Biblia Inafundisha— Kitabu Chetu cha Lazima cha Kujifunzia Biblia
1 Kwenye Mkusanyiko wa Wilaya “Utii wa Kimungu,” tulishangilia sana kupokea kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Mwishoni mwa programu ya Siku ya Posho, wahudhuriaji walifurahi kupokea kila mtu kitabu chake binafsi. Tutatumiaje kitabu hicho kipya katika ufundishaji? Kimekusudiwa kuwa kitabu chetu cha lazima cha kujifunzia Biblia. Ingawa kitabu kipya hicho kitakaziwa kwanza katika toleo la vichapo la mwezi wa Machi, wahubiri wanatiwa moyo waanze kukitumia mara moja ili kuanza na kuongoza mafunzo ya Biblia.
2 Mafunzo ya Biblia Tunayoongoza: Wahubiri wenye kuongoza mafunzo ya Biblia katika kitabu Ujuzi au katika broshua Anataka watatumia utambuzi mzuri katika kuamua jinsi na wakati wa kuanza kutumia kitabu kipya kwenye funzo. Ikiwa funzo lilianzishwa hivi karibuni, mnaweza tu kuanzia mwanzoni mwa kitabu kipya. Ikiwa mmefika mbali katika kitabu Ujuzi, mnaweza kuendelea na funzo katika kitabu Biblia Inafundisha kwenye sura inayolingana na ile iliyo katika kitabu Ujuzi. Ikiwa mnakaribia mwisho wa kitabu Ujuzi, mnaweza kuamua kumaliza kitabu hicho.
3 Bila shaka sisi sote tunajua watu wengi ambao watafaidika kutokana na funzo la kitabu Biblia Inafundisha. Kwa nini tusitolee kila mtu funzo la Biblia katika kitabu hicho chenye kufundisha kweli hatua kwa hatua? Kwa mfano, wale ambao wamejifunza broshua Anataka au kitabu Ujuzi, lakini hawakufanya maendeleo mpaka kufikia wakfu na ubatizo, wanaweza kutaka kurudilia funzo lao kwa kutumia kitabu kipya. Wazazi wanaweza kuamua kutumia kitabu hicho wanapofundisha watoto wao ujuzi sahihi wa mapenzi ya Mungu.—Kol. 1:9, 10.
4 Kujifunza Kitabu cha Pili: Je, kuna mpango wa kwamba mwanafunzi wa Biblia ajifunze kitabu cha pili baada ya kumaliza kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Ndiyo. Ikionekana wazi kwamba mwanafunzi ni mwenye kufanya maendeleo, hata ikiwa ni polepole, na ni mwenye kusitawisha uthamini juu ya yale anayojifunza, funzo la Biblia linaweza kuendelezwa kwa kutumia kitabu Mwabudu Mungu wa Pekee wa Kweli. Tuko hakika kwamba kitabu Biblia Inafundisha kitakuwa kitabu chenye nguvu mikononi mwetu tunapotimiza kazi ya kufanya wanafunzi.—Mt. 28:19, 20.