Je, tunaweza kufanya Aprili 2000 kuwa mwezi wetu bora kuliko yote?
1 Siku ya Tatu jioni, Aprili 19, utakuwa wakati wa maana sana katika mwaka wa utumishi. Siku hiyo, kadiri jua linavyotua hatua kwa hatua kuzunguka dunia, kila kutaniko na kikundi cha Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote watafanya Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Mahali popote tunapoishi, kuadhimisha dhabihu ya Yesu Kristo litakuwa tukio la maana zaidi mwakani. Tarehe ya Ukumbusho inaonyeshwa kwenye kalenda ya Mashahidi wa Yehova ya mwaka 2000.
2 Mwezi wote wa Aprili unatutolea nafasi nzuri ajabu ya kuonyesha kwa nafsi yote shukrani yetu kwa wema usiostahiliwa wa Yehova, wema ulioonyeshwa kupitia dhabihu ya Mwana wake. Namna gani hivyo? Mtume Paulo aliandika: “Upendo alio nao Kristo hutushurutisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote; kwa hiyo, basi, wote walikuwa wamekufa; naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale waishio wapate kuishi si kwa ajili yao wenyewe tena, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na alifufuliwa.” (2 Kor. 5:14, 15) Ndiyo, mnamo Aprili, tunaweza kuonyesha kwamba tunaishi, si kwa ajili yetu wenyewe, lakini kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yetu, tukifanya huo kuwa mwezi wetu bora kuliko yote tukiwa wahudumu wa Ufalme!
3 Jiandikishe kuwa painia msaidizi mnamo Aprili: Mtume Paulo alitutolea mfano wenye kuchochea aliposema: “Sijifanyi nafsi yangu kuwa kitu chenye thamani sana kwangu, kama tu ningepata kumaliza mwendo wangu na huduma niliyopokea ya Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.” (Mdo 20:24) Sisi tuna pendeleo lilelile la kutoa ushahidi kamili kuhusu Yehova Mungu. Kwa kusudi hilo, tunataka kufanya Aprili kuwa mwezi wetu bora kuliko yote katika utendaji wa painia msaidizi!
4 Ukiwa na miisho-juma tano yenye kuenea, Aprili 2000 utakuwa mwezi bora kwa ajili ya wengi kupainia. Huko nyuma mnamo Juni 1997, wakati tulipofikia kilele chetu cha wakati wote cha mapainia wasaidizi katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, wale 8,260 walioshiriki walikuwa sawa na asilimia 9 ya jumla ya wahubiri. Miaka miwili baadaye, hesabu ya jumla ya wahubiri walioripoti mnamo 1999 ilikuwa imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 6. Hilo lamaanisha kwamba kuna uwezekano wa kupita kile kilele chetu kilichotangulia cha mapainia wasaidizi. Kwa kuongezea, kiwango cha saa kimepunguzwa tangu mwaka huo, hilo likifanya wengi zaidi katika kutaniko wawe na uwezo wa kufikia sehemu hiyo ya utumishi. Kila mhubiri mwenye kubatizwa anapaswa kufikiria kwa sala ikiwa anaweza kuwa painia msaidizi mnamo Aprili.
5 Kwa kutumia mwezi wa Aprili kwenye kalenda ya mwaka 2000, panga programu yako sasa kwa ajili ya mwezi ujao. Chagua siku mbalimbali utakapokuwa na uwezo wa kushiriki katika utumishi wa shambani, na ujumlishe saa zote ambazo unafikiri unaweza kutoa katika utendaji wa kuhubiri mnamo mwezi. Tia ndani wakati ambao unaweza kupitisha katika kutoa ushahidi kwa wengine kwa namna yenye kupangwa na ki-vivi-hivi. Je, jumla hiyo inakaribia kiwango cha saa 50 cha mapainia wasaidizi? Ikiwa unakosa saa zenye kuhitajiwa, je, unaweza kufanya marekebisho mengine yoyote katika programu yako kusudi ununue wakati ili kuwa painia msaidizi? Utahitaji kueneza wastani wa saa moja na dakika 40 tu kila siku ili kufikia saa 50 kwa mwezi.
