Baraka Zinazotokana na Kuonyesha Uthamini Kuelekea Upendo wa Yehova—Sehemu ya 1
1 Mtume Yohana aliandika: “Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu [Yehova] alitupenda sisi kwanza.” (1 Yn. 4:19) Tunapofikiria yale yote ambayo Yehova ametutolea, tunachochewa kwa upande wetu tuonyeshe uthamini wenye kina kirefu. Yesu alionyesha mfano katika kufanya hivyo kwa kutoa ushahidi kwa utii kuhusu jina la Mungu na Ufalme wake. (Yn. 14:31) Ni vizuri tufikirie njia fulani ambazo katika hizo tunaweza kuonyesha uthamini wetu kuelekea upendo wa Yehova, na baraka zinazotokana na jambo hilo.
2 Kwenda Nyumba kwa Nyumba: Yesu alifundisha wanafunzi wake jinsi ya kutimiza kazi ya kuhubiri Ufalme. Mwongozo wake unaonyesha waziwazi kwamba walienda nyumba kwa nyumba, wakieneza habari njema. (Luka 9:1-6; 10:1-7) Inaomba kuwa na upendo kwa Mungu na kwa jirani ili kuendelea kuhubiri mlango kwa mlango wakati tunapokutana na kutojali na upinzani. Hata hivyo, tunapofanya hivyo, sisi binafsi hufaidika kwa kuwa imani yetu inakuwa imara zaidi, usadikisho wetu unakuwa wenye nguvu zaidi, na tumaini letu linakuwa lenye kung’aa zaidi.
3 Tukiwa wenye kutumika chini ya uongozi wa kimalaika, tumepata watu wengi walio na njaa na kiu kuhusu kweli. (Ufu. 14:6) Wenye nyumba fulani wamesema kwamba walikuwa wakisali ili kupata msaada wakati Shahidi alipokuja kwenye mlango wao. Mashahidi wawili na mtoto mdogo walikuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba katika kisiwa kimoja cha Karibea. Wakati dada hao walipoamua kusimamisha kazi ya siku hiyo, yule mtoto aliendelea peke yake mpaka kwenye mlango uliofuata na akapiga hodi. Mwanamke kijana akafungua mlango. Wale dada walipoona hilo, wakaenda kuzungumza naye. Akawaalika waingie, naye akawaeleza kwamba wakati huohuo alikuwa akisali ili Mungu atume Mashahidi wamfunze Biblia!
4 Kutoa Ushahidi Barabarani: Kwa kuwa ni vigumu sana mahali fulani kukuta watu nyumbani, kutoa ushahidi barabarani ni njia yenye matokeo ya kutolea watu ushahidi. Kwa kuongezea, watu wengi huishi pamoja katika mitaa yenye malango kwa ajili ya usalama au katika nyumba zenye ulinzi wa hali ya juu hivi kwamba hatuwezi kwenda mlango kwa mlango katika majengo hayo. Hata hivyo, uthamini wetu kuelekea upendo wa Yehova hutuchochea tutumie kila njia inayowezekana, kutia ndani kutoa ushahidi barabarani, ili kupasha watu ujumbe wa Ufalme.—Mez. 1:20, 21.
5 Kufanya Ziara za Kurudia: Kwa kuwa tunatafuta wale “wenye kuona uhitaji wao wa kiroho,” tunataka kufanya yale tuwezayo ili kutimiza uhitaji huo. (Mt. 5:3) Hilo linaomba turudi kutia maji juu ya mbegu za kweli tulizozipanda. (1 Kor. 3:6-8) Dada mmoja katika Australia aliacha trakti kwa mwanamke ambaye hakuonekana kuwa mwenye kupendezwa sana. Hata hivyo, dada huyo aliendelea kujaribu kupata nyumba yake. Alipokutana naye mwishowe, dada yetu akatambua kwamba baada ya ziara ya kwanza, mwanamke huyo alinunua Biblia ya bei ghali. Dada akaanza kujifunza naye!
6 Kuongoza Mafunzo ya Biblia: Hii inaweza kuwa sehemu yenye kufurahisha na yenye kuthawabisha zaidi ya huduma yetu. Ni baraka kama nini kusaidia watu wajifunze kuhusu Yehova, kuwaona wakifanya mabadiliko maishani mwao ili kumpendeza Yehova, na kisha kuwaona wakipata ubatizo wa Kikristo ili kuonyesha kwamba wamejitoa wakfu kwa Mungu!—1 Thes. 2:20; 3 Yn. 4.
7 Katika makala itakayofuata, tutazungumzia njia zaidi ambazo katika hizo tunabarikiwa kwa kuonyesha uthamini kuelekea upendo wa Yehova.