Baraka Zinazotokana na Kuonyesha Uthamini Kuelekea Upendo wa Yehova—Sehemu ya 2
1 Katika sehemu iliyozungumziwa mwezi uliopita kuhusu habari hii, tulikazia njia nne ambazo katika hizo uthamini wetu kuelekea upendo wa Yehova unaweza kuonyeshwa katika huduma. (1 Yn. 4:9-11) Hapa, tutaongeza njia tano za zaidi za kufanya hivyo. Tunabarikiwa wakati tunaposhiriki kikamili kusaidia wengine kiroho.
2 Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi: Hii ni njia yenye matokeo ya kupata watu wenye njaa na kiu kuhusu uadilifu na kuwaachia vichapo vitakavyowasaidia. Ni vizuri ‘kununua wakati wenye kufaa’ na kutoa ushahidi nyakati zote na kwa mtu yeyote tunayekutana naye. (Efe. 5:16) Huenda tukalazimika kujipa moyo ili kutoa ushahidi katika njia hiyo, lakini ikiwa tunathamini upendo wa Mungu na tunaelewa mahitaji ya watu, tutatoa ushahidi kila wakati nafasi inapojitokeza.—2 Tim. 1:7, 8.
3 Mishonari mmoja alibarikiwa sana kwa kuanzisha mazungumzo na msafiri mwenzake katika teksi. Mwanamume huyo alionyesha kupendezwa. Ziara za kurudia zikafanywa, na funzo la Biblia likaanzishwa. Mwanamume huyo akaja katika kweli, naye akafanya maendeleo kufikia kuwa mzee wa kutaniko!
4 Kuandika Barua: Labda hatuwezi kwenda nyumba kwa nyumba kwa sababu ya udhaifu fulani wa kimwili au hali mbaya ya hewa. Tunaweza kuandika barua, tukitoa kwa njia hiyo ushahidi mfupi kwa watu tunaowajua, wale waliopoteza wapendwa katika kifo, au wale ambao hawakuwa nyumbani katika eneo. Katika barua, tunaweza kutia moja ya trakti zetu zenye kupatana na wakati, trakti ambayo ina ujumbe wa Biblia wenye kuvutia na ambayo inatia moyo yule anayeipokea ajibu ikiwa ana maulizo yoyote. Tumia anwani yako binafsi au ile ya Jumba la Ufalme; tafadhali msitumie anwani ya ofisi ya tawi.
5 Kutoa Ushahidi kwa Njia ya Simu: Hii ni njia bora ya kufikia watu tusioweza kukutana nao katika kazi ya nyumba kwa nyumba. Ikiwa tunafanya hivyo kwa busara, kwa wema, na kwa ufundi, tunaweza kupata itikio zuri sana. Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 2001, ukurasa wa 5-6, inatoa mapendekezo yenye kufaa kuhusu jinsi ya kupata matokeo bora zaidi.
6 Wakati dada mmoja alipokuwa akitoa ushahidi kwa njia ya simu, aliuliza mwanamke mmoja ikiwa alikuwa amefikiria sana kile ambacho wakati ujao unamwekea yeye na familia yake. Mwanamke huyo akasema kwamba alikuwa amefikiria jambo hilo. Akafunua kwamba kwa sababu ya kukata kwake tumaini, alikuwa amejitenga nyumbani. Akichochewa na hangaiko la kweli la dada, mwanamke huyo akakubali kukutana naye kwenye soko la kando-kando. Kama tokeo, mwanamke huyo akakubali funzo la Biblia bila kusita!
7 Kukaribisha Wageni: Ikiwa tunapenda majirani zetu, tutakuwa macho ili kutambua mgeni yeyote anayetembelea mahali petu pa mkutano, nasi tutamfanya ajisikie kuwa mwenye kukaribishwa. (Rom. 15:7) Mwonyesheni kwamba yuko katikati ya watu wanaopendezwa sana na hali yake njema ya kiroho. Hangaiko letu lenye unyofu na pendekezo letu la kujifunza Biblia kibinafsi huenda vikamchochea akubali msaada wetu.
8 Mwenendo Wetu Mzuri: Tunapamba kweli kupitia mwenendo wetu mzuri. (Tito 2:10) Wakati watu wa ulimwengu wanaposema vizuri juu yetu tukiwa Mashahidi wa Yehova, wao huleta sifa kwa Mungu wetu. (1 Pet. 2:12) Hilo pia linaweza kusaidia wengine waanze kutembea katika njia inayoongoza kwenye uzima.
9 Kwa nini usirudilie njia hizo tano za kuonyesha uthamini wetu kuelekea upendo mkubwa wa Yehova kwetu na kuzitumikisha? (1 Yn. 4:16) Kwa kufanya hivyo, utavuna baraka nyingi.