6 Kwa kuwa sasa kiwango cha saa kimepunguzwa pia kwa ajili ya mapainia wa kawaida, je, umekuwa ukifikiria kwa uangalifu kuingia huduma ya wakati wote? Kwa nini ungoje hadi mapumziko ya Julai? Aprili utakuwa mwezi mzuri ili kuanza! Ikiwa hauna hakika kuhusu uwezo wako wa kutimiza kiwango cha saa 70 cha mapainia wa kawaida, kwa nini usiwe painia msaidizi mnamo Aprili na kujiwekea mradi wa kutimiza saa 70? Baada ya kuona kwamba unaweza kufanya hivyo, huenda ukawa na mwelekeo zaidi wa kujaza ombi ili kujiunga kwenye mistari ya mapainia wa kawaida mapema zaidi iwezekanavyo.—Ona Huduma Yetu, kurasa 113-14.
7 Shiriki kikamili ukiwa mhubiri wa habari njema: Upendo wetu wa kweli kwa Mungu na kwa jirani hutuchochea sisi sote, wahubiri na mapainia pia, kufanya yote tuwezayo kwa nafsi yote katika utumishi wa Yehova kulingana na hali zetu binafsi. (Luka 10:27) Hivyo, tunaonyesha kwamba “tunafanya kazi kwa bidii na kujikakamua wenyewe, kwa sababu tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa namna zote za watu, hasa wa walio waaminifu.” (1 Tim. 4:10) Ni kwa sababu hiyo tunapaswa kutazamia kuona ushirika wa asilimia 100 mnamo Aprili, huku kila mmoja akishiriki kikamili katika kazi ya Ufalme.
8 Acheni tusisahau himizo la Yesu: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo, ombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” Mara moja baada ya kusema hivyo, Yesu akaita mitume wake 12 na akawatuma waende kuhubiri. (Mt. 9:37, 38; 10:1, 5, 7) Mwaka mmoja hivi baadaye, baada ya wale 12 kuzoezwa vizuri katika utendaji wa kuhubiri, Yesu “akachagua [makumi saba] wengine na kuwatuma,” akiwapa maagizo yaleyale: “Kwa kweli, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache. Kwa hiyo mwombeni Bwana-mkubwa wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Luka 10:1, 2) Kitabu cha Biblia cha Matendo kinaripoti jinsi Yehova alivyojibu sala hizo. Kufikia Pentekoste 33 W.K., hesabu ya wanafunzi ilikuwa imeongezeka hadi 120. Kisha, vilele vyenye kufuatana vya wanafunzi 3,000 na 5,000 vilifikiwa. (Mdo. 1:15; 2:41; 4:4) Baada ya hilo, “idadi ya wanafunzi ikafuliza kuzidi sana.” (Mdo. 6:7) Vivyo hivyo, katika wakati wetu, tunapaswa kuendelea kuomba Bwana-mkubwa atume wahubiri wa Ufalme wengine wengi! Kwa kupatana na sala zetu, kila mhubiri wa kutaniko anapaswa kuchukua mipango kamili ili kushiriki katika huduma kila mwezi.
9 Tafadhali, tazameni tena Aprili kwenye kalenda ya mwaka 2000. Kwa kuwa zile siku mbili za kwanza za mwezi ni Siku ya Posho na Siku ya Yenga, je, unaweza kuchukua mipango ili kushiriki katika utumishi mwisho-juma huo, ukifanyia mwezi mwanzo wa mapema? Je, unaweza kutegemeza kila “Siku ya Magazeti” katika mwezi pamoja na kikundi chako cha Funzo la Kitabu? Namna gani kuhusu kupitisha saa moja au zaidi katika huduma kila Siku ya Yenga? Je, unaweza kuchukua mipango ili kushiriki katika kutoa ushahidi jioni? Na usisahau kufaidika na nafasi zote ulizo nazo ili kutoa ushahidi wa vivi-hivi kazini, shuleni, au wakati unaposhughulika na utendaji mwingine mbalimbali wa kila siku. Tia alama juu ya siku ambazo katika hizo unaweza kupitisha wakati fulani katika huduma, na utumie kalenda hii ili kuandika wakati uliopitisha katika utumishi mnamo mwezi.
