Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 1: Funzo la Biblia Ni Nini?
1 Ulimwenguni pote, karibu mafunzo ya Biblia milioni sita ni yenye kuongozwa na watu wa Mungu kila mwezi. Kwa kutumia njia za kufundisha zenye matokeo, tunaweza kusaidia wanafunzi wa Biblia hao kufanya maendeleo mpaka kufikia wakfu na ubatizo, na kuwa “na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Je, ungependa kusaidia mwanafunzi wako ili afanye maendeleo ya namna hiyo? Kuanzia na toleo hili, Huduma Yetu ya Ufalme itatoa mfululizo wa makala zitakazofafanua sehemu za msingi katika kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo.
2 Wakati wa Kutoa Ripoti ya Funzo la Biblia: Ikiwa una mazungumzo, hata mafupi, ya Biblia pamoja na mtu mwenye kupendezwa, na ikiwa unazungumzia kwa ukawaida na kwa utaratibu habari fulani ukitumia Biblia na kimoja cha vichapo vinavyopendekezwa, unaongoza funzo la Biblia. Hilo ni kweli hata ikiwa funzo linafanyika mlangoni au kwa njia ya simu. Funzo linaweza kuripotiwa ikiwa limeongozwa mara mbili baada ya kumwonyesha mtu jinsi ya kujifunza na ikiwa kuna sababu inayosadikisha kwamba funzo hilo halitakatizwa.
3 Broshua Anataka na kitabu Ujuzi ndivyo vichapo vinavyotumiwa ili kuongoza mafunzo mengi ya Biblia. Baada ya kumaliza vichapo hivyo, ikiwa ni wazi kwamba mtu ni mwenye kufanya maendeleo, hata ingawa ni polepole, na kwamba ni mwenye kuonyesha zaidi uthamini kwa yale anayojifunza, basi mnaweza kuendelea kujifunza kitabu Mwabudu Mungu. Broshua Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! inaweza kutumiwa ili kujifunza na watu wenye elimu ndogo au uwezo mdogo wa kusoma.
4 Kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia imekuwa yenye matokeo katika kusaidia mamilioni ya watu kuwa wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo. (Mt. 28:19, 20) Kwa kutumia mapendekezo yanayotolewa katika makala yatakayofuata ya mfululizo huu, unaweza kuongoza funzo la Biblia lenye maendeleo.