Aprili—wakati wa ‘kufanya kazi kwa bidii na kujitahidi’
1 Kwa watu wa Yehova, majuma yanayozunguka Ukumbusho ni wakati wa kutafakari. Huo ni wakati wa kufikiri kwa uzito juu ya yale yaliyotimizwa na kifo cha Kristo, na kutafakari juu ya tumaini tulilopewa na Mungu, tumaini lililofanywa liwezekane kupitia damu ya Yesu iliyomwagwa. Wakati unaporudi nyuma na kufikiri kuhusu Aprili 19 ya mwaka uliopita, ni nini linalokuja akilini mwako? Je, unaweza kukumbuka sura ulizoziona jioni hiyo? ile hali bora ya kiroho kwenye Ukumbusho? ile hotuba nzito ya Kibiblia na zile sala zenye kutoka moyoni? Labda uliazimia kuonyesha kikamili zaidi kina kirefu cha shukrani zako kuelekea upendo ambao Yehova na Yesu wamekuonyesha wewe. Kutafakari kama huko kuna uvutano gani juu yako sasa?
2 Ni wazi kwamba watu wa Yehova huonyesha shukrani kwa njia nyingi, kuliko kwa maneno tu. (Kol. 3:15, 17) Mnamo mwezi wa Aprili uliopita, hasa, tulijitahidi kuonyesha uthamini wetu kuelekea maandalizi ya Yehova kwa ajili ya wokovu kwa kujitoa wenyewe katika huduma ya Kikristo. Hesabu ya mapainia wasaidizi ilikuwa maelfu, ikizidi kwa asilimia 83 kilele cha mwaka uliopita katika eneo letu. Jitihada ya mapainia hao, pamoja na ile ya watangazaji wengine wote wa Ufalme, ilitokeza vilele vipya vya saa, magazeti ambayo watu waliachiwa, na ziara za kurudia. Furaha yetu iliongezeka kwa kuona maelfu ya mafunzo mapya ya Biblia yakianzishwa, na kuona kilele kipya cha wahudhuriaji kwenye Ukumbusho!
3 Kwa kweli, uhakika wa tumaini letu unatuchochea tutende. Ni kama vile tu alivyoandika mtume Paulo: “Kwa [kusudi hilo] tunafanya kazi kwa bidii na [kujitahidi] wenyewe, kwa sababu tumeweka tumaini letu juu ya Mungu aliye hai, ambaye ni Mwokozi wa namna zote za watu, hasa wa walio waaminifu.”—1 Tim. 4:10.
4 Mnamo kipindi hiki cha Ukumbusho, utaonyeshaje kwamba unaamini maandalizi ya Yehova kwa ajili ya uhai? Mnamo mwezi wa Aprili uliopita, tulipata hesabu kubwa zaidi iliyopata kurekodiwa ya watangazaji wa Ufalme. Je, tunaweza kupita hesabu hiyo mnamo mwezi huu wa Aprili? Tunaweza kufikia mradi huo. Lakini kila mhubiri, aliyebatizwa au asiyebatizwa, atahitaji kushiriki. Wapya wengi pia wanaweza kutimiza matakwa ili kushiriki. Hivyo, huku mkichukua mipango ili kufanya kazi kwa bidii na kujitahidi mnamo mwezi huu wa Aprili, fikirieni njia ambazo katika hizo mnaweza kuchochea wengine, kutia ndani wapya zaidi na wale wasiokuwa na ujuzi mwingi, waambatane nanyi.
5 Tusaidie wengine waanze tena utendaji wao: Ikiwa mnajua watu fulani ambao wamekuwa wasiotoka kwenda katika utumishi wa shambani kwa mwezi mmoja au miwili, labda mnaweza kuwatia moyo na kuwaalika waambatane nanyi katika utumishi wa shambani. Ikiwa wengine katika kutaniko wamekuwa wasiotenda, wazee watafanya jitihada ya pekee ili kuwatembelea na kuwatia moyo waanze tena mnamo Aprili.
