Je, wewe unathamini mambo matakatifu?
1 Tunapoulizwa ikiwa tunathamini mambo matakatifu, yaelekea tutajibu kwa haraka ndiyo! Ni nini mengine ya maandalizi matakatifu ya Mungu ambayo sisi tunathamini?
2 Sisi tunathamini sana kama nini uhusiano wa kibinafsi tunaoruhusiwa kuwa nao pamoja na Baba yetu wa mbinguni! Yeye anatuhakikishia kwamba ikiwa ‘tunamkaribia, naye atatukaribia.’ (Yak. 4:8) Bila dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, hakuna mtu ambaye angepokea uzima wa milele. (Yn. 3:16) Kwa shukrani yenye kutoka moyoni, tunaonyesha kila siku katika sala uthamini wetu wenye kina kirefu kwa zawadi hiyo ya Mungu yenye thamani.
3 Kama vile tengenezo la kidunia la Yehova lilivyo takatifu, Neno la Mungu lililopuliziwa, Biblia, pia ni takatifu kwetu. Tunaonyesha uthamini wenye kufaa kwa maandalizi hayo kutoka kwa Yehova wakati tunapoishi kulingana na kanuni za Biblia, tunapotia nguvu vifungo vya upendo wa kidugu, tunapotii kwa uangalifu utaratibu wa kitheokrasi, na tunaposhirikiana na wale wanaoongoza.—1 Pet. 1:22.
4 Kupitia mtumwa mwaminifu na mwenye busara, sisi hupokea chakula kingi cha kiroho. Hilo litakuwa kweli mwaka huu kwenye Mkusanyiko wa Wilaya “Watekelezaji (Watendaji) wa Neno la Mungu.” Huko tutapokea mafundisho ya maana sana na tutafurahia ushirika wenye shauku ambao tunahitaji sana. Tunawezaje kuonyesha uthamini wenye kutoka moyoni kwa uandalizi huo mtakatifu?
5 Usipuuze Nyumba ya Yehova: Nehemia alionya kwa upole wale ambao walikuwa wametumika sana ili kujenga upya kuta za Yerusalemu; aliwaambia ‘wasiache nyumba ya Mungu wao.’ (Neh. 10:39) Leo, “nyumba” ya Yehova ni mpango wake kwa ajili ya ibada. Mikusanyiko yetu ya wilaya ni sehemu ya mpango huo. Ili tusipuuze mpango huo, tunapaswa kuhudhuria na kuwa waangalifu sana, tukionyesha Yehova kwamba tunathamini maandalizi yake kwa hali ya juu. (Ebr. 10:24, 25) Ni mipango gani ambayo tunapaswa kuchukua sasa ili kuonyesha kwamba tunathamini kikamili tukio hilo takatifu?
6 Hudhuria Siku Zote Tatu: Kila mmoja wetu anapaswa kuchukua mipango ili kuhudhuria siku zote tatu za mkusanyiko. Je, wewe ni mwenye kuchukua mipango ili kufika mapema kila siku na kubaki hadi sala ya mwisho Siku ya Yenga? Ikiwa ni hivyo, utapata baraka tele. Huenda kuhudhuria mkusanyiko kusiwe rahisi sikuzote. Huenda kurekebisha kazi yako ya kimwili kukaomba uchukue msimamo imara. Huenda usafirishaji usiwe wenye kufaa sikuzote. Lakini usiache mambo hayo yakuvunje moyo na kukufanya ukose kuhudhuria mkusanyiko.
7 Fikiria Mfano Huu Bora: Walipokuwa njiani kwenda kwenye mkusanyiko wa wilaya mwaka jana, kikundi cha akina ndugu katika nchi moja ya Afrika ambako kuna msukosuko wa wenyewe kwa wenyewe kilikutana na kikundi cha maaskari. Akina ndugu waliulizwa: “Nyinyi ni nani, na mnakwenda wapi?” Wakajibu: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova, na tunakwenda kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya.” Mmoja wa maaskari akasema: “Nyinyi Mashahidi wa Yehova hamwogopi jambo lolote. Nendeni tu, na mtaweza kufanya mkusanyiko wenu bila tatizo lolote. Walakini, jueni kwamba mtakutana na maaskari wengi. Wakati wote, tembeeni katikati ya barabara! Ikiwa mnakutana na watu wengi wenye kujikusanya, endeleeni kutembea katikati ya barabara!” Walifanya hivyo na walifika kwa usalama kwenye mkusanyiko. Akina ndugu hao walithawabishwa kwa sababu walionyesha uthamini wao kwa mambo matakatifu.
8 Kama vile ndugu zetu katika sehemu nyingine za Afrika, sisi pia tunakabiliana na matatizo. Lakini, hakuna shaka kwamba tunaweza kuiga imani yao na kuazimia kuhudhuria vipindi vyote vya mkusanyiko wetu wa wilaya. Ikiwa marekebisho yanahitajiwa, mwendee Yehova ili upate mwongozo, ukijua kwamba yeye atabariki jitihada zetu za kuhudhuria programu nzima.
9 Vuna Baraka: Tuna hamu sana ya Neno la Mungu, tukijua kwamba kupitia hilo sisi tunaweza kukomaa kufikia wokovu. (1 Pet. 2:2) Kuhudhuria kwetu mkusanyiko wa wilaya na kusikiliza programu kutasaidia kila mmoja wetu kujenga imani yenye nguvu zaidi katika Neno hilo na hivyo kuwa na uwezo zaidi wa kushindana na mashambulizi makali ya Shetani. Katika kufanya hivyo, tutaonyesha Yehova na wale wote wanaotutazama kwamba tunathamini kikamili mambo matakatifu na kwamba sisi “si namna irudiyo nyuma . . . bali namna iliyo na imani kuelekea kuhifadhi hai nafsi.”—Ebr. 10:39; 12:16; Mez. 27:11.
10 Tunaweza kumtazamia Yehova Mungu afungue madirisha ya mbingu na kumwaga juu yetu matone mengi ya baraka za kiroho. (Mal. 3:10) Jiwekee mradi wa kuwa kwenye Mkusanyiko wa Wilaya “Watekelezaji wa Neno la Mungu” tangu mwanzo kabisa wa programu Siku ya Tano asubuhi mpaka sala ya kumalizia na “Ameni!” Siku ya Yenga kisha mchana-kati. Utakuwa mwenye furaha kuona umefanya hivyo!