Kutoa kwa matokeo ushahidi kwa njia ya simu
1 Mradi wetu tukiwa Mashahidi wa Yehova si kushiriki tu katika kuhubiri habari njema bali pia kufanya ujumbe wa Ufalme ufikie kila mtu iwezekanavyo. (Mdo. 10:42; 20:24) Ingawa kazi ya nyumba kwa nyumba inabaki njia yetu kubwa ya kufikia watu, tunatambua kwamba hatukutani na kila mtu hata kwa njia hiyo ya kawaida. Kwa hiyo, ili ‘kutimiza kikamili huduma yetu,’ tunatumia njia nyinginezo—kutia ndani kutoa ushahidi kwa njia ya simu—ili kupata watu wenye mfano wa kondoo.—2 Tim. 4:5.
2 Katika nafasi nyingi, watu huishi katika nyumba zenye ulinzi wa hali ya juu, majengo ambamo familia nyingi hukaa, au mitaa yenye malango kwa ajili ya usalama, ambako ni vigumu kutumia ufundi wetu wa kawaida wa kwenda nyumba kwa nyumba ili kufikia watu. Hata katika maeneo ambako tunaweza kufanya kazi ya nyumba kwa nyumba, hesabu kubwa ya watu hawapatikani nyumbani. Hata hivyo, wahubiri wengi ni wenye kupata matokeo bora katika kufikia wakaaji hao kwa njia ya simu. Walipokuwa katika kazi ya nyumba kwa nyumba asubuhi moja, wenzi wawili wa ndoa hawakukuta watu kenda nyumbani. Baada ya kurudi kwenye Jumba la Ufalme, walitafuta watu hao katika kitabu chenye kutoa mwongozo ambacho kinaorodhesha namba za simu kulingana na anwani. Walipiga simu kwa kutumia namba hizo, nao wakapata wanane kati ya wenye-nyumba wakiwa nyumbani!
3 Je, unasita kutia ushahidi kwa njia ya simu katika huduma yako? Ndugu mmoja anakubali: “Mimi sipendi mtu yeyote anipigie simu nyumbani ili kuniuzishia kitu chochote; kwa hiyo nina kizuizi cha kiakili kuhusiana na namna hiyo ya kutoa ushahidi.” Hata hivyo, baada ya kupiga simu mara mbili tu, yeye akasema: “Ninapenda namna hii ya kutoa ushahidi! Sikufikiri kamwe kwamba hili lingetukia, lakini ninaipenda! Watu ni wenye kutulia kwenye simu, nawe unayo mambo yote unayohitaji karibu nawe. Hili ni jambo lenye matokeo sana!” Dada mmoja alikuwa na itikio hilohilo: “Kutoa ushahidi kwa njia ya simu hakukunifurahisha kwelikweli. Kusema kweli, sikutaka jambo hilo. Lakini nikalijaribu na kuona kwamba ni lenye matokeo sana. Nina ziara za kurudia 37 kutokana na kutoa ushahidi kwa njia ya simu; pia, nina mafunzo mengi zaidi kuliko yale ninayoweza kushughulikia!” Ikiwa unataka kujaribu kutoa ushahidi kwa njia ya simu, wewe pia unaweza kufanikiwa.
4 Kupanga mambo kwa ajili ya kutoa ushahidi kwa njia ya simu: Utendaji wa kutaniko wa kutoa ushahidi unasimamiwa na mwangalizi wa utumishi. Kulingana na uhitaji, baraza la wazee linaweza kuchagua kuweka rasmi mzee mwingine au mtumishi wa huduma mwenye sifa ili kutumika kwa ukaribu pamoja naye katika kupanga kutoa ushahidi kwa njia ya simu. Ndugu anayeshughulika na maeneo anapaswa pia kuhusishwa, kwa kuwa atatoa maeneo na kulinda maandishi ya kisasa. Vivyo hivyo, mwangalizi wa mzunguko atapendezwa na maendeleo ya programu hiyo.
5 Ikiwa kuna sehemu katika eneo lenu ambazo haziwezi kufikiwa kwa kutoa ushahidi wa nyumba kwa nyumba, maeneo kwa ajili ya ushahidi kwa njia ya simu yanapaswa kutayarishwa. Ndugu anayepewa mgawo huo atafanya kwa uangalifu orodha ya anwani mbalimbali ambazo zitageuzwa kuwa maeneo ya namna hiyo, ambayo yanapaswa kufanywa kuwa madogo kwa njia fulani ili yaweze kutumikwa kikawaida. Ramani zote za maeneo zilizo na sehemu kama hizo zinapaswa kuwa na alama yenye kuonyesha kwamba sehemu fulani hasa imetayarishwa kwa ajili ya ushahidi kwa njia ya simu.
