Mikusanyiko—Wakati wa Shangilio!
1 Mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova ni nyakati za shangilio kubwa. Kwa zaidi ya miaka mia moja, mikusanyiko hiyo imechangia katika ongezeko ambalo limekuwa likitukia katika tengenezo letu. Toka mianzo midogo, tumeona baraka tele za Yehova juu ya kazi yetu ya ulimwenguni pote. Kwenye mkusanyiko wetu wa kwanza katika nyakati za kisasa, huko Chicago, Illinois, mnamo 1893, jumla ya watu 70 kati ya wale 360 waliohudhuria walibatizwa ili kuonyesha wakfu wao kwa Yehova. Mfululizo wa mwaka huu uliopita wa Mikusanyiko ya Wilaya “Watendaji wa Neno la Mungu” ulikuwa kwa ujumla na hudhurio la watu 9,454,055, na kulikuwa 129,367 waliobatizwa. Ni sababu nzuri ajabu kama nini ya kushangilia!
2 Wakati wowote tangu nyakati za kibiblia, mikusanyiko ya watu wa Mungu imekuwa njia ya maana sana ya kutoa maagizo kutoka kwa Yehova. Wakati wa Ezra na Nehemia, watu walisikiliza usomaji wa Sheria “toka asubuhi mpaka mchana.” (Neh. 8:2, 3, Biblia Takatifu) Kwa sababu ya kupata uelewevu bora wa Sheria wakati huo, watu walipata “furaha nyingi.” (Neh. 8:8, 12) Sisi pia tunashangilia kuona kwamba mikusanyiko inatutolea nafasi bora ya kupokea maagizo mazuri na chakula cha kiroho “kwa wakati ufaao” kutoka kwa Yehova kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Kwa kuwa Yesu alisema kwamba binadamu anapaswa kuishi kwa “kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova,” mikusanyiko ni ya maana sana kwa ajili ya hali yetu njema ya kiroho.—Mt. 4:4.
3 Kuhudhuria Kunastahili Kufanyiwa Jitihada Yote: Kila mmoja wetu angepaswa kujiwekea kibinafsi mradi wa kuwako kwenye programu nzima ya mwaka huu ya Mkusanyiko wa Wilaya “Walimu wa Neno la Mungu.” Tunapaswa kupanga mambo ili kufika mapema kila siku na kubaki mpaka tutakapojiunga katika kusema “Ameni!” baada ya sala ya kumalizia. Ili kutimiza hilo, huenda tukalazimika kurekebisha programu yetu. Kupata pumziko kutoka kazini ili kuhudhuria mkusanyiko kunaweza kutokeza matatizo fulani. Tunahitaji kuchukua msimamo thabiti, tusiache kitu chochote kitukie kama kwa bahati tu. Ikiwa tunahitaji mahali pa kupanga na/au usafirishaji, tunapaswa kuchukua mipango mapema. Jitihada yoyote tunayolazimika kufanya itakuwa yenye kustahili!
4 Watu wa Yehova hawakadirii kifedha baraka za kuhudhuria mkusanyiko. Ona mifano ya watu fulani walioazimia kuhudhuria Mkusanyiko wa Kimataifa wa Mashahidi wa Yehova, mkusanyiko uliokuwa na kichwa “Mapenzi ya Kimungu” na uliofanyika katika Mji wa New York mnamo 1958. Ndugu mmoja alisimamisha shughuli zake za ujenzi kwa majuma mawili ili atoe kwa kujipendea msaada wake na kuhudhuria mkusanyiko. Ndugu mmoja katika Visiwa Virgini aliuzisha hektari tano za shamba ili familia yake nzima ya watu sita ihudhurie. Mume na mke vijana wenye kuoana waliuzisha boti yao ili wapeleke kwenye mkusanyiko watoto wao wote watatu wenye umri wa kuanzia miezi miwili mpaka miaka saba. Ndugu watatu wa kimwili kutoka Kalifornia waliambiwa kwamba ikiwa wangekosa kuwako kazini mwao, kazi hizo hazingekuwako wakati wa kurudi kwao. Hata hivyo, hilo halikuwazuia wasiende kwenye mkusanyiko huo usioweza kusahaulika.
5 Yehova Hubariki Jitihada Yetu Yenye Bidii: Yehova huona na hubariki jitihada za watu wake. (Ebr. 6:10) Kwa mfano, kwenye Mkusanyiko wa 1950 uliokuwa na kichwa “Ongezeko la Kitheokrasi,” wahudhuriaji walisikia ile hotuba ya maana sana yenye kichwa “Mfumo Mpya wa Mambo.” Ndugu Frederick Franz aliamsha na kuchochea kupendezwa kwa wote kwa kuuliza: “Je, kusanyiko hili la kimataifa lingefurahi kujua kwamba hapa, usiku huu, kati-kati yetu, mna idadi fulani ya watarajiwao kuwa wakuu wa ile dunia mpya?” Zaidi ya miaka 50 baadaye, tungali wenye kufurahia uelewevu huo wenye kufanywa kuwa wazi wa Zaburi 45:16.
6 Baada ya kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya wa mwaka uliopita, baba mmoja wa familia mwenye uthamini aliandika yafuatayo: “Ndugu, hamtajua kamwe kwa kadiri gani mkusanyiko huu umekuwa wenye kuokoa uhai. Familia yangu ilihamia mjini kwa sababu za kazi, matokeo yakiwa kuona hali yetu ya kiroho ikienda kwa taabu. . . . Tulikuwa tumepuuza wajibu wetu mbalimbali wa Kikristo. Tuliacha hata kuhudhuria mikutano na kushiriki katika utumishi pamoja. . . . Mkusanyiko huu umetutia nguvu tena, na mara nyingine tena tunajiwekea miradi ya kiroho, nasi tunapanga mambo yetu ili kutimiza miradi hiyo.”
7 Yehova ni mwenye kututolea chakula cha kiroho tunachohitaji. Yeye hutayarisha meza yenye mambo mengi kwenye mikusanyiko yetu. Uthamini wetu kuelekea uandalizi huo unapaswa kutuwezesha kusema maneno aliyosema Kornelio wakati alipotembelewa na mtume Petro: “Wakati huu sisi tupo sote mbele ya Mungu kuyasikia mambo yote ambayo umeamriwa na Yehova kusema.” (Mdo. 10:33) Acheni tujiwekee mradi wa ‘kuwa mbele ya Mungu’ kwenye kila kipindi cha Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu, mkusanyiko wenye kichwa “Walimu wa Neno la Mungu,” na kushangilia!