Kutilia Biblia Mkazo Zaidi!
1 Katika Oktoba 1, 1919, toleo la kwanza la gazeti Âge d’Or lilichapichwa. Lilionekana kuwa chombo cha thamani sana katika kazi ya kuhubiri. Kwa nini? Kwa kuwa lilifanywa hasa kwa ajili ya watu wote. Lakini haikuwa hivyo kuhusu gazeti Mnara wa Mlinzi, ambalo muda wa miaka mingi, lilionwa kuwa gazeti lililohusu hasa “Kundi dogo.” (Luka 12:32) Wahubiri wa Ufalme walipokea kwa shauku kichapo hicho kipya hivi kwamba kwa muda wa miaka mingi ugawaji wa gazeti Âge d’Or ulizidi sana ule wa Mnara wa Mlinzi.
2 Gazeti Âge d’Or lilichapishwa ili kuonyesha watu kwamba suluhisho la kweli kwa matatizo ya wanadamu ni Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo, ambao utaingiza wanadamu katika enzi bora. Mnamo miaka iliyofuata, gazeti Âge d’Or lilifanyiwa marekebisho fulani yaliyohitajiwa ili lipambane na mabadiliko ya nyakati hizo. Katika 1937 jina layo lilibadilishwa na kuwa Consolation. Katika 1946 likachukua jina la Amkeni!, jina tunalojua leo.
3 Tangu lilipoanza, gazeti hili liliongeza kwa nguvu ushahidi mkubwa ambao umetolewa tangu 1919. (Mt. 24:14) Hata hivyo, kwa sababu ya uharaka wa nyakati zetu, imeonekana kuwa jambo la hekima kufanyia gazeti Amkeni! marekebisho zaidi.
4 Mamilioni ya watu wanafurahia kusoma gazeti Amkeni! kwa kuwa linazungumzia habari mbalimbali nyingi zisizo za kidini katika njia yenye kuvutia. Bila shaka watu wengi wanaohudhuria Ukumbusho kila mwaka ni wasomaji wa kawaida wa gazeti Amkeni! Hata hivyo, ikiwa mtu yeyote anatumaini kufichwa katika “siku ya kasirani ya Yehova,” atahitaji msaada ili kufanya zaidi kuliko tu kuwa msomaji wa kawaida wa vichapo vyetu.—Sef. 2:3; Ufu. 14:6, 7.
5 Kwa hiyo, kuanzia Januari 2006, gazeti Amkeni! litatilia mkazo zaidi Ufalme wa Mungu. Litatia moyo wasomaji kutafuta moja kwa moja suluhisho kuhusu matatizo yao katika Biblia na litaonyesha kwa njia yenye kutokeza zaidi maelezo ya Biblia kuhusu matukio ya kisasa. Katika njia hiyo, wasomaji wataelewa vizuri zaidi matukio ya kisasa na huenda watachochewa na yale wanayosoma ili kujifunza mengi zaidi kuhusu Yehova.—Zek. 8:23.
6 Gazeti Amkeni! litaendelea kukazia habari zenye kupendeza kwa ujumla. Hata hivyo, mkazo utatiliwa sana kwenye Biblia. (1 The. 2:13) Kwa kuwa gazeti Mnara wa Mlinzi linazo habari za Kibiblia zenye kina na kwa kuwa gazeti Amkeni! litakazia habari zaidi za Kimaandiko, inaonekana kuwa si lazima kuendelea kuchapisha Amkeni! mara mbili katika mwezi. Kwa hiyo, kuanzia toleo la Januari 2006, gazeti Amkeni! litachapishwa mara moja kwa mwezi. Jambo hilo litafanya iwe rahisi kutayarisha, kutafsiri, na kusafirisha vichapo vyetu.
7 Badiliko hilo litagusa asilimia 40 hivi ya lugha ambazo katika hizo gazeti Amkeni! linachapishwa. Katika lugha nyingi, Amkeni! ni kichapo kinachochapishwa mara moja kila mwezi au mara nne katika mwaka. Hakutakuwa na badiliko katika kuchapishwa kwa Mnara wa Mlinzi.
8 Wahubiri wanaweza kutolea watu Amkeni! ya kila mwezi pamoja na matoleo mawili ya Mnara wa Mlinzi ya kila mwezi. Wale wanaotolea watu Amkeni! watakuwa na uwezekano wa kutumia toleo hilohilo mnamo mwezi mzima bila kubadili utoaji wao katikati ya mwezi kama tunavyofanya sasa.
9 Kuanzia toleo lake la kwanza katika 1919, gazeti lililojulikana kwa jina la Âge d’Or, Consolation, na sasa Amkeni! limekuwa na fungu la maana katika kazi ya kuhubiri. Tunasali hivi kwamba Yehova aendelee kubariki ugawanyaji wa gazeti hili katika chapa lake lililorekebishwa na kwamba lisaidie watu wengine wengi zaidi kutoka “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” watazamie Ufalme wa Mungu kuwa tumaini lao pekee.—Ufu. 7:9.
[Maulizo ya Funzo]
1. Hapo mwanzoni, gazeti Mnara wa Mlinzi lilichapishwa hasa kwa ajili ya nani, na gazeti Âge d’Or lilichapishwa kwa ajili ya nani?
2. Gazeti Âge d’Or linaitwa namna gani leo, na kusudi layo limekuwa nini tangu mwanzoni?
3. Gazeti Amkeni! limekuwa chombo chenye nguvu katika kutimiza unabii gani?
4. (a) Mtu anahitaji kufanya nini ikiwa atafichwa katika “siku ya kasirani ya Yehova”? (b) Kulingana na Ufunuo 14:6, 7, ‘malaika anayeruka katikati ya mbingu’ anaalika wote kufanya nini?
5. (a) Kuanzia Amkeni! ya Januari 2006, ni jambo gani litakalokaziwa kwa njia yenye kutokeza zaidi? (b) Wengi huenda watachochewa kufanya nini, nalo ni utimizo wa unabii gani?
6, 7. (a) Gazeti Amkeni! litasaidiaje wengi kutumia 1 Wathesalonike 2:13? (b) Gazeti Amkeni! litachapishwa mara ngapi, na badiliko hilo litakuwaje na uvutano juu ya lugha nyingi?
8. Wahubiri wanaweza kutumia Amkeni! na Mnara wa Mlinzi namna gani?
9. Gazeti Amkeni! litaendelea kuwa na fungu gani?