6 Sisi sote tunapaswa kuendelea kuomba roho ya Yehova itutie nguvu katika utumishi wake. (Luka 11:13) Ni nini tunalopaswa kufanya ili kupokea roho hiyo? Someni Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake. (2 Tim. 3:16, 17) Tunapaswa pia ‘kusikia lile ambalo roho huyaambia makutaniko’ kwa kuhudhuria mikutano yote mitano ya kila juma. (Ufu. 3:6) Huu ni wakati wenye kufaa ili kusaidia wale wasio kawaida na wale wasiotenda waboreshe mazoea yao ya funzo na kukomaza ukawaida katika kuhudhuria kwao mikutano. (Zab. 50:23) Tunafanya hivyo huku tukiwa waangalifu sana kwa hali njema yetu wenyewe ya kiroho. Hata hivyo, kitu kingine kinahitajiwa.
7 Mtume Petro alieleza kwamba Mungu hutoa roho yake takatifu kwa “wale wanaomtii yeye akiwa mtawala.” (Mdo. 5:32) Utii kama huo unatia ndani kutii amri ya “kuhubiri watu na kutoa ushahidi kamili.” (Mdo. 1:8; 10:42) Hivyo, ingawa ni kweli kwamba tunahitaji roho ya Mungu itutie nguvu ili kuhubiri, ni kweli pia kwamba Yehova hutusaidia hata zaidi wakati tunapoanza kuonyesha tamaa yetu ya kumpendeza. Acheni tusidharau kamwe umaana wa kuchukua hatua hizo za kwanza za utii wenye nia tayari!
8 Tusaidie watoto: Wazazi, je, mmeona uhakikisho wa kwamba watoto wenu wanataka kuongea na wengine kuhusu kweli? Je, wamekuwa wakiambatana nanyi katika utumishi wa shambani? Je, wao ni wenye kutoa mfano wa kuigwa katika mwenendo wao? Ikiwa ni hivyo, kwa nini mnasita? Karibieni mmoja wa washiriki wa Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko, na mwone ikiwa mtoto wenu anatimiza matakwa ya kuhesabiwa kuwa mhubiri mnamo mwezi huu wa Aprili. (Ona kitabu Huduma Yetu, kurasa za 99-100.) Tambueni kwamba watoto wenu wanaweza kuchangia kwa njia yenye nguvu katika kupaza sauti ya sifa kwa Yehova mnamo kipindi hiki cha Ukumbusho.—Mt. 21:15, 16.
9 Sikuzote, mama mmoja Mkristo alimtia moyo binti wake mchanga aongee na wengine kuhusu Yehova. Mwaka uliopita, wakati mtoto huyo wa kike alipokuwa akishiriki katika huduma pamoja na mama yake, aliachia mwanamume mmoja broshua Anataka, naye akaeleza kwa kifupi yaliyomo. Mwanamume huyo akamwuliza: “Una umri gani wewe?” Mtoto huyo wa kike akasema: “Miaka saba.” Mwanamume huyo alishangaa kumwona akifanya utoaji wenye maana kama huo. Ilitukia kwamba mwanamume huyo alikuwa akishirikiana na Mashahidi wakati alipokuwa mchanga lakini hakuwa kamwe amechukua hilo kwa uzito kuwa njia ya maisha. Upesi, funzo la Biblia lilikuwa likiendeshwa pamoja na mwanamume huyo, mke wake, na binti yake.
10 Vijana wengi tayari ni wahubiri, nasi tunafurahia ushirika wao wakati wanapofanya kazi pamoja nasi katika utumishi. Vijana hao wanaweza kuchochea na kutia moyo vijana wengine wa umri wao. Lakini Aprili ni wakati wenye kufaa pia kwa kila familia moja moja ili kutia nguvu vifungo vyake na kujenga hali ya kiroho kwa kufanya kazi pamoja katika utumishi mtakatifu. Baba wa familia wanapaswa kuchukua uongozi katika jambo hilo.—Mez. 24:27.
11 Tusaidie wapya: Namna gani kuhusu wapya ambao mnajifunza nao Biblia? Je, wanaweza kuchangia katika jitihada hiyo ya pekee mnamo mwezi huu wa Aprili? Labda walionyesha tamaa ya kuambia wengine kuhusu yale waliyokuwa wakijifunza kadiri mlivyozungumzia sura ya 2, fungu la 22, au sura ya 11, fungu la 14, katika kitabu Ujuzi. Ikiwa mnakaribia mwisho wa kitabu hicho, jitayarisheni kuzungumzia jambo hilo waziwazi kadiri mnavyozungumzia sura ya 18, fungu la 8, ambalo linasema: “Labda una hamu ya kuwaambia watu wako wa ukoo, rafiki zako, na wengine juu ya yale unayojifunza. Kwa kweli, huenda ukawa umekuwa ukifanya hivyo tayari, sawa na vile Yesu alivyoshiriki habari njema na wengine katika hali zisizo rasmi. (Luka 10:38, 39; Yohana 4:6-15) Sasa huenda ukataka kufanya zaidi.” Je, hiyo ni kweli kuhusu wale unaojifunza nao?