6 Ni wapi mnakoweza kupata namba za simu? Kitabu chenye mwongozo ambacho kinaorodhesha namba za simu kulingana na anwani kinaweza kupatikana katika maktaba ya watu wote. Ikiwa jengo la watu wengi ambalo ni lenye ulinzi wa hali ya juu lina orodha yalo lenyewe ya simu, labda mnaweza kupata namba kutoka hapo. Kama sivyo, inawezekana kuandika majina ya wakaaji kutoka katika kitabu chenye mwongozo kilicho katika chumba cha kupokelea wageni, na kutafuta majina hayo katika kitabu cha kawaida cha simu.
7 Kwa njia yenye kutenda, wazee wanaweza kupendezwa na kazi hii kwa kuchukua mipango ili wale wenye ujuzi katika kutoa ushahidi kwa njia ya simu wazoeze wengine, labda kupitia programu Mapainia Husaidia Wengine. Pindi kwa pindi, sehemu kuhusu mahitaji ya kutaniko kwenye Mkutano wa Utumishi inaweza kutolewa ili kuongeza mafanikio katika upande huu wa kutoa ushahidi.
8 Wakati wazee wanapofanya ziara za uchungaji kwa wale wasiotoka nyumbani kwa sababu ya ugonjwa, au wale wenye kulemaa, wanaweza kuwa tayari kuwatia moyo ili washiriki katika kutoa ushahidi kwa njia ya simu. Labda mzee anaweza kupigia watu wachache simu huku mhubiri akitazama. Kisha mhubiri anaweza kufurahia nafasi ya kupiga simu. Wengi walioanza hivyo hupitisha dakika chache kila siku katika kazi hiyo, nao huifurahia kwelikweli.
9 Madokezo ili kufanikiwa: Wakati Yesu alipotuma wanafunzi wake waende kuhubiri, ‘aliwatuma wawili-wawili.’ (Luka 10:1) Kwa nini? Alijua kwamba kwa kufanya kazi pamoja wangeweza kutiana moyo, na kila mmoja angeweza kujifunza kutoka kwa mwingine. Jambo hilohilo ni kweli katika kutoa ushahidi kwa njia ya simu. Kwa kutumika mkiwa wenzi wa utumishi, kila mmoja anaweza kujifunza kutoka kwa mwingine; mnaweza kuzungumzia matokeo, na kupeana madokezo kwa ajili ya mazungumzo yatakayofuata. Hata wakati wa kupiga simu, mnaweza kusaidiana kupata habari zenye kufaa.
10 Ili kuendeleza kufikiri kuliko wazi na kukaza fikira, kaa mahali ambapo unaweza kuweka vifaa vyako vya mahubiri—Biblia, kitabu Kutoa Sababu, broshua Anataka, magazeti, na kadhalika—mbele yako. Andika utoaji mbalimbali, na uutie mahali unapoweza kuuona. Uwe tayari kulinda maandishi yaliyo sahihi na kamili, kutia ndani tarehe na wakati wa siku ili kujua wakati wa kufuatia kupendezwa kulikopatikana.
11 Kwa kawaida watu huwa waangalifu wakati wanaposikia kwenye simu sauti wasiyoijua. Kwa hiyo, uwe mwenye shauku, mwenye urafiki, na mwenye busara. Namna ya sauti yako inatosha ili mwenye-nyumba atambue sifa zako na unyofu wako. Tulia na useme kutoka moyoni mwako. Sema polepole na waziwazi na kwa sauti ya kutosha ili usikike. Mpe mwenye-nyumba nafasi ya kusema. Tumia jina lako kamili, na useme kwamba unaishi katika mtaa au mji wa msikilizaji. Hatutaki watu wafikiri kwamba sisi ni watu wenye kuuzisha vitu kwa njia ya simu. Badala ya kusema kwamba unapigia simu wakaaji wote wa nyumba fulani au jengo lenye watu wengi, fanya kupiga kwako simu kuwe jambo la kibinafsi.
12 Utoaji kwenye simu: Mengi ya matangulizi kwenye kurasa 9-15 za kitabu Kutoa Sababu yanaweza kutengenezwa ili yapatane na ushahidi kwa njia ya simu. Unaweza kusema: “Ninakuita kwenye simu kwa kuwa siwezi kuja na kuonana nawe kibinafsi. Kusudi langu la kukupigia simu ni kuuliza maoni yako kuhusu ulizo lenye kupendeza sana.” Kisha, toa ulizo.
