Hubiri Habari Njema kwa Hamu
1 “Nina hamu sana ya kuwaona nyinyi . . . Kuna hamu upande wangu kuitangaza habari njema kwenu pia.” Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyosema mwanzoni mwa barua yake kwa akina ndugu katika Roma. Kwa nini Paulo alikuwa na hamu ya kuwazuru? Yeye alisema: “Ili niweze kujipatia baadhi ya matunda miongoni mwenu pia . . . Kwa maana siaibikii habari njema; kweli hiyo ni nguvu ya Mungu kwa ajili ya wokovu.”—Rom 1:11-16.
2 Paulo alionyesha hamu hiyohiyo katika kusema na wanaume wazee wa Efeso. Aliwakumbusha: “Tangu siku ya kwanza nilipokanyaga wilaya ya Asia . . . , sikuepuka . . . kuwafundisha nyinyi hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba. Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki pia.” (Mdo 20:18-21) Katika eneo lake lote alilogawiwa, Paulo alikusudia kueneza habari njema ya wokovu na kujipatia matunda ya Ufalme. Ni roho nzuri kama nini ya kuiga!
3 Twaweza kujiuliza: ‘Je! mimi naonyesha hamu ileile katika kutangaza habari njema kwa watu wa jamii yangu? Badala ya kuona kazi ya kuhubiri kuwa wajibu tu, je! mimi ni mwenye hamu ya kushiriki habari njema na watu wengi zaidi iwezekanavyo? Je! nimefikiria hali zangu binafsi katika sala? Je! nimefikiria uwezekano wote unaopatikana katika eneo letu, kama vile kuhubiri kutoka mlango hadi mlango, barabarani, katika wilaya za biashara, kwa njia ya simu na mahubiri ya vivi hivi?’
4 Shiriki kwa Hamu Mnamo Aprili: Mwezi wa Aprili ni wakati mzuri wa kuzidisha kushiriki kwetu binafsi katika kazi ya kuhubiri. Kupunguzwa kwa kiwango cha saa kungepaswa kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuwa mapainia wasaidizi. Huenda hali zako zitakuruhusu kutumika ukiwa painia msaidizi mnamo Aprili na Mei. Au yawezekana kwako kujiandikisha kuwa painia wa kawaida, baada ya kufikiri juu ya kiwango cha saa kilichopunguzwa. Ikiwa wewe ni mhubiri wa kutaniko, je! unaweza kupitisha wakati mwingi zaidi kuliko kawaida katika utumishi mnamo mwezi huu na ule ujao, huku ukitegemeza wale walio na uwezo wa kupainia? Jambo hilo lingefanya moyo wa Yehova ufurahi!
5 Kama Paulo, wahubiri wote wa Ufalme wangepaswa kuendelea kuonyesha hamu kwa kujitahidi katika kazi ya kuhubiri. Kufanya yote tuwezayo katika huduma kutatuletea furaha ya kweli. Paulo alikuwa na furaha hiyo katika utumishi wake mtakatifu. Ni vema tuige kielelezo chake bora.—Rom. 11:13; 1 Kor. 4:16.