Kukusanyika Pamoja Ili Kumsifu Yehova
1. Ni nini kichwa cha mkusanyiko, na kwa nini Yehova anastahili sifa yetu?
1 Yehova ni mweza yote katika nguvu, asiyetafutikana katika hekima, mkamilifu katika haki, na mfano halisi wa upendo. Akiwa Muumbaji, Mpaji-Uzima, na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, ni yeye peke yake anayestahili ibada yetu. (Zab. 36:9; Ufu. 4:11; 15:3, 4) Mkusanyiko wa Wilaya wa mwaka huu, wenye kichwa “Mtukuzeni Mungu,” utatia nguvu azimio letu la kumsifu yeye akiwa Mungu wa pekee wa kweli.—Zab. 86:8-10.
2, 3. Kupanga mambo vizuri kutatuwezeshaje kufaidika kikamili?
2 Kupanga Mambo Vizuri Kunahitajiwa: Ili tufaidike kikamili na karamu ya kiroho ambayo Yehova anatuwekea, kupanga mambo vizuri ni kwa lazima. (Efe. 5:15, 16) Je, umekwisha kukamilisha mipango yako ili kupata mahali pa kupanga, usafirishaji, na ruhusa ya kutokwenda kazini au shuleni? Usingoje dakika ya mwisho ili kushughulikia mambo hayo ya maana. Ikiwa unachelewa kuomba ruhusa ya kutokwenda kazini au shuleni, unaweza kukosa sehemu ya tukio hilo lenye shangwe. Baada ya kufanya jitihada kubwa ili kuhudhuria mkusanyiko wa wilaya, hatutapenda kuruhusu jambo lolote lituzuie tusifaidike na programu nzima. Kuna mambo mawili yanayoweza kutufanya tuwe wenye kukengeuka na tusiweze kufuata programu kwa uangalifu wote. Moja linaweza kuwa kukaa nje, bila kitu cha kutulinda dhidi ya nuru ya jua, na jambo lingine ni kwamba mara kwa mara kuna mvua inayokuja bila kutazamiwa. Tukiwa na hayo akilini, tunapendekeza familia ziwe na miavuli, itakayowasaidia kufuata programu ijapokuwa mambo hayo. Sote tunahitaji kuhudhuria kila kipindi cha mkusanyiko.
3 Jiwekee mradi wa kufika mapema mahali pa mkusanyiko kila siku. Hilo litakuwezesha kuwa mwenye kukaa katika kiti chako kabla ya wimbo wa kufungua na litakusaidia kuwa katika hali ya akili inayofaa ili kupokea maagizo yanayotolewa. Milango itafunguliwa pa saa 2:00 za asubuhi kila siku. Tafadhali usichunge viti isipokuwa kwa ajili ya familia yako ya karibu au wale mnaosafiri nao.
4. Kwa nini inaombwa kwamba sisi sote tulete chakula cha mchana kwenye mkusanyiko?
4 Inaombwa kwamba wote walete chakula cha mchana badala ya kutoka mahali pa mkusanyiko ili kununua chakula wakati wa mapumziko ya mchana-kati. Kushirikiana kwako na mpango huo kutachangia hali yenye amani na kutakuachia wakati zaidi ili kushirikiana na waamini wenzako. (Zab. 133:1-3) Tafadhali, kumbuka kwamba vyombo vya glasi na vinywaji vyenye alkoholi haviruhusiwi mahali pa mkusanyiko.
5. Tunawezaje kuanza kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya mkusanyiko?
5 Sikiliza na Ujifunze: Ezra alitayarisha moyo wake kwa njia ya sala ili apokee neno la Mungu. (Ezra 7:10) Alielekeza moyo wake upokee mafundisho ya Yehova. (Mez. 2:2) Hata kabla ya kuondoka nyumbani, tunaweza kuanza kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya mkusanyiko kwa kutafakari juu ya kichwa cha mkusanyiko na kukizungumzia pamoja na familia yetu.
6. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuendelee kukaza akili juu ya programu? (Ona kisanduku.)
6 Mahali wanapokaa wasikilizaji wengi, kunaweza kuwa vitu vingi vya kuona na kusikia ambavyo vinaweza kuvuta uangalifu wetu. Vikengeusha-fikira hivyo vinaweza kwa urahisi kutufanya tusikaze akili juu ya msemaji. Hilo linapotukia, tunapoteza habari yenye thamani. Mapendekezo yanayopatikana katika kisanduku kinachoambatana na makala hii yanaweza kutusaidia ili tuboreshe uwezo wetu wa kukaza fikira.
7, 8. Tunawezaje kuonyesha kwamba tunafikiria wengine?
7 Onyesha Kuwa Unawafikiria Wengine: Kamera za kupiga picha na kamera za kurekodi kwenye vidio-kaseti zinaweza kutumiwa muda wa programu, lakini ili kuepuka kukengeusha wengine, fanya hivyo tu kutoka kiti chako. Simu za mkononi zinapaswa kuzimwa ili zisisumbue wengine. Hakuna vifaa vya watu binafsi vinavyopaswa kuchomekwa kwenye mifumo ya umeme au ya sauti ya mahali pa mkusanyiko.
8 Tunatazamia kama nini kukusanyika pamoja ili kumsifu Yehova! Na tuazimie kumtukuza kwa kuhudhuria kila kipindi cha mkusanyiko, kwa kusikiliza kwa uangalifu, na kwa kutumikisha yale tunayofundishwa.—Kumb. 31:12.
[Kisanduku kwenye ukurasa wa 3]
Kusikiliza Kwenye Mikusanyiko
▪ Tafakari vichwa vya hotuba
▪ Tafuta maandiko
▪ Chukua maandishi mafupi
▪ Tenga mambo ya kutumia
▪ Rudilia unayojifunza