Kuanzisha Mafunzo ya Biblia Mlangoni na kwa Njia ya Simu
1 Leo watu wana shughuli nyingi. Hata hivyo, wengi wanapendezwa na mambo ya kiroho. Tunawezaje kuwasaidia ili watosheleze uhitaji wao wa kiroho? (Mt. 5:3) Wahubiri wengi wanaweza kujifunza Biblia na watu wakiwa wenye kusimama mlangoni au kwa njia ya simu. Je, unaweza kueneza huduma yako katika njia hiyo?
2 Ili kuanzisha mafunzo ya Biblia, tunahitaji kuwa wenye kujitayarisha ili kuonyesha watu jinsi funzo la Biblia linavyoendeshwa, wakati wowote ule nafasi inapojitokeza kwetu. Hilo linaweza kufanyika jinsi gani na wapi?
3 Kwenye Mlango: Unapokutana na mtu anayependezwa na mazungumzo ya Biblia, unaweza tu kufungua kwenye fungu ambalo umetayarisha kimbele, kama vile fungu la kwanza la somo 1 katika broshua Anataka, na kuanza funzo. Soma fungu hilo, soma ulizo, na kisha uzungumzie andiko moja au mawili yanayotajwa. Mara nyingi, hilo linaweza kufanywa mkiwa wenye kusimama kwenye mlango mnamo dakika tano au kumi. Ikiwa mtu anafurahia mazungumzo, fanya mpango ili kuzungumzia fungu linalofuata au mafungu mawili wakati mwingine.—Mapendekezo zaidi kuhusu kutumia njia ya moja kwa moja ili kuanzisha mafunzo yanaweza kupatikana katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Januari 2002, uku. 6.
4 Njia kama hiyo inaweza kutumiwa ili kuanzisha mafunzo ya Biblia wakati wa kufanya ziara za kurudia. Kwa mfano, unaweza kuonyesha broshua Anataka na kukazia jina la Mungu, ukitumia somo 2, fungu la 1-2. Kwenye ziara ijayo, unaweza kuzungumzia yale ambayo Biblia inafunua kuhusu sifa za Yehova, ukitumia fungu la 3-4. Kwenye mazungumzo yanayofuata, unaweza kuchunguza fungu la 5-6 na picha kwenye ukurasa wa 5 ili kukazia jinsi funzo la Biblia linatusaidia tupate kumjua Yehova. Yote hayo yanaweza kufanywa mkiwa wenye kusimama mlangoni.
5 Kwa Njia ya Simu: Watu wengine wanaweza kupendezwa zaidi kujifunza Biblia kwa njia ya Simu badala ya kujifunza na mtu uso kwa uso. Fikiria jambo hili lililoonwa: Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, dada mmoja alikutana na mwanamke mmoja kijana ambaye ni mama na mwenye shughuli nyingi katika kazi yake. Kwa kuwa dada huyo hakuweza kukutana naye tena nyumbani, aliamua kumpigia mwanamke huyo simu. Mwanamke huyo kijana alimwelezea dada kwamba kweli yeye hakuwa na wakati wa kuzungumza juu ya Biblia. Dada huyo alimwambia: “Mnamo dakika 10 au 15, unaweza kujifunza jambo fulani jipya, hata kwa njia ya simu.” Naye mwanamke huyo akamjibu: “Vizuri, basi, ikiwa ni kwa njia ya simu, ninakubali!” Bila kuchelewa, funzo la Biblia la kawaida likawa lenye kuongozwa kwa njia ya simu.
6 Je, watu fulani ambao unatembelea wako tayari kujifunza kwa njia ya simu? Unaweza kujaribu njia iliyozungumziwa hapo juu, au unaweza tu kusema: “Ukitaka, tunaweza kuzungumzia habari ya Biblia kwa njia ya simu. Je, hilo litakufaa zaidi?” Kwa kupatanisha programu yetu ya funzo la Biblia na hali ya wengine, tunaweza kuwasaidia ‘wapate kumjua Mungu.’—Met. 2:5; 1 Kor. 9:23.
[Maulizo ya Funzo]
1, 2. Tunawezaje kurekebisha programu yetu ya kuongoza funzo la Biblia ili kusaidia watu wenye shughuli nyingi?
3. Kwa nini, kwenye ziara ya kwanza, umwonyeshe mtu jinsi funzo la Biblia linavyoendeshwa, na jinsi gani hilo linaweza kufanywa?
4. Tunawezaje kuanzisha funzo la Biblia mlangoni tunapofanya ziara za kurudia?
5, 6. (a) Kwa nini watu fulani wanaweza kupendelea kujifunza Biblia kwa njia ya simu? (b) Ni njia gani tunayoweza kutumia tunapotolea watu funzo kwa njia ya simu?