‘Sikilizeni na Mwongezewe Elimu’
1 Kitabu cha Mezali kinaeleza hekima kuwa yenye kuita: “Sikieni, maana nitasema maneno yaliyo mazuri sana na kufungua kwa midomo yangu kutakuwa maneno ya haki. Shauri ni langu, na maarifa ya kweli: . . . munisikilize: maana heri wale wanaoshika njia zangu. Maana yeye anayeniona mimi anaona uzima, naye atapata ukubali kwa BWANA.” (Mez. 8:6, 14, 32, 35) Maneno hayo yanaeleza elimu inayotungoja kwenye Mkusanyiko wa Wilaya “Walimu wa Neno la Mungu.”
2 Mahitaji ya undugu wa ulimwenguni pote yamefikiriwa, nayo programu ya mkusanyiko imetayarishwa ili kuzungumzia mahitaji hayo. Elimu ya kiroho na madokezo yenye kutumika ambayo yatatolewa yanaweza, ikiwa yanatumikishwa, kutusaidia kuwa wenye furaha, kuendelea kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, na kubaki kwenye barabara iongozayo kwenye uzima wa milele. Kwa kweli, tunayo sababu nzuri ya ‘kusikiliza na kuongezewa elimu.’—Mez. 1:5.
3 Kabla ya Programu: Ili kufaidika kikamili na yale yanayotolewa, tunahitaji kuwa wenye kukaa na kuwa katika hali ya akili yenye kufaa wakati programu inapoanza. Hilo linaomba kupanga vizuri mambo yetu binafsi. Jambo la maana litakalotuwezesha kufanya hivyo ni kuanza mambo mapema. Nendeni kulala mapema usiku unaotangulia. Amkeni mapema vya kutosha ili kutolea kila mmoja katika kikundi chenu wakati wa kujitayarisha na kupata kitu fulani cha kula. Fikeni mapema mahali pa kufanyia mkusanyiko kusudi mpate viti na kushughulikia mambo ya lazima kabla ya programu kuanza. Milango itafunguliwa pa saa 2:00 za asubuhi, na programu itaanza pa saa 3:30 za asubuhi kila siku.
4 Kwa kuwa kusudi la msingi la kukusanyika ni kumsifu Yehova “katika makusanyiko,” kila kipindi cha mkusanyiko kinapaswa kufunguliwa kwa namna yenye kutukuza Mungu wetu. (Zab. 26:12) Kwa kusudi hilo, wote wanatiwa moyo wawe wenye kukaa kabla ya kutangazwa kwa wimbo wa kufungua. Hilo linapatana na shauri la Kima-andiko: “Acheni mambo yote yatukie kwa adabu na kwa mpango.” (1 Kor. 14:40) Hilo linamaanisha nini kwa kila mmoja wetu? Wakati mnapoona mwenyekiti akikaa jukwaani muda wa muziki wa utangulizi, kaeni bila kukawia. Hilo litawawezesha kushiriki kwa moyo wote wimbo unaofungua kila kipindi cha mkusanyiko, mkipaaza sauti kwa kumsifu Yehova.—Zab. 149:1.
5 Muda wa Programu: Ezra “[alitayarisha] moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda.” (Ezra 7:10, UV) Tunawezaje kutayarisha mioyo yetu ili kupokea elimu anayotoa Yehova? Kadiri unavyorudilia vichwa mbalimbali vinavyoorodheshwa kwenye programu iliyochapishwa, jiulize, ‘Yehova ananiambia nini kupitia programu hii? Ninawezaje kutumia habari hii ili kujifaidi mwenyewe na kufaidi familia yangu?’ (Isa. 30:21; Efe. 5:17) Endeleeni kujiuliza maulizo hayo tangu mwanzo mpaka mwisho wa programu. Andikeni nukta mnazopanga kutumia. Chukueni wakati wa kuzizungumzia mwishoni mwa vipindi vya kila siku. Hilo litawasaidia kuweka habari hiyo akilini na kuitumikisha.
6 Kukaza akili kwa saa nyingi wakati uleule kunaweza kuwa jambo gumu. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushindana na mwelekeo wa kupeperushwa akilini? Faidikeni na nguvu ya jicho. Kwa kiasi kikubwa, mambo ambayo juu ya hayo tunakaza macho yetu huongoza uangalifu wetu. (Mt. 6:22) Kwa hiyo, piganisheni kishawishi cha kugeuka kila wakati kunapokuwa makelele au kitendo fulani. Endeleeni kukaza macho yenu juu ya msemaji. Fuateni katika nakala yenu ya Biblia wakati andiko linaposomwa, na mfanye Biblia yenu iendelee kuwa yenye kufunguliwa kadiri andiko linavyozungumziwa.
7 Upendo wa Kikristo utatuchochea tuepuke kuvuruga wengine wakati programu inapokuwa ikiendelea. (1 Kor. 13:5) Huo ni “wakati wa kunyamaza” na kusikiliza. (Mhu. 3:7) Kwa hiyo, epukeni kusema-sema na kutembea-tembea kusiko kwa lazima. Punguzeni safari za kwenda chooni kwa kupanga mambo kimbele. Msile wala kunywa mpaka wakati ulioamuriwa, isipokuwa matatizo mazito ya kiafya yanahusika. Wale wanaoleta vyombo vidogo-vidogo kwa ajili ya kupiga simu, kamera za kurekodi kwenye vidio-kaseti, na kamera za kupiga picha hawapaswi kuzitumia kwa namna yenye kupumbaza wengine. Wazazi wanapaswa kupanga mambo ili familia yao yote—kutia ndani vijana wenye umri wa miaka kati ya kumi na tatu na makumi mawili—ikae pamoja kusudi waweze kuangalia watoto wao kwa njia yenye kufaa.—Mez. 29:15.
8 Mwaka uliopita, mzee mmoja ambaye amekuwa akihudhuria mikusanyiko kwa makumi mengi ya miaka alisema: “Niliona kwamba mkusanyiko huu ulikuwa wenye kutokeza kwa sababu nyingine. Karibu kila msikilizaji alikuwa akiandika, kutia ndani watoto wadogo. Lilikuwa jambo la kufurahisha kuona. Biblia zilitumiwa vizuri wakati msemaji alipoomba zifunguliwe kwenye maandiko fulani.” Usikilizaji kama huo wenye uangalifu ni wa kusifiwa kwelikweli. Si kwamba tu huo unaleta faida kwetu sisi na kwa wajumbe wenzetu kwenye mkusanyiko lakini, zaidi ya yote, unamtukuza Mfundishaji Wetu Mkuu, Yehova Mungu.—Isa. 30:20.