Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo ya Mlangoni na kwa Njia ya Simu
1 Ni furaha kama nini kuanzisha funzo la Biblia! Hata hivyo, kupata mtu anayependezwa na kujifunza Biblia ni hatua ya kwanza tu. Kusudi la funzo ni kumsaidia mtu huyo awe mwanafunzi wa kweli wa Kristo. (Mt. 28:19, 20) Ni nini kinachoweza kutusaidia kufikia kusudi hilo?
2 Watu Wenye Shughuli: Leo watu wana shughuli nyingi sana. Mahali fulani, ni watu wachache wanaokubali mwanzoni kutumia saa nzima ili kujifunza Biblia. Ili kusaidia watu kama hao, tumetiwa moyo kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia kwenye mlango au kwa njia ya simu. Mwanzoni, mafunzo hayo yanaweza kuwa mafupi na ni maandiko machache tu ya Biblia yanayoweza kuchunguzwa ukitumia fungu moja au mafungu mawili katika kichapo kama vile kitabu Biblia Inafundisha. Ni jambo linalostahili pongezi kuona kwamba wahubiri wengi sasa ni wenye kuongoza mafunzo kama hayo, kwenye mlango au kwa njia ya simu.
3 Hata hivyo, je, tutatosheka na kuendelea kuongoza funzo mlangoni sikuzote? Hapana. Ingawa ni jambo la hekima kwamba tusibaki muda mrefu mlangoni tunapoanza hivi karibuni kuongoza funzo la Biblia, Huduma Yetu ya Ufalme ya Desemba 1990, ukurasa wa 8, ilisema: “Funzo litakapoimarishwa na wakati kupendezwa kwa mtu kutakapokomaa, tutaweza kuongeza muda wa kudumu kwa funzo.” Jambo hilo ni la lazima. Tuchukue mfano: Mtoto mchanga mwenye kuteseka kwa njaa anaweza kulishwa mwanzoni kwa kiasi kidogo cha chakula mpaka hamu yake ya kula inaporudishwa, lakini hatuwezi kutazamia kwamba atapata nguvu kamili na kukomaa kwa njia ya kawaida ikiwa analishwa kiasi kidogo hicho cha chakula kwa muda mrefu. Vivyo hivyo, mwanafunzi wa Biblia anahitaji funzo lenye kupangwa na la kawaida ili awe mtumishi mkomavu wa Mungu.—Ebr. 5:13, 14.
4 Mafunzo ya Biblia Nyumbani: Ni vizuri kuongoza funzo mahali pa pekee—yaani nyumbani au mahali pengine penye kufaa. Jambo hilo litasaidia kujifunza katika hali yenye kutulia na kusaidia hivyo mwanafunzi aelewe maana ya Neno la Mungu. (Mt. 13:23) Pia litawezesha sana mwalimu apatanishe habari za kujifunza na mahitaji ya mwanafunzi. Zaidi ya hayo, kujifunza wakati mrefu vya kutosha kutawezesha uchunguzi wa Neno la Mungu uwe wenye kina zaidi na wenye kuimarisha imani.—Rom. 10:17.
5 Unawezaje kufanya funzo la mlangoni liwe lenye kuongozwa nyumbani au mahali pengine penye kufaa? Baada ya kuongoza mafunzo mafupi mara nyingi, kwa nini usipendekeze funzo lenye kuchukua wakati mrefu, au kipindi fulani cha wakati? Au unaweza kutumia njia isiyo ya moja kwa moja kwa kumuuliza mwanafunzi “Je, unaweza kuwa na wakati wa kukaa leo ili tuzungumzie jambo hili pamoja?” au “Unapenda kutumia muda gani leo kwa kuzungumzia habari hii?” Ikiwa hakubali, kwa vyovyote endelea kuongoza mafunzo mafupi mlangoni. Kwa wakati mwingine unaofaa, jaribu tena ili funzo liwe likifanywa nyumbani.
6 Tunapoendelea kutafuta wale wanaostahili, acheni tusisahau mradi wetu wa kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mradi wetu ni kusaidia watu wenye mioyo minyofu wawe watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa. Yehova na abariki jitihada zetu tunapotimiza huduma yetu tukiwa na mradi huo.—2 Tim. 4:5.
[Maulizo ya Funzo]
1. Kusudi letu ni gani tunapoongoza mafunzo ya Biblia?
2. Mafunzo ya Biblia ya mlangoni na kwa njia ya simu ni nini, na kwa nini ni yenye matokeo?
3. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuongeza muda wa kutosha kwenye kipindi tunachotumia kwa ajili ya funzo mlangoni?
4. Ni faida gani zinazotokana na kuongoza funzo la Biblia mkiwa nyumbani au mahali pengine penye kufaa?
5. Tunawezaje kufanya funzo la mlangoni liwe lenye kuongozwa nyumbani au mahali pengine penye kufaa?
6. Tunapaswa kutimiza huduma yetu tukiwa na mradi gani, na mapendekezo yaliyotolewa katika makala hii yanawezaje kutusaidia tufikie mradi huo?