12 Je, mwanafunzi wako anaamini Neno la Mungu? Je, amekuwa akitumikisha kanuni za Biblia? Je, amepatanisha maisha yake na viwango vya Mungu? Je, amekuwa akihudhuria mikutano ya kutaniko? Je, anataka kumtumikia Yehova Mungu? Basi, kwa nini usimtie moyo aongee na wazee kusudi waamue ikiwa anatimiza matakwa ya kuwa mhubiri asiyebatizwa, na kufanya kazi pamoja nawe mnamo Aprili? (Ona kitabu Huduma Yetu, kurasa za 98-9) Katika njia hiyo, anaweza kuanza kuona moja kwa moja jinsi tengenezo la Yehova litakavyomtegemeza katika jitihada zake za kutumikia Yehova.
13 Ni kweli kwamba wanafunzi fulani hufanya maendeleo haraka zaidi kuliko wengine. Hivyo, kwa kupatana na mwongozo katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Juni 2000, ukurasa wa 4, mafungu ya 5-6, wengi wamekuwa wakijifunza kitabu cha pili pamoja na mtu aliyeonyesha kupendezwa hapo kwanza lakini ambaye alihitaji msaada wa ziada ili kuwa mshiriki mwenye kutenda. Hatuachi kamwe kutumaini kwamba watu hao wenye mioyo minyofu watakuwa wanafunzi wa kweli wa Kristo, iwe kwamba ni “bado kidogo, au bado muda mrefu.” (Mdo. 26:29, Biblia Takatifu) Hata hivyo, ikiwa hesabu ya miezi ambayo mmekuwa mkijifunza na watu kama hao inaelezwa vizuri zaidi kuwa “muda mrefu,” je, kipindi hiki cha Ukumbusho kinaweza kuwa nafasi nzuri kwa mwanafunzi wako ili kuanza kuonyesha kina kirefu cha uthamini wake kuelekea ukombozi wa Kristo?
14 Jinsi ya kuwasaidia washiriki: Kuhusu kusaidia wale wenye kutimiza matakwa waanze kwenda katika huduma, tunajifunza mengi kwa kuchunguza jinsi Yesu alivyozoeza wengine. Hakukuta tu umati na kuambia mitume wake waanze kusema. Alikazia kwanza sababu iliyofanya kazi ya kuhubiri ihitajiwe; alichochea mtazamo wa kusali sana, na kisha akawapa maandalizi matatu ya msingi: mwenzi wa kazi, mgawo wa eneo, na ujumbe. (Mt. 9:35-38; 10:5-7; Mk. 6:7; Luka 9:2, 6) Unaweza kufanya hivyohivyo. Iwe kwamba utakuwa ukisaidia mtoto wako mwenyewe, mwanafunzi mpya, au mtu mwingine ambaye hakuripoti utendaji wowote kwa muda fulani, linaweza kuwa jambo lenye kufaa kufanya jitihada ya pekee ili kufuatia miradi ifuatayo.
15 Kazia uhitaji: Ingiza moyoni mwa mtu umaana wa kazi ya kuhubiri. Uwe mwenye kuchangamkia kazi hiyo. Eleza mambo yaliyoonwa ambayo yanaonyesha yale ambayo kutaniko linatimiza katika huduma. Onyesha mtazamo ambao Yesu alionyesha kwenye Mathayo 9:36-38. Tia moyo yule anayetazamiwa kuwa mhubiri au yule asiyetenda asali kwa ajili ya kushiriki kwake binafsi katika huduma, na pia kwa ajili ya mafanikio ya kazi ulimwenguni pote.
16 Fanya mtu atafakari kuhusu zile nafasi nyingi za kutoa ushahidi: Taja uwezekano wa kukutana na kikundi cha funzo la kitabu kwa ajili ya kutoa ushahidi wa nyumba kwa nyumba. Sema kuhusu kuongea na washiriki wa familia na watu anaojuana nao au kuongea na wafanyakazi au wanashule wenzake muda wa mapumziko kwa ajili ya chakula cha mchana. Wakati wa kusafiri katika vyombo vya watu wote, mtu anaweza kuanzisha mazungumzo kwa kuonyesha tu kupendezwa na wasafiri wenzake. Wakati tunapochukua hatua ya kwanza, hilo mara nyingi hufungua njia ya kutoa ushahidi bora. Kwa kweli, kuna nafasi nyingi za kushiriki tumaini letu pamoja na wengine “siku kwa siku.”—Zab. 96:2, 3.
