Kisanduku cha maulizo
◼ Mtu ambaye amekuwa asiyetenda kwa muda mrefu anawezaje kusaidiwa ili kutimiza tena matakwa ya kuwa mhubiri wa habari njema?
Wakati mtu asiyetenda anapotoa uhakikisho kwamba anayo tamaa yenye kutoka moyoni ya kumtumikia Yehova, hiyo ni sababu ya kushangilia. (Luka 15:4-6) Yaelekea kwamba mtu huyo aliruhusu upinzani au mikazo ya maisha isimwachie wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma ya shambani. Msaada wa kibinafsi unawezaje kutolewa kwa njia bora zaidi ili mtu huyo afanye maendeleo ya kiroho?
Sisi sote tunapaswa kuchukua hatua ili kuhakikishia mtu huyo upendo wa kweli wa Kikristo tulio nao kumwelekea yeye. Wazee watakuwa tayari ili kukadiria mahitaji yake kamili ya kiroho. (Yak. 5:14, 15) Ikiwa kutotenda kulidumu muda mfupi, msaada kutoka kwa mhubiri mwenye ujuzi unaweza kuwa ndilo jambo pekee linalohitajiwa ili kufanya mtu huyo awe tena mwenye kutenda katika utumishi wa shambani. Hata hivyo, ikiwa yule mtu asiyetenda hakushirikiana na kutaniko kwa muda mrefu, bila shaka msaada mwingi zaidi utahitajiwa. Ili kujenga imani na uthamini, funzo la Biblia pamoja na mtu huyo katika kichapo chenye kufaa linaweza kuwa jambo zuri. Katika hali hiyo, mwangalizi wa utumishi atachukua mipango ili mhubiri mwenye sifa aongoze funzo hilo. (Ebr. 5:12-14; ona Majibu ya Maulizo Yenu katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Novemba 1998.) Ikiwa mnajua mtu fulani anayehitaji msaada kama huo, ongeeni na mwangalizi wa utumishi katika kutaniko lenu.
Kabla ya kualika mtu ambaye amekuwa asiyetenda kwa muda mrefu ashiriki tena katika huduma, ni vizuri kwamba wazee wawili wakutane naye ili kuona ikiwa anatimiza matakwa ya kuwa mhubiri wa Ufalme. Watafuata njia ya kufanya mambo yenye kufanana na ile inayotumiwa wakati wa kukutana na wapya wanaotafuta kutimiza matakwa ya kuwa wahubiri wa habari njema. (Ona Mnara wa Mlinzi wa Novemba 15, 1988, ukurasa 17.) Mtu yule asiyetenda anapaswa kuwa na tamaa yenye kuchukua mambo kwa uzito ya kushiriki habari njema pamoja na wengine. Anapaswa pia kutimiza yale matakwa ya msingi yanayoonyeshwa kwa kifupi kwenye kurasa 98-9 za kitabu Huduma Yetu na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida.
Kuwa na programu nzuri ya kiroho kutatimiza mengi ili kusaidia yule mwenye kurudi atie nguvu na kuendeleza uhusiano wake wa thamani pamoja na Yehova, na kuendelea kutembea kwenye barabara iongozayo kwenye uzima wa milele. (Mt. 7:14; Ebr. 10:23-25) Kufanya kwake “jitihada yote yenye bidii” na kukuza sifa za Kikristo ambazo hudumu kutamzuia asiwe tena ‘asiyetenda au asiyezaa matunda’ akiwa mwanafunzi wa Kristo.—2 Pet. 1:5-8.