Programu Mpya ya Kusanyiko la Mzunguko
Maana moja ya woga ni heshima yenye kina kirefu na hofu, hasa kuelekea Mungu. Hiyo inafafanua woga wenye kufaa unaotajwa katika Maandiko kuwa “mwanzo wa akili.” (Zab. 111:10) Kinyume na hilo, aina nyingine ya woga inatawala ulimwengu wa Shetani unaotuzunguka. Tunawezaje kuepuka hisia hiyo isiyofaa na wakati huohuo kukomaza woga wenye heshima kwa Yehova? Programu mpya ya kusanyiko la mzunguko la mwaka wa utumishi wa 2002 inazungumzia ulizo hilo. Kichwa ni “Ogopeni Mungu na Kumpa Utukufu.” (Ufu. 14:7) Tutafikia kufahamu zile njia nyingi ambazo katika hizo woga wa Yehova unatufaidi tukiwa watu mmoja-mmoja na tukiwa tengenezo.
Ingawa woga unaweza kuhusisha hangaiko au kupoteza ujasiri na kusita kupambana na hali ngumu, Biblia inasema: “Heri ni kila mtu anayeogopa [Yehova].” (Zab. 128:1) Programu ya kusanyiko itatuonyesha jinsi tunavyoweza kushughulikia kwa mafanikio matatizo yanayoikabili ibada ya kweli. Tutaona jinsi ya kusaidia wapya wakuze huo woga wa Mungu wenye kufaa, ambao kwa kweli utawachochea watake kumtumikia kwa moyo wao wote, kwa nafsi yao yote, kwa akili yao yote, na kwa nguvu yao yote. (Mk. 12:30) Siku ya kwanza itamalizika kwa hotuba ya mwangalizi wa wilaya, hotuba yenye kichwa “Karibieni Zaidi na Zaidi Wale Mnaowapenda.” Ataeleza jinsi tunavyoweza kubaki macho dhidi ya jitihada ya Ibilisi ya kutugeuza kutoka kwa Yehova, familia yetu, na ndugu zetu Wakristo.
“Ogopeni Yehova, Si Wanadamu” ndicho kichwa cha hotuba-mfululizo yenye sehemu nne tutakayokuwa nayo siku ya pili. Itaeleza kwa nini na jinsi gani tunapaswa kushinda woga wowote unaotuzuia tusitimize kikamili huduma yetu au kudumisha uaminifu wetu na dhamiri safi shuleni na mahali pa kazi. Hotuba ya watu wote “Ogopeni Mungu na Kushika Amri Zake” ni yenye msingi juu ya mfululizo wa matukio yanayoelezwa kwenye Ufunuo sura ya 14. Kusanyiko la mzunguko litamalizika kwa mwongozo wenye kutia moyo wa ‘Kuendelea Kutembea Katika Woga wa Yehova.’
Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi wa kielelezo, hotuba ya ubatizo, na kifupi cha Funzo la Mnara wa Mlinzi ni mambo makuu ya ziada ya programu ambayo hamtataka kukosa. Alikeni wanafunzi wenu wa Biblia wahudhurie pamoja nanyi. Yeyote anayetaka kubatizwa anapaswa kumwambia mwangalizi msimamizi mapema zaidi iwezekanavyo. Sisi sote tutataka kuonyesha woga wenye kufaa tulio nao kuelekea Yehova na kutoa utukufu kwake kwa kutokosa sehemu yoyote ya programu hii yenye kutokeza!