17 Hata hivyo, yaelekea kwamba ingekuwa vizuri zaidi kwako na yule mhubiri mpya kufanya pamoja kazi ya nyumba kwa nyumba mapema zaidi iwezekanavyo. Ikiwa umejiwekea mradi wa kuongeza utumishi wako mnamo Aprili, uliza mtumishi wa huduma anayeshughulika na maeneo ikiwa eneo lenye kufaa linapatikana. Ikiwa linapatikana, jambo hilo litakutolea nafasi za kulitumika kikamili. Kwa mfano, wakati unapomaliza utumishi au unaposafiri kwenda kwenye mikutano au mahali penginepo, unaweza kutambua kwamba mtu fulani yuko nyumbani kwenye makao ambako hapo mbele hakukupatikana mtu yeyote au ambapo kupendezwa kulionyeshwa. Ikiwa hilo ni jambo lenye kufaa, fanya ziara fupi wakati ambapo kufanya hivyo kutakuwa kwenye matokeo zaidi. Kwa upande mwingine, hilo litachangia katika hisia ya kutimiza mambo na furaha katika huduma.
18 Tayarisha ujumbe wenye kuvutia: Mtu fulani anaweza kutaka kushiriki ujumbe wa Ufalme, lakini huenda asijisikie mwenye hakika kuhusu namna ya kuutoa, zaidi sana ikiwa yeye ni mpya au hakuwa ametoka kwenda katika utumishi kwa muda mrefu. Kusaidia wapya na wale wasiotenda wajitayarishe ni wakati unaopitishwa vizuri. Mikutano ya utumishi na mikutano kwa ajili ya utumishi wa shambani inaweza kutoa mawazo yenye kusaidia, lakini hakuna kitu kinachoweza kuchukua mahali pa matayarisho ya kibinafsi.
19 Mnawezaje kusaidia wapya wajitayarishe kwa ajili ya utumishi? Anzeni na utoaji wa gazeti, na mfanye utoaji huo kuwa mwepesi na mfupi! Waombeni wafikiri kuhusu matukio katika vyombo vya habari, matukio ambayo yatakuwa yenye kupendeza watu wa eneo, na kisha tafuteni katika moja la magazeti ya sasa nukta ambayo inahusiana na jambo hilo. Jizoezeni utoaji huo pamoja, na utumieni katika huduma mapema zaidi iwezekanavyo.
20 Tukomaze uwezekano wetu wa kuwa na ongezeko wakati ujao: Mwaka uliopita, hudhurio la ulimwenguni pote kwenye Ukumbusho lilipita milioni 14.8. Hesabu ya wahubiri waliotoa ripoti ilikuwa zaidi ya milioni sita tu. Hilo linamaanisha kwamba karibu watu milioni 8.8 walikuwa wenye kupendezwa vya kutosha ili kuja kwenye programu hiyo ya pekee ambako walisikia moja la mafundisho makubwa ya Biblia likielezwa. Walipata kujua kibinafsi wamoja kati yetu, jambo ambalo yaelekea liliwagusa moyo kwa njia yenye kufaa. Wengi wao husema vizuri sana juu yetu, hutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, nao hututetea mbele ya wengine. Kikundi hicho kikubwa kinatoa uwezekano wa kuwa na ongezeko wakati ujao. Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia wafanye maendeleo ya ziada?
21 Wengi wa wapya wanaohudhuria Ukumbusho hufanya hivyo kama tokeo la mwaliko wa kibinafsi kutoka kwa mmoja wetu. Kwa kawaida, hilo linamaanisha kwamba wana angalau mtu mmoja wanayejuana naye kati ya wasikilizaji. Ikiwa mtu fulani anahudhuria kwa kuitikia mwaliko wetu, tunalo daraka la kumfanya ajisikie mwenye kukaribishwa, na kumsaidia afaidike kikamili na programu. Kwa kuwa jumba litakuwa na watu wengi, msaidie apate mahali pa kukaa. Mwazime Biblia, na umwombe ashiriki pamoja nawe kitabu chako cha nyimbo. Jibu maulizo yoyote anayoweza kuuliza. Uangalifu wako binafsi wenye shauku unaweza kuwa jambo la maana katika kukomaza kupendezwa kwake. Bila shaka, sisi sote tunashiriki daraka hilo—ikiwa tunaona mtu tusiyemjua, acheni tumkaribishe kwa shauku na kuzungumza naye kwa kifupi ili kupata kujuana.