13 Utoaji wa kwanza chini ya kichwa “Uhalifu/Kutopatwa na Madhara” unaweza kutumiwa ifuatavyo: “Jambo. Jina langu ni. Ninaishi katika mtaa (au mji) huu. Ninataka kukuhakikishia kwamba siuzishi kitu chochote wala sifanyi uchunguzi. Ninakupigia simu kwa sababu ninahangaikia mambo ya usalama wa kibinafsi. Kuna uvunjaji wa sheria mwingi kutuzunguka, na huo una uvutano juu ya maisha yetu. Je, unafikiri wakati utakuja ambapo watu wote wataweza kutembea barabarani usiku bila kuogopa hatari? [Acha mtu ajibu.] Acha nisome yale ambayo Mungu ameahidi kufanya.”
14 Kutumia ufundi wa moja kwa moja ili kupendekeza mafunzo ya Biblia kupitia simu kumekuwa na matokeo mazuri. Kuonyesha jinsi funzo linavyoendeshwa kunaweza kufanywa kwa dakika chache. Pendekeza kutembelea msikilizaji nyumbani kwake ili kuendeleza funzo, au ikiwa mtu huyo ni mwenye kusita, pendekeza kuendeleza funzo kwa njia ya simu siku nyingine.
15 Wakati unapomaliza mazungumzo, linda akilini jambo fulani litakalokuongoza umtembelee mtu nyumbani kwake au kumtumia kichapo fulani kwa njia ya posta. Ikiwa mtu anasita kukutolea anwani yake, pendekeza kumpigia simu tena. Huenda ikaomba kumpigia simu mara nyingi kabla ya yeye kujisikia mwenye hakika vya kutosha ili kukualika nyumbani kwake.
16 Kuchukua hatua ya kwanza: Dada mmoja mwenye umri wa miaka 15 alianza utumishi wake wa asubuhi kwa kupiga simu. Mwanamke ambaye aliongea naye akakubali kuchukua kitabu Ujuzi. Wakati dada alipomwachia kitabu nyumbani, mwanamke huyo akataka kujua jinsi dada huyo kijana alivyojua namba yake ya simu, kwa kuwa hiyo haikuorodheshwa. Dada alikuwa ameita namba hiyo kimakosa! Mwanamke huyo akakubali funzo kwa furaha, naye sasa ni mhubiri asiyebatizwa.
17 Dada mmoja alipokea eneo kwa ajili ya kutoa ushahidi kwa njia ya simu lakini akaacha kwa majuma matatu kulitumika kwa sababu ya woga. Ni nini kilichompa uhodari wa kuanza? Alikumbuka makala katika Amkeni! ya Januari 22, 1997, makala yenye kichwa “Ninapokuwa Dhaifu, Ndipo Niwapo Mwenye Nguvu.” Ilihusu Shahidi mmoja anayehubiri kwa njia ya simu ingawa vizuizi vyake vya kimwili. Dada anasema: “Nikasali kwa Yehova na kumwomba nguvu. Nilimwomba anipe maneno yenye kufaa ili nitoe utoaji wangu.” Ni nini lilikuwa tokeo la siku yake ya kwanza ya kutoa ushahidi kwa njia ya simu? Anaripoti: “Yehova alijibu sala yangu. Watu walinisikiliza, nami nikachukua mipango kwa ajili ya ziara ya kurudia.” Baadaye, ushahidi wake kwa njia ya simu ukatokeza funzo la Biblia. Anamalizia kwa kusema: “Yehova alinifundisha mara nyingine kumtumainia yeye wala si kujitumainia mimi mwenyewe.”—Mez. 3:5.
18 Kutoa kweli kwa njia ya simu kumekuwa ufundi wenye matokeo wa kuhubiri habari njema. Jitayarishe vizuri, na ushiriki kwa moyo wote. Usivunjike moyo ikiwa jibu lenye kufaa halitokei mara ya kwanza unapojaribu. Omba mwongozo wa Yehova, na ulinganishe maandishi pamoja na wengine wanaohubiri kwa namna hiyo yenye kusisimua. Tukiwa na tamaa ya kutokosa mtu yeyote katika eneo letu, acheni tutimize kikamili huduma yetu kwa uharaka.—Rom. 10:13, 14.