Jinsi ya Kuwazoeza Wapya Kuhubiri
1. Ulijisikia namna gani ulipoenda katika mahubiri kwa mara ya kwanza?
1 Je, unakumbuka siku ambayo ulihubiri nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza? Labda, uliogopa sana. Ikiwa ulihubiri pamoja na mwalimu wako wa Biblia ao mhubiri mwingine, bila shaka ulifurahi alipokusaidia. Sasa kwa kuwa umekuwa na uzoefu katika kazi ya kuhubiri, unaweza pia kuwazoeza wapya kuhubiri.
2. Wahubiri wapya wanahitaji kujifunza nini?
2 Wahubiri wapya wanahitaji kujifunza jinsi ya kuanzisha mazungumzo pamoja na msikilizaji, kutumia Biblia wanapozungumza na mutu, kurudilia watu, na kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Wanapaswa pia kujifunza jinsi ya kushiriki katika sehemu mbalimbali za kazi ya kuhubiri, kama vile kuhubiria watu barabarani na mahali pa biashara. Unaweza kuwasaidia wafanye maendeleo katika sehemu hizo kwa kuwaonyesha mfano na kwa kuwatolea mapendekezo.
3. Namna gani tunaweza kuwasaidia wengine kwa kuwaonyesha mfano?
3 Waonyeshe Mfano: Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake jinsi ya kuhubiri. (Luka 8:1; 1 Pet. 2:21) Unapopanga kuhubiri na mhubiri mpya, tayarisha namna iliyo nyepesi ya kutoa ushahidi ambayo mhubiri mpya anaweza kuiga, labda unaweza kutumia namna ya kutoa ushahidi inayoonyeshwa katika vichapo vyetu. Kisha, mwonyeshe kwamba utahubiri nyumba moja ao mbili ili asikie yale utakayosema. Munapotoka kwenye nyumba fulani kuelekea kwenye nyumba nyingine, unaweza kumwomba mhubiri atoe maoni yake kuhusu namna yako ya kutoa ushahidi. Hilo litamsaidia aone umaana wa kuhubiri pamoja na wengine na kumfanya akubali kwa urahisi mapendekezo yote unayomtolea kisha yeye kuhubiri.
4. Namna gani tunaweza kumsaidia mhubiri mpya tukiisha kusikiliza namna yake ya kuhubiri
4 Watolee Mapendekezo: Yesu aliwatolea pia wanafunzi wake maagizo kuhusu jinsi ya kuhubiri. (Mt. 10:5-14) Unaweza kumsaidia mhubiri mpya kwa njia hiyo. Ikiwa ni wakati wake wa kusema, umsikilize kwa uangalifu. Kisha, munapoondoka kwenye nyumba, usijizuie kumpongeza kwa moyo wote kuhusu jambo fulani hata ikiwa, katika namna yake ya kutoa ushahidi, uliona sehemu ambazo anahitaji kufanyia maendeleo. Mbele ya kumtolea pendekezo fulani, unaweza kumsikiliza kwanza kwenye nyumba inayofuata ili kuona ikiwa amefanya maendeleo. Labda alikuwa na woga tu. Kumbuka pia kwamba wahubiri wana uwezo tofauti-tofauti, na kwamba mara nyingi kuna namna mbalimbali za kufanya jambo fulani kwa njia yenye kufaa.—1 Kor. 12:4-7.
5. Tunaweza kusema nini tunapomtolea mhubiri mpya mapendekezo?
5 Wakati fulani mhubiri mpya anaweza kukuomba umtolee mapendekezo. Lakini ikiwa hafanye hivyo, chukua hatua ya kumsaidia. Namna gani unaweza kufanya hivyo bila kumkwaza? Wahubiri fulani wenye uzoefu wanauliza tu hivi, “Je, naweza kukutolea msaada?” ao, “uliona namna yako ya kuhubiri jinsi gani?” Ao unaweza kusema hivi, “Nilipokuwa mhubiri mpya, ilikuwa vigumu kwangu ku . . . , lakini jambo lililonisaidia ni . . .” Nyakati fulani ni jambo lenye kufaa kuchunguza pamoja naye kitabu Kutoa Sababu. Ili usimvuruge na habari nyingi, mtolee mapendekezo kuhusu sehemu moja tu ya namna yake ya kutoa ushahidi.
6. Kuhusiana na kazi ya kuhubiri, namna gani ‘chuma kinanoa chuma’?
6 Chuma Kinanoa Chuma: Paulo alimtia moyo Timotheo, mhubiri mwenye uzoefu, aendelee kufanya bidii katika kufundisha na kufanya maendeleo. (1 Tim. 4:13, 15) Hata ikiwa kumepita miaka mingi tangu ulipohubiri kwa mara ya kwanza, usiache kufanya maendeleo. Jifunze kutoka kwa ndugu na dada unaohubiri nao, hata wale wasio na uzoefu mwingi, na kwa fazili, uwe tayari kuwasaidia wengine, hasa wahubiri wapya, ili wawe wahubiri wa habari njema wenye ufundi.—Met. 27:17.