22 Kuhudhuria Ukumbusho kunaweza kuwa na uvutano wa kweli juu ya mafikiri ya mtu. Jambo la kwamba amekuja kwenye mkutano linaweza kumaanisha kwamba hakupata kile anachotafuta mahali pengine na kwamba sisi tunamtolea kitu fulani ambacho anasikia uhitaji wa kukichunguza kwa ukaribu zaidi. Maelezo kuhusu uandalizi mzuri ajabu wa ukombozi yanaweza kuwa ufunuo wenye kina kirefu kwa mtu ambaye hana wazo lolote kuhusu upendo wa Yehova usio na mipaka. Huenda akaona kwa vyepesi kwamba sisi tuko tofauti—wanyofu, wenye urafiki, wenye upendo, na wenye adabu. Jumba letu halina kitu chochote chenye kufanana na yale aliyoyaona katika makanisa ambayo yanatoa nafasi ya kwanza kwa sanamu na desturi zisizo na maana. Wapya wana hakika ya kuona kwamba kikundi cha wasikilizaji kinafanyizwa na watu kutoka daraja mbalimbali za maisha na kwamba hakuna fedha zinazoombwa. Mambo hayo wanayoona yanaweza kuwa kichocheo chenye nguvu ili warudi.
23 Baada ya Ukumbusho, mtu fulani anapaswa kufanya haraka ili kutoa msaada wenye kufuatia mambo kwa kila mtu mpya aliyehudhuria. Ikiwa ulialika wapya, unalo daraka la pekee. Kabla ya wao kuondoka, hakikisha kwamba wanajua kuhusu mikutano mingine kwenye Jumba la Ufalme. Taja kichwa cha hotuba ya watu wote yenye kufuata. Wajulishe kuhusu mahali na wakati wa Funzo la Kitabu lililo karibu zaidi na makao yao. Baadaye, watolee nakala ya kitabu Muumbaji, na uwajulishe kwamba mazungumzo kwa ajili ya juma toka Aprili 30 ni “Unaweza Kujifunza Nini Juu ya Muumba Katika Kitabu?” (Patanisha mambo ikiwa kutaniko linajifunza kitabu Ujuzi.) Eleza kwa nini kutaniko zima linapanga kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa karibu ambao unapangwa wakati ujao ulio karibu.
24 Chukueni mipango kwa ajili ya ziara yenye uchangamfu nyumbani kwao. Hakikisheni kwamba wanazo nakala za broshua Anataka na kitabu Ujuzi, ambazo zinawafahamisha mafundisho ya msingi ya Biblia. Ikiwa hawajaanza kujifunza, watoleeni funzo la Biblia. Pendekezeni wasome broshua Mashahidi wa Yehova, ambayo inatoa picha iliyo wazi kuhusu jinsi tunavyofanya kazi tukiwa tengenezo. Waalikeni watazame vidio zetu, kama vile Our Whole Association of Brothers [Toute la communauté de nos frères]. Chukueni mipango ili wakutane na wengine katika kutaniko. Katika miezi inayokuja, endeleeni kukutana na wapya; waalikeni wahudhurie mikutano wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko au wakati mnapokuwa na kusanyiko la mzunguko au kusanyiko la pekee la siku moja. Wapeni kila nafasi ya kujionyesha kuwa ‘wenye mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uhai udumuo milele’!—Mdo. 13:48.