10 Aprili utakuwa wakati wenye kufaa kwa wote walio na sifa za kuwastahilisha na waliokubaliwa na wazee kuanza kutumika wakiwa wahubiri wasiobatizwa. Ikiwa unajifunza Biblia pamoja na mtu fulani, je, mtu huyo umefanya maendeleo ya kutosha ili kumkaribia mwangalizi msimamizi ili kuomba mtu huyo afikiriwe kuwa mhubiri wa habari njema? Ikiwa una watoto wasiobatizwa, je, umezungumzia maendeleo yao ya kiroho pamoja na wazee? Je, huu si wakati mzuri kwao kuanza kuhubiri?—Ona Huduma Yetu, kurasa 97-100.
11 Katika jitihada zetu za kufanya Aprili 2000 kuwa mwezi wetu bora kuliko yote, sisi sote tunahitaji kushiriki katika huduma na kisha kutoa ripoti yetu ya utumishi wa shambani mwishoni mwa mwezi. (Linganisha Marko 6:30.) Wale wahubiri wapya wasiobatizwa ambao wanashiriki katika utumishi wa shambani kwa mara ya kwanza wanapaswa kutiwa moyo waripoti utendaji wao bila kuchelewa. Kwa kutimiza fungu letu, tunaweza kuchangia vizuri katika ripoti ya Aprili na katika mlio mkubwa wa sifa utakaotolewa kwa Yehova kupitia jitihada zetu za kutoa ushahidi.
12 Peleka wengine pamoja nawe kwenye ukumbusho: Je, halitakuwa jambo lenye kusisimua kwetu kuona kilele kipya kikihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo mnamo mwaka 2000? Ndiyo! Hilo litamaanisha kwamba watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote wamekusanyika ili kuonyesha shukrani yao kwa wonyesho wa upendo ambao Yehova Mungu na Yesu Kristo wametoa kwa ajili yetu! (Yn. 3:16; 15:13) Chukua mipango yote inayohitajiwa kusudi jambo lolote lisikuzuie, wewe na familia yako, kuhudhuria Ukumbusho.
13 Sasa pia ndio wakati wa kuanza kualika wengine kwenye Ukumbusho. Fanya orodha ya kila mtu ambaye ungetaka kuona anahudhuria. Tia ndani mtu yeyote ambaye amejifunza Biblia wakati uliopita, wale wanaojifunza sasa, na wale wote unaorudilia. Ongeza kwenye orodha hiyo watu unaojuana nao kazini, shuleni, na katika ujirani, na pia mtu yeyote unayefanya biashara naye. Usisahau kutia ndani watu wengine unaojuana nao na pia watu wa jamaa. Baada ya kufanya orodha, anza kwa bidii kutoa mwaliko kwa kila mmoja. Onyesha wazi wakati na mahali ambapo Ukumbusho utafanyika. Kadiri Aprili 19 inavyokaribia, kumbusha wale walio kwenye orodha yako, ukiwafikia kibinafsi au kwa njia ya simu. Waombe waambatane nawe uendapo kwenye Ukumbusho usiku huo.
14 Kwa kupatana na mwongozo uliotangulia kutoka kwa Sosaiti, baraza la wazee litakuwa likifanya jitihada ya pekee ili kutia moyo wahubiri wote wasiotenda katika eneo kusudi wahudhurie Ukumbusho. (Mt. 18:12-14) Wazee watataka kurudilia barua ya Sosaiti ya Februari 2, 1999. Mwandishi wa kutaniko anapaswa kufanya orodha ya wahubiri wote wasiotenda, na mwangalizi wa utumishi atatoa mgawo kwa wazee ili watembelee wasiotenda hao na kuwaalika kwenye Ukumbusho. Labda kwa kupata ziara ya uchungaji yenye kutia-moyo mapema zaidi iwezekanavyo, hao wasiotenda wanaweza kusaidiwa wawe wenye kutenda tena katika huduma ya shambani, hata mnamo Aprili. Litakuwa jambo lenye kujenga kwao kualikwa kushiriki katika utumishi wa shambani pamoja na wahubiri wenye ujuzi.
