Uwe Muhubiri Mwenye Kufanya Maendeleo
1. Ni mifano gani ya siku za mitume ambayo inaonyesha kwamba tunapaswa kuwa wahubiri wenye kufanya maendeleo?
1 Wakristo wanapaswa kufanya maendeleo katika mahubiri. Ndio sababu Yesu alipatia wanafunzi wake mazoezi ambayo yaliwasaidia wakomalishe ufundi wao wa kuhubiri. (Lu. 9:1-5; 10:1-11) Sababu hiyo ilifanya pia Akila na Prisila wamuchukue Apolo na ‘kumufafanulia [kumufasiria] kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.’ (Mdo. 18:24-26) Sababu hiyo hiyo ilimuchochea Paulo amutie moyo Timotheo aendelee kukomalisha ufundi wake wa kufundisha, ili maendeleo yake “yawe wazi kwa watu wote.” (1 Tim. 4:13-15) Hata kama tumekuwa wahubiri wa habari njema kwa muda murefu, tuna lazima ya kuendelea kukomalisha ufundi wetu wa kuhubiri.
2. Tunaweza kuiga wengine namna gani?
2 Iga Wengine: Njia moja ya kutusaidia tukomalishe ufundi wetu wa kuhubiri ni kuiga wengine. (Met. 27:17) Kwa hiyo, wakati muhubiri mwenzako anaanzisha mazungumuzo, fuata kwa uangalifu. Omba wahubiri wenye uzoefu mashauri, na usikilize mapendekezo yao kwa uangalifu. (Met. 1:5) Utafanya nini ikiwa uko na matatizo ya kurudilia watu, kuanzisha funzo la Biblia, ao kufanya sehemu ingine ya mahubiri? Omba mwangalizi wa kikundi chenu cha mahubiri ao ndugu mwengine mwenye uzoefu akuzoeze. Pia kumbuka kwamba roho takatifu ya Yehova inaweza kuongeza uwezo wetu, kwa hiyo, muombe Yehova roho yake mara kwa mara.—Lu. 11:13.
3. Tunapaswa kufanya nini wakati ndugu ao dada anatupatia pendekezo fulani ambalo pengine hatukuomba?
3 Ndugu ao dada akikupatia pendekezo fulani la kukusaidia ukomalishe ufundi wako, usikasirike hata kama haukumuomba musaada wowote. (Mhu. 7:9) Kama Apolo, ukubali pendekezo hilo kwa unyenyekevu na umushukuru. Kufanya hivyo kunaonyesha kama uko na hekima.—Met. 12:15.
4. Yesu alitoa sababu gani kubwa ambayo inatuchochea tuwe wahubiri wenye kufanya maendeleo?
4 Kufanya Maendeleo Kunamutukuza Mungu: Yesu alitumia mufano ili kuwatia moyo wafuasi wake wawe wahubiri wenye kufanya maendeleo. Alijilinganisha na muzabibu na alilinganisha wafuasi wake watiwa mafuta na matawi. Alisema kwamba Baba anasafisha kila tawi ambalo linazaa matunda ili “lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yoh. 15:2) Bwana wa shamba la mizabibu anatamani matawi ya mizabibu yake yawe yenye kuzaa matunda zaidi, vilevile Yehova anataka tuendelee kukomalisha uwezo wetu wa kuzaa “tunda la midomo.” (Ebr. 13:15) Wakati tunakuwa wahubiri wenye kufanya maendeleo, matokeo yanakuwa nini? Yesu anatupatia jibu: ‘Baba yangu anatukuzwa katika hili, kwamba muendelee kuzaa matunda mengi.’—Yoh. 15:8.