25 Yale ambayo wazee wanaweza kufanya: Kwa kiasi kikubwa, mafanikio ya jitihada yenye kuongezeka katika huduma mnamo mwezi huu wa Aprili itategemea wazee. Ikiwa wewe ni kiongozi wa funzo la kitabu, fanya orodha ya mambo unayoweza kufanya ili kusaidia kila mmoja katika kikundi chako cha funzo la kitabu ashiriki katika utendaji huo wa pekee. Je, kuna wowote walio katika kikundi chako ambao ni vijana, wapya, wasio kawaida, au wasiotenda? Chunguza mambo ili uone ikiwa wazazi, mapainia, au wahubiri wengine wamechukua hatua za kuwasaidia. Toa msaada wowote wa kibinafsi ambao wewe mwenyewe unaweza kutoa. Dada mmoja ambaye alikuwa amekuwa asiyetenda katika utumishi wa shambani kwa miaka miwili alipitisha zaidi ya saa 50 katika huduma mnamo mwezi wa Aprili uliopita. Ni nini lililofanya mambo yawe tofauti kwake? Alisema kwamba zilikuwa ziara za uchungaji zenye kujenga zilizofanywa na wazee.
26 Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kushirikiana ili kuhakikisha kwamba kuna eneo la kutosha, magazeti, na vichapo kwa ajili ya mwezi ujao. Je, mikutano ya ziada kwa ajili ya utumishi wa shambani inaweza kupangwa? Ikiwa ni hivyo, fanyeni mipango hiyo ya pekee ijulikane. Zaidi ya yote, katika sala zenu za peupe na za siri, ombeni baraka ya Yehova juu ya mwezi wetu wa utendaji wenye kuongezeka wa Ufalme.—Rom. 15:30, 31; 2 Thes. 3:1.
27 Katika kutaniko moja mwezi wa Aprili uliopita, wazee walichochea kwelikweli utendaji wenye kuongezeka katika huduma. Kwenye mikutano kila juma, walialika wahubiri wafikiri kwa njia ya sala ili waone ikiwa wangeweza kujiandikisha kuwa mapainia wasaidizi. Wazee na watumishi wa huduma wote walitumia kila nafasi ili kusema kwa shauku kuhusu kufanya Aprili kuwa mwezi bora kuliko yote. Kama tokeo, asilimia 58 ya wahubiri, kutia ndani wazee wote na watumishi wa huduma, walipainia mnamo mwezi huo!
28 Furaha ya kushiriki kikamili: Ni nini baraka za ‘kufanya kazi kwa bidii na kujitahidi’ katika huduma? (1 Tim 4:10) Kuhusu utendaji wenye bidii wa kutaniko lao mnamo mwezi wa Aprili uliopita, wazee waliotajwa hapo juu waliandika: “Akina ndugu na dada wanasema mara nyingi kuhusu upendo na ukaribu mwingi zaidi ambao kila mmoja alihisi kuelekea mwingine kwa kuwa walianza kufanya kazi zaidi katika huduma ya shambani.”
29 Ndugu mmoja kijana asiye na uwezo mwingi wa kutembea alitamani kushiriki katika utendaji wa pekee mnamo mwezi wa Aprili uliopita. Kwa kupanga mambo kwa uangalifu, na kwa msaada wa mama yake na ndugu na dada zake wa kiroho, ndugu huyo alifurahia mwezi wenye kuzaa matunda akiwa painia msaidizi. Alijisikia namna gani kuhusu jambo hilo lililoonwa? Alisema: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu, nilijisikia kama vile mwanamume mwenye nguvu.”
30 Hakuna shaka kwamba Yehova hubariki sana wale wanaothamini kwa hali ya juu pendeleo lao la kuongea kuhusu ufalme wake. (Zab. 145:11, 12) Huku tukiadhimisha kifo cha Bwana wetu, tunafahamu kwamba baraka zinazotokana na ujitoaji-kimungu zitakuwa hata nyingi zaidi wakati ujao. Mtume Paulo alikuwa na hamu sana ya thawabu ya uzima wa milele. Hata hivyo, alijua kwamba hilo halikuwa jambo fulani ambalo angetumainia tu bila kufanya jambo lolote. Aliandika: “Kwa [kusudi hilo] kwa kweli ninafanya kazi kwa bidii, [nikijitahidi] mwenyewe kwa kupatana na utendaji wake na unaofanya kazi ndani yangu kwa nguvu.” (Kol. 1:29) Yehova, kupitia Yesu, alifanya Paulo awe mwenye nguvu ili atimize huduma yenye kuokoa uhai, naye anaweza kufanya hivyohivyo kwa ajili yetu leo. Je, hilo litakuwa jambo utakalojionea mwenyewe mnamo mwezi huu wa Aprili?
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Ni Nani Unayeweza Kutia Moyo Ahubiri Mnamo Aprili?
Mtoto wako?
Mwanafunzi wa Biblia?
Mtu fulani ambaye amekuwa asiyetenda?