15 Toeni kitia-moyo kwa ajili ya utegemezo mzuri mnamo Aprili! Ili kufanya Aprili kuwa mwezi wetu bora kuliko yote, itaomba wazee, watumishi wa huduma, na vichwa vya familia wasimamie mambo vizuri. Wazee watakuwa wenye bidii katika kufanya mambo yote yapangwe vizuri na katika kuchukua uongozi. (Ebr. 13:7) Inafaa kuchukua mipango yenye kufaa kwa ajili ya mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani katika siku za juma na kwenye miisho-juma. Mikutano ya ziada kwa ajili ya utumishi inaweza kupangwa kwa ajili ya utendaji wa kisha mchana-kati na ule wa mapema jioni. Programu kamili ya mambo yote yenye kupangwa mnamo Aprili inapaswa kuwekwa kwenye ubao wa matangazo. Itafaa kutoa mgawo kwa mtu fulani ili kuongoza kila mkutano unaopangwa kwa ajili ya utumishi. Eneo la kutosha linapaswa kuandaliwa ili kutosheleza mahitaji ya kila kikundi.
16 Mnamo Aprili, toleo la vichapo litakuwa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ili kujitahidi kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani, tunapaswa kutoa broshua Anataka kwa wale wanaoonyesha kupendezwa. Kwa sababu hiyo, akiba za kutosha za magazeti na broshua zinapaswa kuandaliwa.
17 Mwishoni mwa mwezi, viongozi wote wa mafunzo ya kitabu na wasaidizi wao watataka kutia moyo kila mtu katika kikundi chao atoe ripoti ya utumishi mara moja baada ya mwezi kwisha. Labda hilo linaweza hata kufanywa Siku ya Yenga, Aprili 30. Kisha, wakati mwandishi anapokusanya ripoti, ikiwa anatambua kwamba wahubiri fulani hawakutoa ripoti zao, yeye anaweza kwa wema kuwakumbusha wafanye hivyo kabla ya Mei 6, wakati ambapo anapaswa kutoa ripoti ya kutaniko kwa Sosaiti. Anaweza kuomba viongozi wa mafunzo ya kitabu wamsaidie kukutana na wahubiri mmoja-mmoja.
18 Majira ya Ukumbusho ndio wakati wa maana zaidi kwa watu wa Mungu. Huo unapaswa kuwa kwetu sote wakati wenye shughuli sana katika utumishi wa Yehova. Itakuwa hivyo ikiwa kila mmoja anashiriki kikamili zaidi iwezekanavyo akiwa mhubiri wa habari njema, ikiwa wale wanaoweza kujiandikisha kuwa mapainia wasaidizi wanafanya hivyo, na ikiwa tunajitahidi kupeleka wengine pamoja nasi kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Acheni tuombe kwa bidii baraka tele za Yehova kadiri tunavyojitahidi sana kufanya Aprili 2000 kuwa mwezi wetu bora kuliko yote, tukifanya yote kwa ajili ya sifa na utukufu wa Mungu! —Ebr. 13:15.
[Box on page 3]
Mapainia Wasaidizi
Kilele Chetu cha Wakati Wote:
Congo-Kinshasa: 8,260 (Juni 1997)
Congo-Brazzaville: 472 (1995)
[Box on page 4]
Jumla ya Wahubiri
Kilele Chetu cha Wakati Wote:
Congo-Kinshasa: 114,071
(Septemba 1999)
Congo-Brazzaville: 4,001
(Oktoba 1998)
[Box on page 5]
Waliohudhuria Ukumbusho
Kilele Chetu cha Wakati Wote:
Congo-Kinshasa: 574,736 (1997)
Congo-Brazzaville: 20,144 (1997)