe ni nani anayeweza kukubali funzo, usisite kupendekeza hilo kwa kila mtu unayekutana naye. Mjulishe Yehova jambo hilo katika sala, na utumike kupatana na sala zako. Unaweza kuona upesi kwamba mtu fulani unayetolea funzo la Biblia atalikubali!—1 Yn. 5:14, 15.